Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABISHARA wa soko la Maili Moja
wilayani Kibaha wamesema kuwa endapo soko lao litahamishwa kutokana na kuwa
kwenye eneo la hifadhi ya barabara na kuhamishiwa eneo la Kitovu cha Mji endapo
halitajengwa jirani na stendi hawatakuwa tayari kwenda huko.
Waliyasema hayo wakati wa mkutano wao
na mkuu wa Wilaya ya Kibaha Asumter Mshama ambaye alikwenda sokoni hapo
kusikiliza changamoto zinazowakabiliwa wafanyabiashara hao ambao wanatakiwa
kuondoka kwenye eneo hilo ifikapo Septemba mwaka huu.
Aliyekuwa mwenyekiti wa soko hilo
Ally Gonzi alisema kuwa tayari wameshaambiwa waondoke hapo lakini wanashindwa
kuhama kutokana na Halmashauri kushindwa kujenga soko tangu mwaka 2013 ambapo
walidai kuonyeshwa hadi michoro.
“Sisi hatutakuwa tayari kuhamia huko
wanakotaka endapo hatawajenga soko letu jirani na stendi kwani vitu hivi
vinakwenda kwa pamoja awali ramani ilionyesha kuwa tungekuwa jirani na stendi
lakini baadaye tukasikia wanataka kutupeleka eneo la Mnarani maarufu kama Loliondo
au Sagulasagula huko stendi ikiwa kitovu cha Mji,” alisema Gonzi.
Alisema kuwa kuwatenganisha
kutawafanya wasipate wateja kwani wanunuzi wengi ni wale ambao wanasafiri
pamoja na wateja kupata urahisi wa usafiri mara wanaponunua bidhaa ambapo kwa
sasa soko lilipo ni jirani na stendi hivyo wanataka viende kwa pamoja.
“Awali Halmashauri walitushirikisha
vizuri lakini walipobadili jinsi tutakavyokaa huko hawakutushirikisha lakini
sisi tunasema tukitenganishwa hatutakuwa tayari kuhamia huko hivyo katika
mipango yao wahakikishe wanatuweka pamoja na stendi ili huduma ziwe bora na
sisi tupate wateja,” alisema Gonzi.
Akijibu suala hilo kaimu mkurugenzi
Lucy Kimoi alisema kuwa ujenzi wa soko la kisasa unatarajiwa kuanza katika
bajeti ya mwaka huu ya 2016-2017 na taratibu za ujenzi zitafuatwa ili wafanyabiashara
wawe kwenye mpangilio mzuri na wasiwe na wasiwasi.
Kimoi alisema kuwa waliomba mkopo
kutoka benki ya uwezeshaji ya TIB kwa ajili ujenzi wa soko na stendi ambapo kwa
sasa wanakamilisha kupata vibali toka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
(TAMISEMI) ili kupata fedha za kuanza ujenzi huo.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya
Asumter Mshama aliitaka Halmashauri kuhakikisha inafanya ujenzi huo kwa muda
uliopangwa na haitawahamisha wafanyabiashara hao hadi pale soko hilo
litakapokuwa limejengwa ili kuwaondolea usumbufu wafanyabiashara hao mara zoezi
la bomobomoa litakapofanyika.
Mshama alisema kuwa stendi na soko
vitakuwa pamoja hivyo wasiwe na wasiwasi kwani taratibu zote zitawekwa vizuri
ili waweze kufanya biashara vizuri na kwa utaratibu na wafanyabiashara wote
watapata nafasi kwenye soko jipya kwa kuzingatia aina ya biashara.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment