Sunday, December 27, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA MKOA WA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajiwa kuwa moja ya mikoa ambayo itakuwa kwa kasi kutokana na kuongezeka kwa shughuli nyingi za uwekezaji za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa bandari wilayani Bagamoyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa mkoa una fursa nyingi za uwekezaji na watu binafsi pamoja na makampuni yameonyesha nia ya kuwekeza.

Ndikilo alisema kuwa uwekezaji umeanza kuchukua nafasi yake baada ya Jiji la Dar es Salaam kuonekana kuwa limejaa hivyo fursa iliyopo ni mkoa huo ambao uko jirani na Dar es Salaam.

“Kwa sasa tunajivunia na mojawapo ya uwekezaji mkubwa ni ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo ambayo itaongeza pato la mkoa huo kwani utazalisha ajira nyingi na wageni wengi wataingia kwa ajili ya shughuli nyingi za kibiashara,” alisema Ndikilo.

Alisema uwekezaji mwingine ni pale Kisarawe ambapo kimejengwa kiwanda cha saruji, Kibaha kuna viwanda vya Jipsam, Nondo na uwekezaji sehemu nyingine mbalimbali za wilaya zinazounda mkoa huo.

“Tukija kwenye zao kuu la biashara la Korosho nalo limezidi kunufaisha wakulima ambapo kwa sasa kilo ya korosho imepanda na kwa mnada sasa inauzwa kati ya 2,600 na 2,700 kutoka chini ya shilingi 1,000 na hii ni kutokana na mfumo wa stakabadhi ghalani,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa kwa kipindi kirefu mkoa huo haukuwa na fursa nyingi hali ambayo ilisababisha uonekane kama uko nyuma kiuchumi tofauti na ilivyo sasa fursa zimekuwa nyingi sana hivyo mafanikio ya kiuchumi yatakuwa makubwa.

Aliwataka watu wa mkoa huo hususani vijana kutumia fursa hizo zilizopo ambazo zimejitokeza kwa sasa ili kujikwamua na hali ngumu ya kimaisha pia watumie fursa za kilimo ambazo ni nyingi.

Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unaendelea na uhakiki wa watu walioweka mashamba pori ili taarifa zipelekwe kwa Waziri husika na baadaye kwa Rais ili kutengua umiliki wao endapo watashindwa kuyaendeleza hususani wale walionunua kwenye kitovu cha Mji wa Kibaha.

Kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kuna mashamba pori mengi makubwa ambayo hayajaendelezwa kwenye wilaya zote za mkoa huo ikiwa ni pamoja na Kibaha, Kisarawe, Rufiji, Bagamoyo na Mkuranga.

Ndikilo alisema kuwa tayari wameshaanza kuyafanyia kazi mashambapori hayo kwa kushirikiana na wakurugenzi wa Halmashauri kwa mashamba yasiyoendelezwa.

“Tayari tumeshawapelekea notisi baadhi yao ili wajieleze ni kwanini wameshindwa kuyaendeleza mashamba hayo na kwanini wasinyanganywe kutokana na kushindwa kuyaendeleza,” alisema Ndikilo.

Kwa upande wa kitovu cha Mji wa Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa huo alisema kuwa wamiliki binafsi pamoja na taasisi ambazo ni nyingi wameshapewa barua kujieleza kwanini hawakuviendeleza viwanja hivyo.

“Tunawashangaa ni kwa nini wameshindwa kuendeleza viwanja hivyo ambavyo endapo vingejengwa vingeweka suraa nzuri ya mji kwani hapo ndiyo kwenye mandari ya uso wa mji,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa licha ya kutakiwa kujieleza kwa nini hawakuviendeleza viwanja hivyo pia waeleze kuwa watavijenga lini na muda watakaokubaliana hawapaswi kuupitisha tena.

“Kwa watakaoshindwa kuviendeleza baada ya makubaliano watanyanganywa viwanja hivyo ili wapewe wengine watakaoweza kuviendeleza kwa kujenga kwa wakati ukaoakuwa umepangwa,” alisema Ndikilo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

JUMUIYA ya Wazazi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kibaha Mjini kimezigawia Jumuiya za Kata ardhi yenye ukubwa wa hekari moja kwa lengo la kuziendeleza kiuchumi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha baada ya zoezi hilo la kuwagawia ardhi hiyo ambalo lilifanyika kwenye sherehe za siku ya Uhuru, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Kibaha Mjini Dk Athuman Mokiwa alisema kuwa eneo hilo litakuwa kitovu cha uchumi wa Jumuiya hiyo.

Mokiwa alisema kuwa eneo hilo lenye ukubwa wa hekari 15 wameligawa kwa kata 14 za kichama ambapo kila kata inapaswa kuziendeleza kwa kulima na baadaye kufanya ujenzi.

“Kipindi cha nyuma tulishindwa kuliendeleza kutokana na kukosa fedha kwa ajili ya kulipima lakini baada ya kulipima sasa tumegawa kila kata wawe na eneo lao kwa ajili ya shughuli za kiuchumi,”alisema Dk Mokiwa.

Alisema kuwa shamba hilo lilikuwa likivamiwa na watu kutokana na kutokuwa na hati za umiliki lakini kwa sasa wameshalimiliki kisheria hivyo hakuna mtu atakayeweza kuvamia tena.

Naye katibu wa Wazazi kata ya Kibaha lilipo shamba hilo Rehema Ally alisema kuwa wanaushukuru uongozi kwa kuwapatia eneo ambapo wanatarajia kuliendeleza na hiyo ni rasilimali yao kiuchumi.

Ally alisema kuwa baada ya kupatikana hati watawakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kujenga taasisi zikiwemo za shule au zaahanati na huduma nyingine za kijamii.

Viongozi wa Jumuiya hizo za kata wamekubaliana kufanya usafi kila baada ya wiki mbili ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais Dk John Magufuli juu ya usafi kukabiliana na magonjwa ya milipuko pia kuweka maeneo mbalimbali katika hali ya usafi.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA dereva wa Pikipiki wa Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani Ally Rashid (35) kuuwawa kwa kupigwa risasi na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kisha kumpora pikipiki aliyokuwa akiieendesha madereva wenzake wameomba uchunguzi wa kina ufanyike kuhusiana na tukio hilo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa Chama Cha Madereva Pikipiki Kibaha (CHAWAMAPIKI) Shaban Kambi alisema tukio hilo ni la kushangaza kwa watu kutumia bunduki kwa ajili ya kupora pikipiki likiwa ni tukio la pili.
Kambi alisema kuwa kumekuwa na matukio ya wizi wa pikipiki lakini kwa kutumia bunduki si hali ya kawaida hivyo tunaomba polisi wafuatilie tukio hilo la kusikitisha kwa mwenzetu kuuwawa.

“Matukio ya kutumia silaha ni matatu ambapo mtu mmoja alivamiwa nyumbani kwake na kupigwa risasi na kufa la pili ni mwenzetu mwingine alipigwa risasi ya mguuni na kuporwa pikipiki lakini hakufa huku mwenzetu wa juzi naye alipigwa risasi na kufa ambapo cha kushangaza matukio yote yametokea upande mmoja,” alisema Kambi.

Alisema matukio yote hayo yametokea maeneo ya machinjioni hali ambayo inawapa hofu wakazi wa Maili Moja kwa kuona kuwa maisha yao sasa yako hatarini kwa watu hao kufanya uahalifu kwa kutumia bunduki.

“Tumesha waambia madereva pikipiki kuwa makini kwani kuna baadhi ya maeneo kwa sasa ni hatarishi pia wakiwa na wasiwasi wasiwabebe watu wasiowafahamu hasa nyakati za usiku hasa katika kipindi hichi cha mwisho wa mwaka,” alisema Kambi.

Aidha alisema kuwa wao wako tayari kushirikiana na jeshi la polisi katika kufuatilia watu wanaojihusisha na matukio hayo ya uporaji wa pikipiki pamoja na mali za watu.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajia kujenga Kituo Kikubwa cha Mabasi pamoja na Soko baada ya kupata mkopo toka Benki ya Uwekezaji ya (TIB) na kuufanya mji wa Kibaha kuwa wakisasa.

Hayo yalisemwa na mkuu wa mkoa wa Pwani alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo na kusema kuwa kwa sasa taratibu zinaendelea baina ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha na benki hiyo.

Ndikilo alisema kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa mara taratibu za kitaalamu zitakapokamilika ambapo kwa sasa bado zinaendelea.

“Tunatarajia kuwa na stendi ya kisasa pamoja na soko hasa ikizingatiwa mkoa ulikuwa hauna soko kubwa bali lililopo ni dogo na halina uwezo wa kuchukua bidhaa nyingi,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa wafanyabiashara wa mkoa wa Pwani hususani wale wa makao makuu ya mkoa Maili Moja na vitongoji vyake huwalazimu kwenda kununua bidhaa Kariakoo au kwenye masoko mengine Jijini Dar es Salaam jambo ambalo linafanya bei za bidhaa kuwa juu.

“Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa ni kama malango wa Jiji la Dar es Salaam lakini bidhaa zimekuwa zikipita hapa na kwenda huko kisha wafanyabiashara kwenda kununua na kuzirudisha hapa hivyo kupandisha bei kutokana na gharama kuwa kubwa,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa soko hilo ambalo litajengwa sambamba na stendi litakuwa la kisasa ambapo magari yatakuwa na uwezo wa kuingia na kushusha bidhaa na si kama ilivyo sasa ambapo kutokana na udogo wa soko lililopo hubidi magari ya bidhaa yashindwe kuingia.

Mwisho.
  

   

   

  




WATAKA TAFSIRI YA UPANUZI WA BARABARA WAPATE HAKI ZAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Kijiji cha Kiluvya B wilaya ya Kisarawe mkoa wa Pwani wameiomba Wizara ya Ujenzi na Makazi iangalie upya tafsiri ya upanuzi wa barabara kuu kwani upanuzi uliofanyika ni urefu wa mita 120 upande mmoja wakati sheria inasema kila upande wa barabara itapanuliwa kwa urefu wa mita 60 kwa 60 kutoka katikati ya barabara kuu.
Kutokana na sheria hiyo kutafsiriwa mita 120 nyumba zilizojengwa kando ya Barabara ya Morogoro baadhi zimebomolewa na nyingine zimeekewa alama ya X zikitakiwa kubomolewa baada ya muda usiozidi zaidi ya wiki moja na kupelekea kilio kikubwa kwa wakazi hao.
Wakizungumza waandishi wa habari waliotembelea kijiji hicho moja ya wakazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Abubakary Yusuph alisema kuwa athari ya kubomolewa nyumba hizo ni kubwa sana hivyo kuomba suala hilo liangaliwe upya.
Yusuph alisema kuwa wao hawana tatizo la kuondoka kwenye eneo hilo kwa ajili ya kupisha shughuli za maendeleo bali wameomba sheria ifuatwe ili wasinyimwe haki zao kwani wao wako hapo tangu vilipoanzishwa vijiji vya ujamaa miaka ya 70.
“Tunaomba wizara na serikali kuliangalia upya suala hili kwani sisi hatuna shida kwa wale waliojenga ndani ya mita 60 kwani tunajua suala hilo ni la kisheria lakini mita 120 tunaona kuwa hatujatendewa haki ni vema wanapotekeleza suala hilo wakazingatia sheria ya barabara na kama wanataka eneo zaidi ni vema wakatulipa ndipo waendelee na zoezi hilo,” alisema Yusuph.
Alisema kuwa watu wengi walijenga umbali zaidi ya mita 60 kwani walikuwa wakijua kuwa kama watakuwa ndani ya mita hizo basi bomobomoa ikija wangebomolewa nyumba zao lakini walikojenga walijua wako salama wanashangaa kuona nyumba zao zinabomolewa.
Naye Alfonce Kejo alisema kuwa baadhi yao ni wastaafu na hawana kipato chochote na waliwekeza kwenye nyumba zao kwa ajili ya makazi mara baada ya kustaafu kazi hivyo wanaomba suala lao lishughulikiwe ili wapate haki yao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Julius Bukoli ambaye naye amekumbwa na bomoa bomoa hiyo alisema kuwa nyumba yake aliijenga kabla ya mwaka 2000 na iko umbali wa karibu mita 100 toka barabara kuu lakini ametakiwa kubomoa.
Bukoli alisema kuwa hata wanaohusika katika kubomoa nyumba hizo hawafuati taratibu za kutoa taarifa kwenye uongozi wa Kijiji bali wanakuja nyakati za jioni na kubomoa au kuweka alama za X kisha kuondoka.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Kuweka na Kukopa Cha TCCIA Saccos mkoa wa Pwani kimeweza kukopesha mikopo inayofikia zaidi ya shilingi milioni 398 kwa wanachama wake.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, Meneja wa chama hicho Arestide Temu alisema kuwa fedha hizo zimetolewa kwa  wanachama waliofuata taratibu za mikopo kwa lengo la kukuza mitaji yao ya biashara.

Temu alisema kuwa hata hivyo biashara nyingi kwenye mkoa huo zinashindwa kukua vizuri kutokana na kutokuwa na mzunguko mkubwa wa fedha kwa sababu ya kuwa na shughuli chache za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa viwanda.

“Sababu nyingine ya wafanyabiashara kushindwa kufikia malengo ni kutokana na kufanya biashara zinazofanana na kusababisha kushindwa kufikia malengo hata hivyo tumepata mafanikio tumeweza kupata faida ya shilingi milioni 26 tofauti na lengo la kupata faida ya shilingi milioni 20 tulizokuwa tumejipangia kwa mwaka huu ambapo faida hiyo ni hadi mwezi Novemba mwaka huu,” alisema Temu.

Alisema kuwa maendeleo ya chama yanakwenda vizuri ambapo kwa sasa wamanachama wanaweza kukopa mara tatu ya fedha walaizojiwekea kama akiba na wanaweza kukopa hadi shilingi milioni 15 kwa mara moja.

“Riba ni asilimia 15 ya mkopo wowote anaoomba mwanachama ambapo hisa moja inauzwa kiasi cha shilingi 10,000 huku mwanachama akitakiwa kununua hisa kuanzia 10 na kuendelea,” alisema Temu.
Aidha alisema kuwa chama hicho cha kuweka na kukopa kilianzishwa mwaka 2001 kikiwa na wanachama 600 ambapo kwa sasa kina wanachama 227 huku wengine wakiwa wameondolewa kwa kushindwa kufuata taratibu za chama.   

Mwisho.




Saturday, December 26, 2015

BONANZA LA KUAGA MWAKA 2015 NA KUUKARIBISHA 2016 KUFANYIKA JANUARI MOSI KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
BONANZA la kuuaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka 2016 linatarajiwa kufanyika Januari Mosi mwakani kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Msajili Msaidizi wa Vilabu na Vyama vya Michezo wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Abdul Haufi alisema kuwa Bonanza hilo litakuwa la wazi kwa watu wote.
Haufi alisema kuwa shindano hilo litakuwa la michezo mbalimbali litashirikisha mashirika ya Umma, binafsi pamoja na watu binafsi au mtu mmoja mmoja kwenye michezo ya soka, mpira wa pete kwa wanawake, kuvuta kamba, riadha mita 100.
Alitaja michezo mingine kuwa ni kukimbia na magunia, kurusha kisahani, tufe, mpira wa wavu, kijiko na ndimu ambapo usajili unafanyika kwenye ofisi za Halmashauri hiyo.
“Tunatarajia jumla ya wanamichezo 250 kushiriki Bonanza hilo la aina yake kufanyika mjini Kibaha na vitongoji vyake ambapo lengo ni kuhamasisha watu kushiriki michezo pamoja na kudumisha urafiki baina ya mashirika bianafsi, ya umma pamoja na watu binafsi,” alisema Haufi.
Aidha alisema kuwa juu ya wadhamini tayari baadhi wameshajitokeza huku wakiwasubiri wengine wamalizia taratibu za kudhamini Bonanza hilo na matarajio ni kutolewa zawadi nono.
Bonanza hilo limeandaliwa kwa pamoja na Halmashauri ya Mji Kibaha, Majeshi ya mkoani Pwani ikiwa ni pamoja na Magereza, Polisi na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Mwisho.
  


WAVAMIZI WA VIWANJA VYA MICHEZO WAONYWA NA WAZIRI

Na John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watu wanaovamia maeneo ya viwanja vya michezo kukomesha tabia hiyo kwani inawanyima fursa vijana kushiriki kwenye michezo.
Aliyasema hayo hivi karibu mjini Kibaha wakati akifunga michuano ya kombe la Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka (Koka Cup) kwenye uwanja wa Mwendapole wilayani humo na kusema kuwa watu hao hawapaswi kuungwa mkono kwani wanawanyima ajira vijana.
Wambura alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo ya michezo na kujenga jambo ambalao linakwenda kinyume na matumizi yaliyopangwa na serikali hivyo vijana kushindwa kuendeleza vipaji vyao.
“Watu wenye tabia hii inabidi waiache kwani inadumaza azma ya serikali kuendeleza michezo mbalimbali hapa nchini hasa ikizingatiwa licha ya michezo kuwa ni burudani lakini pia inatoa fursa ya ajira hasa kwa vijana,” alisema Wambura.
Alisema kuwa serikali imekuwa na mipango mbalimbali ya kuendeleza michezo ikiwa ni pamoja na kuwa na viwanja ambavyo vitawawezesha vijana kushiriki michezo hivyo watu wanaovamia na kujenga ni dhahiri wanakwamisha juhudi hizo.
“Tunaomba wadau wa michezo wahamasishe ujengwaji wa viwanja vya kisasa ambapo baadhi ya watu wameonyesha uzalendo kwa kujenga viwanja ambavyo vinaendeleza jitihada za serikali kuendeleza michezo,” alisema Wambura.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kuandaa mashindano hayo ni kuwahamasisha vijana kushiriki michezo kwenye Jimbo lake ambapo alizipatia timu zote vifaa vya michezo kwa ajili ya kushiriki ligi hiyo.
Koka alisema kuwa jumla ya timu 168 katika Jimbo hilo zilishiriki ligi hiyo iliyoanzia ngazi ya mitaa hadi kata na baadaye kupata mshindi wa Jimbo ambapo jumla ya wachezaji zaidi ya 4,000 walishiriki michuano hiyo na bingwa alikuwa ni Home City toka kata ya pangani baada ya kuifunga Lisborn kutoka kata ya Kongowe kwa Penati 6-5.
Mshindi wa tatu ni Phata Farm ya Mkuza iliyoifunga Visiga  3-0, Bingwa alijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na kombe huku mshindi wa pili akijinyakulia 500,000 na medali na mshindi wa tatu akijinyakulia 200,000 ngao na medali 

Mwisho.

KATIBU TFF AWATAKA WABUNGE WAIBUE VIPAJI VYA SOKA VIJIJINI

Na John Gagarini, Bagamoyo

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka Nchini (TFF) Selestine Mwesigwa amewaomba wabunge kwenye Majimbo mbalimbali kuendeleza soka ngazi za chini ili kuibua wachezaji watakaokuwa wachezaji wa vilabu vikubwa pamoja na timu ya Taifa kwa siku za baadaye.

Aliyasema hivi karibuni wakati akikabidhi zawadi za washindi wa kombe la Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa (Kawambwa Cup) ambapo timu ya Jitegemee iliibuka mabingwa baada ya kuichapa Buma 2-0 kwenye uwanja wa Mwanakalenge wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.

Mwesigwa alisema kuwa wachezaji wengi walianzia ngazi za chini hivyo wabunge wana nafasi kubwa ya kuibua vipaji ambavyo vimejificha huko Vijijini na mashindano kama hayo ndiyo yenye uwezo wa kuwaibua vijana.

“Wabunge wengine wanapaswa kuiga mfano wa mashindano hayo ya Kawawmbwa Cup ni jambo la busara kwani linainua vipaji vya vijana, kujenga afya zao pia nakuomba usiishie hapa anzisha na mashindano ya mpira wa wanawake na sisi TFF tutakuunga mkono kwa hilo”, alisema Mwesigwa.

Aliwataka wachezaji wanaopata nafasi ya kwenda kucheza kwenye timu kubwa kujenga nidhamu na kuzingatia mafunzo ya makocha ili waweze kufikia mafanikio makubwa.

 Kwa upande wake Dk Kawambwa aliwashukuru wadau wote walioshirikiana nae kufanikisha mashindano hayo na kusema kuwa mashindano hayo yamedumu kwa miaka 10 mfululizo ambapo ameahidi kuyaboresha na kuyaendeleza katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Dk.Kawambwa alisema lengo la kuanzisha mashindano hayo ni kuibua vipaji vya vijana kuanzia vijiji, kata na wilaya pamoja na kuwaepusha kukaa vijiweni bila shughuli yoyote.
Timu ya Jitegemee Fc kata ya Magomeni iliibuka Kidedea katika mashindano hayo ya 2015 nakujinyakulia zawadi ya kombe, seti ya jezi, mipira miwili, pikipiki na medali ya dhahabu.

Mshindi wa pili alikuwa ni Buma waliopata seti ya jezi na mipira, na mshindi wa tatu timu ya Mwambao ilikabidhiwa seti ya jezi na mipira na  timu yenye nidhamu pamoja na kipa bora walipatiwa zawadi ya ngao. Mashindano ya Kawambwa Cup yalishirikisha vilabu 73 kutoka kata Saba za Jimbo la Bagamoyo.

Mwisho.

Friday, December 25, 2015

WAKWEPA USHURU WATAKIWA KUTUBU

Na John Gagarini, Kibaha
WATU waliokuwa wakijihusisha na ukwepaji kodi hapa nchini wametakiwa kutubu mbele za Mungu na kurejesha kile walicho kila ikiwa ni sehemu ya kuonyesha utii kwa mamlaka iliyopo madarakani kwani imewekwa na Mungu.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja Kibaha Isai Ntele kwenye Ibaada ya Krismasi na kusema kuwa kurejesha kile walichokwepa ni kumwogopa Mungu ambaye anataka kila mtu awajibike kwa kiongozi aliye madarakani.
Mch Ntele alisema kuwa Mungu alisikiliza kilio cha watanzania kwa kuwapa kiongozi ambaye ana uchungu na wananchi wake kwani ameonyesha dhahiri kuwa hataki haki za wanyonge zipotee kwa kudhulumiwa na wachache.
“Hata Biblia ina sema kila mtu aitii mamlaka iliyo kuu kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu na ile iliyopo nimeaminiwa  na Mungu hivyo aisye na mamlaka asipotii anashindana na agizo la Mungu hivyo watapata hukumu,” alisema Mch Ntele.
Alisema wakwepa kodi wanapingana na agizo la Mungu hivyo kwa wale waliofranya hivyo wanapaswa kulipa kodi au ushuru ili kuonyesha utii kwa mamlaka iliyopo sasa na watakuwa wamemweshimu Mungu.
“Waliokuwa wakikwepa wasirfanye hivyo tena na watubu na watasamehewa dhambi hiyo waliyoifanya na Mungu atatuelekeza kwenda kwenye njia sahihi kwani tutapata mema ya nchi yetu kama Mungu alivyo agiza,” alisema Mch Ntele.
Aliwataka wakristo kutumia kumbukumbu ya kuzaliwa kristo kwa kutenda mema na kuachana na matendo maovu ambayo hupelekea uvunjifu wa amani ili kuenzi upendo wa Yesu ambao ndiyo unaobeba sherehe hizi za Krismasi.
Naye mwinjilisti wa mtaa wa Luguruni Huruma Foya alisema kuwa watu wanapaswa kumwombea Rais akae kwenye mkono wa Mungu atatekeleza yale ambayo Mungu atamuelekeza katika kuiongoza nchi.
Foya alisema kuwa wakimwombea atakuwa ni msafi na hatatoa maamuzi ya kukurupuka ambayo yatawaumiza wananchi bali ataongozwa na Mungu katika shughuli mbalimbali za kuwatumikia wananchi.
Mwisho. 

WAVAMIZI WA VIWANJA VYA MICHEZO WAONYWA

John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watu wanaovamia maeneo ya viwanja vya michezo kukomesha tabia hiyo kwani inawanyima fursa vijana kushiriki kwenye michezo.
Aliyasema hayo hivi karibu mjini Kibaha wakati akifunga michuano ya kombe la Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka (Koka Cup) kwenye uwanja wa Mwendapole wilayani humo na kusema kuwa watu hao hawapaswi kuungwa mkono kwani wanawanyima ajira vijana.
Wambura alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo ya michezo na kujenga jambo ambalao linakwenda kinyume na matumizi yaliyopangwa na serikali hivyo vijana kushindwa kuendeleza vipaji vyao.
“Watu wenye tabia hii inabidi waiache kwani inadumaza azma ya serikali kuendeleza michezo mbalimbali hapa nchini hasa ikizingatiwa licha ya michezo kuwa ni burudani lakini pia inatoa fursa ya ajira hasa kwa vijana,” alisema Wambura.
Alisema kuwa serikali imekuwa na mipango mbalimbali ya kuendeleza michezo ikiwa ni pamoja na kuwa na viwanja ambavyo vitawawezesha vijana kushiriki michezo hivyo watu wanaovamia na kujenga ni dhahiri wanakwamisha juhudi hizo.
“Tunaomba wadau wa michezo wahamasishe ujengwaji wa viwanja vya kisasa ambapo baadhi ya watu wameonyesha uzalendo kwa kujenga viwanja ambavyo vinaendeleza jitihada za serikali kuendeleza michezo,” alisema Wambura.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kuandaa mashindano hayo ni kuwahamasisha vijana kushiriki michezo kwenye Jimbo lake ambapo alizipatia timu zote vifaa vya michezo kwa ajili ya kushiriki ligi hiyo.
Koka alisema kuwa jumla ya timu 168 katika Jimbo hilo zilishiriki ligi hiyo iliyoanzia ngazi ya mitaa hadi kata na baadaye kupata mshindi wa Jimbo ambapo jumla ya wachezaji zaidi ya 4,000 walishiriki michuano hiyo na bingwa alikuwa ni Home City toka kata ya pangani baada ya kuifunga Lisborn kutoka kata ya Kongowe kwa Penati 6-5.
Mshindi wa tatu ni Phata Farm ya Mkuza iliyoifunga Visiga  3-0, Bingwa alijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na kombe huku mshindi wa pili akijinyakulia 500,000 na medali na mshindi wa tatu akijinyakulia 200,000 ngao na medali  
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha
BONANZA la kuuaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka 2016 linatarajiwa kufanyika Januari Mosi mwakani kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Msajili Msaidizi wa Vilabu na Vyama vya Michezo wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Abdul Haufi alisema kuwa Bonanza hilo litakuwa la wazi kwa watu wote.
Haufi alisema kuwa shindano hilo litakuwa la michezo mbalimbali litashirikisha mashirika ya Umma, binafsi pamoja na watu binafsi au mtu mmoja mmoja kwenye michezo ya soka, mpira wa pete kwa wanawake, kuvuta kamba, riadha mita 100.
Alitaja michezo mingine kuwa ni kukimbia na magunia, kurusha kisahani, tufe, mpira wa wavu, kijiko na ndimu ambapo usajili unafanyika kwenye ofisi za Halmashauri hiyo.
“Tunatarajia jumla ya wanamichezo 250 kushiriki Bonanza hilo la aina yake kufanyika mjini Kibaha na vitongoji vyake ambapo lengo ni kuhamasisha watu kushiriki michezo pamoja na kudumisha urafiki baina ya mashirika bianafsi, ya umma pamoja na watu binafsi,” alisema Haufi.
Aidha alisema kuwa juu ya wadhamini tayari baadhi wameshajitokeza huku wakiwasubiri wengine wamalizia taratibu za kudhamini Bonanza hilo na matarajio ni kutolewa zawadi nono.
Bonanza hilo limeandaliwa kwa pamoja na Halmashauri ya Mji Kibaha, Majeshi ya mkoani Pwani ikiwa ni pamoja na Magereza, Polisi na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Mwisho.