Wednesday, March 30, 2016

MABONDIA KUWANIA MKANDA TPBO KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
MABONDIA Said Seleman Ambokile Chusa wajijini Dar es Salaam leo wanatarajia kupambana kwenye pambano la ngumi la kuwania ubingwa TPBO uzito wa kati pambano litakalo pigwa kwenye ukumbi wa Container Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha moja ya wasimamizi wa pambano hilo ambaye ni mwalimu wa ngumi Gordon Tambwe maarufu kama Mawe alisema kuwa pambano hilo litakuwa kali na la kuvutia.
Mawe alisema kuwa lengo la kufanya pambano hilo Kibaha ni kuhamasisha mchezo huo mikoani pia kuinua vipaji kwa mabondia wa mikoani ili nao waweze kuonyesha uwezo wao.
“Tumeleta pambano hili Kibaha ili kuhamasisha mchezo wa ngumi sehemu mbalimbali mikoani kwani michezo ni ajira na ngumi zimewasaidia vijana wengi kujiajiri kupitia mchezo huo,” alisema Mawe.
Aidha alisema kuwa mabondia hao watapigana raundi 10 na pia kutakuwa na mapambano ya utangulizi ambayo yatausisha mabondia kutoka mkoa wa Pwani na wageni wao kutoka Jijini Dar es Salaam.
Kwa upande wake Seleman alisema kuwa amejiandaa ipasavyo na anatarajia kummaliza mapema mpinzani wake kwa KO kwani hatakuwa na muda wa kupoteza katika kumaliza pambano hilo.
Naye Chusa alisema kuwa amekwenda Kibaha kwa ajili ya kutafuta ubingwa na si kutalii na anatarajia kumpiga mpinzani wake ili kuwapa raha wapenzi wake hivyo wasiwe na wasiwasi. Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa diwani wa Viti maalumu Selina Wilson.

Mwisho.

Saturday, March 26, 2016

MABASI YA MIKOANI 48 YAKUTWA NA MAKOSA MBALIMBALI

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya mabasi 48 ya abiria ya kwenda mikoani yamekutwa na makosa mbalimbali kufuatia zoezi la ukaguzi lillofanywa kwa ushirikiano baina ya Jeshi la Polisi na Mamlaka ya Usafirishaji Majini na Nchi Kavu (SUMATRA).  
Zoezi hilo lilifanywa kwenye Stendi Kuu ya Ubungo, Maili Moja na Chalinze kwa lengo la kudhibiti ajali pamoja na madereva wanaokiuka taratibu za usalama barabarani kwa mabasi hayo yaendayo mikoani .
Akizungumza na gazeti hili Kaimu Kamanda wa Kikosi cha Usalama barabarani nchini ACP Fortunatus Musilimu alisema kuwa zoezi hilo ambalo lilikuwa la kushtukiza litakuwa endelevu ili kuhakikisha ajali zinapungua na kuwaondolea usumbufu abiria.
Musilimu alisema kuwa waliyafanyia ukaguzi mabasi 169 na kuyabaini mabasi hayo 48 kuwa na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mwendokasi mabasi 24, kutofunga mikanda mabasi tisa, kuwazidishia nauli nane, ubovu basi moja, kukiuka ratiba basi moja na leseni basi moja.
“Pia tulimakamata dereva mmoja kwa kutumia kilevi ambapo alikuwa na kiwango cha juu cha ulevi cha 77.7 ambapo kwa kawaida kinatakiwa kuwa 00.8 kwa mujibu sheria hali iliyosababisha dereva huyo kushushwa na kupelekwa rumande,” alisema Musilimu.
Alisema kuwa ukaguzi huo unandelea kote nchi ambapo tayari makamanda wa usalama barabarani mikoani wameshapewa maagizo ya kufanya ukaguzi wa mabasi kwani ukaguzi hauwezi kuyakagua mabasi yote kutokana na eneo la ukaguzi kuwa dogo hali ambayo inawafanya wafanyie ukaguzi mabasi matano matano kwa wakati mmoja huku mengine yakiendelea na safari.
Aidha alisema kuwa mbali ya kukagua mabasi hayo pia walikagua malori ya mchanga 13 na kuyakuta na makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mwendo kasi magari saba, mabovu matano, kuyapita magari mengine pasipo kuzingatia sheria.
Aliwataka abiria kutoa taarifa kwenye vyombo husika kwa madereva ambao wanaoendesha magari kwa mwendo wa kasi pia wasiwashabikie kwani ni moja ya vyanzo vya ajali za barabarani ambazo zinasababisha vifo vya watu wengi.
Mwisho.

Friday, March 25, 2016

RC AUNDA TUME KUCHUNGUZA KIWANDA JUU YA HAKI ZA WAFANYAKAZI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ameunda Tume kutoka idara ya kazi ya mkoa huo kutembelea kiwanda cha Hong Yu Steel cha kuzalisha nondo kilichopo wilayani Kibaha kwa kushindwa kuzingatia masharti ya uendeshaji wa kiwanda na maslahi ya wafanyakazi.
Aliunda tume hiyo ya watu watatu itakayofanya kazi kwa wiki moja kufuatilia malalamiko hayo ya wafanyakazi kwa lengo la kuleta uwajibikaji kwa pande zote mbili katia ya wafanyakazi na wamiliki hao baada ya malalamiko kuzidi na kufanya ziara kujionea hali halisi.
Ndikilo alifikia hatua hiyo baada ya kupata malalamiko toka kwa wafanyakazi kuwa wamiliki wa kiwanda hicho hawajali usalama kazini kwa wafanyakazi wao kwa kushindwa kuweka vifaa vya kuwalinda kutokana na mazingira wanayofanyia kazi ambayo ni hatarishi kwa maisha yao.
“Tumesikia wafanyakazi na tumeona wafanyakazi wakifanya kazi huku wakiwa hawana vifaa vya kufanyia kazi kama vile baadhi yao hawajavaa kofia ngumu, gloves na mabuti kwa ajili ya kujikinga na hatari zinazoweza kujitokeza wakati wa kufanya kazi,” alisema Ndikilo.
Alisema wafanyakazi wamelalamikia mambo mengi ikiwa ni pamoja na mshahara mdogo, kutokuwa na mikataba ya kazi, kutolipwa masaa ya ziada, kukatwa mishahara mara wanaposhindwa kwenda kazini kutokana na kuumwa au kuumia kazini, huduma ya kwanza kuchelewa pamoja na kutokuwa na mapumziko hata nyakati za sikukuu na mwisho wa wiki.
“Tumeona kuna matatizo mengi hivyo itaundwa tume kwa ajili ya kukaa na uongozi kwa ajili ya kurekebisha kasoro zilizopo kwa kuzingatia sheria za kazi kwani kila mtu anamtegemea mwenzake kati ya mwajiri na mfanyakazi hivyo hakuna sababu ya upande mmoja kumnyanysa mwenzake,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa tume hiyo itatembelea vitengo vyote kwa kuonana na viongozi wa vitengo husika na baadaye kukaa na uongozi ili kuangalia namna ya kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya wafanyakazi.
Kwa upande wake kaimu ofisa kazi wa mkoa Swalehe Njoma alisema kuwa haki nyingi za wafanyakazi zimevunjwa hivyo kuna haja ya kurekebisha na kuweka mazingira bora ya kazi ili haki iweze kupatikana kwani malalamiko ni mengi.
Njoma alisema kuwa moja ya haki za mfanyakazi ni kuwa na muda wa mapumziko na hata kama atafanya kazi kwa masaa ya ziada lazima alipwe na mfanyakazi anapoumwa au kuumia kazini hapaswi kukatwa fedha kutokana na kushindwa kwenda kazini kutokana na kujiuguza.
Naye ofisa mwajiri wa kiwanda hicho Asantemungu Filbert alikiri kuwepo na matatizo ambapo alisema kuwa yeye ni mgeni na hana muda mrefu ila kwa mtangulizi wake hakuweza kuweka mazingira mazuri ya wafanyakazi.
Filbert alisema kuwa tayari ameandaa utaratibu wa kushughulikia kero za wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi ili kukabiliana na changamoto zilizopo na kufanya utendaji kazi kuwa mzuri.
Mwisho.   

SUMATRA NA POLISI WAKAMATA MABASI

Na John Gagarini, Kibaha
MAMLAKA ya Usafirishaji Majini na nchi kavu SUMATRA kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini wamefanya operesheni ya kushtukiza ya kukagua mabasi yaendayo mikoani na kubaini makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya madereva kutumia vilevi na kuwzidishia nauli abiria.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha wakati wa zoezi hilo Mkurugenzi wa SUMATRA, Johnsen Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanywa ili kuwadhibiti wamiliki pamoja na madereva ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.
Kahatano alisema kuwa operesheni hiyo imefanikiwa kwani wameweza kukamata makosa kadhaa ambayo mengine ni ya barabarani na mengine ni ya kuwazidishia nauli abiria jambo ambalo ni kosa kisheria ambapo mabasi yaliyofanya makosa wamiliki wake watafikishwa mahakamani.
“Tumefanikiwa kumkamata dereva mmoja alikutwa akiwa ametumia kilevi na tulimkamata na kulizuia basi hilo hadi walipoleta dereva mwingine kwa ajili ya safari  jambo ambalo ni la hatari kwa usalama wa abiria,” alisema Kahatano.
Alisema kuwa mabasi sita yalikamatwa yakiwa yamezidisha nauli ambpao abiria waliokuwa wakienda Moshi walkatiwa nauli ya kwenda Arusha ambayo ni shilingi 33,000 huku nauli halali kwa watu wanaoshukia Moshi ni shilingi 28,500.
“Mabasi yaliyowazidishia abiria walirudishiwa nauli zao kama taratibu zinavyoonyesha na hili ni kosa kisheria na abiria wanapaswa kulipa nauli halali ambazo zimepitishwa kisheria na wanapaswa kwenda kulalamika endapo watabaini wamezidishiwa,” alisema Kahatano.
Naye Kaimu Kamishna wa Usalama Barabarani Fortunatus Musilimu alisema kuwa abiria nao ni wadau muhimu katika vita ya kupambana na madereva au wamiliki wanaokiuka taratibu za usalama barabarani na kupunguza ajali hivyo wanapaswa kutoa taarifa kwao ili hatua ziweze kuchukuliwa.
Musilimu alisema kuwa watu wanataka kuishi na maendeleo si kukatishwa uhai kutokana na ajali ambazo zinaweza kuzuilika na kutoa taarifa polisi kwa kutumia njia ya simu ambazo ziko kwenye mabasi yote lengo likiwa ni kupunguza ajali.
Mwisho.     


Thursday, March 24, 2016

WAWILI WASHIKILIWA KWA UTAPELI WAWILI WAKIMBIA

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kutaka kumtapeli mtu mmoja kiasi cha shilingi milioni tatu kwa kumuuzia madini aina ya Almasi ambayo ni bandia.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kamanda wa polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao ambao walikuwa wanne wengine wawili walifanikiwa kukimbia walikamatwa baada ya kutaka kukimbia kutokana na mlalamikaji kupiga kelele ya kuomba msaada.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo limetokea juzi eneo la CCM Mkoani wilayani Kibaha majira ya saa 3:30 asubuhi baada ya mlalamikaji kutoka kuchukua fedha kwenye benki ya NMB Tawi la Kibaha.
“Mlalamikaji mara baada ya kuchukua fedha alikutana na watuhumiwa hao ambapo waliongea naye na kumwambia kuwa wanauza madini aina ya Almasi ambapo walikubalina na akawakabidhi fedha hizo,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa watuhumiwa hao wakiwa kwenye gari aina ya Primio lenye namba za usajili T 668 DFY walianza kuondoka lakini mlalamikaji akagundua kuwa madini yale si halisi na kuanza kupiga kelele za wezi kuomba msaada ndipo waendesha pikipiki walipoanza kuwafukuza na baadaye polisi nao wakatokea na kuwakamata.
“Watuhumiwa hao baada ya kuona wamezingirwa walikimbia hata hivyo wawili walikamatwa na wengine wawili walifanikiwa kutokomea kusiko julikana nab ado tunaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine ili kuwafikisha mahakamani kujibu tuhuma hizo,” alisema Mushongi.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mwantumu Juma maarufau kama Hawa, Fidelis Buberwa au Finas Barongo ambao wanashikiliwa kutokana na tukio hilo ambapo gari hilo linashikiliwa.
Kufuatia tukio hilo kamanda aliwataka wananchi kutokubali kuuziwa madini mikononi badala yake waende sehemu husika ambazo ziko rasmi kwa ajili ya uuzaji wa madini ili kuepukana na watu kama hao.
Mwisho

MMOJA AFA 10 WALAZWA KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja amefariki dunia wilayani Kibaha mkoani Pwani kutokana na ugonjwa wa Kipindupindu huku wengine 10  wakiwa wanaugua ugonjwa huo kwenye hospitali mbalimbali wilayani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha Ofisa afya wa mkoa wa Pwani Simon Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uligundulika Aprili 17 mwaka huu katika Shule ya Sekondari ya Ruvu wilayani Kibaha.
Malulu alisema kuwa ugonjwa huo uliwakumba wanafunzi 21 wa shule hiyo ambapo awali waliona kuwa ni mchafuko wa matumbo kwani wanafunzi hao walikuwa wakiharisha.
“Baada ya kuona hali imezidi kuwa mbaya kwa wanafunzi walimu waliwapeleka wanafunzi kwenye Zahanati ya Kijiji cha hicho cha Ruvu Station na kuchukua sampuli ya kinyesi kwa wanafunzi tisa ambapo mmoja aligundulika kuwa na ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Alisema kuwa baada ya kubaini hilo ilibidi mkuu wa wilaya aifunge shule hiyo ili kuwaepusha wanafunzi zaidi kuambukizwa ugonjwa huo ambapo wanafunzi waliokumbwa na ugonjwa huo wengi walikuwa ni wanafunzi wakike ambao wako bweni.
“Hadi sasa kwenye Zahanati ya Ruvu kuna wagonjwa wanne, Zahanati ya Dutumi watatu na Mlandizi wako watatu ambao wanendelea kupatiwa matibabu ya ugonjwa huo,” alisema Malulu.
Aidha alisema kuwa chanzo cha kuenea ugonjwa huo ni kinyesi ambacho kinatokana na watu wengi kujisaidia kwenye Mto Ruvu ambapo maji yake wanafunzi na wananchi wa Kijiji cha Ruvu Station.
“Tumechukua hatua za kufungua kambi kwenye maeneo yote yenye ugonjwa ikiwa ni pamoja na Ruvu Station, Dutumi na Mlandizi pia kuwaptia dawa ya kusafishia maji ili kutibu maji hayo ambayo wananchi wamekuwa wakiyatumia bila ya kuyachemsha,” alisema Malulu.
Aliongeza kuwa wananchi wanatakiwa kutumia vyoo pia wanatoa elimu ya jisni ya kujikinga na ugonjwa huo na kufanya ukaguzi  wa taasisi za umma, shule, nyumba za watumishi kuzuia upikwaji wa vyakula na uuzaji wa vinywaji na kuweka mazingira katika hali ya usafi.
Ugonjwa huo mwaka jana Agosti ulitokea mkoani Pwani na kuisha Desemba ambapo 293 waliambukizwa huku 98 walibainika kuwa na ugonjwa huo huku watu watatu walipoteza maisha.
Mwisho.

Saturday, March 19, 2016

SHULE YAKABILIWA NA UHABA WA WALIMU INA WALIMU WAWILI TU

Na John Gagarini, Bagamoyo
MAZINGIRA magumu yanayokikabili Kijiji cha Kitame Kata ya makurunge wilayani bagamoyo mkoani Pwani yamesababisha walimu walimu wawili wanaofundisha shule hiyo kufundisha kwa siku 90 kwa mwaka mzima.   
Kutokana na shule hiyo kuwa kwenye mazingira magumu walimu wengi wamekuwa hawako tayari kufundisha shule hiyo yenye wanafunzi 51 wa kuanzia darasa la kwanza hadi la saba ambayo ni idadi ndogo kutokana na mazingira hayo.
Akizungumza mbele ya Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa, moja ya wakazi wa Kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Adam Rashid alisema kuwa moja ya changamoto zinazowakabili ni pamoja na kutokuwa na usafiri wa uhakika kutokana na ubovu wa miundombinu.
“Usafiri wa kutokana Kijijini hapa hadi makao makuu ya wilaya ni kilometa 54 kwa njia ya barabara na usafiri wake ni pikipiki na gharama yake ni kiasi cha shilingi 50,000 huku ule wa kutumia njia ya bahari mitumbwi gharama yake ni kiasi cha shilingi 60,000 kwenda na kurudi,”  alisema Rashid.
Alisema gharama hizo ni kubwa sana ajambo ambalo linawafanya walimu washindwe kwenda kufundisha kutokana na mazingira hayo ambapo walimu hao wawili wamekuwa wakipokezana kufundisha madarasa hayo.
“Wanafunzi wanafundishwa siku chache kutokana na walimu hao wakati mwingine kutofika kabisa shuleni hali ambayo inawakatisha tamaa wanafunzi na kusababisha kuwa na idadi ndogo ya wanafunzi wanaosoma shuleni hapo,” alisema Rashid.
Aidha aliiomba serikali kusaidia kupatikana kwa walimu ili kukabiliana na hali ya wanafunzi hao kukosa masomo na kusababisha elimu kuwa duni hali ambayo itatoa matokeo mabaya kwa wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Makurunge Kabile Paulo alisema kuwa walimu wengi wanashindwa kwenda kufundisha shuleni hapo kutokana na mazingira magumu kwani hakuna huduma muhimu za jamii hivyo kushindwa kukaa huko.
Paulo alisema kuwa baadhi ya huduma ambazo hazipo ni pamoja na huduma ya afya kwani hakuna zahanati na huduma nyingine muhimu ambazo huwabidi kuzifuata Bagamoyo au maeneo mengine jambo ambalo limekuwa likiwagharimu.
Naye mbunge wa Jimbo hilo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa alisema kuwa kweli hiyo ni changamoto ambayo inawakabili wakazi na walimu hao lakini kwa kushirikiana na diwani wa kata hiyo watahakikisha wanaitatua.
Dk Kawambwa alisema kuwa Halmashauri itafanya mgao wa walimu na ataiomba itoe kipaumbele kwa shule hiyo kwa kuwapatia walimu ili waweze kwenda huko na kuongeza nguvu ya ufundishaji kwenye shule hiyo ambayo iko pembezoni na kuwataka vijana waliosoma vyuo vya ualimu na ni wenyeji wa kata hiyo kujitolea kwenda kufundisha kama njia mbadala ya upungufu huo wa walimu.
Mwisho.  
  

VIJANA KUENDESHA MRADI WA SAMAKI MTAA WA KIBONDENI

Na John Gagarini, Kibaha
MTAA wa Kibondeni Kata ya Mkuza wilayani Kibaha utawapatia mafunzo ya ufugaji wa samaki vijana 40 wa mtaa huo ili waendeshe mradi wa ufugaji wa samaki kwenye bwawa la mtaa ambalo limerudishwa baada ya kuuzwa kimakosa kwa mtu binafsi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Hamis Mwarizo alisema kuwa vijana hao watapewa mafunzo hayo kutoka ofisi ya kata ili vijana waweze kujua namna ya kufuga samaki.
Mwarizo alisema kuwa mafunzo hayo yatatolewa kwa vijana ambao watakuwa wameunda vikundi ambavyo vitaendesha mradi huo ambao utatoa ajira kwa vijana hao na watakuwa wakipeana zamu ya kusimamia.
“Lengo la mradi huo ni kuongeza ajira kwa vijana ambapo asilimia 70 ya mapato yatakwenda kwenye kikundi na asilimia 30 yatakwenda kwenye mtaa kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo ya jamii ya mtaa wetu,” alisema Mwarizo.
Alisema kuwa kwa sasa tayari vijana 16 wameshapatikana kwa ajili ya kuanzisha kikundi cha mwanzo na wengine wanaendelea kujiandikisha na baadaye kikundi hicho kitasajiliwa ili kitambulike kisheria baada ya mradi huo kupitishwa ana wananchi kwenye mkutano mkuu wa mtaa.
“Kundi la kwanza litaendesha kwa kipindi cha miaka 10 na baadaye litapewa kundi lingine kwa ajili ya kuendeleza mradi huo ambao mbali ya kuwapatia vijana ajira pia utaipatia jamii ya eneo hilo na maeneo jirani lishe kwa ajili ya kuboresha afya,” alisema Mwarizo.
Katika hatua nyingine alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na taratibu za kulipima eneo la bwawa hilo ili kujua mipaka yake halisi ambapo maji yake baada ya kupimwa yalibainika kuwa hayafai kwa kunywa kwani yana viluilui ambavyo vinaweza kusababisha maradhi ya ugonjwa wa tumbo hivyo yatatumika kwa ajili ya kulimia bustani pamoja na kufulia.
Mwisho.


WAFANYABIASHARA WA NAFAKA WAIOMBA HALMASHAURI KUWAONDOLEA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA wa jumla na rejareja wa mazao ya nafaka kwenye soko la maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji huo kuondoa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la kilogramu 100 la nafaka linaloingia sokoni hapo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa umoja wa wauzaji wa mazao ya nafaka sokoni hapo Ramadhan Maulid alisema kuwa sheria hiyo ya utozaji wa ushuru wa shilingi 1,000 kwa gunia la la nafaka lenye uzito wa kilogramu 100 ina kinzana na sheria mama ambayo inataka ushuru ukatwe mara moja tu.
Maulid alisema kuwa wao wanaponunua nafaka hizo huko mikoani wanatozwa ushuru wa shilingi kati ya 2,000 hadi 5,000 kutegemeana na Halmashauri hivyo wanashangaa kutozwa tena mara wanapofikisha mzigo sokoni hapo.
“Kututoza ushuru tena ni sawa na kuwatoza ushuru mara mbili kwani hata sheria ndogo hiyo iliyowekwa na Halmashauri haikuwashirikisha wao kama watekelezaji wa sheria hiyo ambayo ilipitishwa mwaka 2007 na kutakiwa kuanza kutumika mwaka 2008 lakini haikuwahi kutumika licha ya kwamba kwa miaka ya nyuma ilikuwa ikitumika,” alisema Maulid.
Alisema kuwa waliletewa taarifa ya kutakiwa kulipa ushuru huo hivi karibuni lakini walijaribu kuonana na viongoizi wa halmashauri bila ya mafanikio ili kuzungumzia suala hilo ambalo kwao ni moja ya ushuru ambao ni kero.
“Mbali ya kutakiwa kulipia kiasi hicho pia gharama nyingine ni pamoja na kulipia Kizimba kiasi cha shilingi 9,000, Ardhi 3,000 na mlinzi 6,000 ambazo hulipa kila mwezi hivyo malipo hayo ni sawa na kuwaongezea mzigo wa ushuru,” alisema Maulid.
Aidha alisema kuwa kwa sasa wanawasiliana na wanasheria ili kutoa tafsiri ya sheria hizo mbili kati ya sheria mama na sheria ndogo ya Halmashauri ambapo inaonekana kama zinakinzana na kuleta mkanganyiko kwao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa soko hilo Ally Gonzi alisema kuwa tangu walipoletewa sheria hiyo ndogo ambayo ilipitishwa kwenye baraza la madiwani walijaribu kufanya vikao mbalimbali na Halmashauri ili kuangalia namna ya kupunguza ushuru huo lakini ilishindikana ambapo Halmashauri iliwaambia kuwa kama wanataka uondolewe basi wafuate taratibu.
Naye mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Gladdys Dyamvunye alisema kuwa wafanyabiashara hao wanapaswa kulipa ushuru huo kwani uko kisheria na tayari vyombo vya sheria vimetoa siku 14 kwa wafanyabiashara hao kulipa na endapo hawatalipa watashitakiwa.
Mwisho.


RAS PWANI KUFUNGUA MAFUNZO YA MPIRA WA WAVU

Na John Gagarini, Kibaha
KATIBU Tawala (RAS) Mkoa wa Pwani Mgeni Baruani anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa mafunzo ya walimu wa mchezo wa wavu Volleyball yatakayoanza Machi 24 hadi Aprili Mosi mwaka huu kwenye viwanja vya shule ya Msingi Kibaha.
Akizungumza na waandishi wa habari katibu wa chama cha mchezo huo mkoani Pwani (COREVA) Lonjin Mzava alisema kuwa wanatarajia mafunzo hayo yatawahusisha walimu wa mchezo huo kwa shule za msingi walimu wanne , sekondari walimu wanne , vyuo pamoja na wadau wengine wanaopenda kujifunza mchezo huo.  
Mzava alisema kuwa washiriki watatoka wilaya zote za mkoa wa Pwani ambapo kwa walimu tayari barua za kuomba ushiriki wao zimepelekwa kwa wakurugenzi wa Halmashauri ili kuwpaatia ruhusa ya kushiriki mafunzo hayo.
“Wanafunzi wa mchezo huo watajifunza masomo ya darasani pamoja nay a vitendo ili kuwajengea uwezo wa kuujua mchezo huo hata watakapokwenda kuwafundisha wengine wawe na maarifa ya kutosha na mafunzo haya yameandaliwa kwa pamoja na chama cha mchezo huo nchini (TAVA) alisema Mzava.
Alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwapa ujuzi wa kutosha walimu wa mchezo huo ili waweze kujua sheria na namna mchezo unavyochezwa na kuusimamia kama sheria za mchezo huo zinavyoonyesha na kupitishwa na chama cha mchezo huo cha kimataifa FIVB.
“Hadi sasa walimu kutoka Hlamashauri za Bagamoyo, Mkuranga, Rufiji na Kibaha Mji tayari wamethibitisha kushiriki mafunzo hayo na waliobaki wanapaswa kuthibitisha kabla ya tarehe 22 Machi ili waweze kuwekewa utaratibu wa kushiriki mafunzo hayo,” alisema Mzava.
Aidha alisema kuwa walimu watakaofanya vizuri kwenye mafunzo hayo watapata nafasi ya kushiriki mafunzo ya Kimataifa ya Beach yatakayofanyika Aprili mwaka huu Jijini Dar es Salaam hivyo itasaidia kuutangaza mkoa kupitia mchezo huo.
“Tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kudhamini mafunzo haya kwani hata wakitoa maji au kitu chochote itasaidia kupunguza gharama za kuendesha mafunzo hayo kwani hadi sasa hakuna wadhamini waliojitokeza kuzamini mafunzo hayo,” alisema Mzava.
Alibainisha kuwa matarajio ni kuzalisha walimu wengi wa mchezo huo hasa mashuleni na itasaidia kupunguza gharama za kuwalipa walimu toka nje hawa wakati wa mashindano ya Umoja wa Shule za Msingi na Utamaduni Tanzania( UMITASHUMTA) na Umoja wa Shule za Sekondari na Sanaa Tanzania (UMISSETA).

Mwisho. 

Monday, March 14, 2016

CHUO CHA KILIMO NA MIFUGO CHAKABILIWA NA CHANGAMOTO YA ZANA ZA KILIMO

Na John Gagarini, Bagamoyo
CHUO cha Kilimo na Mifugo Kaole wilayani Bagamoyo kinachomilikiwa na Jumuiya ya wazazi Tanzania kinakabiliwa na upungufu wa madawa ya kujifunzia kwenye maabara pamoja na zana za kujifunzia hali ambayo inasababisha wanachuo kushindwa kujifunza kikamilifu.
Hayo yalisemwa Bagamoyo na Rais wa Chuo hicho Abas Kasusumo wakati wa ziara iliyofanywa na Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo ambao walitembelewa na Jumuiya hiyo wilaya ya Temeke kuangalia shughuli zinazofanywa na Jumuiya hiyo.
Kasusumo alisema kuwa changamoto hizo zinawasababisha washindwe kujifunza ipasavyo hali ambayo inawafanya wawe katika wakati mgumu kuelewa masomo yao.
“Tunaomba tusaidiwe vifaa vya kujifunzia kama vile matrekta ambayo hapa yapo lakini hayafanyi kazi hivyo tunaiomba serikali na Jumuiya ambayo ndiyo wamiliki wa chuo chetu ili tupate vifaa vya kujifunzia,” alisema Kasusumo.
Alisema kuwa kutokana na chuo hichi kuwa cha mifugo pia kuna changamoto ya ukosefu wa madawa mbalimbali kwa ajili ya kujifunzia masomo yetu kwani wakitoka hapo watategemewa kufanya kazi kutokana na walivyojifunza.
Kwa upande wake mwalimu mkuu wa chuo hicho Carthert Liwa alisema kuwa changamoto nyingine ni umeme ambapo wanatumia mita ya Luku ambayo haiwezi kumudu matumizi makubwa.
Liwa alisema kuwa changamoto zimekuwa nyingi kwani chuo hicho kimeanza upya baada ya kutokea matatizo hivyo wadau wanaombwa kujitokeza kukisaidia ili kiweze kutoa mafunzo kwa viwango vinavyotakiwa.
Naye mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo ambao ndiyo wamiliki wa chuo hicho Abdul Sharif alisema kuwa watahakikisha wanshirikiana na wadau wengine ili kuhakikisha kinatoa mafunzo kwa ubora.
Sharif alisema kuwa changamoto zilizotajwa ni za kweli na Jumuiya kwa kushirikiana na makao makuu watazifanyia kazi changamoto hizo ili elimu bora iweze kupatikana chuoni hapo. Chuo hicho kina wanafunzi 36 lakini uwezo wake ni wanachuo 600 ambapo hali hiyo ilitokana na kuchelewa kuandikisha wanachuo.
Mwisho.    
    
  
  

    

Thursday, March 10, 2016

DIWANI AKUMBWA NA BOMOBOMOA KIBAHA


Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la bomoa bomoa kwa watu waliojenga kwenye hifadhi ya barabara ya Morogoro lililoanza Machi 8 mwaka huu wilayani Kibaha mkoani Pwani limemkumba diwani wa kata ya Sofu Yusuph Mbonde ambaye alijenga chumba cha biashara kwenye  eneo la Picha ya Ndege naye amekumbwa na kadhia hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari kwenye eneo hilo diwani huyo alisema kuwa yeye naye alikuwa akifanya biashara ya kujipatia riziki yake hapo na alijua bomoa bomoa hiyo ilikuwa ni kwenye barabara mpya lakini akashangaa zoezi hilo kupita hadi barabara ya zamani.
“Zoezi hili limeathiri watu wengi na wote tuliojenga hapa na kufanyabiashara hapa tulipewa taarifa ya kubomoa lakini nilijaribu kumwomba meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kutuongezea muda lakini alisema watu wabomoe ambapo walitoa muda wa kubomoa na watu wengi hawakuamini kama watabomolewa kwani taarifa zilikuwa zikitolewa bila utekelezaji,” alisema Mbonde.
Alisema eneo ambalo limebomolewa ni zaidi ya wafanyabiashara 200 ambako ni pamoja na eneo la soko na maduka ya kuuza bidhaa mbalimbali pamoja na nyumba za makazi ya watu wanaokadiriwa kufikia zaidi ya 1,000 kwa mitaa miwili ya Picha ya Ndege na Msufini ambayo ina wakazi 13,000.
“TANROADS iliwataka watu wanaotumia eneo la hifadhi ya barabara kutojenga vibanda vya kudumu lakini watu walijenga vibanda vya kudumu pamoja na nyumba kama siyo sehemu ya muda tunakubaliana na serikali hatuna jinsi tutatafuta eneo mbadala kwa ajili ya kufanya biashara,” alisema Mbonde.
 Naye Zakia Yusuph alisema kuwa zoezi hilo limewaathiri sana hasa akinamama ambao walikuwa wakiendesha biashara zao za kujipatia kipato ambapo wengine ni wajane na wana watoto ambao wanasoma.
Yusph alisema kuwa yeye yeye alikopa mkopo benki wa shilingi milioni tano na hajui atazirudisha vipi na kuiomba serikali kuwapatia eneo lingine kwa ajili ya kufanyia biashara zao za kuwapatia kipato cha kuendeshea familia zao.
Kwa upande wake meneja wa TANROADS Tumaini Sarakikya alisema kuwa zoezi hilo la bomoabomoa litadumu kwa kipindi cha siku 15 ambapo wataondoa nyumba zote zilizojengwa kwenye hifadhi ya barabara zilizo ndani ya mita 22.5 kila upande wa barabara kwa sheria ya barabara ya mwaka 1930 baada ya kutoa notisi za mara kwa mara.
Sarakikya alisema kuwa zoezi hilo ni la kudumu na litafanyika kwenye barabara zote zilizochini ya wakala kwenye wilaya za mkoa huo ambapo kwa njia ya Morogoro zoezi hilo litaenda hadi Bwawani mpakani mwa mikoa ya Pwani na Morogoro.
“Barabara ya Tanga watatekeleza zoezi hilo hadi eneo la Manga mpakani mwa mikoa hiyo huku kwa upande wa Bagamoyo litafanyika hadi Bunju mpakani mwa Pwani na Dar es Salaam na Kongowe hadi Marendego kwa barabara iendayo mikoa ya Kusini,” alisema Sarakikya.
Akizungumzia kuhusu eneo la Maili Moja ambako ndiyo makao makuu ya mkoa wa Pwani amesema kuwa eneo hilo litakuwa la mwisho kutokana na halmashauri kuomba hadi pale watakapojenga Stendi na soko ambavyo ndiyo chanzo kikuu cha mapato ya Halmashauri hiyo lakini mara ujenzi huo utakapokamilika watabomoa ndani ya mita 100 kila upande.

Mwisho.

DK KIGANGWALA AMPA SAA 24 MKURUGENZI KUANDIKA BARUA YA KUJIELEZA KWANINI ASIONDOLEWE KWENYE NAFASI HIYO, AFUNGA CHUMBA CHA MAITI ATAKA WAFANYE MAREKEBISHO NDANI YA SIKU TATU

Na John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Dk Hamis Kigangwala ametoa saa 24 kwa Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Dk Cyprian Mpemba kuandika barua ya kwa nini asiondolewe kwenye nafasi hiyo kwa kushindwa kuendesha Hospitali Teule ya Rufaa ya Tumbi iliyopo wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Waziri Dk Simbachawene alitoa agizo hilo huku mkurugenzi huyo akiwa hayupo na kumwagiza Kaimu Mkurugenzi wa Shirika hilo Anase Nko kumfikishia ujumbe huo Dk Mpemba kwa ajili ya kutoa maelezo hayo.
Dk Kigangwala aliyasema hayo jana mara baada ya kutembelea hospitali hiyo kutokana na kuwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na kushindwa kusimamia maslahi ya watumishi ambao wamekosa morali ya kufanya kazi.
Alisema kuwa hali iliyopo kwenye hospitali hiyo ni mbaya sana na inasikitisha sana huku ofisi ya mkurugenzi ikiwa inatumia fedha ambazo zingesaidia kuboresha huduma kwenye hospitali hiyo.
“Shirika limeshindwa kuendesha natoa saa 24 hadi leo saa nane mchana awe ameandika barua ya kujieleza kwanini asiondolewe kwenye nafasi hiyo kwani ameshindwa kusimamia hospitali hiyo kwani vitu vingi haviko sawa kuanzia mochwari ambapo imekuwa ikitoa harufu mbaya kutokana na baadhi ya vifaa vya majokofu kuharibika,” alisema Dk Kigwangala.
“Nataka atoe maelezo yanayojitosheleza kwani inaonekana hakuna jambo ambalo linaweza kufanyika kwenye hospitali bila ya mkurugenzi ambapo fedha za hospitali zimekuwa zikitumika kwenye matumizi mengine,” alisema Dk Kigangwala.
Aidha alisema kuwa mbali ya hivyo pia kuanzia sasa shirika hilo lisisimamie masuala ya fedha za Hospitali hiyo bali ijisimamie yenyewe ili kuangalia vipaumbele vinavyohusu hospitali kwani huduma hazisubiri utaratibu.
“Tumeona kuwa tatizo ni utawala ambao unaonekana umeshindwa kusimamia hospitali nilipokuja nilifikiri tatizo ni meneja wa Huduma za afya Dk Peter Datani lakini una bahati nilikuja kwa ajili ya kukutimua wewe kumbe wewe huusiki,” alisema Dk Kigwangwala.
Alibainisha kuwa kuna changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na chumba cha upasuaji kutokuwa na hadhi kwani ni sawa na stoo, viyoyozi havifanyi kazi, chumba cha wagonjwa mahututi nacho hakiko sawa na vifaa vinaharibika hakuna matengenezo hivyo huduma kuwa mbaya.
“Inashangaza kuona kuwa hospitali inakosa vifaa tiba pamoja na madawa licha ya kuwa inaingiza fedha nyingi kati ya shilingi milioni 120 hadi 150 kwa mwezi lakini inashindwa kujiendesha inashindwa hata kutoa milioni sita kwa ajili ya kununulia mifuko ya kuhifadhia damu inasikitisha sana hospitali hii inaendeshwa kiujanja ujanja tu lazima mjiendeshe kwa mikakati siyo kwenda tu,” alisema Kigwangwala.
Kutokana na hali hiyo ameagiza chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali hiyo ifungwe na iwe imefanyiwa matengenezo ndani ya siku tatu na watajua maiti watazipeleka wapi kwani haiwezekani chumba hicho kuwa kwenye hali hiyo pia miezi mitatu wanatakiwa wawe wamehakikisha maji yanapatikana kwa kujenga matenki ya kuhifadhia maji.
Alimtaka mkuu wa mkoa kupata ushauri kwa  wataalamu ili kuangalia mahusiano baina ya hospitali hiyo na sekretarieti ya mkoa pia inaonekana ni vema hospitali hiyo ikasimamiwa na mkoa badala ya shirika.
Alisisitiza kuwa endapo watashindwa kukarabati chumba hicho cha maiti ndani ya siku tatu atawaondoa kwenye nafasi zao kwani watakuwa wameshindwa kutekeleza agizo la serikali kwani haiwezekani huduma kutolewa kwenye mazingira magumu wakati fedha zinapatikana.
Kwa upande wake msajili wa hospitali nchini Dk Pamela Sawa alisema kuwa walifanya ukaguzi kwenye hospitali mwaka 2010 hadi 2011 ambapo walikuta hospitali nyingi zina mapungufu mengi mafano hospitali ya Mawenzi mkoani Kilimanjaro ilikuwa ikitumia chumba cha upasuaji kilichokuwa kikitumika enzi za mkoloni lakini walibadilisha baada ya kuifunga pia hospitali ya Mbeya nayo ilikuwa na matatizo ya maji.
Naye Dk Datani alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo hospitalini hapo ni ukosefu wa fedha kwani waliomba kiasi cha shilingi milioni 600 lakini walipewa kiasi cha milioni sita tu hivyo kujikuta wakiwa kwenye wakati mgumu wa kuboresha maslahi ya wafanyakazi pamoja na kununua vifaa tiba pamoja na madawa.
Mwisho.

   

Friday, March 4, 2016

ALBINO APOTEA

Na John Gagarini, Mkuranga
KIJANA mwenye ulemavu wa ngozi Albino Said Abdala mkazi wa Kijiji cha Mbezi Mlungwana kata ya Pazuo wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani amepotea tangu Januari 31 mwaka huu na hajulikani alipo baada ya kwenda kutembea nyakati za usiku.
Abdala ambaye alikuwa akiishi na wenzake wawili wenye ulemavu huo akitokea mkoani Morogoro huku wenzake Tabora kwa lengo la kuepuka vitendo vya kushambuliwa na watu ambao wamekuwa wakiwa kata viungo au kuwaua hali iliyowafanya wakae huko chini ya Shirika la Under The Same Sun.
Akizungumza mbele ya mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo, Samwel Masaga alisema kuwa mwenzao aliondoka siku hiyo majira ya jioni kwenda kutembea lakini hakurudi tena hadi wakati anatembelea mkuu huyo.
Masaga alisema kuwa mwenzao alikuwa na tabia ya kutoka na kutembetembea lakini wanashangaa ni kwa nini hajarudi na jitihada za kumtafuta zimeshindikana licha ya kutoa taarifa sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na polisi na ofisi ya mkuu wa wilaya.
“Tunasikitika kupotea kwa mwenzetu na hatuji tutampataje tunaomba vyombo vinavyohusika vitusaidie ili mwenzetu aweze kupatikana kwani hatujui mwenzetu nini kimemsibu kwani ni muda mrefu umepita hakuna taarifa yoyote juu yake,” alisema Masaga.
Alisema kuwa mazingira wanayosihi kwa bahati mbaya hayana ulinzi wowote lakini wamekuwa wakiishi vizuri na wenyeji wao ambao waliwapokea vizuri na wamekuwa wakiishi vizuri bila ya matatizo ila hawajui mwenzao yuko wapi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Hassan Kafeni alisema kuwa walemavu hao wako hapo tangu mwaka 2014 na ni wa awamu ya pili baada ya awamu ya kwanza kukaa hapo kisha kuondoka ndipo walipoombewa hao wakae hapo ili nao waishi kama wanakijiji.
Kafeni alisema kuwa Abdala tangu alipopotea walifanya jitihada za kumtafuta lakini hata hivyo hawajamwona na bado wanaendelea kumtafuta hadi watakapompata na wameshangazwa na tukio la kupotea kwake.
Kutokana na hali hiyo mkuu wa mkoa wa Pwani injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa shirika hilo linapaswa kuangalia upya namna ya kuwatunza watu hao kwani mazingira waliyopo usalama wake ni mdogo.
Ndikilo alisema kuwa shirika hilo linaonyesha lina nia nzuri lakini mazingira waliyopo si salama sana kwani hakuna ulinzi wa kutosha hali ambayo imesababisha Abdala kupotea na kuwataka kuwahamishia sehemu nyingine.
“Nawashauri wawatafutie sehemu nyingine ya kuishi kwani pale walipo hakuna usalama kwani kama mtu anania mbaya ni rahisi kuwazuru kwani serikali inataka waishi kwenye mazingira yenye usalama wa maisha yao,” alisema Ndikilo.
Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa Jeshi hilo linaendelea na msako wa kumtafuta Abdala na watahakikisha wanamtafuta hadi wanampata ili aungane na wenzake waishi kama kawaida.
Mushongi alisema kuwa ushirikiano na wananchi utasaidia kupatikana kwake hivyo watoe ushirikiano ili kufanikisha Abdala kupatikana kwani jambo hilo si la kawaida kutokea na kuwataka wananchi kuwalinda Albino kwani nao wana haki ya kuishi.
Mwisho.           


