Sunday, August 10, 2014

POLISI YAKANUSHA MTU KUCHUNWA NGOZI PWANI


JESHI la Polisi mkoani Pwani limekanusha uvumi ulioenea na kudai kuwa mkazi wa Kijiji cha Dondo wilaya ya Mkuranga Hamis Mahimbwa (20) kuwa amekufa kwa kuchunwa ngozi mwili mzima ila ni kutokana na kuungua na moto.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana mjini Kibaha kaimu kamanda wa Polisi mkoani humo mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa amesema kuwa hakuna tukio kama hilo mkoani hapo.
Akifafanua juu ya tukio la mtu huyo kufa amesema kuwa mnamo Agosti 6 mwaka huu majira ya saa 2:00 usiku huko katika kijiji cha Dondo Tutani kata ya Kisiju wilayani humo Hamis Mahimbwa (27) alikutwa na wananchi akiwa ameungua moto mwili mzima.
Kamanda Mwambalaswa amesema marehemu alipiga kelele kuomba msaada baada ya kuungua na moto na kumchukua na kumpeleka hospitali kwenye kituo cha afya cha Kalole Kisiju na kuanza kupatiwa matibabu lakini kutokana na kuungua sana na moto alifariki dunia Agosti 7 mwaka huu majira ya saa 11:00 alfajiri.
Amesema kuwa baada ya kifo hicho ilipelekwa taarifa kwenye kituo cha polisi cha Mkuranga na jalada la uchunguzi MKU/IR/1202/2014 lilifunguliwa ili kubaini kifo chake.
Amebainisha kuwa baada ya kufunguliwa jalada hilo Ofisa Mpelelezi Mkuu wa Polisi wa makosa ya Jinai wa wilaya akiwa na timu ya askari wa upelelezi waliungana na maofisa wa usalama waliungana na Daktari wa wilaya ya Mkuranga Kibela kwenda kwenye eneo la tukio na kituo cha afya cha Kisiju kwa uchunguzi zaidi wa tukio hilo.
Aidha amesema kuwa daktari alichukua sampuli ya ngozi ambapo kwenye eneo la tukio ilikutwa suruali, majivu ya tisheti aliyokuwa amevaa, kandambili, kibiriti, chupa ya plastiki ya soda ambayo ilikuwa na mafuta ya petroli na katika eneo hilo hakukuwa na purukushani ya watu wengi ambapo mashahidi waliokwenda kumsaidia alipopiga kelele walimkuta marehemu akiwa anongea na kudai kuwa ameungua kwa moto bila ya kusema aliye muunguza.
Kaimu kamanda wa polisi huyo wa mkoa wa Pwani amesema baba mlezi wa marehemu Athuman Mahimbwa alipohojiwa alisema kuwa mwanae alikuwa akiugua ugonjwa wa Kifafa kwa miaka 17 na alimwambia kuwa anakufa kwa kuungua na moto na kutokana na uchunguzi uliofanywa na polisi pamoja na daktari umebainisha kuwa kifo chake kimesababishwa na moto na si kuchunwa ngozi.



No comments:

Post a Comment