Sunday, August 24, 2014

MWANARIADHA AOMBA WAFADHILI AENDE KAMBINI KENYA

Na John Gagarini, Kibaha
MWANARIADHA John Mwandu wa mkoani Pwani amewaomba wadau mbalimbali kujitokeza kumsaidia kwa hali na mali ili aweze kwenda kambini Eldoret nchini Kenya kwenye kambi aliyotokea mkimbiaji maarufu duniani David Rudisha wa nchi hiyo.
Rudisha ambaye ni bingwa wa dunia wa mbio za mita 800 amekuwa akiwandaa vijana wengi wa nchi ya Kenya kwa ajili ya kuinua vipaji vya vijana ambapo Mwandu ameomba kujiunga na kambi hiyo na tayari amekubaliwa kujiunga nayo kwa ajili ya mazoezi yam bio za mita 1,500.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha Mwandu alisema kuwa tayari ameruhusiwa kwenda kwenye kambi hiyo kwa mwaka mmoja lengo kubwa likiwa ni kujiandaa na mashindano ya Olimpiki ya mwaka 2016 yatakayofanyika Rio de Janeiro nchini Brazil.
 “Lengo langu la kwenda Kenya ni kujifunza mbinu wanazozitumia katika mchezo huo na kuwafanya kuwa mabingwa wa dunia wa riadha, kwani Mungu akipenda Olimpiki ijayo nitahakikisha naiwakilisha nchi yangu na kuiletea medali kwani inawezekana na diyo sababu ya kuanza maandalizi mapema,” alisema Mwandu.
Alisema anatarajia kwenda huko mwezi Desemba mwaka huu kwa ajili ya kambi hiyo ambayo ni nzuri na imetoa wakimbiaji wengi na ana uhakika akifanikiwa kwenda huko atarudi akiwa na mbinu nyingi za ukimbiaji ambazo anaamini zitamfanya aweze kufanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali.
“Changamoto kubwa niliyonayo ni ukosefu wa fedha za kuweza kunipeleka kwenye kambi hiyo lakini naamini Mungu ataniwezesha kuweza kufanikisha kwenda kwenye kambi hiyo ambapo tayari nimeshafanya mawasiliano na Rudisha na ameahidi kunisaidia,” alisema Mwandu.
Aidha alisema kuwa Tanzania inashindwa kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa kutokana na wachezaji wanaochaguliwa hawana uwezo na huchaguliwa kwa upendeleo na wale wenye uwezo kuachwa hali ianayosababisha kutofanya vizuri.
Alibainisha kuwa aliwahi kushinda kwenye mbio za Afrika Mashariki chini ya miaka 17 akiwa anasoma Tegeta High School alikuwa wa pili, Tabora Marathon kilomita 21, mashindano ya Voda Com kilomita tano ambapo alishika nafasi ya pili na Ruaha Marathon kilomita sita ambapo alishika nafasi ya tatu.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment