Wednesday, August 27, 2014

WALILIA FIDIA YA MASHAMBA YAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI nane wa kitongoji cha Benki kata ya Igunga wilaya ya Igunga mkoani Tabora wameiomba Halmashauri ya wilaya kuwalipa fidia ya mashamba yao ambayo yamechukuliwa na Halmashauri hiyo kwa ajili ya upanuzi wa hospitali ya wilaya.
Wakazi hao walitoa ombi hilo kufuatia Halmashauri hiyo kuwa kimya kwa muda mrefu baada ya mashamba yao kuchukuliwa tangu mwaka 2010 nakufanyiwa tathmini mwezi Februari mwaka huu lakini hadi sasa bado hawajalipwa fidia za maeneo yao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha mwenyekiti wa kamati ya waathirika hao  Daniel Shamalatu alisema kuwa mashamba yao yana ukubwa wa zaidi ya hekari 24 ambazo zilichukuliwa kwa ajili ya upanuzi huo wa hospitali ya wilaya.
Shamalatu alisema kuwa maeno yao yalichukuliwa bila ya wao kupewa taarifa ambapo mazao yao waliyokuwa wameyapanda yalifyekwa na ujenzi kuanza bila ya kupewa fidia.
“Tulipoona kimya tulikwenda mahakamani ili tuweze kulipwa fidia zetu lakini baraza la madiwani liliingilia kati na kututaka tuondoe kesi mahakamani ili tukubaliane nje ya mahakama, kweli tuliondoa kesi hiyo mahakamani lakini hakuna kinachoendelea ambapo sasa ni karibu mwaka umepita lakini tunaona kimya na tunapofuatilia halmashauri tunaambiwa suala letu linashughulikiwa,” alisema Shamalatu.
Alisema kuwa wao hawapingi ujenzi huo lakini wanachotaka ni kulipwa fidia kutokana na ukubwa wa mashamba yao na si kiwanja kimoja kila heka kama walivyotaka kufanya na pia wanataka kujua malipo yao yatafanyika lini.
 Akitolea ufafanuzi suala hilo kwa njia ya simu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Rustika Turuka alisema kuwa ni kweli mashamba yao yalichukuliwa kwa ajili ya upanuzi wa hospitali hivyo kutakiwa kupisha ujenzi huo kufanyika.
Turuka alisema kuwa kwa sasa maeneo hayo tayari yameshafanyiwa tathmini na taarifa ya uthamini imepelekwa wizarani kwa ajili ya kuandaliwa malipo baada ya kujua takwimu sahihi kutokana na maeneo hayo na kiasi ambacho watastahili kulipwa ili halmashauri itenge bajeti kwani maeneo mengine ambayo yalichukuliwa wamelipwa na wao watalipwa mara taratibu zitakapokamilika.
“Mthamini toka Tabora alishafika na kufanya kazi hiyo na kwa sasa tunachokisubiri ni taarifa toka wizarani baada ya kuipitia tathmini hiyo ili watu wanaodai fidia waweze kulipwa hivyo wanapaswa kuwa na subiri kwani mambo haya lazima yafuate taratibu na kila mtu atapewa haki zake pia eneo hilo  kwa sasa ni mji haipaswi kuwa na mashamba,” alisema Turuka
Aidha alisema wanasubiri taarifa hiyo ambayo itaonyesha ni kiasi gani wanastahili kulipwa na ndipo watatafuta fedha hizo kisha kuwalipa watu ambao wanadai ila wanataka walipwe haraka lakini serikali ina taratibu zake za kufanya malipo.
“Masuala ya malipo ya fidia za viwanja si suala la haraka linachukua muda mrefu hivyo lazima wawe na subiri wakati masuala yao yanashughulikiwa ambapo maeneo mengine tayari wameshalipwa hivyo na wao wanapaswa kuwa na subira na kila mtu atapata malipo yake,” alisema Turuka.
Mwisho.

     

No comments:

Post a Comment