Thursday, December 19, 2024

STAMICO YATAKA WATANZANIA WATAKIWA KUTUMIA NISHATI SAFI NA SALAMA YA MKAA WA RAFIKI BRIQUETTES


KATIKA kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limewataka Watanzania kutumia Mkaa wa Rafiki Briquettes.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na ofisa masoko wa (Stamico) Hope Mahokola wakati wa maonyesho ya Uwekezaji na Biashara ya Mkoa wa Pwani.

Mahokola amesema kuwa mkaa huo ni nishati safi na salama na una uwezo wa kuwaka kwa zaidi ya saa tatu baada ya kuwashwa.

"Tunamuunga mkono Rais Dk Samia Suluhu Hassan kuhamasisha matumizi ya nishati safi ili kulinda mazingira ili kutoharibu uoto wa asili ili usisababishe mabadiliko tabianchi hivyo Watanzania watumie mkaa wa Rafiki Briquettes ili kulinda mazingira,"amesema Mahokola.

Amesema kuwa mkaa huo unatolana na mabaki ya makaa ya mawe hauna moshi na ni safi na salama katika kupikia na unachangia kupunguza mabadiliko ya Tabianchi.

"Mkaa huu unaweza kutumika nyumbani, vyuoni, mashuleni na sehemu nyingine zenye uhitaji wa nishati ya kupikia,"amesema Mahokola.

Aidha amesema kuwa mkaa huo ni rafiki kwa matimizi, mazingira na gharama na mkaa huo unatokana na makaa ya mawe yanayochimbwa kwenye mgodibwa Kiwira-Kabulo Mkoani Songwe.

TAASISI YA ANJITA YATAKA USHIRIKIANO KUKABILIANA NA UKATILI WA KIJINSIA










TAASISI ya Anjita Child Development Foundation iliyopo Halmashauri ya Mji Kibaha imeomba wadau wa kupinga ukatili kushirikiana ili kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwenye jamii.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia Mkurugenzi wa Taasisi hiyo ya Anjita Janeth Malela amesema kuwa ili kufikia hatua ya kupunguza matukio hayo lazima watu, taasisi na mashirika waungane kukabili vitendo hivyo.

Malela amesema kuwa kabla ya kufikia hitimisho la siku hizo 16 za kupinga ukatili walitoa elimu kwa jamii juu ya kukabiliana na vitendo hivyo ambapo jamii imepata uelewa kwani wamejengewa uwezo.

"Tumetoa elimu hiyo na imeonyesha kuwa ndani ya jamii bado matukio kama hayo yanajitokeza hivyo tumewapatia uelewa na namna ya kuripoti mara waonapo matukio kama hayo ili hatua stahiki zichukuliwe,"amesema Malela.

Amesema kuwa ili kupunguza au kutokomeza vitendo hivyo lazima wadau waungane kwa pamoja kwa kutoa elimu kwa jamii ili kukabili vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Taasisi ya Anjita inashughulisha zinazohusiana na watoto na vijana pia kundi la watu wazima kupitia elimu ya malezi changamshi  kwa wazazi na walezi kupitia mradi wa Mtoto Kwanza.

Katika kuhitimisha kilele hicho cha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili Taasisi ya Anjita ilipewa cheti cha pongezi na ófisi ya mkuu wa Mkoa wa Pwani cha kushiriki kikamilifu katika kutoa elimu ya kupambana na ukatili wa kijinsia maeneo mbalimbali ya Mji wa Kibaha.

Wednesday, December 18, 2024

KINGLION KUTOA AJIRA



KIWANDA cha kuzalisha malighafi zitumikazo kwenye uzalishaji vyuma na mabati na usambazaji wa pikipiki cha Kinglion kinatarajia kutoa ajira kwa watu 1,500 ajira za kudumu na ajira za muda zaidi ya 5,000.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa wiki ya maonyesho  ya Biashara na Viwanda ya Mkoa wa Pwani meneja wa kiwanda hicho Anold Lyimo amesema kuwa kiwanda hicho kitafunguliwa muda siyo mrefu.

Lyimo amesema kuwa mara kiwanda hicho kitakapoanza uzalishaji vijana wengi watapata ajira na kuongeza pato la Taifa kwani kitakuwa kiwanda kikubwa na kitauza bidhaa zake hadi nje ya Tanzania yaani nchi jirani.

"Kiwanda kilikuwa kianze uzalishaji mwaka huu lakini kuna changamoto kidogo ikiwa ni pamoja na barabara na gesi ambavyo serikali inavifanyia kazi ili kukabili changamoto hizo,"amesema Lyimo.

Aidha alisema kuwa wanatarajia kiwansa kitakapoanza kazi kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 35,000 kwa mwaka.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema kuwa Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini Tanzania (TARURA) wataijenga barabara ya kuelekea kiwandani huko yenye urefu wa kilometa 2.5.

Kunenge amesema kuwa pia wanatarajia kusambaziwa gesi kwenye eneo la viwanda la Zegereni ikiwemo kwenye kiwanda hicho cha Kinglion.

MLEZI WA KAMATI YA USALAMA BARABARANI ACP MORCASE AONGOZA KIKAO CHA KAMATI


Mlezi wa Kamati ya usalama barabarani Mkoa wa Pwani, Kamishina Msaidizi wa Polisi Salim Morcase Disemba 17 amekiongoza kikao cha kamati ya usalama barabarani ambacho kimejadili maswala mbalimbali ikiwemo kuondoa msongamano wa foleni kwenye barabara kuu za Mkoa wa Pwani na kuweka mikakati ya pamoja ya kumaliza foleni hizo ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua kali kwa madereva watakaobainika kupandisha nauli za mabasi kwenye kipindi hiki cha sikukuu za mwisho wa mwaka pamoja na madereva wanaokaidi kutii Sheria za usalama barabarani kwa watumiaji wengine wa barabara.

Saturday, December 14, 2024

VITENDO VYA UKATILI PWANI VYAPUNGUA










HUKU Tanzania ikiwa imehitimisha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili matukio kwa Mkoani wa Pwani yamepungu kutoka matukio 8,573 mwaka 2023 na kufikia matukio 6,916 mwaka huu sawa na asilimia 19.3.

Hayo yamesemwa na Edna Kataraiya kutoka Ofisi ya Mipango na Uratibu Mkoa wa Pwani wakati wa kuhitimisha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili kimkoa zilifanyika Kwa Mbonde Wilayani Kibaha.

Kataraiya amesema kuwa ofisi yake inashughulikia matukio yanayohusiana na matukio hayo kwa asilimia 40 huku matukio mengine asilimia 60 yanashughulikiwa na idara ya afya.

Kwa upande wake Polisi Kata ya ya Picha ya Ndege Ibrahim Makaruti amesema kuwa moja ya changamoto inayojitokeza ni baadhi ya wazazi kumalizana nyumbani pasipo kuyapeleka kwenye vyombo vya sheria.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Watu Wenye Ulamavu Tanzania (SHIVYAWATA) Kibaha Mjni Jabir Makasala alisema kuwa kutungwe sera ya kuwakopesha wazazi wenye watoto wenye ulemavu ili wafanye shughuli za ujasiriamali kwani wazazi hao hawana kipato chochote.

Naye Mkurugenzi wa African Talent Forum (ATF) Rosemery Bujash amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu ya kupinga vitendo vya ukatili kwa vijana wa makundi mbalimbali kupitia sanaa na michezo.

Akitoa salamu za taasisi ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Mariam Mnengwah amesema kuwa wao walitoa elimu iliyosaidia kuibua vitendo vya ukatili na kutoa msaada wa kisheria na msaada wa matibabu.





  

CATHERINE MWENYEKITI MTAA WA SOFU NA MKAKATI WA KUJENGA OFISI SERIKALI YA MTAA.


**Catherine baada ya kumshinda Mwenyekiti mwanaume aliyeongoza kwa miaka 10 na kuambiwa Mtaa hauwezi kuongozwa na Mwanamke aondoa mawazo hayo, lengo lake ni kujenga ofisi ya Serikali ya Mtaa**

MWENYEKITI wa Mtaa wa Sofu kata ya Sofu wilaya ya Kibaha Catherine Lyimo ameweka mikakati ya kuhakikisha mtaa huo unakuwa na ofisi yake badala ya kupanga.

Lyimo akizungumza na mwandishi wa habari hizi amesema kuwa hilo ndiyo jambo ambalo ni kipaumbele chake mara baada ya kuchguliwa kwenye uchaguzi wa serikali za mita uliofanyika hivi karibuni na yeye kushinda nafasi hiyo.

Amesema kuwa eneo tayari wanalo wanachofanya ni kuwaandikia wadau wa maendeleo kwenye mtaa huo kwa kushirikiana na wananchi kufanya ujenzi huo ambao ni ndoto yake kuhakikisha mkakati wa kuwa na ofisi unafanikiwa.

“Mpango mkakati wa mtaa kwa sasa ni kuwa na ofisi yake badala ya kutumia ofisi za watu wengine tunataka tuwe na ofisi yetu wenyewe ili tufanye kazi kwa uhuru badala ya kutegemea wengine kwani kutumia ofisi za watu wengine kuna changamoto zake,”amesema Lyimo.

Aidha amesema kuwa anamatumaini ofisi itajengwa kutokana na ushirikiano anaoupata kutoka kwa wananchi na wadau wa maendeleo kwani anaamini ushirikiano huo utafanikisha kupatikana kwa ofisi ya mtaa huo.

“Nataka kwa kushirikiana wananchi na wadau kuhakikisha tunaacha alama ya uongozi kwa kujenga ofisi yetu kwani tukiwa na ofisi yetu tutakuwa na uhuru na tutajenga kutokana na mahitaji ya mtaa wetu ambapo itakuwa na vyumba kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi,”amesema Lyimo.

Amebainisha kuwa jambo lingine ambalo atahakikisha linafanyika ni kuwagawia wananchi eneo la kufanyiabiashara kwa ananchi wa mtaa huo ili waweze kupata huduma ya soko karibu kwani wanataka liwe soko dogo ili kuwaongezea wananchi kipato na kutoa huduma.

“Tunahitaji tuwe na eneo ambalo litakuwa kama soko ambapo wananchi watauza bidhaa zao badala ya kwenda mbali kufuata mahitaji yao nyumbani tunataka wapate hapa jirani na pia itakuwa ni sehemu ya kujiongezea kipato,”amesema Lyimo.

Lyimo alifanikiwa kushinda nafasi hiyo baada ya kumshinda aliyekuwa mwenyekiti wa Mtaa huo Lazaro Joseph ambaye aliongoza kwa vipindi viwili vya miaka 10 huku yeye akiwa ni mjumbe wa serikali ya mtaa huo ambapo alishindwa kwenye nasafi hiyo na mtangulizi wake mwaka 2019 na alikuwa ni mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania Kata ya Sofu na Mjumbe wa mtaa.

Friday, December 13, 2024

MBONI MWANAMKE WA SHOKA AWEKA MIKAKATI YA UJENZI WA MATUNDU YA VYOO VYA SEKONDARI BAMBA


**Licha ya kuwa Mjane haukumzuia kupambana kutoka ujumbe hadi Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa ndoto yake kujenga Sekondari  ndani ya Mtaa anaoungoza kuwapunguzia watoto umbali kwenda shule** 

WAKAZI wa Mtaa wa Bamba Wilaya ya Kibaha wamejipanga kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa vyoo vya shule ya sekondari Bamba inakamilika ili ikifika Januari mwaka 2025 ifunguliwe na kupokea wanafunzi zaidi ya 100 wa mtaa huo ambao wanasoma shule za sekondari za mbali ambapo hutembea umbali wa kilometa sita kwenda na kurudi shuleni. 

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake Mwenyekiti wa Mtaa huo Mboni Mkomwa amesema kuwa shule hiyo shule hiyo ina madarasa manne yamekamilika isipokuwa wana mahitaji ya matundu nane ili ikamilke na kuanza masomo kwa wanafunzi wanaotoka mtaa huo.

Mkomwa amesema kuwa kwa sasa anaandaa mpango wa kukutana na wadau wa maendeleo wa mtaa huo ili kufanya harambee ya kuchangia kukamilisha ujenzi wa vyoo hivyo kabla ya mwaka huu kwisha ili hadi Januari viwe vimekamilika na wanafunzi kuanza kusoma.

“Wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa huu wanasoma shule za sekondari za Mwambisi na Miembe Saba ambako ni mbali hivyo baada ya kuona changamoto hiyo tulikaa na wananchi na kukubaliana kujenga madarasa ambapo manne yamekamilika kilichobaki ni vyoo  matundu nane yakikamilika hayo shule inaanza,”amesema Mkomwa.

Amesema kuwa wanaishukuru serikali ambayo ilitoa kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi huo pia wananchi nao walichangia kila kaya 2,000 na kufanikisha ujenzi huo kufikia hapo na kubaki hatua ndogo ili ianze.

“Tuliomba tena fedha ila walituambia kuwa wasubiri hadi kipindi cha bajeti ambapo malengo yetu hayatafikia kwani bajeti ni katikati ya mwaka ambapo mwanzo wa mwaka tunataka wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa wetu waanze kusoma hapo pia itasaidia maeneo ya mitaa jirani ambao nao watanufaika,”amesema Mkomwa.

Aidha amesema kuwa changamoto nyingine ambayo iko kwenye mipango yake katika kuitatua ni baadhi ya wakazi wa mtaa wake wapatao 23 hawana huduma ya maji kabisa hali ambayo inawasababisha kupata shida ya kupata maji kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya kawaida.

“Wakazi hao waliandika barua baada ya kukaa kikao lakini wakifika Dawasa wanaambia watoe milioni mbili au wasubiri mradi upite maeneo yao jambo ambalo kwao bado ni mtihani na wanahitaji bomba kubwa la nchi sita ili wananchi waweze kuvuta maji kwa urahisi ambapo kwa sasa wanapotaka kuvuta maji kwa majirani huwabidi kuwalipa na kuilipa Daawasa hivyo kujikuta wakilipa mara mbili,”amesema Mkomwa.

Mkomwa alishinda kwenye uchaguzi wa wenyeviti uliofanyika hivi karibuni na alichaguliwa akiwa anatoka kuwa mjumbe wa mtaa huo kwa kipindi cha miaka mitano pia alikuwa mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) tawi la Bamba ambapo mtaa huo una jumla ya wananchi 7,546 yeye ni mjane akiwa na watoto watatu na alifiwa na mume wake mwaka 2015 na ni mjasiriamali.