Friday, March 4, 2016

JESHI LA POLISI LAPEWA SIKU TATU KUMALIZA UHALIFU UNAOFANYWA NA WAVAMIZI

Na John Gagarini, Mkuranga
MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ametoa siku tatu kwa Jeshi la Polisi mkoani humo kuwakamata watu wanaojihusisha na vitendo vya kuwavamia kisha kuwapora viwanja na kufanya mauji kwa wakazi wa Kijiji cha Tambani kata ya Tambani wilaya ya Mkuranga.
Kutokana na tishio hilo limesababisha uongozi wa Kijiji hicho kushindwa kwenda baadhi ya maeneo wakihofia maisha yao kutokana na watu hao kutumia silaha mbalimbali za kijadi kwa ajili ya kufanya uhalifu.
Aliyasema hayo juzi Kijijini hapo alipotembelea kusikiliza kero hiyo ambayo imewafanya baadhi ya wakazi wa eneo hilo kuhama na kushindwa kufanya shughuli za maendeleo kwenye maeneo yao kutokana na hofu ya kuuwawa.   
“Natoa siku tatu kuanzia leo hakikisheni mmewakamata watu hao ambao kwa bahati majina mmnayo hakuna haja ya watu kushindwa kuishi kwa amani nchi hii haijafikia hatua ya watu kushindwa kukaa kwenye maeneo yao au viongozi kuogopa kwenda kwenye eneo lao la utawala,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa wananchi wa Kijiji hicho wamekwenda ofisini kwake zaidi ya mara tano wakilalamikia kundi hilo la watu ambao wametajwa kuwa ni kikundi cha watu 15 kabila la Kikurya ambao wanadaiwa kutokea eneo la Msongola wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam.
“Wananchi wamekuwa wakilalamika kuwa licha ya kulalamika kwa Jeshi hilo ngazi ya wilaya lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa ambapo hadi sasa watu watatu wameuwawa na kundi hilo la watu ambao ni wavamizi wa ardhi pia wamekuwa wakifanya vitendo vya uhalifu wa kuvunja nyumba, kuiba na kufanya vitendo vya ubakaji,” alisema Ndikilo.
“Inashangaza kuona kuwa mgogoro huu wa wavamizi ulianza tangu mwaka 2014 lakini hadi sasa hakuna hatua madhubuti ambazo zimechukuliwa za kudhibiti kundi hili ambalo ni hatari kwa wananchi ambao hawana hatia na kilio chao lazima kisikilizwe na si kuwaacha walalamike wakati viongozi wapo,” alisema Ndikilo.
Awali mwenyekiti wa Kijiji hicho Amir Mbamba alisema kuwa walishachukua hatua mbalimbali katika kuhakikisha suala hilo linakomeshwa kwa kulipeleka kwa mkuu wa wilaya lakini kundi hilo bado limeendelea kuendesha matukio hayo bila ya woga.
Mbamba alisema kuwa wananchi wake kutokana na kuona kuwa hawasikilizwi walikwenda kwa Waziri Mkuu pamoja Tume ya Haki za Binadamu ili waweze kusaidiwa tatizo lao na baadaye kwa mkuu wa mkoa ambaye leo umefika kujua ukweli wa tukio hili.
“Wananchi wamesema kuwa wataandamana hadi Ikulu kwa Rais endapo suala lao halitashughulikiwa ipasavyo hivyo kwa kuwa mkuu umekuja mwenyewe ukweli umeupata hatua madhubuti zitasaidia kumaliza mgogoro,” alisema Mbamba.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa watahakikisha kuwa watu hao wanakamatwa na amani itarudi kama ilivyokuwa zamani kwani watajipanga ili kukomesha uhalifu huo.
Mushongi alisema kuwa kwa kuanzia katika kulikabili suala hilo watashirikiana na kamati ya ulinzi na usalama ya Kijiji pamoja na mgambo ili nao washiriki kikamilifu katika kulifuatilia suala hilo ili watu waishi kwa amani bila ya hofu.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment