Thursday, March 24, 2016

WAWILI WASHIKILIWA KWA UTAPELI WAWILI WAKIMBIA

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kutaka kumtapeli mtu mmoja kiasi cha shilingi milioni tatu kwa kumuuzia madini aina ya Almasi ambayo ni bandia.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kamanda wa polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao ambao walikuwa wanne wengine wawili walifanikiwa kukimbia walikamatwa baada ya kutaka kukimbia kutokana na mlalamikaji kupiga kelele ya kuomba msaada.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo limetokea juzi eneo la CCM Mkoani wilayani Kibaha majira ya saa 3:30 asubuhi baada ya mlalamikaji kutoka kuchukua fedha kwenye benki ya NMB Tawi la Kibaha.
“Mlalamikaji mara baada ya kuchukua fedha alikutana na watuhumiwa hao ambapo waliongea naye na kumwambia kuwa wanauza madini aina ya Almasi ambapo walikubalina na akawakabidhi fedha hizo,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa watuhumiwa hao wakiwa kwenye gari aina ya Primio lenye namba za usajili T 668 DFY walianza kuondoka lakini mlalamikaji akagundua kuwa madini yale si halisi na kuanza kupiga kelele za wezi kuomba msaada ndipo waendesha pikipiki walipoanza kuwafukuza na baadaye polisi nao wakatokea na kuwakamata.
“Watuhumiwa hao baada ya kuona wamezingirwa walikimbia hata hivyo wawili walikamatwa na wengine wawili walifanikiwa kutokomea kusiko julikana nab ado tunaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine ili kuwafikisha mahakamani kujibu tuhuma hizo,” alisema Mushongi.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mwantumu Juma maarufau kama Hawa, Fidelis Buberwa au Finas Barongo ambao wanashikiliwa kutokana na tukio hilo ambapo gari hilo linashikiliwa.
Kufuatia tukio hilo kamanda aliwataka wananchi kutokubali kuuziwa madini mikononi badala yake waende sehemu husika ambazo ziko rasmi kwa ajili ya uuzaji wa madini ili kuepukana na watu kama hao.
Mwisho

No comments:

Post a Comment