Na John
Gagarini, Bagamoyo
UONGOZI Chama
Cha Ushirika wa Wakulima wa Umwagiliaji Ruvu (CHAURU) wamewataka wafugaji
walioko kwenye shamba hilo kuhamisha mifugo yao ambayo imekuwa ikifanya
uharibifu wa mazao pamoja na miundombinu ya umwagiliaji.
Akizungumza
kwenye kikao cha wakulima na wafugaji waliopo kwenye shamba hilo ambalo liko
kwenye kitongoji cha Msigala Kijiji cha Visezi kata ya Ruvu wilayani Bagamoyo
mwenyekiti wa chama hicho Sadala Chacha amesema kuwa uharibifu uliofanywa ni
mkubwa sana.
Chacha
amesema kuwa kutokana na baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo kwenye shamba hilo
la umwagiliaji la mpunga kumewasababishia hasara kubwa wanachama wake na
uharibifu wa miundombinu.
Amesema kuwa
serikali ilishawatengea eneo lao liitwalo Mnyanama lakini hawataki kwenda
wakidai kuwa hakuna huduma za kijamii jambo ambalo limewafanya waendelee kukaa
hapo na huku mifugo hiyo hasa ngombe wakiendelea kufanya uharibu wa miundombinu
na kula mazao ya wakulima.
Aidha amesema
kuwa wamekuwa wakikaa vikao vya mara kwa mara ili kujaribu kuangalia utaratibu
wa namna ya kufuga na wao kulima lakini wao wamekuwa wakilishia mifugo kwenye
mashamba hayo ya wakulima na kusababisha ugomvi mara kwa mara.
Ameongeza
kuwa wamechoshwa na vitendo hivyo vya wafugaji vya kuingiza ngombe kwenye
shamba hilo huku sheria aikikataza mifugo kuingia kwenye eneo hilo lakini
utekelezaji wa suala hilo umekuwa mgumu kwani mifugo bado inaingizwa shambani
hapo.
Kwa upande
wake mmoja wa wafugaji Lupina Kirayo amesema kuwa tatizo kubwa linatokana na
baadhi ya wafugaji wanaoleta mifugo toka maeneo ya mbali kwa ajili ya kwenda
kuuza ngombe kwenye mnada wa Ruvu ndiyo wamekuwa wakiingiza mifugo kwenye shamba
hilo la ushirika wakitafuta maji.
Lupina
amesema kuwa wao kama wenyeji wa Kitongoji hicho wako makini na mifugo yao
ambapo wakati mwingine wachungaji wao wamekuwa wakishindwa kuwadhibiti ngombe
na kuingia kwenye shamba hilo ambapo wamekuwa wakiwafukuza wachungaji wazembe
ili kuondoa migongano na kuomba radhi na kutaka kuwe na maridhiano na kuangalia
njia nzuri ya kudhibiti mifugo isiingie kwenye shamba hilo lakini siyo
kuwaondoa hapo.
Naye
mwenyekiti wa Kitongoji hicho cha Msigala Otiniel Mbura amekiri kutokea
changamoto ya ngombe kuingizwa kwenye shamba hilo na kusema kuwa ili kuondoa
tatizo hilo ni wafugaji hao kuondoa mifugo hiyo na kuipeleka kule walikopangiwa.
Mbura amesema
kuwa wafugaji hao hawataki kwenda huko kwa madai kuwa hakuna huduma za kijamii
kama zahanati, shule na malambo ya maji kwa ajili ya mifugo yao hali ambayo
imefanya ugomvi kwenye shamba hilo kutokwisha kwa muda mrefu sasa.
Shamba hilo
la umwagiliaji mpunga lilianzishwa miaka ya 60 na lina wanachama wapatao 894 na
lina ukubwa wa hekta 3,209 huku za makazi zikiwa hekta 720 ambapo baada ya
mavuno ya mpunga wanachama hulima mazao mengine kama vile mahindi,ufuta na
mtama pamoja na kilimo cha mbogamboga.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment