Tuesday, July 26, 2016

WADAU WACHANGIA BWENI LA SEKONDARI YA CHALINZE ILIYOUNGUA

Na John Gagarini, Kibaha
KUFUATIA kuungua bweni la shule ya sekondari ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kuungua kwa moto baadhi ya wadau wameanza kuichangia shule hiyo ili kusaidia wanafunzi ambao vifaa vyao vyote viliungua.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi diwani wa kata ya Bwiringu Lucas Lufunga alisema kuwa kutokana na tukio hilo waliitisha kikao cha kata kwa ajili ya kuangalia namna ya kuisaidia shule hiyo.
Lufunga alisema kuwa katika kikao hicho walifanikiwa kupata kiasi cha shilingi 449,000 na kunua vyakula kwa ajili ya kusaidia kwani vyakula viliungua na moto huo ambao ulitokea usiku wakati wanafunzi wakiwa wanjisomea masomo ya usiku.
“Tunaomba watu mbalimbali wajitokeze kuwasaidia wanafunzi walikuwa wakiishi kwenye bweni hilo kwani kufuatia moto huo hakuna kilichotoka kwani vyote viliteketea kabisa hivyo kuna haja ya kulichukulia kwa uzito wake tatizo hilo,” alisema Lufunga.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwalimu mkuu wa Shule hiyo Emanuel Kahabi alisema kuwa moto huo ulitokea wakati wanafunzi hao wakiwa wanajisomea madarasani usiku.
Kahabi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Julai 12 majira ya saa 2:50 usiku ambapo moto huo haukuweza kufahamika ulitokea wapi na kusababisha hasara kubwa ya bweni hilo na vifaa mbalimbali vikiwemo vya wanafunzi.
“Bweni hilo ambalo lilikuwa bwalo la chakula baada ya wanafunzi hao zaidi ya 100 kuhamishiwa humo kutokana na bweni lao kuungua kwa moto miezi michache iliyopita,” alisema Kahabi.
Alisema kuwa anawashukuru wadau ambao wameanza kuisaidi shule yake kutokana na moto huo ambao hadi sasa haijafahamika chanzo chake ni nini na kuwataka watu wakiwemo wakazi wa Chalinze, wilaya na mkoa amzima kuwasaidia wanafunzi hao.
Mwisho. 

ZOEZI LA UBOMOAJI LAZUA TAFRANI

     
Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la ubomoaji kwa amri ya Mahakama vibanda vya biashara vilivyopo eneo la mtaa wa Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani umeingia kwenye mgogoro baada ya familia ya iliyodaiwa kujenga kwenye eneo ambalo si lao wamedai vimebomolewa kimakosa.
Ubomoaji huoa ambao ulifanywa Julai 15 na kampuni ya udalali ya Coast Auction Mart baada ya kesi hiyo ambayo imedumu kwa kipindi cha miaka 35 familia hiyo ya iliyoongozwa na Eva Pwele ambaye alikuwa mlalamikaji bada ya baba yake mzazi Pwele Showe ailiyefungua kesi hiyo kufariki dunia kumlalamikia Tonga Fueta kudai eneo hilo ni mali yake ambapo mahakama ilimpa ushindi.
Akizungumza na mwandishi wa habari mdai Eva Pwele alisema kuwa maamuzi ya mahakama yalikuwa ni  mlalamikiwa kupewa eneo lenye ukubwa wa mita 3 na nchi 7 kwa mita 3 na nchi 5 na si mita 352.92 ikiwa ni maamuzi yaliyotolewa na mahakama ya Mwanzo Kibaha mwaka 1980.
Pwele alisema kuwa baada ya maamuzi ya mahakama hayo miezi mitatu iliyopita alifuatwa na dalali na kutakiwa avunje mwenyewe lakini yeye hakufanya hivyo na kusema kuwa yeye anachojua ni kumkabidhi eneo lenye ukubwa wa mita 3 na nchi 7 tu na si hadi kwenye eneo walilojenga mabanda hayo ya biashara.
“Cha kushangaza siku ya tukio nililiona watu wakija wakiwa Dalali na kuanza kubomoa mabanda yetu ambayo yalijengwa hivi karibuni baada ya kutokuwa na wasiwasi juu ya eneo hilo kwani mapitio ya hukumu yalisema kuwa katika maamuzi ya mwanzo hayakuonyesha ukubwa wa eneo lakini mapitio hayo ya mwaka 2005 ndiyo yaliyosema kuwa mlalamikiwa alipaswa kurudishiwa sehemu iliyotajwa hapo juu,” alisema Pwele.
Alisema kuwa mbali ya maamuzi kukiukwa pia alishangaa wahusika wa bomoa hiyo kutokuwa na barua yoyote ambayo inawaruhusu kufanya ubomoaji huo ambao umewatia hasara kubwa kutokana na mabanda hayo kuvunjwa kwa madai ya kujengwa kwenye eneo la mlalamikiwa.
Kwa upande wake Tonga Fueta alisema kuwa kwanza anamshukuru Mungu kwani baada ya kuhangaika kwa miaka 35 hatimaye haki yake imepatikana kwani tangu mwanzo wa kesi hiyo ilipofunguliwa na mlalamikaji alikuwa akishinda kuanzia mahakama ya mwanzo hadi mahakama kuu kabla ya kukatiwa rufaa na mlalamikaji baada ya hukumu ya kwanza iliyotolewa na hakimu Chungulu mwaka 1981.
Fueta alisema kuwa alinunua eneo hilo mwaka 1969 kwa kiasi cha shilingi 400 toka kwa mtu aliyetajwa kwa jina la Ramadhan na mwaka huo huo alimpa sehemu ya eneo hilo Pwele Showe ambaye kwa sasa ni marehemu lakini aliongeza na eneo lake.
“Mwaka 1971 nyumba zetu na mdai wangu zilivunjwa kupisha ujenzi wa barabara ya Morogoro ndipo naye akamfuata Ramadhan ili amuuzie eneo na kumuuzia kwa shilingi 500 na ndipo aliponimbia nivunje banda langu kwakuwa yeye ameshanunua ndipo tatizo hilo lilipoanzia,” alisema Fueta.
Kufuatia bomoabomoa hiyo familia ya Pwele imesema kuwa itatafuta haki yao kwenye vyombo vya kisheria kwani ubomoaji huo umekiuka amri ya mahakama kwa kuvunja sehemu ambayo haihusiki kwani wao walikuwa wakijiandaa kumkabidhi eneo kama ilivyoagizwa na mahakama.

Mwisho.

MAKUSANYO YA STENDI YAMSIKITISHA MKUU WA WILAYA


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Asumter Mshama amesikitishwa na mapato yanayokusanywa kama ushuru ya shilingi milioni 1.5 kwa mwezi kwenye soko kuu la Maili Moja kuwa ni madogo sana ikilinganishwa na idadi ya wafanyabiashara sokoni hapo.
Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki mjini Kibaha wakati alipofanya mkutano na wafanyabiashara wa soko hilo kujua changamoto zinazowakabili na kusema kuwa mapato hayo ni madogo sana na Halmashauri hiyo inapaswa kuangalia namna ya ukusanyaji mapato hayo ili yaendanena na hali halisi.
Mshama alisema kuwa soko hilo ni chanzo kikuu cha mapato ya Halmashauri lakini ukusanyaji huo unakatisha tamaa kwani inaonekana kuna fedha hazifiki hivyo kuna haja ya suala hilo kufanyiwa kazi ili mapato halali yaweze kuonekana.
“Kiasi kilichotajwa cha shilingi milioni 1.5 kwa mwezi hakikubaliki vinginevyo tutafanya uhakiki wa wafanyabiashara wote kwa kupitia kibanda kwa kibanda ili tuweze kujiridhisha juu ya usahihi wa mapato sokoni hapo ambapo ushuru ni shilingi 300 kwa siku kwa kila mfanyabiashara ambapo kuna wafanyabiashara zaidi ya 500,” alisema Mshama.
Alisema kuwa kama ni mgodi soko hilo ndiyo mgodi wa kuchimbwa hivyo lazima makusanyo yake yafanywe kwa usahihi ili kutopoteza fedha kwenda kwenye mifuko ya watu binafsi.
“Makusanyo kama haya haiwezekani kwa soko hili hapa kuna tatizo lazima tupate ukweli kwani hili halikubaliki au mmeshindwa kukusanya kama tunakuja hapa kudaili milioni moja nadhani hata hichi kikao hakina maana ni bora tuondoke tukaendelee na shughuli nyingine,” alisema Mshama.
Akizungumzia juu ya Halmashauri kujitoa kuweka ulinzi alisema kuwa hilo ni kosa lazima ulinzi uwe chini ya Halmashauri na si kuwatwika mzigo wafanyabiashara mzigo huo kwani huduma hiyo ni faida kwa Halamshauri hivyo hakuna sababu ya wao kulinda wenyewe.
“Inashangaza kuona kuwa eti sehemu inayotuingizia mapato hatuiwekei ulinzi mbona pale ofisini mmeweka walinzi tena wa kampuni na hapa lazima mlinde hamna hoja katika hili ninachotaka jukumu hili mlichukue kama mlivyokuwa mkifanya zamani kama hamna fedha chukueni hizo mnazokusanya hapo za ushuru mlipe walinzi hili halina mjadala,” alisema Mshama.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi Lucy Kimoi alisema kuwa juu ya ulinzi ni utaratibu uliowekwa na Halmashauri kuwaondoa vibarua wote hali iliyosababisha na walinzi ambao walikuwa vibarua kuondolewa hivyo kukodisha kampuni ya ulinzi kulinda ofisi ya Halmashauri na sokoni jukumu hilo likaudi kwa wafanyabiashara.
Kimoi alisema kuwa hiyo ni sheria ya kuwaondoa vibarua ikiwa ni utaratibu wa serikali ndiyo sababu ya kulirudisha suala hilo kwa wafanyabiashara wa soko hilo ambao walikuwa wakichanga fedha kwa ajili ya ulinzi.

Mwisho.

WATAKA SOKO LIJENGWE JIRANI NA STENDI

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABISHARA wa soko la Maili Moja wilayani Kibaha wamesema kuwa endapo soko lao litahamishwa kutokana na kuwa kwenye eneo la hifadhi ya barabara na kuhamishiwa eneo la Kitovu cha Mji endapo halitajengwa jirani na stendi hawatakuwa tayari kwenda huko.
Waliyasema hayo wakati wa mkutano wao na mkuu wa Wilaya ya Kibaha Asumter Mshama ambaye alikwenda sokoni hapo kusikiliza changamoto zinazowakabiliwa wafanyabiashara hao ambao wanatakiwa kuondoka kwenye eneo hilo ifikapo Septemba mwaka huu.
Aliyekuwa mwenyekiti wa soko hilo Ally Gonzi alisema kuwa tayari wameshaambiwa waondoke hapo lakini wanashindwa kuhama kutokana na Halmashauri kushindwa kujenga soko tangu mwaka 2013 ambapo walidai kuonyeshwa hadi michoro.
“Sisi hatutakuwa tayari kuhamia huko wanakotaka endapo hatawajenga soko letu jirani na stendi kwani vitu hivi vinakwenda kwa pamoja awali ramani ilionyesha kuwa tungekuwa jirani na stendi lakini baadaye tukasikia wanataka kutupeleka eneo la Mnarani maarufu kama Loliondo au Sagulasagula huko stendi ikiwa kitovu cha Mji,” alisema Gonzi.
Alisema kuwa kuwatenganisha kutawafanya wasipate wateja kwani wanunuzi wengi ni wale ambao wanasafiri pamoja na wateja kupata urahisi wa usafiri mara wanaponunua bidhaa ambapo kwa sasa soko lilipo ni jirani na stendi hivyo wanataka viende kwa pamoja.
“Awali Halmashauri walitushirikisha vizuri lakini walipobadili jinsi tutakavyokaa huko hawakutushirikisha lakini sisi tunasema tukitenganishwa hatutakuwa tayari kuhamia huko hivyo katika mipango yao wahakikishe wanatuweka pamoja na stendi ili huduma ziwe bora na sisi tupate wateja,” alisema Gonzi.
Akijibu suala hilo kaimu mkurugenzi Lucy Kimoi alisema kuwa ujenzi wa soko la kisasa unatarajiwa kuanza katika bajeti ya mwaka huu ya 2016-2017 na taratibu za ujenzi zitafuatwa ili wafanyabiashara wawe kwenye mpangilio mzuri na wasiwe na wasiwasi.
Kimoi alisema kuwa waliomba mkopo kutoka benki ya uwezeshaji ya TIB kwa ajili ujenzi wa soko na stendi ambapo kwa sasa wanakamilisha kupata vibali toka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ili kupata fedha za kuanza ujenzi huo.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya Asumter Mshama aliitaka Halmashauri kuhakikisha inafanya ujenzi huo kwa muda uliopangwa na haitawahamisha wafanyabiashara hao hadi pale soko hilo litakapokuwa limejengwa ili kuwaondolea usumbufu wafanyabiashara hao mara zoezi la bomobomoa litakapofanyika.
Mshama alisema kuwa stendi na soko vitakuwa pamoja hivyo wasiwe na wasiwasi kwani taratibu zote zitawekwa vizuri ili waweze kufanya biashara vizuri na kwa utaratibu na wafanyabiashara wote watapata nafasi kwenye soko jipya kwa kuzingatia aina ya biashara.

