Tuesday, July 26, 2016

RC AKATAA KUSIKIA HALMASHAURI IMEPATA HATI CHAFU

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo Ndikilo amesema kuwa kuanzia sasa hataki kusikia Halmashauri za Miji au wilaya za mkoa huo kuwa zimepata hati chafu.
Sambamba na hilo amezitaka Halmashauri hizo kuwatumia wakaguzi wa hesabu wa ndani ili kuweka mambo yao katika mpangilio mzuri ili kuondokana na hati chafu ambazo zimekuwa zikiziandama baadhi ya Halmashauri hizo.
Ndikilo aliyasema hayo wakati wa kikao na Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Miji za Mikoa hiyo ambao waliapishwa hivi karibuni baada ya kuteuliwa na Rais Dk John Magufuli.   
Alisema kuwa taarifa za hesabu za kila Halmashauri zinapaswa kupelekwa kwa wakati kulingana na utartibu uliowekwa na serikali pia hoja za mkaguzi mkuu wa serikali (CAG) zijibiwe mapema.
“Kuanzia sasa sitaki kusikia Halmashauri imepata hati chafu kutokana na uzembe kwani wakati mwingine inatokana na kushindwa kuonyesha risiti ambazo ni za manunuzi jambo ambalo liko ndani ya uwezo wenu hakuna sababu ya kuharibu sifa za utendaji kazi wenu kwa mambo madogomadogo,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa jambo jingine ambalo wakurugenzi wa halmashauri tisa za mkoa huo wanapaswa kulizingatia ni kutekeleza miradi kwa thamani halisi ya fedha na si kutekeleza miradi hiyo chini ya kiwango.
“Mnapaswa kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi kwa wakati na kama mnaona kuna mtendaji ambaye anafanya vibaya hakuna sababu ya kumuonea haya dawa ni kumwondoa,” alisema Ndikilo.
Mkuu huyo wa mkoa wa Pwani alisema kuwa wakurugenzi hao wanapaswa kukuisanya mapato kwa nguvu kwani makusanyo makubwa ndiyo yatakayoifanya Halmashauri kuweza kuendesha shughuli zake ikiwa ni pamoja na kuchangia uchumi wa wananchi na Taifa.
“Watu wanaohusika na vyanzo vya mapato wanapaswa kuwa wabunifu wa kuanzisha vyanzo vipya na siyo kuwa na vyanzo vilevile miaka yote pia wavifanyie uchambuzi ili kutokusanya mapato chini kutokana na taarifa za wazabuni ambao wamekuwa wakiidanganya Halmashauri juu ya mapato huku mengine yakiingia mifukoni mwao,” alisema Ndikilo.
Kwa upande wake mkurugenziwa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Jenifa Omolo alisema kuwa amejipanga vyema kutekeleza majukumu ya serikali kama walivyokula kiapo ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi pamoja na ukusanyaji wa mapato.
Naye Tatu Seleman mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha alisema kuwa atahakikisha anashirikiana na wananchi katika kutekeleza majukumu ya Halmashauri kwani ushirikishwaji utasaidia kupatikana kwa maendeleo hasa kupitia kwenye huduma za kiajamii.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment