Tuesday, July 26, 2016

VIONGOZI WAKATAA KUKABIDHI OFISI ZA SOKO


Na John Gagarini, Kibaha
UONGOZI wa zamani wa soko la mkoa la Maili Moja wamegoma kuwakabidhi ofisi uongozi mpya uliochaguliwa mbele ya mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama wakidai kuwa taratibu za uchaguzi huo zilikiukwa.
Makabidhiano ya ofisi ambayo yalikuwa yakisimamiwa na diwani wa kata ya Maili Moja Theodory Joseph, ofisa mtendaji wa mtaa wa Maili Moja John Dotto, mwenyekiti mpya wa soko Ramadhan Maulid na katibu Elias Kisandu yalishindikana kutokana na uongozi wa zamani kutoridhia jinsi walivyoondolewa madarakani
Akizungumza baada ya makabidhiano ya soko hilo kushindikana katibu wa zamani wa soko hilo Muhsin Yusuph alisema kuwa hawawezi kukabidhi mali za soko hilo bila ya taratibu kwani soko hilo lilikuwa liko kwenye mfumo wa ushirika.
Yusuph alisema kuwa taratibu za ushirika zinafahamika hivyo sisi hatuwezi kuwakabidhi uongozi mpya bila ya taratibu ikiwa ni pamoja na kufanya uchaguzi chini ya mrajisi wa vyama vya ushirika.
“Huu ni ushirika na ushirika una taratibu zake sasa sisi hatuwezi kuukabidhi uongozi mpya bila ya kufuata utaratibu kwani uchaguzi haukufanyika kwa kufuata katiba ya ushirika ambapo mrajisi ndiye aliyetakiwa kuwa msimamizi,” alisema Yusuph.
Alisema kuwa siku walipochaguliwa viongozi wapya ilikuwa ni mkutano na mkuu wa wilaya kujua changamoto zinazotukabili lakini haukuwa mkutano wa uchaguzi ambao unakuwa ni maalumu na unasimamiwa na mrajisi wa vyama vya ushirika.
Mwenyekiti wa kamati ya makabidhiano diwani Theodory Joseph alisema kuwa wao walikuwa wakikamilisha taratibu kwani uchaguzi ulifanyika na uongozi huo wa zamani kushindwa na kutakiwa kuwakabidhi ofisi viongozi wapya.
Joseph alisema kwa kuwa wamekataa watawasiliana na ngazi zinazohusiaka kwa taratibu zaidi lakini wao hawana la zaidi kwani kila kitu kilikuwa kinajulikana hivyo watasubiri taratibu zingine.
Kwa upande wake mwenyekiti mpya Ramadhan Maulid alisema kuwa kwa kuwa uongozi uliopita umegoma kukabidhi ofisi watawasiliana na mkuu wa wilaya ili kujua nini cha kufanya juu ya hatua hiyo.
Soko hilo lilikuwa likiendeshwa kwa taratibu za ushirika ambapo kuna zaidi ya wafanyabiashara zaidi ya 500 ambapo baadhi ni wanachama wa ushirika na wengine si wanachama wa ushirika ambapo mkuu wa wilaya alishauri ni vema uongozi ukawa tofauti kati ya ule wa ushirika na soko ili kuondoa muingiliano wa majukumu.

Mwisho.  

No comments:

Post a Comment