Tuesday, July 26, 2016

OFISI YA MKUU WA MKOA INAKABILIWA NA UHABA WA MAGARI


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amesema kuwa mkoa wake unakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa magari hali ambayo inawafanya kuazima magari kwenye wilaya katika shughuli za kikazi katika mkoa huo.    
Aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa mkutano wake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Angella Kairuki alipokuwa akizungumza na watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa na wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Miji za mkoa huo.
Ndikilo alisema kuwa changamoto hiyo kwa wataalamu wa mkoa ni kubwa hali ambayo inawafanya wafanye kazi kwenye mazingira magumu hasa kwenye maeneo ya mbali ikiwa ni pamoja na kwenye Halmashauri za mkoa huo.
“Waziri mkoa una changamoto kubwa ya ukosefu wa magari ikiwemo ofisi yangu na wataalamu wangu inapofika hatua ya kwenda kwenye maeneo ya mbali inakuwa mtihani mkubwa kwani inatubidi tuazime magari ya kwenye wilaya kwa ajili ya kufika baadhi ya maeneo,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa hata mkuu wa wilaya ya Kibaha gari alilonalo ni bovu ambapo hivi karibuni alipata ajali ya kuligonga gari jingine kutokana na breki kugoma naye mkuu wa wilaya ya Mkuranga naye gari lake siyo zuri sana, wilaya Mpya ya Kibiti yenyewe haina gari kabisa.
“Usafiri kwa mkoa wetu ni changamoto kubwa hivyo tunaomba mtusaidie ili katika bajeti ijayo mtufikirie kwa kutupatia usafiri ili tuweze kutekeleza majukumu yetu vizuri ili kukabiliana na changamoto hii ambayo inatupa wakati mgumu inapofikia suala la usafiri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ni ukomo wa bajeti ambayo kwa mwaka 2014-2015 ulishuka kwa asilimia 40 ikilinganishwa na bajeti iliyopita, fedha za maendeleo kuchelewa, madeni ambayo yamefikia milioni 152, watumishi kuhama kutafuta maslahi mazuri, vitendea kazi na upandishwaji wa madaraja.
Akijibu baadhi ya hoja Waziri Kairuki alisema kuwa Wizara inazifanyia kazi changamoto hizo na pale fedha zitakapopatikana itaboresha mazingira ya watumishi ili wafanye kazi vizuri kwani serikali inawathamini wafanyakazi na haitaki wafanye kazi katika mazingira magumu.
Kairuki alisema kuwa juu ya maofisa utumishi waliokuwa wakilipa mshahara watumishi hewa itabidi wawajibike ambapo kwa sasa inawsafuatilia kwani inaonekana nao walichangia kulipa mishahara kwa watumishi ambao hawakustahili.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment