Thursday, August 21, 2014

UTINGO AFA AJALINI OFISA WA OFISI YA DCI ANUSURIKA AJALINI

Na John Gagarini, Kibaha
UTINGO wa lori la mizigo Adam Rashid (28) mkazi wa Bwiringu kata ya Pera wilaya ya Bagamoyo amekufa baada ya lori alilokuwa akisafiria kugongana na lori lingine
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kaimu kamanda wa polisi mkoani humo Mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa malori hayo yaligongana uso kwa uso.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 19 mwaka huu majira ya saa 10 jioni eneo la Sweet Corner.
“Marehemu alikuwa kwenye gari namba T 650 BED aina ya Fuso lililokuwa likiendeshwa na na Ramadhan Mwarami (40) mkazi wa Bwiringu likiwa limebeba simenti likitokea Jijini Dar es Salaam kwenda Chalinze,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alisema kuwa lori alilokuwa amepanda marehemu liligongana na lori lenye namba za usajili T 853 APA aina ya Fuso ambalo lilikuwa likitokea mkoani Mbeya kwenda Dar es Salaam likiwa limebeba Mahindi likiendeshwa na Shan Iddi (28) mkazi wa Mwanga liligongana na lori hilo na kusababisha kifo hicho.
Aidha alisema kuwa dereva wa lori alilokuwa amepanda marehemu aliumia kidogo ambapo marehemu alifariki dunia wakati akipata matibabu kwenye hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani ya Tumbi.
Wakati huo huo Ofisa Mwandamizi wa jeshi hilo anayeshughulikia majalada ya kesi katika ofisi ya mkurugenzi wa makosa ya jinai  (DCI) Ilembo amenusurika kifo baada ya gari alilokuwa akisafiria kugonga mti.
Akifafanua kuhusiana na tukio hilo Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa ofisa huyo alikuwa akitokea mkoani Iringa kikazi.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 20 mwaka huu majira ya saa 9 alfajiri eneo la Vigwaza kata ya Pera wilayani Bagamoyo.
“Chanzo cha ajali hiyo ni gari hilo la polisi kutaka kugongana uso kwa uso na gari lingine baada ya kulipita gari lililokuwa mbele yao na alipotokeza akakutana na hilo gari hali iliyofanya dereva akwepe kisha kuserereka kwenye mtaro na baadaye kugonga mti,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa gari hilo lilipasuka matairi na vioo vilivunjika ambapo gari lililohusika na tukio hilo halikuweza kusimama mara baada ya tukio hilo

Mwisho.

No comments:

Post a Comment