Saturday, March 26, 2016

MABASI YA MIKOANI 48 YAKUTWA NA MAKOSA MBALIMBALI

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya mabasi 48 ya abiria ya kwenda mikoani yamekutwa na makosa mbalimbali kufuatia zoezi la ukaguzi lillofanywa kwa ushirikiano baina ya Jeshi la Polisi na Mamlaka ya Usafirishaji Majini na Nchi Kavu (SUMATRA).  
Zoezi hilo lilifanywa kwenye Stendi Kuu ya Ubungo, Maili Moja na Chalinze kwa lengo la kudhibiti ajali pamoja na madereva wanaokiuka taratibu za usalama barabarani kwa mabasi hayo yaendayo mikoani .
Akizungumza na gazeti hili Kaimu Kamanda wa Kikosi cha Usalama barabarani nchini ACP Fortunatus Musilimu alisema kuwa zoezi hilo ambalo lilikuwa la kushtukiza litakuwa endelevu ili kuhakikisha ajali zinapungua na kuwaondolea usumbufu abiria.
Musilimu alisema kuwa waliyafanyia ukaguzi mabasi 169 na kuyabaini mabasi hayo 48 kuwa na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mwendokasi mabasi 24, kutofunga mikanda mabasi tisa, kuwazidishia nauli nane, ubovu basi moja, kukiuka ratiba basi moja na leseni basi moja.
“Pia tulimakamata dereva mmoja kwa kutumia kilevi ambapo alikuwa na kiwango cha juu cha ulevi cha 77.7 ambapo kwa kawaida kinatakiwa kuwa 00.8 kwa mujibu sheria hali iliyosababisha dereva huyo kushushwa na kupelekwa rumande,” alisema Musilimu.
Alisema kuwa ukaguzi huo unandelea kote nchi ambapo tayari makamanda wa usalama barabarani mikoani wameshapewa maagizo ya kufanya ukaguzi wa mabasi kwani ukaguzi hauwezi kuyakagua mabasi yote kutokana na eneo la ukaguzi kuwa dogo hali ambayo inawafanya wafanyie ukaguzi mabasi matano matano kwa wakati mmoja huku mengine yakiendelea na safari.
Aidha alisema kuwa mbali ya kukagua mabasi hayo pia walikagua malori ya mchanga 13 na kuyakuta na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mwendo kasi magari saba, mabovu matano, kuyapita magari mengine pasipo kuzingatia sheria.
Aliwataka abiria kutoa taarifa kwenye vyombo husika kwa madereva ambao wanaoendesha magari kwa mwendo wa kasi pia wasiwashabikie kwani ni moja ya vyanzo vya ajali za barabarani ambazo zinasababisha vifo vya watu wengi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment