Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist
Ndikilo amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuanzisha daftari maalumu la wakuu
wa Idara kwenda kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi Vijijini kila
mwezi.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa
kikao baina yake na wakurugenzi walioteuliwa hivi karibuni na Rais Dk John
Magufuli juu ya utekelezaji wa majukumu yao ya kikazi.
Ndikilo alisema kuwa umefika wakati
sasa wa watendaji kwenda kuwatumikia wananchi na si kukaa ofisini wakati
wananchi wakiwa na matatizo mengi huku wao wakiwa wamekaa ofisini tu.
“Nataka nione wakurugenzi mkiwa
mmetengeneza dafatari hilo ambalo litamwonyesha mkuu wa idara kazi aliyoifanya
kwa ajili ya kutatua kero na kule wanako kwenda lazima kuwe na sahihi zao kuwa
walifika kwenye vijiji husika ili iwe ushahidi wa utendaji kazi wao na si kukaa
tu ofisini,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa sambamba na hilo
wakurugenzi lazima watenge siku maalumu ya kusikiliza kero za wananchi na mfumo
wa kupata taarifa za matatizo kwa kila kata ili iwe rahisi kufuatilia ikiwa ni
pamoja na kuweka sanduku la kero za wananchi ili zishughulikiwe mapema.
“Mnapaswa kushughulikia kero za
wananchi kwa wakati kwani ucheleweshaji wa kutatua kero kwa muda muafaka
husababisha matatizo kuongezeka na kufanya malalamiko kutoisha ambapo wananchi
wamekuwa wakikimbilia kwa wakuu wa wilaya na mkoa huku kukiwa hakuna utatuzi
ngazi ya Halmashauri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa wakurugenzi
wanapaswa kusimamia suala la ulinzi na usalama na wasiliache kwa serikali kuu
ili wananchi waweze kufanya shughuli zao wakiwa na amani kwani kukiwa na
uvunjifu wa amani itakuwa ni vigumu watu kufanya shughuli za maendeleo.
“Changamoto ni nyingi ikiwa ni pamoja
na migogoro ya ardhi, wakulima na wafugaji, migogoro kutoshughulikiwa kwa
wakati na mipaka pamoja na changamoto nyingine nyingi ambapo wajibu wa
wakurugenzi ni kuwasimamia watendaji mbalimbali na hawapaswi kuwa na urafiki
usiokuwa wa maendeleo kwa watendaji,” alisema Ndikilo.
Aliwataka wakurugenzi hao kuwasimamia
watendaji wao ili wasikae ofisini kusubiri maelekezo toka ngazi za juu bali
waende kwa wananchi kwani muda huu si wa kukaa bali wanapaswa kuwa wabunifu na
si kukaa tu kwani lazima wawe wawajibikaji.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment