Friday, March 25, 2016

RC AUNDA TUME KUCHUNGUZA KIWANDA JUU YA HAKI ZA WAFANYAKAZI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ameunda Tume kutoka idara ya kazi ya mkoa huo kutembelea kiwanda cha Hong Yu Steel cha kuzalisha nondo kilichopo wilayani Kibaha kwa kushindwa kuzingatia masharti ya uendeshaji wa kiwanda na maslahi ya wafanyakazi.
Aliunda tume hiyo ya watu watatu itakayofanya kazi kwa wiki moja kufuatilia malalamiko hayo ya wafanyakazi kwa lengo la kuleta uwajibikaji kwa pande zote mbili katia ya wafanyakazi na wamiliki hao baada ya malalamiko kuzidi na kufanya ziara kujionea hali halisi.
Ndikilo alifikia hatua hiyo baada ya kupata malalamiko toka kwa wafanyakazi kuwa wamiliki wa kiwanda hicho hawajali usalama kazini kwa wafanyakazi wao kwa kushindwa kuweka vifaa vya kuwalinda kutokana na mazingira wanayofanyia kazi ambayo ni hatarishi kwa maisha yao.
“Tumesikia wafanyakazi na tumeona wafanyakazi wakifanya kazi huku wakiwa hawana vifaa vya kufanyia kazi kama vile baadhi yao hawajavaa kofia ngumu, gloves na mabuti kwa ajili ya kujikinga na hatari zinazoweza kujitokeza wakati wa kufanya kazi,” alisema Ndikilo.
Alisema wafanyakazi wamelalamikia mambo mengi ikiwa ni pamoja na mshahara mdogo, kutokuwa na mikataba ya kazi, kutolipwa masaa ya ziada, kukatwa mishahara mara wanaposhindwa kwenda kazini kutokana na kuumwa au kuumia kazini, huduma ya kwanza kuchelewa pamoja na kutokuwa na mapumziko hata nyakati za sikukuu na mwisho wa wiki.
“Tumeona kuna matatizo mengi hivyo itaundwa tume kwa ajili ya kukaa na uongozi kwa ajili ya kurekebisha kasoro zilizopo kwa kuzingatia sheria za kazi kwani kila mtu anamtegemea mwenzake kati ya mwajiri na mfanyakazi hivyo hakuna sababu ya upande mmoja kumnyanysa mwenzake,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa tume hiyo itatembelea vitengo vyote kwa kuonana na viongozi wa vitengo husika na baadaye kukaa na uongozi ili kuangalia namna ya kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya wafanyakazi.
Kwa upande wake kaimu ofisa kazi wa mkoa Swalehe Njoma alisema kuwa haki nyingi za wafanyakazi zimevunjwa hivyo kuna haja ya kurekebisha na kuweka mazingira bora ya kazi ili haki iweze kupatikana kwani malalamiko ni mengi.
Njoma alisema kuwa moja ya haki za mfanyakazi ni kuwa na muda wa mapumziko na hata kama atafanya kazi kwa masaa ya ziada lazima alipwe na mfanyakazi anapoumwa au kuumia kazini hapaswi kukatwa fedha kutokana na kushindwa kwenda kazini kutokana na kujiuguza.
Naye ofisa mwajiri wa kiwanda hicho Asantemungu Filbert alikiri kuwepo na matatizo ambapo alisema kuwa yeye ni mgeni na hana muda mrefu ila kwa mtangulizi wake hakuweza kuweka mazingira mazuri ya wafanyakazi.
Filbert alisema kuwa tayari ameandaa utaratibu wa kushughulikia kero za wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi ili kukabiliana na changamoto zilizopo na kufanya utendaji kazi kuwa mzuri.
Mwisho.   

No comments:

Post a Comment