Thursday, August 28, 2014

HALMASHAURI ZAKATAZWA KUTOZA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE mkoa wa Pwani umetoa tamko la kuzizuia Halmashauri za mkoa huo kuendelea kutoza ushuru wa hoteli na nyumba za kulala wageni ambao ulifutwa na bunge mwaka 2009 huku Halmashauri ya mji wa Kibaha ikiwa inaendelea kuutoza na kusababisha malalamiko ya wafanyabiashara hao.
Kufuatia halmashauri hiyo kuendelea kutoza ushuru huo kupitia umoja wao Wamiliki wa Hoteli wilayani Kibaha mkoani Pwani (UGEHOKI) walipeleka malalamiko yao ofisi ya katibu tawala wa mkoa huo kupinga kutozwa ushuruhuo wa asilimia 20.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Kaimu Katibu Tawala wa mkoa huo Mhandisi Michael Mrema, alisema kuwa halmashauri zote zilipewa miongozo kutoka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) juu ya kusitisha utozaji huo hadi watakapopewa utartibu mwingine wa ukusanyaji.
“Tulipokea barua toka kwa wamiliki hao juu ya kulalamikia ushuruhu huo ambao ulisitishwa wakati wizara zinazohusika zitakapokuwa zimeweka utaratibu mwingine wa namna ya ukusanyaji wa ushuru huo ambao ulilalamikiwa na wamiliki hao kuwa ni mkubwa sana,” alisema Mrema.
Mrema alisema kuwa barua hiyo toka TAMISEMI ya kusitisha ushuru huo yenye kumbukumbu namba Na. FA 2/266/01/10 ya Mei ya mwaka 2014 kwa halmashauri zote nchini ambayo ilitokana na barua yenye kumbukumbu Na. CE.325/387/03/47 ya tarehe 16 ya mwezi wa Aprili mwaka 2014 iliyotoa uafafanuzi zaidi.
“Katika ufafanuzi TAMISEMI ilisema kuwa ushuru wa nyumba za kulala wageni umeainishwa katika sheria ya fedha sura 290 kifungu cha 6(1)(q) na 7(1)(u) na kwamba awali ushuru huo ulikuwa ukitozwa kupitia sheria ya hoteli sura 105 ambayo imefutwa baada ya kutungwa sheria mpya sheria ya Utalii na 29 ya mwaka 2008 na kuanza kutumika rasmi Julai Mosi 2009 baada ya kutangazwa kwenye gazeti la serikali namba 212 la tarehe 1 Julai 2009 ni wazi kuendelea kutozwa ni kukiuka sheria za Utalii,” alisema Mrema.
Aidha Mrema alisema kutokana na barua hizo Halmashauri zilipaswa kutoendelea kutoza ushuru huo hivyo hazipaswi kuendelea kuutoza na zikiendelea kutoza kunaweza kusababisha halmashauri na watoa huduma  hao ni kusababisha migogoro mikubwa ya kisheria na kwa sasa wizara za TAMISEMI, Wizara ya Fedha na Wizara ya Maliasili na Utalii zipo katika majadiliano ya kuamua namna bora ya kurejesha ushuru huo.

Alizitaka halmashauri hizo kutekeleza agizo hilo na maagizo mengine yanayotoka ngazi za juu ili kuepusha migogoro na watoa huduma na wananchi katika suala zima la ukusanyaji wa mapato mbalimbali.

No comments:

Post a Comment