Sunday, September 21, 2014

MAJAMBAZI YAVAMIA YAUA YAJERUHI

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

WATU wanne wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wanatuhumiwa kumwua mtu mmoja mwenye umri kati ya miaka (35) na (40) ambaye jina lake halikuweza kufahamika na kumjeruhi mwingine baada ya kufanya tukio la uhalifu kwenye maduka yaliyopo kwenye stendi ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani jirani na kituo cha polisi.

Kutokana na tukio hilo Jeshi la polisi Mkoani Pwani linawatafuta watu hao ambao walikuwa na bunduki hao ambao walivamia duka liitwalo Bahati mali ya Hashim Kisaka na ofisi ya kukatia tiketi ya mabasi yaendayo mikoani kisha kupora fedha kwenye maduka hayo.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kaimu kamanda wa polisi mkoani
humo Athumani Mwambalasa alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 2 kasoro usiku Septemba 20 mwaka huu.

“Watu hao walivamia katika maeneo hayo wakiwa na silaha ambayo bado haijafahamika na kumuua mtu huyo kwa kumpiga na risasi ya kifuani kisha kumjeruhi mguuni  mfanyabishara wa korosho Ambwene Mwambungu wakati wa tukio hilo ambalo lilifanyika huku umeme ukiwa umekatika na hali iliyofanya kukawa na giza nene na watu hao kutumia mwanya huo kutekeleza tukio hilo,” alisema Kamanda Mwambalaswa.

Kamanda Mwambalasa alielezea kuwa kwenye tukio hilo watu hao wakiwa na silaha hiyo walivamia katika maduka hayo na kuanza
kupiga risasi hewani hali iliyowafanya watu waliokuwa katika eneo hilo kukimbia hovyo huku wakiacha mali zao kuhofia usalama wao kisha kupora fedha na mali ambayo thamani yake bado haijafahamika.

“Marehemu alifikwa na mauti wakati akipelekwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Pwani ya Tumbi  huku majeruhi wa tukio hilo bado amelazwa akipatiwa matibabu kutokana na majeraha ya mguu aliyoyapata,” alisema Kamanda Mwambalaswa.


Aliwataka wananchi kushirikiana kwa pamoja kutoa taarifa mara moja watakapobaini walipo watu hao pia kutoa taarifa  mara wanapohisi watu wasioeleweka katika maeneo yao.

Mwisho

Saturday, September 20, 2014

KINANA AIBUA MAKUBWA KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahman Kinana amezishauri Halmashauri nchini kulipatia Shirika la Nyumba Tanzania (NHC) viwanja bure ili liweze kujenga nyumba kwa bei nafauu ambazo wananchi wa hali ya chini wataweza kuzinunua.
Aliyasema hayo jana mjini Kibaha kwenye mkutano wa hadhara pamoja na kukabidhiwa mashine rahisi za kufyatulia matofali kwa vijana wa mkoa wa Pwani kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani hapa.
Kinana alisema kuwa tatizo la ukosefu wa nyumba za kuishi ni kubwa hasa kwenye miji hivyo endapo NHC ingejenga nyumba nyingi ingesaidia wananchi kuweze kununua nyumba hizo kwa bei nafuu au kupangisha kwa gharama ndogo.
“Nawapongeza NHC kwa kufanya mageuzi makubwa ya ajira kwa kuwasaidia vijana pia kwa kuwapatia mashine hizi ambazo zitakuwa ni mkombozi kwao kwani mbali ya kujiongezea kipato pia wataweza kujenga nyumba kwa gharama nafuu na za kisasa,” alisema Kinana.
Alisema haya ni mapinduzi makubwa na mapya kwenye Taifa ambalo liko kwenye kazi kubwa ya kuhakikisha vijana wanapata ajira kwani mashine hizo zitawazalishia fedha na kuleta mabadiliko kwenye sekta ya ujenzi hapa nchini na kufanya gharama za nyumba kushuka.
Akimkabidhi mashine hizo meneja wa NHC Paulina Mrango alisema kuwa wameamua kutoa mashine hizo kwa lengo la kuisaidia serikali kukabiliana na uhaba wa ajira pia kufanya ujenzi kwa gharama nafuu.
Mrango alisema kuwa wametoa mashine 28 kwa vikundi vya vijana kwenye Halmashauri zote za mkoa wa Pwani ambapo mpango huo utakuwa kwa nchi nzima ili kufanikisha ufyatuaji wa matofali ya kisasa kwa kutumia gharama ndogo ya malighafi.
“Tumetoa mashine hizo 28 zenye thamani ya shilingi milioni 12.6 kwa Halmashauri na tutazipatia fedha kiasi cha shilingi 500,000 kama mtaji wa kuwakopesha wanavikundi hao ambapo vikundi vitakavyopewa mashine hizi vitapatiwa mafunzo ya wiki mbili na wakufunzi kutoka VETA ili wajue namna ya kuzitumia,” alisema Mrango.
Aidha alisema kuwa mbali ya tofali hizo kuwa za gharama nafuu pia itasaidia utunzaji wa mazingira kwani maeneo ya vijijini wengi wanatumia tofali za kuchoma ambazo zinachomwa kw akutumia kuni zinazotokana na miti hivyo kuharibu mazingira.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHIRIKISHO la Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba serikali kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu na wazee wanapata dawa wanazoandikiwa na daktari mara waendapo hospitalini.
Akiuliza swali mbele ya katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahman Kinana kwenye mkutano wa hadhara wakati wa ziara yake mkoani humo, mwenyekiti wa shirikisho hilo Ally Mkanga alisema kuwa wamekuwa wakinyimwa dawa na kutakiwa kwenda kununua kwenye maduka ya dawa.
Mkanga alisema kuwa sera inasema kuwa wazee, watoto chini ya miaka mitano na wanawake wanaojifungua huduma ni bure lakini hupaswa kununua pia mbali ya kutakiwa kulipia dawa  kwenye mahospitali hazipatikani na kutakiwa kununua kwenye maduka hayo.
“Tunaiomba serikali ihakikishe sera zake za matibabu bure kwa makundi yanayopaswa kutolipia dawa hayalipishwi kwani inakuwa changamoto kubwa kwao hasa wazee na watu wenye ulemavu,” alisema Mkanga.
Alisema watu wenye ulemavu wanapata shida wanapokwenda hospitali kwani mazingira kwao si rafiki hivyo wameiomba serikali kuhakikisha inaweka mazingira rafiki kwa wao kupata huduma za afya.
Akijibu swali hilo mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa ni kweli kuna changamoto hizo lakini wameweka madirishwa kwa ajili ya wa wazee kwenye hospitali ya wilaya ya Mkoani lakini tatizo dawa wanazopewa ni za hadhi ya kituo cha afya.
“Kituo cha afya cha Mkoani kilipandishwa hadhi na kuwa hospitali ya wilaya lakini mgao wake wa dawa inapata kama kituo cha afya na si hospitali ya wilaya jambo ambalo ni changamoto kubwa hasa ikizingatiwa Hospitali ya Tumbi imepandishwa hadhi  na kuwa mkoa ya Rufaa ambapo wagonjwa wote wanatakiwa waanzie hapa hivyo kumekuwa na mlundikano mkubwa wa wagonjwa,” alisema Kihemba.