Mwisho.

TFS KANDA YA MASHARIKI YAKUSANYA MABILIONI

Na John Gagarini, Kibaha
WAKALA wa Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki imefanikiwa kukusanya mapato yenye tahamani ya shilingi bilioni 13 kwa mwaka jana kutokana na tozo mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha meneja wa TFS Kanda ya Mashariki Dk Abel Masota alisema kuwa tozo hizo ni pamoja na faini zinazotokana na ukiukwaji wa taratibu za matumizi ya rasilimali za misitu ya hifadhi.
Dk Abel alisema kuwa mapato hayo ni pamoja na ukataji wa vibali kwa ajili ya wafanyabiashara wa mazao ya misitu 17 kwenye misitu iliyo chini ya wakala hiyo kwenye kanda yake.
“Mapato hayo ni kwa kipindi cha mwaka uliopita wa 2015 ambapo ni pamoja na leseni za biashara za mazao ya misitu, faini na vibali mbalimbali vya biashara hizo za misitu na tunawataka wafanyabiashara hao wafuate taratibu ili kuinusuru misitu yetu kwa kuvuna kufuatatana na taratibu zilizowekwa,” alisema Dk Abel.
Alisema kuwa katika kuhakikisha misitu inakuwa salama uvunaji wa mazao ya misitu umepangwa kwenye mashamba ya miti ambayo si misitu ya hifadhi bali ni mistu ya wazi ambapo asilimia tano ya mapato hurudi kwenye maeneo ya vijiji kwa ajili ya upandaji miti.
“Tunashirikiana na serikali za vijiji kuhakikisha tano ya mapato zirudi kwa ajili ya upandaji miti kwa lengo la kuwa na sehemu ya uvunaji wa miti kwani kama hakutakuwa na mashamba ya miti ni dhahiri watu wafanyabiashara watakuwa wakivuna kwenye misitu ya hifadhi jambo ambalo ni kinyume cha sheria,” alisema Dk Abel.
Alisema kuwa changamoto zinazoikabili wakala ni pamoja na uvamizi wa watu kwenye hifadhi ya misitu, vitendea kazi, kilimo na ufugaji kwenye hifadhi, uchomaji moto na uharibifu mwingine unaofanywa na watu kwenye misitu hiyo ambayo iko kisheria na kuingia humo ni kinyume cha sheria.
Aidha alisema wamekuwa wakifanya doria alkini kutokana na misitu hiyo kuwa mikubwa ni vigumu kuweza kuwadhibiti wahalifu wa misitu ambao wamekuwa wakivizia na kuingia na kufanya uharibifu na Kanda ya Mashariki inaundwa na mikoa ya Pwani, Morogoro na Dar es Salaam.
Mwisho.

WAKURUGENZI WA HALMASHAURI WATAKIWA KUANDAA DAFTARI LA CHANGAMOTO ZA WANANCHI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuanzisha daftari maalumu la wakuu wa Idara kwenda kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi Vijijini kila mwezi.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati wa kikao baina yake na wakurugenzi walioteuliwa hivi karibuni na Rais Dk John Magufuli juu ya utekelezaji wa majukumu yao ya kikazi.
Ndikilo alisema kuwa umefika wakati sasa wa watendaji kwenda kuwatumikia wananchi na si kukaa ofisini wakati wananchi wakiwa na matatizo mengi huku wao wakiwa wamekaa ofisini tu.
“Nataka nione wakurugenzi mkiwa mmetengeneza dafatari hilo ambalo litamwonyesha mkuu wa idara kazi aliyoifanya kwa ajili ya kutatua kero na kule wanako kwenda lazima kuwe na sahihi zao kuwa walifika kwenye vijiji husika ili iwe ushahidi wa utendaji kazi wao na si kukaa tu ofisini,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa sambamba na hilo wakurugenzi lazima watenge siku maalumu ya kusikiliza kero za wananchi na mfumo wa kupata taarifa za matatizo kwa kila kata ili iwe rahisi kufuatilia ikiwa ni pamoja na kuweka sanduku la kero za wananchi ili zishughulikiwe mapema.
“Mnapaswa kushughulikia kero za wananchi kwa wakati kwani ucheleweshaji wa kutatua kero kwa muda muafaka husababisha matatizo kuongezeka na kufanya malalamiko kutoisha ambapo wananchi wamekuwa wakikimbilia kwa wakuu wa wilaya na mkoa huku kukiwa hakuna utatuzi ngazi ya Halmashauri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa wakurugenzi wanapaswa kusimamia suala la ulinzi na usalama na wasiliache kwa serikali kuu ili wananchi waweze kufanya shughuli zao wakiwa na amani kwani kukiwa na uvunjifu wa amani itakuwa ni vigumu watu kufanya shughuli za maendeleo.
“Changamoto ni nyingi ikiwa ni pamoja na migogoro ya ardhi, wakulima na wafugaji, migogoro kutoshughulikiwa kwa wakati na mipaka pamoja na changamoto nyingine nyingi ambapo wajibu wa wakurugenzi ni kuwasimamia watendaji mbalimbali na hawapaswi kuwa na urafiki usiokuwa wa maendeleo kwa watendaji,” alisema Ndikilo.
Aliwataka wakurugenzi hao kuwasimamia watendaji wao ili wasikae ofisini kusubiri maelekezo toka ngazi za juu bali waende kwa wananchi kwani muda huu si wa kukaa bali wanapaswa kuwa wabunifu na si kukaa tu kwani lazima wawe wawajibikaji.

Mwisho.

PWANI YATAKIWA KUMALIZA ZOEZI LA WATUMISHI HEWA


Na John Gagarini, Kibaha
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Angella Kairuki ameutaka uongozi wa mkoa wa Pwani kuhakikisha unamaliza kushughulikia tatizo la watumishi hewa haraka.
Mkoa huo una jumla ya watumishi hewa 272 ambao wamebainika na kuitia serikali hasara ya shilingi bilioni 1.4 kufuatia zoezi la uhakiki wa watumishi hewa kufanyika kutokana na agizo la Rais Dk John Magufuli.
Kairuki aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa mkutano wake na uongozi wa mkoa huo, wakurugenzi wa Halmashauri na Miji za mkoa huo pamoja na watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa ili kujua changamoto zinazowakabili watumishi wa Umma.
Alisema kuwa kwa kuwa tayari agizo la Rais lilishatoka tangu mwezi Machi mwaka huu kinachotakiwa ni kuwachukulia hatua wahusika baada ya kuwabaini na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili na si kuwaacha tu.
“Rais alitoa maagizo kubainisha watumishi hewa na baada ya kubainika wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani kwani wamefanya makosa ya kuiibia serikali hivyo hakuna sababu ya kutowachukulia hatua stahiki,” alisema Kairuki.
Aidha alisema kuwa hatua stahiki zichukuliwe mapema ikiwa ni pamoja na kurekebisha taarifa za watumishi hao ikiwa ni pamoja na kusitisha mishahara yao kabla ya malipo yamwezi Agosti ili tatizo hilo lisije likaendelelea.
“Pia nataka kusiwe na data chafu ambazo Halmashauri ziliweka kwa watumishi hao ambazo ni pamoja na kutopandishwa madaraja, malipo kwa watu ambao wana umri zaidi ya miaka 60 na watumishi kutokuwepo kwenye vituo vyao vya kazi huku wakiendelea kulipwa,” alisema Kairuki.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa mkoa huo una watumishi 16,156 huku ukiwa na upungufu wa watumishi 3,306 na watumishi hewa waliobainika ni 272 kwenye Halmashauri saba za mkoa huo ambazo ni Kibaha Mjini, Kibaha, Mafia, Rufiji, Mkuranga, Kisarawe na Bagamoyo.
Ndikilo alisema kuwa mkoa unalishughulikia suala la watumishi hewa ambapo wanashirikiana na Jeshi la Polisi pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa na kusema kuwa zoezi hilo ni gumu hivyo inabidi walifanye kwa umakini ili lisije likaleta matatizo na watalikamilisha mapema.

Mwisho.

OFISI YA MKUU WA MKOA INAKABILIWA NA UHABA WA MAGARI


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amesema kuwa mkoa wake unakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa magari hali ambayo inawafanya kuazima magari kwenye wilaya katika shughuli za kikazi katika mkoa huo.    
Aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa mkutano wake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Angella Kairuki alipokuwa akizungumza na watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa na wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Miji za mkoa huo.
Ndikilo alisema kuwa changamoto hiyo kwa wataalamu wa mkoa ni kubwa hali ambayo inawafanya wafanye kazi kwenye mazingira magumu hasa kwenye maeneo ya mbali ikiwa ni pamoja na kwenye Halmashauri za mkoa huo.
“Waziri mkoa una changamoto kubwa ya ukosefu wa magari ikiwemo ofisi yangu na wataalamu wangu inapofika hatua ya kwenda kwenye maeneo ya mbali inakuwa mtihani mkubwa kwani inatubidi tuazime magari ya kwenye wilaya kwa ajili ya kufika baadhi ya maeneo,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa hata mkuu wa wilaya ya Kibaha gari alilonalo ni bovu ambapo hivi karibuni alipata ajali ya kuligonga gari jingine kutokana na breki kugoma naye mkuu wa wilaya ya Mkuranga naye gari lake siyo zuri sana, wilaya Mpya ya Kibiti yenyewe haina gari kabisa.
“Usafiri kwa mkoa wetu ni changamoto kubwa hivyo tunaomba mtusaidie ili katika bajeti ijayo mtufikirie kwa kutupatia usafiri ili tuweze kutekeleza majukumu yetu vizuri ili kukabiliana na changamoto hii ambayo inatupa wakati mgumu inapofikia suala la usafiri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ni ukomo wa bajeti ambayo kwa mwaka 2014-2015 ulishuka kwa asilimia 40 ikilinganishwa na bajeti iliyopita, fedha za maendeleo kuchelewa, madeni ambayo yamefikia milioni 152, watumishi kuhama kutafuta maslahi mazuri, vitendea kazi na upandishwaji wa madaraja.
Akijibu baadhi ya hoja Waziri Kairuki alisema kuwa Wizara inazifanyia kazi changamoto hizo na pale fedha zitakapopatikana itaboresha mazingira ya watumishi ili wafanye kazi vizuri kwani serikali inawathamini wafanyakazi na haitaki wafanye kazi katika mazingira magumu.
Kairuki alisema kuwa juu ya maofisa utumishi waliokuwa wakilipa mshahara watumishi hewa itabidi wawajibike ambapo kwa sasa inawsafuatilia kwani inaonekana nao walichangia kulipa mishahara kwa watumishi ambao hawakustahili.

Mwisho.

VIONGOZI WAKATAA KUKABIDHI OFISI ZA SOKO


Na John Gagarini, Kibaha
UONGOZI wa zamani wa soko la mkoa la Maili Moja wamegoma kuwakabidhi ofisi uongozi mpya uliochaguliwa mbele ya mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama wakidai kuwa taratibu za uchaguzi huo zilikiukwa.
Makabidhiano ya ofisi ambayo yalikuwa yakisimamiwa na diwani wa kata ya Maili Moja Theodory Joseph, ofisa mtendaji wa mtaa wa Maili Moja John Dotto, mwenyekiti mpya wa soko Ramadhan Maulid na katibu Elias Kisandu yalishindikana kutokana na uongozi wa zamani kutoridhia jinsi walivyoondolewa madarakani
Akizungumza baada ya makabidhiano ya soko hilo kushindikana katibu wa zamani wa soko hilo Muhsin Yusuph alisema kuwa hawawezi kukabidhi mali za soko hilo bila ya taratibu kwani soko hilo lilikuwa liko kwenye mfumo wa ushirika.
Yusuph alisema kuwa taratibu za ushirika zinafahamika hivyo sisi hatuwezi kuwakabidhi uongozi mpya bila ya taratibu ikiwa ni pamoja na kufanya uchaguzi chini ya mrajisi wa vyama vya ushirika.
“Huu ni ushirika na ushirika una taratibu zake sasa sisi hatuwezi kuukabidhi uongozi mpya bila ya kufuata utaratibu kwani uchaguzi haukufanyika kwa kufuata katiba ya ushirika ambapo mrajisi ndiye aliyetakiwa kuwa msimamizi,” alisema Yusuph.
Alisema kuwa siku walipochaguliwa viongozi wapya ilikuwa ni mkutano na mkuu wa wilaya kujua changamoto zinazotukabili lakini haukuwa mkutano wa uchaguzi ambao unakuwa ni maalumu na unasimamiwa na mrajisi wa vyama vya ushirika.
Mwenyekiti wa kamati ya makabidhiano diwani Theodory Joseph alisema kuwa wao walikuwa wakikamilisha taratibu kwani uchaguzi ulifanyika na uongozi huo wa zamani kushindwa na kutakiwa kuwakabidhi ofisi viongozi wapya.
Joseph alisema kwa kuwa wamekataa watawasiliana na ngazi zinazohusiaka kwa taratibu zaidi lakini wao hawana la zaidi kwani kila kitu kilikuwa kinajulikana hivyo watasubiri taratibu zingine.
Kwa upande wake mwenyekiti mpya Ramadhan Maulid alisema kuwa kwa kuwa uongozi uliopita umegoma kukabidhi ofisi watawasiliana na mkuu wa wilaya ili kujua nini cha kufanya juu ya hatua hiyo.
Soko hilo lilikuwa likiendeshwa kwa taratibu za ushirika ambapo kuna zaidi ya wafanyabiashara zaidi ya 500 ambapo baadhi ni wanachama wa ushirika na wengine si wanachama wa ushirika ambapo mkuu wa wilaya alishauri ni vema uongozi ukawa tofauti kati ya ule wa ushirika na soko ili kuondoa muingiliano wa majukumu.

Mwisho.  

RC AKATAA KUSIKIA HALMASHAURI IMEPATA HATI CHAFU

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo Ndikilo amesema kuwa kuanzia sasa hataki kusikia Halmashauri za Miji au wilaya za mkoa huo kuwa zimepata hati chafu.
Sambamba na hilo amezitaka Halmashauri hizo kuwatumia wakaguzi wa hesabu wa ndani ili kuweka mambo yao katika mpangilio mzuri ili kuondokana na hati chafu ambazo zimekuwa zikiziandama baadhi ya Halmashauri hizo.
Ndikilo aliyasema hayo wakati wa kikao na Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Miji za Mikoa hiyo ambao waliapishwa hivi karibuni baada ya kuteuliwa na Rais Dk John Magufuli.   
Alisema kuwa taarifa za hesabu za kila Halmashauri zinapaswa kupelekwa kwa wakati kulingana na utartibu uliowekwa na serikali pia hoja za mkaguzi mkuu wa serikali (CAG) zijibiwe mapema.
“Kuanzia sasa sitaki kusikia Halmashauri imepata hati chafu kutokana na uzembe kwani wakati mwingine inatokana na kushindwa kuonyesha risiti ambazo ni za manunuzi jambo ambalo liko ndani ya uwezo wenu hakuna sababu ya kuharibu sifa za utendaji kazi wenu kwa mambo madogomadogo,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa jambo jingine ambalo wakurugenzi wa halmashauri tisa za mkoa huo wanapaswa kulizingatia ni kutekeleza miradi kwa thamani halisi ya fedha na si kutekeleza miradi hiyo chini ya kiwango.
“Mnapaswa kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi kwa wakati na kama mnaona kuna mtendaji ambaye anafanya vibaya hakuna sababu ya kumuonea haya dawa ni kumwondoa,” alisema Ndikilo.
Mkuu huyo wa mkoa wa Pwani alisema kuwa wakurugenzi hao wanapaswa kukuisanya mapato kwa nguvu kwani makusanyo makubwa ndiyo yatakayoifanya Halmashauri kuweza kuendesha shughuli zake ikiwa ni pamoja na kuchangia uchumi wa wananchi na Taifa.
“Watu wanaohusika na vyanzo vya mapato wanapaswa kuwa wabunifu wa kuanzisha vyanzo vipya na siyo kuwa na vyanzo vilevile miaka yote pia wavifanyie uchambuzi ili kutokusanya mapato chini kutokana na taarifa za wazabuni ambao wamekuwa wakiidanganya Halmashauri juu ya mapato huku mengine yakiingia mifukoni mwao,” alisema Ndikilo.
Kwa upande wake mkurugenziwa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Jenifa Omolo alisema kuwa amejipanga vyema kutekeleza majukumu ya serikali kama walivyokula kiapo ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi pamoja na ukusanyaji wa mapato.
Naye Tatu Seleman mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha alisema kuwa atahakikisha anashirikiana na wananchi katika kutekeleza majukumu ya Halmashauri kwani ushirikishwaji utasaidia kupatikana kwa maendeleo hasa kupitia kwenye huduma za kiajamii.

Mwisho.

JAKAYA AKARIBISHWA KISHUJAA BAGAMOYO

Na John Gagarini, Bagamoyo

RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne Dk Jakaya Kikwete amesema kuwa hakuna kitu kilichokuwa kikimpa wakati mgumu kama kushindwa katika uongozi wake wa miaka 10 iliyopita.

Aliyasema hayo juzi mjini Bagamoyo wakati wa sherehe iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Sanaa Bagamoyo (TASUBA) ya kumkaribisha nyumbani baada ya kukabidhi uongozi kwa mwenyekiti mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk John Magufuli mjini Dodoma hivi karibuni.

Dk Kikwete alisema kuwa hali ya kushindwa ilikuwa ikimpa wakati mgumu na kujiona kuwa kama endapo angeshindwa basi ange waangusha Wanabagamoyo na Pwani nzima.

“Kila nilipokuwa nikifikiria kushindwa kwenye jambo lolote la uongozi wangu kwa nchi au kwenye Chama lakini namshukuru Mungu kwani tulifanikiwa sana katika suala la maendeleo kwa nchi nzima kwani huwezi ukapendelea sehemu uliyotoka au ukawanyima maendeleo ni kitu ambacho hakiwezekani,” alisema Dk Kikwete.

Alisema kuwa wakati fulani alikuwa akilalamikiwa na baadhi ya wabunge kuwa anapendelea Bagamoyo jambo ambalo si la kweli ambapo walidai kuwa amehamisha fedha za ujenzi wa barabara na kuzihamishia kwenye ujenzi wa barabara ya Msata Bagamoyo.

“Hali kama hiyo Ilikuwa inanipa wakati mgumu kwnai kila sehemu inataka maendeleo na nisingeweza kutofanya maendeleo kwa watu wa Bagamoyo kwani hata wao wanahitaji maendeleo kama sehemu nyingine,” alisema Dk Kikwete.

Aidha alisema kuna wakati ilibidi ahamishe fedha kutoka Bagamoyo na kufanya ujenzi kwenye maeneo ya Geita-Sengerema hadi Usagara wakati huo waziri wa Ujenzi alikuwa Basil Mramba lakini hawakuliona lakini anasema alishukuru Mungu kwani ujenzi kwenye barabara hizo ulifanyika vizuri.

“Namshukuru Mungu katika uongozi wangu tulifanya kazi na kuleta maendeleo makubwa na tumeiacha nchi mahali pazuri na salama kwnai imetulia licha ya mwaka 2015 wakati wa uchaguzi ambapo baadhi ya watu walisema kuwa Rais gani hata hafanyi mpango wa kubadilisha katiba ili aendelee kukaa madarakani kwani watu walishindana lakini hawakupigana wala kumwaga damu na uchaguzi ulipokwisha maisha yaliendelea salama kabisa,” alisema Dk Kikwete.

Alibainisha kuwa Watanzania wanapaswa kumuombea Rais Dk John Magufuli ili aweze kuleta maendeleo kwani ni mpenda maendeleo hivyo lazima asaidiwe aweze kuleta maendeleo ya watu.

Akizungumzia kuhusu Chama alisema kuwa kiko vizuri na hakuna kinachoiweza CCM kwani anajua hakuna chama cha kuweza kukishinda kwani havina uwezo ikizingatiwa ni chama kikubwa na viongozi wake ni imara.

Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo Maskuzi alisema kuwa katika uongozi wake alifanikiwa kuleta maendeleo makubwa kuanzia kwenye elimu na mpango wa shule za kata sasa umeonyesha mafanikio ambapo shule hizo kwa mwaka huu zimeongoza kwenye matokeo.

Maskuzi alisema kuwa umeme ni moja ya mafanikio ambapo kwa sasa umefika hadi vijijini kupitia mpango wa Umeme Vijijini REA, ujenzi wa barabara na masuala mengine ya kimaendeleo kwenye nchi ambayo ni ya kujivunia.

Katika sherehe hiyo ambayo ilihudhuriwa na familia ya Dk Kikwete alipewa zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na mifugo kama vile ngombe, mbuzi, kuku, bata, mavazi ya jadi na vitu mbalimbali ambavyo vilitolewa na wananchi wa mkoa wa Pwani.


Mwisho.

BAGAMOYO YAGUNDUA WTUMISHI HEWA ZAIDI 83 WAGUNDULIKA

 Na John Gagarini, Bagamoyo

WILAYA ya Bagamoyo mkoani Pwani imebaini uwepo wa watumishi hewa 83 na kuifanya wilaya hiyo kwa sasa kuwa na watumishi hewa 91 ambapo wakati zoezi hilo linaanza lilibaini watumishi hewa nane tu.

Akizungumza wakati wa zoezi la kuzindua madawati 300 yaliyotengenezwa na wadau mbalimbali na kuzinduliwa na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo, mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga alisema kuwa watumishi hao wamebainika baada ya kuundwa kikosi kazi kuchunguza watumishi hao.

Mwanga alisema kuwa awali baada ya agizo lililotolewa na Rais Dk John Magufuli kulibainika watumishi hewa nane lakini sasa idadi hiyo imeongezeka baada ya kufanywa kwa kina.

Alisema kuwa kikosi kazi kilichoundwa na watu sita wanaoundwa na kamati ya ulinzi na usalama na kugundua watumishi hewa wengi ni kutoka idara ya elimu hasa kwenye shule za msingi na sekondari.

“Watumishi wengi ni walimu ambao wengi wamekwenda masomoni bila ya kuaga na hawana ruhusa na baadhi walishaacha kazi lakini cha kushingaza mishahara yao ilikuwa inaingizwa kama kawaida jambo ambalo ni kinyume cha taratibu,” alisema Mwanga.

Aidha alisema kuwa tatizo kubwa linaonyesha ni idara ya elimu kushindwa kutoa maamuzi ya haraka mara walimu wanapoomba kwenda masomoni hivyo huamua kuondoka kienyeji.

“Watumishi wengine walibainika kuwa hawana vielelezo vyo vyote vya vya juu ya ajira zao na tunaomba hatua kali zichukuliwe kwa watumishi hao ambao ni hewa na wamekuwa wakilipwa mishahara huku hawafanyi kazi wanachukua mishahara ya bure,” alisema Mwanga.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kutokana na kubainika watumishi hao 83 hewa wilayani Bagamoyo kwa sasa mkoa wamefikia watumishi hewa 272.

Ndikilo alisema kuwa zoezi hilo bado linaendelea na kukipongeza kikosi kazi cha wilaya hiyo kuweza kuwabaini watumishi hao hewa na itaendelea kuchunguza hadi kuondoa kabisa suala hilo.


Mwisho.

Tuesday, July 5, 2016

WAFUGAJI WATAKA WASIONDOLEWE CHAURU

Na John Gagarini,Bagamoyo

WAFUGAJI wanaoishi kwenye Kitongoji cha Msigala Kijiji cha Visezi kata ya Ruvu wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wamepinga kupelekwa Kitongoji cha Mnanyama kutokana na kutokuwa na huduma za kijamii.

Wakizungumza na waandishi wa habari Kijijini hapo wamesema kuwa eneo walilopangiwa halina huduma hizo ndiyo sababu ya wao kuendelea kukaa hapo walipo sasa.

Akizungumzia juu ya hali hiyo Lupina Kirayo alisema kuwa chanzo cha wao kutakiwa kuondoka ni kutokana na madai ya wakulima wa shamba la Chama Cha Ushirika wa Umwagiliaji Ruvu (CHAURU) kuwa ngombe wao wamekuwa wakiingia kwenye mashamba na kuharibu mazao.

Kirayo alisema kuwa wao wako hapo kwa muda mrefu lakini wanashangaa kutakiwa kuondoka na kwenda Mnanyama ambako hakuna huduma hyoyote ya Kijamii.

“Zamani kijiji hicho kiliweka njia kwa ajili ya ngombe kupita kwenda kunywa maji mtoni lakini wakulima walifunga njia ya kupita ngombe na ndiyo chanzo cha migogoro ya wakulima na wafugaji ilipoanza,” alisema Kirayo.

Alisema kuwa tatizo kubwa linatokana na baadhi ya wafugaji wanaoleta mifugo toka maeneo ya mbali kwa ajili ya kwenda kuuza ngombe kwenye mnada wa Ruvu ndiyo wamekuwa wakiingiza mifugo kwenye shamba hilo la ushirika wakitafuta maji.

Aidha alisema kuwa wao kama wenyeji wa Kitongoji hicho wako makini na mifugo yao ambapo wakati mwingine wachungaji wao wamekuwa wakishindwa kuwadhibiti ngombe na kuingia kwenye shamba hilo ambapo wamekuwa wakiwafukuza wachungaji wazembe ili kuondoa migongano na kuomba radhi na kutaka kuwe na maridhiano na kuangalia njia nzuri ya kudhibiti mifugo isiingie kwenye shamba hilo lakini siyo kuwaondoa hapo.

Naye Elizabeth Meja amesema kuwa yeye alizaliwa hapo na kipindi cha nyuma wamekuwa wakiishi vizuri lakini kwa sasa wanaambiwa waondoke ambako kule huduma ya afya hakuna ambapo kwa akinamama hasa pale wanapokuwa wajawazito huhitaji kupata huduma za mara kwa mara.

Meja alisema kuwa sehemu wanayotaka kuhamishiwa kuna umbali wa km 20 hadi kufika kwenye huduma za afya na hata watoto wanapozaliwa hupaswa kupelekwa kliniki lakini kutokana na umbali huo itakuwa ni matatizo pia watoto wao kwa sasa licha ya kutumia masaa zaidi ya mawili kwenda shule ni karibu tofauti na wakienda kule hatapata fursa ya kusoma kutokana na umbali huo.

“Hata suala la maji ni tatizo kwani hapa tunatumia maji ya shilingi 20,000 kwa siku lakini kule tunakotakiwa twende maji hakuna kabisa hivyo ni vema wakaweka miundombinu kwanza ili huduma kama hizo zipatikane,” alisema Meja.

Naye mwenyekiti wa kitongoji hicho cha Msigala Otiniel Mbura alisema kuwa tayari serikali iliamua wafugaji hao kwenda huko ili kuondoa migogoro inayojitokeza kila wakati.

Mbura alisema kuwa ni vema wafugaji hao wakenda kwanza na serikali itawapelekea huduma kuliko hivi sasa wanavyokataa kwenda huko walikopangiwa.


CHAURU YAWATAKA WAFUGAJI KUONDOA NGOMBE KWENYE SHAMBA LAO

Na John Gagarini, Bagamoyo

UONGOZI Chama Cha Ushirika wa Wakulima wa Umwagiliaji Ruvu (CHAURU) wamewataka wafugaji walioko kwenye shamba hilo kuhamisha mifugo yao ambayo imekuwa ikifanya uharibifu wa mazao pamoja na miundombinu ya umwagiliaji.

Akizungumza kwenye kikao cha wakulima na wafugaji waliopo kwenye shamba hilo ambalo liko kwenye kitongoji cha Msigala Kijiji cha Visezi kata ya Ruvu wilayani Bagamoyo mwenyekiti wa chama hicho Sadala Chacha amesema kuwa uharibifu uliofanywa ni mkubwa sana.

Chacha amesema kuwa kutokana na baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo kwenye shamba hilo la umwagiliaji la mpunga kumewasababishia hasara kubwa wanachama wake na uharibifu wa miundombinu.

Amesema kuwa serikali ilishawatengea eneo lao liitwalo Mnyanama lakini hawataki kwenda wakidai kuwa hakuna huduma za kijamii jambo ambalo limewafanya waendelee kukaa hapo na huku mifugo hiyo hasa ngombe wakiendelea kufanya uharibu wa miundombinu na kula mazao ya wakulima.

Aidha amesema kuwa wamekuwa wakikaa vikao vya mara kwa mara ili kujaribu kuangalia utaratibu wa namna ya kufuga na wao kulima lakini wao wamekuwa wakilishia mifugo kwenye mashamba hayo ya wakulima na kusababisha ugomvi mara kwa mara.

Ameongeza kuwa wamechoshwa na vitendo hivyo vya wafugaji vya kuingiza ngombe kwenye shamba hilo huku sheria aikikataza mifugo kuingia kwenye eneo hilo lakini utekelezaji wa suala hilo umekuwa mgumu kwani mifugo bado inaingizwa shambani hapo.

Kwa upande wake mmoja wa wafugaji Lupina Kirayo amesema kuwa tatizo kubwa linatokana na baadhi ya wafugaji wanaoleta mifugo toka maeneo ya mbali kwa ajili ya kwenda kuuza ngombe kwenye mnada wa Ruvu ndiyo wamekuwa wakiingiza mifugo kwenye shamba hilo la ushirika wakitafuta maji.

Lupina amesema kuwa wao kama wenyeji wa Kitongoji hicho wako makini na mifugo yao ambapo wakati mwingine wachungaji wao wamekuwa wakishindwa kuwadhibiti ngombe na kuingia kwenye shamba hilo ambapo wamekuwa wakiwafukuza wachungaji wazembe ili kuondoa migongano na kuomba radhi na kutaka kuwe na maridhiano na kuangalia njia nzuri ya kudhibiti mifugo isiingie kwenye shamba hilo lakini siyo kuwaondoa hapo.

Naye mwenyekiti wa Kitongoji hicho cha Msigala Otiniel Mbura amekiri kutokea changamoto ya ngombe kuingizwa kwenye shamba hilo na kusema kuwa ili kuondoa tatizo hilo ni wafugaji hao kuondoa mifugo hiyo na kuipeleka kule walikopangiwa.

Mbura amesema kuwa wafugaji hao hawataki kwenda huko kwa madai kuwa hakuna huduma za kijamii kama zahanati, shule na malambo ya maji kwa ajili ya mifugo yao hali ambayo imefanya ugomvi kwenye shamba hilo kutokwisha kwa muda mrefu sasa.

Shamba hilo la umwagiliaji mpunga lilianzishwa miaka ya 60 na lina wanachama wapatao 894 na lina ukubwa wa hekta 3,209 huku za makazi zikiwa hekta 720 ambapo baada ya mavuno ya mpunga wanachama hulima mazao mengine kama vile mahindi,ufuta na mtama pamoja na kilimo cha mbogamboga.

Mwisho.


WATENDAJI WATAKAOSHINDWA KUKAMILISHA ZOEZI LA UPATIKANAJI MADAWATI KUJIFUKUZISHA KAZI

Na John Gagarini, Kibaha

MKUU mpya wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Asumter Mshama ametoa siku 24 kwa watendaji wa kata na maofisa tarafa kuhakikisha wanakamilisha zoezi la upatikanaji wa madawati na atakayeshindwa kukamilisha zoezi hilo kwenye sehemu yake atakuwa amejifukuzisha kazi mwenyewe.

Mshama ametoa agizo hilo mjini Kibaha kwenye mkutano alioundaa na mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha na watendaji hao na baadhi ya wakuu wa Idara za Elimu, Ardhi na Mazingira na kusema kuwa watendaji hao wanapaswa kukamilisha zoezi hilo ifikapo Julai 29 mwaka huu.

Amesema kuwa agizo la Rais Dk John Magufuli ilikuwa ni Juni 30 mwaka huu hivyo hakuna sababu ya watedaji hao kushindwa kutekeleza agizo hilo kwani muda uliotolewa ulishapita.

Aidha amesema kuwa Baadhi ya watendaji wamefanikiwa kukamilisha zoezi nawapongeza lakini wengine wameshindwa kukamilisha hivyo anatoa muda hadi Julai 29 wawe wamekamilisha na atakayeshindwa atakuwa kajifukuzisha kazi mwenyewe kwa kushindwa kuwajibika.

Akielezea juu ya uwezekano wa kukamilisha hilo amesema kuwa yeye kule alikotoka wilaya ya Wangingombe mkoani Njombe alipambana na kufanikiwa kukamilisha zoezi hilo kwa ufanisi mkubwa ambapo madawati yalipatikana na kuwa na ziada ya madawati 2,000 hivyo hata Kibaha hakuna sababu ya kushindwa kufanya hivyo kwani hakuna jambo ambalo linashindikana.

Amesisitiza kuwa Maagizo waliyopewa wao wakuu wa wilaya na Rais ni kuhakikisha hakuna mwanafunzi anayekaa chini kwani haiwezekani nyumbani watoto wakae kwenye makochi au sofa lakini wakifika shule wanakaa chini lazima watendaji hao wahamasishe wananchi kuchangia miundombinu ya elimu.

Mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha amesema kuwa watendaji hao wanapaswa kuwahamasisha wananchi kuchangia unpatikanaji wa madawati hakuna haja ya kusema kuwa eti watu wagumu kuchangia.

Amesisitiza kuwa Kama mtendaji ameshindwa kukamilisha zoei hilo ni kwamba ameshindwa kazi kwani sheria zipo na wanapaswa kuzitumia ili kufanikisha zoezi hilo la upatikaaji wa madawati.

Naye mtendaji wa kata ya Kongowe Said Kayangu alikiri kuwa baadhi ya maeneo zoezi hilo limeshindwa kufanikiwa kutokana na changamoto mbalimbali.

Kayangu amesema kuwa watahakikisha muda uliosalia wanakamilisha zoezi hilo na kusema kuwa watajipanga vizuri ili kufanikisha zoezi hilo ili kutekeleza agizo la Rais Dk John Magufuli ili kila mtoto aweze kukaa kwenye dawati.

mwisho.



Saturday, July 2, 2016

johngagariniblog: WAKUU WA WILAYA WAPYA WAAPISHWA PWANI

johngagariniblog: WAKUU WA WILAYA WAPYA WAAPISHWA PWANI: Na John Gagarini, Kibaha   MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewataka wakuu wapya wa wilaya wlioteuliwa na Rais Dk John...

Friday, July 1, 2016

WAKUU WA WILAYA WAPYA WAAPISHWA PWANI


Na John Gagarini, Kibaha

 

MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewataka wakuu wapya wa wilaya wlioteuliwa na Rais Dk John Magufuli mkoani humo kuinua pato la wananchi wa mkoa huo kutoka milioni 1.2 kwa mwaka hadi milioni 3 kwa mwaka.

 

Aliyasema hayo jana mjini Kibaha wakati akiwaapisha wakuu hao wa wilaya wapya na kusema kuwa pato la mwananchi wa mkoa wa Pwani liko chini sana licha ya kuwa na fursa mbalimbali za kipato.

 

Ndikilo alisema kuwa kutoakana na pato hilo la wananchi kuwa dogo kiasi hicho hata mchango wa mkoa kwa Pato la Taifa ni dogo sana la asilimia 1.8 jambo ambalo linapaswa kuwekewa mkakati wa kupandisha pato hilo ili liwe na mchango mkubwa kwa mwananchi na Taifa kwa ujumla.

 

“Nawapongezeni kwa kuchaguliwa kwenye nafasi hizi na mkoa tayari umeandaa mpango kazi wake kwa ajili ya kuinua pato la mwananchi hivyo mnapaswa kuweka vipaumbele ambavyo vitasaidia kuinua uchumi wa wananchi wa wilaya unayoongoza,” alisema Ndikilo.

 

Alisema kuwa hakuna sababu ya mkoa kuendelea kuwa na pato dogo huku kukiwa na vyanzo vingi vya mapato ikiwa ni pamoja na rasilimali mbalimbali kama vile uvuvi, kilimo, korosho, maliasili ikiwa ni pamoja na mbuga za wanyama na madini mbalimbali.

 

“Mfano ni majumba mengi yanayojengwa Dar es Salaam kokoto na mawe yanatoka mkoa wa Pwani hivyo hakuna sababu ya kuwa maskini tuna zao la korosho ambapo kwa msimu uliopita wakulima waliuza korosho zenye tahamani ya shilingi bilioni 18,” alisema Ndikilo.

 

Aliwataka wahakikisha wanawajibika na kutowalea watumishi ambao ni kikwazo na wenye urasimu wa kuwahudumia wananchi ambao hufika ngazi ya mkoa kulalamika ili hali ngazi za chini kuna watendaji ambao wangeweza kutatua matatizo hayo.

 

“Changamoto ni nyingi ikiwa ni pamoja na suala la ulinzi na usalama, wahamiaji haramu, matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi nisingependa mambo haya yatokee tena hakikisheni mnatimiza wajibu wenu na kuwaondolea kero wananchi,” alisema Ndikilo.

 

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga alisema kuwa moja ya changamoto ambazo atakabiliana nazo ni pamoja na wahamiaji haramu kw akudhibiti bandari 19 ambazo zimekuwa ni njia ya wahamiaji hao haramu.

 

Naye Asumpter Mshama alisema kuwa moja ya mambo atayapaa kipaumbele ni kuhakikisha fedha kwa makundi ya vijana na akinamama asilimia 10 zinatoka ili wananchi waweze kujenga uchumi wao na ule wa Taifa.

 

Wakuu wapya walioapishwa jana ni pamoja na Shaibu Nunduma wilaya ya Mafia, Filberto Sanga Mkuranga, Gulamu Kifu wilaya ya Kibiti, Asumpter Mshama wilaya ya Kibaha, Juma Njwayo wilaya ya Rufiji na Majid Mwanga wilaya ya Bagamoyo huku Happyness William hakuweza kuapishwa kutokana na dharura.

 

Mwisho.


 MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo kushoto akimkabidhi zana za kufanyia kazi mkuu wa wilaya ya Kibiti Gulamu Kifu, baada ya kumwapisha kwenye hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya mkuu huyo wa mkoa

Mkuu mpya wa wilaya ya Kibaha Asumpter Mshama kulia akiapa mbele ya mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo kushoto wakati wa hafla iliyofanyika mjini Kibaha ya kuwaapisha wakuu wapya wa wilaya za mkoa huo ambao waliteuliwa hivi karibuni na Rais Dk John Magufuli

Mkuu mpya wa wilaya Rufiji Juma Njwayo kulia akiapa mbele ya mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati wakiapishwa wakuu wa wilaya za mkoa huo kwenye viwanja vya ofisi ya mkuu wa mkoa huo.