Friday, March 25, 2016

SUMATRA NA POLISI WAKAMATA MABASI

Na John Gagarini, Kibaha
MAMLAKA ya Usafirishaji Majini na nchi kavu SUMATRA kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini wamefanya operesheni ya kushtukiza ya kukagua mabasi yaendayo mikoani na kubaini makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya madereva kutumia vilevi na kuwzidishia nauli abiria.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha wakati wa zoezi hilo Mkurugenzi wa SUMATRA, Johnsen Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanywa ili kuwadhibiti wamiliki pamoja na madereva ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.
Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanikiwa kwani wameweza kukamata makosa kadhaa ambayo mengine ni ya barabarani na mengine ni ya kuwazidishia nauli abiria jambo ambalo ni kosa kisheria ambapo mabasi yaliyofanya makosa wamiliki wake watafikishwa mahakamani.
“Tumefanikiwa kumkamata dereva mmoja alikutwa akiwa ametumia kilevi na tulimkamata na kulizuia basi hilo hadi walipoleta dereva mwingine kwa ajili ya safari  jambo ambalo ni la hatari kwa usalama wa abiria,” alisema Kahatano.
Alisema kuwa mabasi sita yalikamatwa yakiwa yamezidisha nauli ambpao abiria waliokuwa wakienda Moshi walkatiwa nauli ya kwenda Arusha ambayo ni shilingi 33,000 huku nauli halali kwa watu wanaoshukia Moshi ni shilingi 28,500.
“Mabasi yaliyowazidishia abiria walirudishiwa nauli zao kama taratibu zinavyoonyesha na hili ni kosa kisheria na abiria wanapaswa kulipa nauli halali ambazo zimepitishwa kisheria na wanapaswa kwenda kulalamika endapo watabaini wamezidishiwa,” alisema Kahatano.
Naye Kaimu Kamishna wa Usalama Barabarani Fortunatus Musilimu alisema kuwa abiria nao ni wadau muhimu katika vita ya kupambana na madereva au wamiliki wanaokiuka taratibu za usalama barabarani na kupunguza ajali hivyo wanapaswa kutoa taarifa kwao ili hatua ziweze kuchukuliwa.
Musilimu alisema kuwa watu wanataka kuishi na maendeleo si kukatishwa uhai kutokana na ajali ambazo zinaweza kuzuilika na kutoa taarifa polisi kwa kutumia njia ya simu ambazo ziko kwenye mabasi yote lengo likiwa ni kupunguza ajali.
Mwisho.     


No comments:

Post a Comment