Kihemba alibainisha pia katika kukabiliana na tatizo la dawa kwenye mahospitali wameunda kamati ya dawa ili kuhakikisha inafuatilia suala la upatikanaji wa dawa na kutolewa kwa utaratibu unaotakiwa ili kuondoa malalamiko kwa wagonjwa wanaopata huduma kwenye halmashauri ya wilaya.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA wadogo wilayani Kibaha mkoani Pwani wameilalamikia Halmashauri ya wilaya ya Kibaha kwa kuwalipisha kodi na ushuru mkubwa na kuwa mzigo mkubwa kwao hivyo kushindwa kufanya biashara.
Akiuliza swali mbele ya katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahman Kinana ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mkutano wa hadhara ambao ulifanyika kwenye uwanja wa Bwawani wa Bwawani Maili Moja wilayani Kibaha, mwenyekiti wa soko la Maili Moja Ally Gonzi alisema wamekuwa wakilipa kodi nyingi.
Gonzi alisema kuwa halmashauri hiyo imekuwa ikiwatoza kodi na ushuru mbalimbali na kuwa kero kwa wafanyabiashara wadogo kwenye soko na maeneo mengine ya mji huo na kuwafanya wawe kwenye wakati mgumu wa kufanya biashara zao.
“Tunaiomba serikali itupunguzie mzigo wa kodi kwa ni nyingi na wengine biashara zao ni ndogondogo na za mkopo lakini tunabanwa tulipie tunajikuta mitaji inakufa kutokana na kodi hizo ambazo ni kubwa kuanzia 50,000 na hadi zaidi ya 100,000 hivyo tunashindwa kujikwamua kwenye hali ngumu,” alisema Gonzi.
Aidha alisema kuwa  Halmashauri imekuwa ikitumia nguvu kubwa kwa kutumia askari wenye silaha au mgambo wakati wa kuja kuchukua kodi kwa wafanyabiashara ambao wanajitafutia riziki za familia zao.     
Kwa upande wake  Kinana alizitaka Halmashauri nchini kupunguza kodi ambazo ni kero kwa wananchi pia ziwashirikishe wafanyabiashara kabla ya kuzipitisha kwani baadhi yao wanatafuta hela za kula tu.
Kinana alisema kuwa miaka michache iliyopita serikali ilifuta kodi ambazo zilikuwa kero lakini kodi hizo zimerudi mlango wa nyuma na kuwafanya wafanyabiashara wadogo wazilalamikie kwani zimekuwa mzigo mkubwa kwao.
“Hawa wanajitafutia fedha kwa ajili ya familia ili wapate chakula na riziki hivyo lazima halmashauri zifikirie upya suala la kodi kuwa nyingi kwa wafanyabiashara wadogo kutokana na hali hii nitaongea na wabunge wa CCM ili kuondoa kodi ambazo ni mzigo kwa wafanyabiashara wadogo,” alisema Kinana.
Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Adhu Mkomambo alisema kuwa wao kama Halmashauri watakaa kuangalia namna ya kurekebisha kodi na ushuru mbalimbali ili kuondoa kero hizo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WALINZI wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wameulalamikia uongozi wa Halmashauri hiyo kwa kushindwa kuwaajiri kwa kipindi cha  miaka 10 sasa.
Akizungmza kwa niaba ya wenzake mbela ya katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdulrahman Kinana kwenye mkutano wa hadhara kwenye uwanja wa Bwawani wilayani Kibaha mkoani Pwani, Jafar Mtimbuka alisema kuwa amefanya kazi kwa kipindi cha miaka 10 bila ya kuajiriwa huku akiwa kama kibarua.
Mtimbuka alisema kuwa wamefanya kazi kama vibarua kwa kipindi hicho pasipo kuajiriwa na kuambiwa kuwa hawana sifa jambo ambalo si la kweli kwani baadhi yao wamehitimu mafunzo ya mgambo na wengine Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
“Katibu hata kama nitafukuzwa kazi sawa lakini tunaomba utusaidie kwani tumefanyakazi muda mrefu kama vibarua bila ya ajira wanasema hatuna sifa wakati mimi nimehitimu mafunzo ya JKT nashangaa wanasema kuwa hatuna sifa,” alisema Mtimbuka.
Kwa upande wake mkurugenzi wa halmashauri hiyo Jenifa Omolo alipotakiwa kujibu suala hilo alisema kuwa analifahamu suala hilo lakini walinzi hao hawana sifa na halmashauri haikuwa na utaratibu wa kuajiri kada hizo zikiwemo zile za chini.
Omolo alisema kuwa kwa sasa wamepata kibali kwa ajili ya kuajiri kada za chini wakiwemo walinzi na wengine hivyo kama watakuwa na sifa wataajiriwa kulingana na uwezo wao.
Naye katibu Mkuu Kinana alisema kuwa mtu kafanya kazi miaka 10 anaambiwa hana sifa jambo ambalo halipendezi inabidi waangaliwe na wanastahili kuajiriwa kama wafanyakazi wengine.
“Mwenye sifa aajiriwe na huyu wa miaka 10 ana haki ya kuajiriwa haiwezekani mseme hana sifa kwa miaka hiyo aliyofanyakazi kwani sheria ni miezi mitatu na amefanyiwa vibaya si haki,” alisema Kinana.
Kinana alisema kuwa mlinzi huyo aajiriwe na fedha zake za utumishi kwa kipindi hicho ziunganishwe kwenye mafao yake wakati wa kustaafu kwenye pensheni yake.
Mwisho.      
        
     

      

Friday, September 12, 2014

MSHINDI WA TABORA MARATHON AOMBA UFADHILI KUPIGA KAMBI NCHINI KENYA

Mwanariadha John Mwandu akihojiwa na vyombo vya habari baada ya kushinda mbio za Tabora Marathon kwenye mashindano yaliyofanyika mkoani Tabora mwaka 2013


John Mwandu akimaliza mbio za mita 1,500 kwenye mashindano ya Taifa yaliyofanyika kwenye uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam mwezi Julai mwaka 2014.

Mwanariadha John Mwandu akifanya mazoezi kabla ya kuingia kwenye mashindano ya Taifa yaliyofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro mwaka 2013

Mwanariadha John Mwandu watatu kutoka kulia kwenda kushoto akianza kukimbia mbio za mita 800, mwaka 2013 huko uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro

Mwanariadha John Mwandu watatu kutoka kushoto akiwa ameshika medali na kombe baada ya kushinda mashindano ya Tabora Marathon akiwa na washindi wengine,  wapili kulia aliyevaa suti nyeusi ni mkuu wa Wilaya ya Tabora Mjini Kumchaya. Mashindano hayo yalifanyika mkoani Tabora mwaka 2013

Mwanariadha John Mwandu akiwa na washindi wngine na baadhi ya viongozi wa serikali mara baada ya kuibuka mshindi wa mashindano ya Tabora Marathon yaliyofanyika mwaka  2013,nyuma juu ni picha mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Mwanariadha John Mwandu akiwa na washindi wengine baada ya kushinda mbio za Tabora Marathon mashindano yaliyofanyika mkoani Tabora mwaka 2013

Mwanariadha John Mwandu akivalishwa medali na mkuu wa wilaya ya Tabora Mjini Kumchaya baada ya kushinda mashindano ya Tabora Marathon yaliyofanyika mwaka 2013

Hii ni barua ambayo inayoonyesha kukubaliwa kwa mwanariadha John Mwandu kwenda kwenye kambi ya riadha ya Mara Runners Club ya nchini Kenya ambapo Mwandu anatarajia kwenda Desemba mwaka huu hivyo anaomba wafadhili mbalilmbali kujitokeza kumsaidia ambapo barua hiyo imesainiwa mwalimu wa kituo hicho Samwel Koech (IAAF, Toecs/coach Lev. 2)

Thursday, September 11, 2014

ABAKWA ANYONGWA ATUPWA KICHAKANI


Na John Gagarini, Kibaha
MKAZI wa Kijiji cha Bupu kata ya Bupu Tarafa ya Mkamba wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani Forodesi Ntabegera (30) ameuwawa kwa kubakwa kisha kunyongwa na watu wasiojulikana kisha mwili wake kutupwa kichakani.
Kwa mujibu wa taarifa ziliotolewa na kaimu kamanda wa polisi mkoani Pwani Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo Mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa Marehemu kuwa marehemu alinyongwa na watu hao kwa kutumia kitenge chake alichokuwa amekivaa.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 9 mwaka huu majira ya saa 8:00 mchana baada ya wakazi wa kijiji hicho kufanya msako wa kumtafuta marehemu ambaye alipotea Septemba 8.
“Baada ya msako huo kufanyika mwili wa marehemu ulikutwa kwenye kichaka umbali wa mita 30 kutoka barabarani ambapo mwili wake ulimwagiwa unga sehemu za kichwani na mgongoni,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alisema watu hao walitumia mfuko wa salfeti aliokuwa amebebea unga aliotoka kuusaga mashine, kumvisha miguuni kisha mwili wake waliulaza kifudifudi.
Aidha alisema kuwa taarifa za kupotea marehemu zilitolewa na kituo cha polisi Kimazinchana na mwenyekiti wa Kijiji cha Bupu Kasimu Kambangwa walioongozana na watoto wa marehemu ambao walidai mama yao alitoweka baada ya kuaga kuwa anakwenda kusaga na hakuonekana tena hadi mwili wake ulipokutwa kwenye eneo hilo.
Mwisho.

MASHINE ZA EFD

Na John Gagarini, Kibaha
JUMUIYA ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) mkoa wa Pwani imeiomba serikali kuangalia upya mfumo wa mashine za risiti za Kieletroniki (EFD) ili itambue gharama za manunuzi ya bidhaa.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na mwenyekiti wa Jumuiya hiyo mkoani hapa Abdala Ndauka na kusema kuwa mashine hiyo inatambua ulichouza tu na haitambui gharama zingine.  
Ndauka alisema kuwa wafanyabiashara hao hawana tatizo la kununua mashine hizo kwani wao ni wazalendo na wana nia ya kuchangia mapato ya serikali.
“Changamoto yetu kubwa ni gharama zingine na sisi tuko tayari kuzinunua mashine hizo ila serikali ingeweka mfumo wa kutambua gharama nyingine ili kuwe na unafuu,” alisema Ndauka.
Alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara wanafanya biashara zao kwa njia ya mikopo na mitaji yao ni midogo hivyo ni vema ingeweka mazingira ya kujua na gharama za manunuzi ya bidhaa na gharama za uendeshaji.
“Mashine hizo zinauzwa kati ya shilingi 800,000 na 600,000 kutegemeana na biashara kwa mfanyabiashara mchanga au mwenye mtaji mdogo hawezi kumudu kuinunua,” alisema Ndauka.
Aidha alisema kuwa walifanya kikao na Naibu Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba huko Dodoma ambapo walikubaliana kuwa wafanyabiashara wasifungiwe maduka huku majadiliano yakiendelea.
“Makubaliano na Waziri huko Dodoma yamekiukwa kwani hata kamishna mkuu wa Mamlaka ya Mapato (TRA) aliwaambia watendaji mikoani kutoyafunga maduka kutokana na kukosa mashine hizo lakini wanashangaa mkoa wa Pwani maduka yanafungwa na mamlaka hiyo,” alisema Ndauka.
Akizungumzia suala hilo ofisini kwake, meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Pwani, Highness Chacky, alisema kuwa mashine hizo ni muhimu kwa ajili ya malipo sahihi na wao kutunza kumbukumbu za biashara zao.
Chacky alisema hiyo ni awamu ya pili ambayo inahusisha wafanyabiashara ambao mapato yao kwa mwaka ni kuanzi kiasi cha shilingi milioni 14 hadi 39 kwa mwaka  na biashara ambazo zilikuwa na misamaha ya kodi ya ongezeko la thamani  (VAT).
“Mashine zina bei totauti kutegemeana na biashara ni kati ya shilingi 800,000 na 600,000 ni mali yao na serikali haina hela za kuweza kuwanunulia mashine hizo lakini wakishazinunua fedha zao zitarejeshwa kwa kutolipia kodi ambazo wanakuwa wamekadiriwa kwa mwaka hadi pale hela yao itakapokuwa imekwisha na baada ya hapo wataendelea kulipa kodi,” alisema Chacky.
Alisema kuwa wanaweza kulipia mashine hizo kwa awamu toka kwa mawakala wa mashine hizo hadi pale watakapomaliza na kukabidhiwa mashine na si kufanya mgomo kwani ni kuwanyima haki wateja na kusema kuwa hajapata barua yoyote ya kuitaka TRA isitishe zoezi hilo.

Mwisho.   

Thursday, August 28, 2014

RT YATAKIWA KUANDAA MKUTANO WA KATIBA

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Riadha Tanzania (RT) kimetakiwa kiandae mkutano mkuu wa chama ili kupitia rasimu ya katiba baada ya mkutano kama huo kuahirishwa Juni na kutakiwa kufanyika Novemba mwaka jana lakini hadi sasa hakuna taarifa ya kufanyika mkutano kama huo .
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha mwenyekiti wa chama cha riadha mkoa wa Pwani (CRAA) Joseph Luhende alisema kuwa baada ya kushindikana kufanyika kwa mkutano kwa ajili ya kupitisha rasimu hiyo huko mkoani Morogoro iliamuliwa kuwa mkutano kama huo ufanyike lakini hadi sasa imekuwa kimya.
Luhende alisema kuwa upitishaji wa rasimu ya chama ilishindikana kutokan na kuchelewa hivyo kupangwa Novemba mwaka jana na hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya kufanyika mkutano kwa ajili ya kukamilisha zoezi hilo.
“Mbali ya kushindikana kupitishwa kwa rasimu ya katiba hiyo pia vyama vilitakiwa visitumie katiba ya zamani na tulivyouliza tuliambiwa kuwa tusubiri na sasa inakaribia kufika mwaka lakini hakuna lolote linaloendelea hali ambayo inakatisha tamaa,” alisema Luhende.
Alisema mchezo wa riadha unakumbwa na changamoto nyingi hivyo rasimu hiyo ingepitishwa ingesaidia kuboresha riadha lakini utekelezaji umekuwa mgumu na rasimu ndiyo inayopelekea kupata katiba ambayo ni kila kitu sawa na dira ya mwelekeo wa mchezo huo.
“Utendaji kazi unakuwa mgumu kutokana na kutakiwa tusitumie katiba ya zamani hivyo ni vema rasimu hiyo ikapitishwa ili tuweze kupata katiba mpya ambayo itatuongoza,” alisema Luhende.
Aidha alisema kuwa kutokana na mipango ya RT kutokuwa mizuri kumechangia nchi kufanya vibaya kwenye michuano ya kimataifa mfano ile ya Olimpiki ambapo Tanzania iliambulia patupu kwenye mchezo huo na kuwataka viongozi wa shirikisho hilo kuwa makini katika kutekeleza majukumua yao.
Akijibu kuhusiana na suala hilo kwa njia ya simu katibu mkuu wa RT Suleiman Nyambui alisema kuwa tatizo kubwa lililopo ni ukosefu wa fedha ndiyo inapelekea wao kushindwa kuandaa mkutano mkuu wa kupitisha rasimu hiyo ya katiba ili kupata katiba mpya.
“Tunaendelea kuwasiliana na wafadhili mbalimbali ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya kuandaa mkutano huo wa kupata katiba ambayo itaongoza chama baada ya mkutano wa awali kushindwa kuendelea baada ya viongozi wa mikoa ambao walisema hawajaisoma vizuri hivyo ikashindika kuijadili rasimu hiyo,” alisema Nyambui.
Nyambui alisema walipeleka katiba mikoani kwa ajili ya wao kutoa mapendekezo lakini hawakuweza kuyapeleka ambapo ni mikoa mitatu tu ndiyo iliyotoa mapendekezo yake  ambayo ni Dar es Salaam, Arusha na Dodoma huku mingine ikiwa bado.
“Tunatarajia kuitisha mkutano mkuu kabla ya mwaka haujaisha ili kukamilisha zoezi la kupata katiba baada ya marekebisho kufanyika kwenye mkutano na kikwazo kikuu ni ukosefu wa fedha,” alisema Nyambui.
Mwisho.



HALMASHAURI ZAKATAZWA KUTOZA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE mkoa wa Pwani umetoa tamko la kuzizuia Halmashauri za mkoa huo kuendelea kutoza ushuru wa hoteli na nyumba za kulala wageni ambao ulifutwa na bunge mwaka 2009 huku Halmashauri ya mji wa Kibaha ikiwa inaendelea kuutoza na kusababisha malalamiko ya wafanyabiashara hao.
Kufuatia halmashauri hiyo kuendelea kutoza ushuru huo kupitia umoja wao Wamiliki wa Hoteli wilayani Kibaha mkoani Pwani (UGEHOKI) walipeleka malalamiko yao ofisi ya katibu tawala wa mkoa huo kupinga kutozwa ushuruhuo wa asilimia 20.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Kaimu Katibu Tawala wa mkoa huo Mhandisi Michael Mrema, alisema kuwa halmashauri zote zilipewa miongozo kutoka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) juu ya kusitisha utozaji huo hadi watakapopewa utartibu mwingine wa ukusanyaji.
“Tulipokea barua toka kwa wamiliki hao juu ya kulalamikia ushuruhu huo ambao ulisitishwa wakati wizara zinazohusika zitakapokuwa zimeweka utaratibu mwingine wa namna ya ukusanyaji wa ushuru huo ambao ulilalamikiwa na wamiliki hao kuwa ni mkubwa sana,” alisema Mrema.
Mrema alisema kuwa barua hiyo toka TAMISEMI ya kusitisha ushuru huo yenye kumbukumbu namba Na. FA 2/266/01/10 ya Mei ya mwaka 2014 kwa halmashauri zote nchini ambayo ilitokana na barua yenye kumbukumbu Na. CE.325/387/03/47 ya tarehe 16 ya mwezi wa Aprili mwaka 2014 iliyotoa uafafanuzi zaidi.
“Katika ufafanuzi TAMISEMI ilisema kuwa ushuru wa nyumba za kulala wageni umeainishwa katika sheria ya fedha sura 290 kifungu cha 6(1)(q) na 7(1)(u) na kwamba awali ushuru huo ulikuwa ukitozwa kupitia sheria ya hoteli sura 105 ambayo imefutwa baada ya kutungwa sheria mpya sheria ya Utalii na 29 ya mwaka 2008 na kuanza kutumika rasmi Julai Mosi 2009 baada ya kutangazwa kwenye gazeti la serikali namba 212 la tarehe 1 Julai 2009 ni wazi kuendelea kutozwa ni kukiuka sheria za Utalii,” alisema Mrema.
Aidha Mrema alisema kutokana na barua hizo Halmashauri zilipaswa kutoendelea kutoza ushuru huo hivyo hazipaswi kuendelea kuutoza na zikiendelea kutoza kunaweza kusababisha halmashauri na watoa huduma  hao ni kusababisha migogoro mikubwa ya kisheria na kwa sasa wizara za TAMISEMI, Wizara ya Fedha na Wizara ya Maliasili na Utalii zipo katika majadiliano ya kuamua namna bora ya kurejesha ushuru huo.

Alizitaka halmashauri hizo kutekeleza agizo hilo na maagizo mengine yanayotoka ngazi za juu ili kuepusha migogoro na watoa huduma na wananchi katika suala zima la ukusanyaji wa mapato mbalimbali.