Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la bomoa bomoa kwa watu
waliojenga kwenye hifadhi ya barabara ya Morogoro lililoanza Machi 8 mwaka huu
wilayani Kibaha mkoani Pwani limemkumba diwani wa kata ya Sofu Yusuph Mbonde ambaye
alijenga chumba cha biashara kwenye eneo
la Picha ya Ndege naye amekumbwa na kadhia hiyo.
Akizungumza na waandishi wa
habari kwenye eneo hilo diwani huyo alisema kuwa yeye naye alikuwa akifanya
biashara ya kujipatia riziki yake hapo na alijua bomoa bomoa hiyo ilikuwa ni
kwenye barabara mpya lakini akashangaa zoezi hilo kupita hadi barabara ya
zamani.
“Zoezi hili limeathiri watu wengi
na wote tuliojenga hapa na kufanyabiashara hapa tulipewa taarifa ya kubomoa
lakini nilijaribu kumwomba meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS)
kutuongezea muda lakini alisema watu wabomoe ambapo walitoa muda wa kubomoa na
watu wengi hawakuamini kama watabomolewa kwani taarifa zilikuwa zikitolewa bila
utekelezaji,” alisema Mbonde.
Alisema eneo ambalo limebomolewa
ni zaidi ya wafanyabiashara 200 ambako ni pamoja na eneo la soko na maduka ya
kuuza bidhaa mbalimbali pamoja na nyumba za makazi ya watu wanaokadiriwa
kufikia zaidi ya 1,000 kwa mitaa miwili ya Picha ya Ndege na Msufini ambayo ina
wakazi 13,000.
“TANROADS iliwataka watu
wanaotumia eneo la hifadhi ya barabara kutojenga vibanda vya kudumu lakini watu
walijenga vibanda vya kudumu pamoja na nyumba kama siyo sehemu ya muda
tunakubaliana na serikali hatuna jinsi tutatafuta eneo mbadala kwa ajili ya
kufanya biashara,” alisema Mbonde.
Naye Zakia Yusuph alisema kuwa zoezi hilo
limewaathiri sana hasa akinamama ambao walikuwa wakiendesha biashara zao za
kujipatia kipato ambapo wengine ni wajane na wana watoto ambao wanasoma.
Yusph alisema kuwa yeye yeye
alikopa mkopo benki wa shilingi milioni tano na hajui atazirudisha vipi na
kuiomba serikali kuwapatia eneo lingine kwa ajili ya kufanyia biashara zao za
kuwapatia kipato cha kuendeshea familia zao.
Kwa upande wake meneja wa
TANROADS Tumaini Sarakikya alisema kuwa zoezi hilo la bomoabomoa litadumu kwa
kipindi cha siku 15 ambapo wataondoa nyumba zote zilizojengwa kwenye hifadhi ya
barabara zilizo ndani ya mita 22.5 kila upande wa barabara kwa sheria ya
barabara ya mwaka 1930 baada ya kutoa notisi za mara kwa mara.
Sarakikya alisema kuwa zoezi hilo
ni la kudumu na litafanyika kwenye barabara zote zilizochini ya wakala kwenye
wilaya za mkoa huo ambapo kwa njia ya Morogoro zoezi hilo litaenda hadi Bwawani
mpakani mwa mikoa ya Pwani na Morogoro.
“Barabara ya Tanga watatekeleza
zoezi hilo hadi eneo la Manga mpakani mwa mikoa hiyo huku kwa upande wa
Bagamoyo litafanyika hadi Bunju mpakani mwa Pwani na Dar es Salaam na Kongowe
hadi Marendego kwa barabara iendayo mikoa ya Kusini,” alisema Sarakikya.
Akizungumzia kuhusu eneo la Maili
Moja ambako ndiyo makao makuu ya mkoa wa Pwani amesema kuwa eneo hilo litakuwa
la mwisho kutokana na halmashauri kuomba hadi pale watakapojenga Stendi na soko
ambavyo ndiyo chanzo kikuu cha mapato ya Halmashauri hiyo lakini mara ujenzi
huo utakapokamilika watabomoa ndani ya mita 100 kila upande.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment