Tuesday, July 26, 2016

BAGAMOYO YAGUNDUA WTUMISHI HEWA ZAIDI 83 WAGUNDULIKA

 Na John Gagarini, Bagamoyo

WILAYA ya Bagamoyo mkoani Pwani imebaini uwepo wa watumishi hewa 83 na kuifanya wilaya hiyo kwa sasa kuwa na watumishi hewa 91 ambapo wakati zoezi hilo linaanza lilibaini watumishi hewa nane tu.

Akizungumza wakati wa zoezi la kuzindua madawati 300 yaliyotengenezwa na wadau mbalimbali na kuzinduliwa na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo, mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga alisema kuwa watumishi hao wamebainika baada ya kuundwa kikosi kazi kuchunguza watumishi hao.

Mwanga alisema kuwa awali baada ya agizo lililotolewa na Rais Dk John Magufuli kulibainika watumishi hewa nane lakini sasa idadi hiyo imeongezeka baada ya kufanywa kwa kina.

Alisema kuwa kikosi kazi kilichoundwa na watu sita wanaoundwa na kamati ya ulinzi na usalama na kugundua watumishi hewa wengi ni kutoka idara ya elimu hasa kwenye shule za msingi na sekondari.

“Watumishi wengi ni walimu ambao wengi wamekwenda masomoni bila ya kuaga na hawana ruhusa na baadhi walishaacha kazi lakini cha kushingaza mishahara yao ilikuwa inaingizwa kama kawaida jambo ambalo ni kinyume cha taratibu,” alisema Mwanga.

Aidha alisema kuwa tatizo kubwa linaonyesha ni idara ya elimu kushindwa kutoa maamuzi ya haraka mara walimu wanapoomba kwenda masomoni hivyo huamua kuondoka kienyeji.

“Watumishi wengine walibainika kuwa hawana vielelezo vyo vyote vya vya juu ya ajira zao na tunaomba hatua kali zichukuliwe kwa watumishi hao ambao ni hewa na wamekuwa wakilipwa mishahara huku hawafanyi kazi wanachukua mishahara ya bure,” alisema Mwanga.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kutokana na kubainika watumishi hao 83 hewa wilayani Bagamoyo kwa sasa mkoa wamefikia watumishi hewa 272.

Ndikilo alisema kuwa zoezi hilo bado linaendelea na kukipongeza kikosi kazi cha wilaya hiyo kuweza kuwabaini watumishi hao hewa na itaendelea kuchunguza hadi kuondoa kabisa suala hilo.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment