Saturday, March 19, 2016

WAFANYABIASHARA WA NAFAKA WAIOMBA HALMASHAURI KUWAONDOLEA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA wa jumla na rejareja wa mazao ya nafaka kwenye soko la maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji huo kuondoa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la kilogramu 100 la nafaka linaloingia sokoni hapo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa umoja wa wauzaji wa mazao ya nafaka sokoni hapo Ramadhan Maulid alisema kuwa sheria hiyo ya utozaji wa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la la nafaka lenye uzito wa kilogramu 100 ina kinzana na sheria mama ambayo inataka ushuru ukatwe mara moja tu.
Maulid alisema kuwa wao wanaponunua nafaka hizo huko mikoani wanatozwa ushuru wa shilingi kati ya 2,000 hadi 5,000 kutegemeana na Halmashauri hivyo wanashangaa kutozwa tena mara wanapofikisha mzigo sokoni hapo.
“Kututoza ushuru tena ni sawa na kuwatoza ushuru mara mbili kwani hata sheria ndogo hiyo iliyowekwa na Halmashauri haikuwashirikisha wao kama watekelezaji wa sheria hiyo ambayo ilipitishwa mwaka 2007 na kutakiwa kuanza kutumika mwaka 2008 lakini haikuwahi kutumika licha ya kwamba kwa miaka ya nyuma ilikuwa ikitumika,” alisema Maulid.
Alisema kuwa waliletewa taarifa ya kutakiwa kulipa ushuru huo hivi karibuni lakini walijaribu kuonana na viongoizi wa halmashauri bila ya mafanikio ili kuzungumzia suala hilo ambalo kwao ni moja ya ushuru ambao ni kero.
“Mbali ya kutakiwa kulipia kiasi hicho pia gharama nyingine ni pamoja na kulipia Kizimba kiasi cha shilingi 9,000, Ardhi 3,000 na mlinzi 6,000 ambazo hulipa kila mwezi hivyo malipo hayo ni sawa na kuwaongezea mzigo wa ushuru,” alisema Maulid.
Aidha alisema kuwa kwa sasa wanawasiliana na wanasheria ili kutoa tafsiri ya sheria hizo mbili kati ya sheria mama na sheria ndogo ya Halmashauri ambapo inaonekana kama zinakinzana na kuleta mkanganyiko kwao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa soko hilo Ally Gonzi alisema kuwa tangu walipoletewa sheria hiyo ndogo ambayo ilipitishwa kwenye baraza la madiwani walijaribu kufanya vikao mbalimbali na Halmashauri ili kuangalia namna ya kupunguza ushuru huo lakini ilishindikana ambapo Halmashauri iliwaambia kuwa kama wanataka uondolewe basi wafuate taratibu.
Naye mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Gladdys Dyamvunye alisema kuwa wafanyabiashara hao wanapaswa kulipa ushuru huo kwani uko kisheria na tayari vyombo vya sheria vimetoa siku 14 kwa wafanyabiashara hao kulipa na endapo hawatalipa watashitakiwa.
Mwisho.


No comments:

Post a Comment