JESHI LA POLISI LAPEWA SIKU TATU KUMALIZA UHALIFU UNAOFANYWA NA WAVAMIZI

Na John Gagarini, Mkuranga
MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo ametoa siku tatu kwa Jeshi la Polisi mkoani humo kuwakamata watu wanaojihusisha na vitendo vya kuwavamia kisha kuwapora viwanja na kufanya mauji kwa wakazi wa Kijiji cha Tambani kata ya Tambani wilaya ya Mkuranga.
Kutokana na tishio hilo limesababisha uongozi wa Kijiji hicho kushindwa kwenda baadhi ya maeneo wakihofia maisha yao kutokana na watu hao kutumia silaha mbalimbali za kijadi kwa ajili ya kufanya uhalifu.
Aliyasema hayo juzi Kijijini hapo alipotembelea kusikiliza kero hiyo ambayo imewafanya baadhi ya wakazi wa eneo hilo kuhama na kushindwa kufanya shughuli za maendeleo kwenye maeneo yao kutokana na hofu ya kuuwawa.   
“Natoa siku tatu kuanzia leo hakikisheni mmewakamata watu hao ambao kwa bahati majina mmnayo hakuna haja ya watu kushindwa kuishi kwa amani nchi hii haijafikia hatua ya watu kushindwa kukaa kwenye maeneo yao au viongozi kuogopa kwenda kwenye eneo lao la utawala,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa wananchi wa Kijiji hicho wamekwenda ofisini kwake zaidi ya mara tano wakilalamikia kundi hilo la watu ambao wametajwa kuwa ni kikundi cha watu 15 kabila la Kikurya ambao wanadaiwa kutokea eneo la Msongola wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam.
“Wananchi wamekuwa wakilalamika kuwa licha ya kulalamika kwa Jeshi hilo ngazi ya wilaya lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa ambapo hadi sasa watu watatu wameuwawa na kundi hilo la watu ambao ni wavamizi wa ardhi pia wamekuwa wakifanya vitendo vya uhalifu wa kuvunja nyumba, kuiba na kufanya vitendo vya ubakaji,” alisema Ndikilo.
“Inashangaza kuona kuwa mgogoro huu wa wavamizi ulianza tangu mwaka 2014 lakini hadi sasa hakuna hatua madhubuti ambazo zimechukuliwa za kudhibiti kundi hili ambalo ni hatari kwa wananchi ambao hawana hatia na kilio chao lazima kisikilizwe na si kuwaacha walalamike wakati viongozi wapo,” alisema Ndikilo.
Awali mwenyekiti wa Kijiji hicho Amir Mbamba alisema kuwa walishachukua hatua mbalimbali katika kuhakikisha suala hilo linakomeshwa kwa kulipeleka kwa mkuu wa wilaya lakini kundi hilo bado limeendelea kuendesha matukio hayo bila ya woga.
Mbamba alisema kuwa wananchi wake kutokana na kuona kuwa hawasikilizwi walikwenda kwa Waziri Mkuu pamoja Tume ya Haki za Binadamu ili waweze kusaidiwa tatizo lao na baadaye kwa mkuu wa mkoa ambaye leo umefika kujua ukweli wa tukio hili.
“Wananchi wamesema kuwa wataandamana hadi Ikulu kwa Rais endapo suala lao halitashughulikiwa ipasavyo hivyo kwa kuwa mkuu umekuja mwenyewe ukweli umeupata hatua madhubuti zitasaidia kumaliza mgogoro,” alisema Mbamba.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa watahakikisha kuwa watu hao wanakamatwa na amani itarudi kama ilivyokuwa zamani kwani watajipanga ili kukomesha uhalifu huo.
Mushongi alisema kuwa kwa kuanzia katika kulikabili suala hilo watashirikiana na kamati ya ulinzi na usalama ya Kijiji pamoja na mgambo ili nao washiriki kikamilifu katika kulifuatilia suala hilo ili watu waishi kwa amani bila ya hofu.
Mwisho.

Tuesday, March 1, 2016

RAIA 35 WA ETHIOPIA WADAKWA WAKIISHI NCHINI BILA YA KIBALI


Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia Raia 35 wa Ethiopia baada ya kukamatwa wakituhumiwa kuishi nchini bila ya kibali huku likimsaka David Myovela mkazi wa Kilangalanga wilayani Kibaha kwa tuhuma za kuwahifadhi raia hao.
Kwa mujibu wa kamanda wa Polisi mkoani humo Boniventura Mushongi  alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 29 mwaka huu majira ya 5:30 usiku huko Kilangalanga tarafa ya Mlandizi wilaya ya Kibaha.
Kamanda Mushongi alisema kuwa watuhumiwa hao walikutwa nyumbani kwa mtuhumiwa huyo baada ya taarifa kutolewa na wasamaria wema juu ya kuwepo kwa wageni hao ambao walikuwa hawana kibali cha kuishi nchini.
“Wahamiaji hao haramu waliingia nchini wakitokea Mombasa nchini Kenya kupitia mkoa wa Tanga kwa njia ya barabara huku wakiwa kwenye gari la mizigo aina ya Fuso na Noah na kufikia kwenye nyumba ya mtuhumiwa huyo wakijiandaa kwa safari ya kwenda Afrika ya Kusini,” alisema Mushongi.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Tatela Erdadu, Tafesa Tesfaye, Ercuias Hailu, Teseahun Abrahom, Gizochew Bergeno, Meies Kasa, Azole Chebow, Samuel Game, Abtama Falak na Barka Lambamu.
Wengine ni Gazu Abame, Tesk Wark, Gejerm Ababey, Aman Ekdapu, Gadon Hayie, Danak Danel, Tamer Yoanes, Eshey Ayaia , Tasam Ayaia, Tamasoen Dam, Yesak Danei, Gezcho Sugebo, Beramu Make na Abinet Elias.
Aidha aliwataja wengine kuwa ni Mulugeta Abayno, Mehumud Kedery, Mubary Naes, Lmebo Demise, Tamesfen Tadse, Tariku Amato, Tedsue Cueba, Akhelu Moses, Tenekuden Bekeil, Aborome Arizoto, Berhom Kedir ambapo watuhumiwa hao watakabidhiwa kwa idara ya Uhamiaji kwa ajili ya hatua za kisheria.
Mwisho.