Tuesday, July 5, 2016

WAFUGAJI WATAKA WASIONDOLEWE CHAURU

Na John Gagarini,Bagamoyo

WAFUGAJI wanaoishi kwenye Kitongoji cha Msigala Kijiji cha Visezi kata ya Ruvu wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wamepinga kupelekwa Kitongoji cha Mnanyama kutokana na kutokuwa na huduma za kijamii.

Wakizungumza na waandishi wa habari Kijijini hapo wamesema kuwa eneo walilopangiwa halina huduma hizo ndiyo sababu ya wao kuendelea kukaa hapo walipo sasa.

Akizungumzia juu ya hali hiyo Lupina Kirayo alisema kuwa chanzo cha wao kutakiwa kuondoka ni kutokana na madai ya wakulima wa shamba la Chama Cha Ushirika wa Umwagiliaji Ruvu (CHAURU) kuwa ngombe wao wamekuwa wakiingia kwenye mashamba na kuharibu mazao.

Kirayo alisema kuwa wao wako hapo kwa muda mrefu lakini wanashangaa kutakiwa kuondoka na kwenda Mnanyama ambako hakuna huduma hyoyote ya Kijamii.

“Zamani kijiji hicho kiliweka njia kwa ajili ya ngombe kupita kwenda kunywa maji mtoni lakini wakulima walifunga njia ya kupita ngombe na ndiyo chanzo cha migogoro ya wakulima na wafugaji ilipoanza,” alisema Kirayo.

Alisema kuwa tatizo kubwa linatokana na baadhi ya wafugaji wanaoleta mifugo toka maeneo ya mbali kwa ajili ya kwenda kuuza ngombe kwenye mnada wa Ruvu ndiyo wamekuwa wakiingiza mifugo kwenye shamba hilo la ushirika wakitafuta maji.

Aidha alisema kuwa wao kama wenyeji wa Kitongoji hicho wako makini na mifugo yao ambapo wakati mwingine wachungaji wao wamekuwa wakishindwa kuwadhibiti ngombe na kuingia kwenye shamba hilo ambapo wamekuwa wakiwafukuza wachungaji wazembe ili kuondoa migongano na kuomba radhi na kutaka kuwe na maridhiano na kuangalia njia nzuri ya kudhibiti mifugo isiingie kwenye shamba hilo lakini siyo kuwaondoa hapo.

Naye Elizabeth Meja amesema kuwa yeye alizaliwa hapo na kipindi cha nyuma wamekuwa wakiishi vizuri lakini kwa sasa wanaambiwa waondoke ambako kule huduma ya afya hakuna ambapo kwa akinamama hasa pale wanapokuwa wajawazito huhitaji kupata huduma za mara kwa mara.

Meja alisema kuwa sehemu wanayotaka kuhamishiwa kuna umbali wa km 20 hadi kufika kwenye huduma za afya na hata watoto wanapozaliwa hupaswa kupelekwa kliniki lakini kutokana na umbali huo itakuwa ni matatizo pia watoto wao kwa sasa licha ya kutumia masaa zaidi ya mawili kwenda shule ni karibu tofauti na wakienda kule hatapata fursa ya kusoma kutokana na umbali huo.

“Hata suala la maji ni tatizo kwani hapa tunatumia maji ya shilingi 20,000 kwa siku lakini kule tunakotakiwa twende maji hakuna kabisa hivyo ni vema wakaweka miundombinu kwanza ili huduma kama hizo zipatikane,” alisema Meja.

Naye mwenyekiti wa kitongoji hicho cha Msigala Otiniel Mbura alisema kuwa tayari serikali iliamua wafugaji hao kwenda huko ili kuondoa migogoro inayojitokeza kila wakati.

Mbura alisema kuwa ni vema wafugaji hao wakenda kwanza na serikali itawapelekea huduma kuliko hivi sasa wanavyokataa kwenda huko walikopangiwa.


No comments:

Post a Comment