Thursday, March 24, 2016

MMOJA AFA 10 WALAZWA KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja amefariki dunia wilayani Kibaha mkoani Pwani kutokana na ugonjwa wa Kipindupindu huku wengine 10  wakiwa wanaugua ugonjwa huo kwenye hospitali mbalimbali wilayani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Ofisa afya wa mkoa wa Pwani Simon Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uligundulika Aprili 17 mwaka huu katika Shule ya Sekondari ya Ruvu wilayani Kibaha.
Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uliwakumba wanafunzi 21 wa shule hiyo ambapo awali waliona kuwa ni mchafuko wa matumbo kwani wanafunzi hao walikuwa wakiharisha.
“Baada ya kuona hali imezidi kuwa mbaya kwa wanafunzi walimu waliwapeleka wanafunzi kwenye Zahanati ya Kijiji cha hicho cha Ruvu Station na kuchukua sampuli ya kinyesi kwa wanafunzi tisa ambapo mmoja aligundulika kuwa na ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Alisema kuwa baada ya kubaini hilo ilibidi mkuu wa wilaya aifunge shule hiyo ili kuwaepusha wanafunzi zaidi kuambukizwa ugonjwa huo ambapo wanafunzi waliokumbwa na ugonjwa huo wengi walikuwa ni wanafunzi wakike ambao wako bweni.
“Hadi sasa kwenye Zahanati ya Ruvu kuna wagonjwa wanne, Zahanati ya Dutumi watatu na Mlandizi wako watatu ambao wanendelea kupatiwa matibabu ya ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Aidha alisema kuwa chanzo cha kuenea ugonjwa huo ni kinyesi ambacho kinatokana na watu wengi kujisaidia kwenye Mto Ruvu ambapo maji yake wanafunzi na wananchi wa Kijiji cha Ruvu Station.
“Tumechukua hatua za kufungua kambi kwenye maeneo yote yenye ugonjwa ikiwa ni pamoja na Ruvu Station, Dutumi na Mlandizi pia kuwaptia dawa ya kusafishia maji ili kutibu maji hayo ambayo wananchi wamekuwa wakiyatumia bila ya kuyachemsha,” alisema Malulu.
Aliongeza kuwa wananchi wanatakiwa kutumia vyoo pia wanatoa elimu ya jisni ya kujikinga na ugonjwa huo na kufanya ukaguzi  wa taasisi za umma, shule, nyumba za watumishi kuzuia upikwaji wa vyakula na uuzaji wa vinywaji na kuweka mazingira katika hali ya usafi.
Ugonjwa huo mwaka jana Agosti ulitokea mkoani Pwani na kuisha Desemba ambapo 293 waliambukizwa huku 98 walibainika kuwa na ugonjwa huo huku watu watatu walipoteza maisha.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment