Tuesday, July 26, 2016

JAKAYA AKARIBISHWA KISHUJAA BAGAMOYO

Na John Gagarini, Bagamoyo

RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne Dk Jakaya Kikwete amesema kuwa hakuna kitu kilichokuwa kikimpa wakati mgumu kama kushindwa katika uongozi wake wa miaka 10 iliyopita.

Aliyasema hayo juzi mjini Bagamoyo wakati wa sherehe iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Sanaa Bagamoyo (TASUBA) ya kumkaribisha nyumbani baada ya kukabidhi uongozi kwa mwenyekiti mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk John Magufuli mjini Dodoma hivi karibuni.

Dk Kikwete alisema kuwa hali ya kushindwa ilikuwa ikimpa wakati mgumu na kujiona kuwa kama endapo angeshindwa basi ange waangusha Wanabagamoyo na Pwani nzima.

“Kila nilipokuwa nikifikiria kushindwa kwenye jambo lolote la uongozi wangu kwa nchi au kwenye Chama lakini namshukuru Mungu kwani tulifanikiwa sana katika suala la maendeleo kwa nchi nzima kwani huwezi ukapendelea sehemu uliyotoka au ukawanyima maendeleo ni kitu ambacho hakiwezekani,” alisema Dk Kikwete.

Alisema kuwa wakati fulani alikuwa akilalamikiwa na baadhi ya wabunge kuwa anapendelea Bagamoyo jambo ambalo si la kweli ambapo walidai kuwa amehamisha fedha za ujenzi wa barabara na kuzihamishia kwenye ujenzi wa barabara ya Msata Bagamoyo.

“Hali kama hiyo Ilikuwa inanipa wakati mgumu kwnai kila sehemu inataka maendeleo na nisingeweza kutofanya maendeleo kwa watu wa Bagamoyo kwani hata wao wanahitaji maendeleo kama sehemu nyingine,” alisema Dk Kikwete.

Aidha alisema kuna wakati ilibidi ahamishe fedha kutoka Bagamoyo na kufanya ujenzi kwenye maeneo ya Geita-Sengerema hadi Usagara wakati huo waziri wa Ujenzi alikuwa Basil Mramba lakini hawakuliona lakini anasema alishukuru Mungu kwani ujenzi kwenye barabara hizo ulifanyika vizuri.

“Namshukuru Mungu katika uongozi wangu tulifanya kazi na kuleta maendeleo makubwa na tumeiacha nchi mahali pazuri na salama kwnai imetulia licha ya mwaka 2015 wakati wa uchaguzi ambapo baadhi ya watu walisema kuwa Rais gani hata hafanyi mpango wa kubadilisha katiba ili aendelee kukaa madarakani kwani watu walishindana lakini hawakupigana wala kumwaga damu na uchaguzi ulipokwisha maisha yaliendelea salama kabisa,” alisema Dk Kikwete.

Alibainisha kuwa Watanzania wanapaswa kumuombea Rais Dk John Magufuli ili aweze kuleta maendeleo kwani ni mpenda maendeleo hivyo lazima asaidiwe aweze kuleta maendeleo ya watu.

Akizungumzia kuhusu Chama alisema kuwa kiko vizuri na hakuna kinachoiweza CCM kwani anajua hakuna chama cha kuweza kukishinda kwani havina uwezo ikizingatiwa ni chama kikubwa na viongozi wake ni imara.

Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo Maskuzi alisema kuwa katika uongozi wake alifanikiwa kuleta maendeleo makubwa kuanzia kwenye elimu na mpango wa shule za kata sasa umeonyesha mafanikio ambapo shule hizo kwa mwaka huu zimeongoza kwenye matokeo.

Maskuzi alisema kuwa umeme ni moja ya mafanikio ambapo kwa sasa umefika hadi vijijini kupitia mpango wa Umeme Vijijini REA, ujenzi wa barabara na masuala mengine ya kimaendeleo kwenye nchi ambayo ni ya kujivunia.

Katika sherehe hiyo ambayo ilihudhuriwa na familia ya Dk Kikwete alipewa zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na mifugo kama vile ngombe, mbuzi, kuku, bata, mavazi ya jadi na vitu mbalimbali ambavyo vilitolewa na wananchi wa mkoa wa Pwani.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment