Tuesday, July 26, 2016

MAKUSANYO YA STENDI YAMSIKITISHA MKUU WA WILAYA


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Asumter Mshama amesikitishwa na mapato yanayokusanywa kama ushuru ya shilingi milioni 1.5 kwa mwezi kwenye soko kuu la Maili Moja kuwa ni madogo sana ikilinganishwa na idadi ya wafanyabiashara sokoni hapo.
Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki mjini Kibaha wakati alipofanya mkutano na wafanyabiashara wa soko hilo kujua changamoto zinazowakabili na kusema kuwa mapato hayo ni madogo sana na Halmashauri hiyo inapaswa kuangalia namna ya ukusanyaji mapato hayo ili yaendanena na hali halisi.
Mshama alisema kuwa soko hilo ni chanzo kikuu cha mapato ya Halmashauri lakini ukusanyaji huo unakatisha tamaa kwani inaonekana kuna fedha hazifiki hivyo kuna haja ya suala hilo kufanyiwa kazi ili mapato halali yaweze kuonekana.
“Kiasi kilichotajwa cha shilingi milioni 1.5 kwa mwezi hakikubaliki vinginevyo tutafanya uhakiki wa wafanyabiashara wote kwa kupitia kibanda kwa kibanda ili tuweze kujiridhisha juu ya usahihi wa mapato sokoni hapo ambapo ushuru ni shilingi 300 kwa siku kwa kila mfanyabiashara ambapo kuna wafanyabiashara zaidi ya 500,” alisema Mshama.
Alisema kuwa kama ni mgodi soko hilo ndiyo mgodi wa kuchimbwa hivyo lazima makusanyo yake yafanywe kwa usahihi ili kutopoteza fedha kwenda kwenye mifuko ya watu binafsi.
“Makusanyo kama haya haiwezekani kwa soko hili hapa kuna tatizo lazima tupate ukweli kwani hili halikubaliki au mmeshindwa kukusanya kama tunakuja hapa kudaili milioni moja nadhani hata hichi kikao hakina maana ni bora tuondoke tukaendelee na shughuli nyingine,” alisema Mshama.
Akizungumzia juu ya Halmashauri kujitoa kuweka ulinzi alisema kuwa hilo ni kosa lazima ulinzi uwe chini ya Halmashauri na si kuwatwika mzigo wafanyabiashara mzigo huo kwani huduma hiyo ni faida kwa Halamshauri hivyo hakuna sababu ya wao kulinda wenyewe.
“Inashangaza kuona kuwa eti sehemu inayotuingizia mapato hatuiwekei ulinzi mbona pale ofisini mmeweka walinzi tena wa kampuni na hapa lazima mlinde hamna hoja katika hili ninachotaka jukumu hili mlichukue kama mlivyokuwa mkifanya zamani kama hamna fedha chukueni hizo mnazokusanya hapo za ushuru mlipe walinzi hili halina mjadala,” alisema Mshama.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi Lucy Kimoi alisema kuwa juu ya ulinzi ni utaratibu uliowekwa na Halmashauri kuwaondoa vibarua wote hali iliyosababisha na walinzi ambao walikuwa vibarua kuondolewa hivyo kukodisha kampuni ya ulinzi kulinda ofisi ya Halmashauri na sokoni jukumu hilo likaudi kwa wafanyabiashara.
Kimoi alisema kuwa hiyo ni sheria ya kuwaondoa vibarua ikiwa ni utaratibu wa serikali ndiyo sababu ya kulirudisha suala hilo kwa wafanyabiashara wa soko hilo ambao walikuwa wakichanga fedha kwa ajili ya ulinzi.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment