Na John Gagarini, Kibaha
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Angella Kairuki ameutaka
uongozi wa mkoa wa Pwani kuhakikisha unamaliza kushughulikia tatizo la
watumishi hewa haraka.
Mkoa huo una jumla ya watumishi hewa
272 ambao wamebainika na kuitia serikali hasara ya shilingi bilioni 1.4
kufuatia zoezi la uhakiki wa watumishi hewa kufanyika kutokana na agizo la Rais
Dk John Magufuli.
Kairuki aliyasema hayo juzi mjini
Kibaha wakati wa mkutano wake na uongozi wa mkoa huo, wakurugenzi wa
Halmashauri na Miji za mkoa huo pamoja na watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa
ili kujua changamoto zinazowakabili watumishi wa Umma.
Alisema kuwa kwa kuwa tayari agizo la
Rais lilishatoka tangu mwezi Machi mwaka huu kinachotakiwa ni kuwachukulia
hatua wahusika baada ya kuwabaini na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria
kujibu tuhuma zinazowakabili na si kuwaacha tu.
“Rais alitoa maagizo kubainisha
watumishi hewa na baada ya kubainika wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria
ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani kwani wamefanya makosa ya kuiibia
serikali hivyo hakuna sababu ya kutowachukulia hatua stahiki,” alisema Kairuki.
Aidha alisema kuwa hatua stahiki
zichukuliwe mapema ikiwa ni pamoja na kurekebisha taarifa za watumishi hao
ikiwa ni pamoja na kusitisha mishahara yao kabla ya malipo yamwezi Agosti ili
tatizo hilo lisije likaendelelea.
“Pia nataka kusiwe na data chafu
ambazo Halmashauri ziliweka kwa watumishi hao ambazo ni pamoja na kutopandishwa
madaraja, malipo kwa watu ambao wana umri zaidi ya miaka 60 na watumishi
kutokuwepo kwenye vituo vyao vya kazi huku wakiendelea kulipwa,” alisema
Kairuki.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani
Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa mkoa huo una watumishi 16,156 huku ukiwa
na upungufu wa watumishi 3,306 na watumishi hewa waliobainika ni 272 kwenye
Halmashauri saba za mkoa huo ambazo ni Kibaha Mjini, Kibaha, Mafia, Rufiji,
Mkuranga, Kisarawe na Bagamoyo.
Ndikilo alisema kuwa mkoa
unalishughulikia suala la watumishi hewa ambapo wanashirikiana na Jeshi la
Polisi pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa na kusema kuwa zoezi
hilo ni gumu hivyo inabidi walifanye kwa umakini ili lisije likaleta matatizo
na watalikamilisha mapema.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment