Monday, March 14, 2016

CHUO CHA KILIMO NA MIFUGO CHAKABILIWA NA CHANGAMOTO YA ZANA ZA KILIMO

Na John Gagarini, Bagamoyo
CHUO cha Kilimo na Mifugo Kaole wilayani Bagamoyo kinachomilikiwa na Jumuiya ya wazazi Tanzania kinakabiliwa na upungufu wa madawa ya kujifunzia kwenye maabara pamoja na zana za kujifunzia hali ambayo inasababisha wanachuo kushindwa kujifunza kikamilifu.
Hayo yalisemwa Bagamoyo na Rais wa Chuo hicho Abas Kasusumo wakati wa ziara iliyofanywa na Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo ambao walitembelewa na Jumuiya hiyo wilaya ya Temeke kuangalia shughuli zinazofanywa na Jumuiya hiyo.
Kasusumo alisema kuwa changamoto hizo zinawasababisha washindwe kujifunza ipasavyo hali ambayo inawafanya wawe katika wakati mgumu kuelewa masomo yao.
“Tunaomba tusaidiwe vifaa vya kujifunzia kama vile matrekta ambayo hapa yapo lakini hayafanyi kazi hivyo tunaiomba serikali na Jumuiya ambayo ndiyo wamiliki wa chuo chetu ili tupate vifaa vya kujifunzia,” alisema Kasusumo.
Alisema kuwa kutokana na chuo hichi kuwa cha mifugo pia kuna changamoto ya ukosefu wa madawa mbalimbali kwa ajili ya kujifunzia masomo yetu kwani wakitoka hapo watategemewa kufanya kazi kutokana na walivyojifunza.
Kwa upande wake mwalimu mkuu wa chuo hicho Carthert Liwa alisema kuwa changamoto nyingine ni umeme ambapo wanatumia mita ya Luku ambayo haiwezi kumudu matumizi makubwa.
Liwa alisema kuwa changamoto zimekuwa nyingi kwani chuo hicho kimeanza upya baada ya kutokea matatizo hivyo wadau wanaombwa kujitokeza kukisaidia ili kiweze kutoa mafunzo kwa viwango vinavyotakiwa.
Naye mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo ambao ndiyo wamiliki wa chuo hicho Abdul Sharif alisema kuwa watahakikisha wanshirikiana na wadau wengine ili kuhakikisha kinatoa mafunzo kwa ubora.
Sharif alisema kuwa changamoto zilizotajwa ni za kweli na Jumuiya kwa kushirikiana na makao makuu watazifanyia kazi changamoto hizo ili elimu bora iweze kupatikana chuoni hapo. Chuo hicho kina wanafunzi 36 lakini uwezo wake ni wanachuo 600 ambapo hali hiyo ilitokana na kuchelewa kuandikisha wanachuo.
Mwisho.    
    
  
  

    

No comments:

Post a Comment