Wednesday, December 18, 2024

MLEZI WA KAMATI YA USALAMA BARABARANI ACP MORCASE AONGOZA KIKAO CHA KAMATI


Mlezi wa Kamati ya usalama barabarani Mkoa wa Pwani, Kamishina Msaidizi wa Polisi Salim Morcase Disemba 17 amekiongoza kikao cha kamati ya usalama barabarani ambacho kimejadili maswala mbalimbali ikiwemo kuondoa msongamano wa foleni kwenye barabara kuu za Mkoa wa Pwani na kuweka mikakati ya pamoja ya kumaliza foleni hizo ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua kali kwa madereva watakaobainika kupandisha nauli za mabasi kwenye kipindi hiki cha sikukuu za mwisho wa mwaka pamoja na madereva wanaokaidi kutii Sheria za usalama barabarani kwa watumiaji wengine wa barabara.

Saturday, December 14, 2024

VITENDO VYA UKATILI PWANI VYAPUNGUA










HUKU Tanzania ikiwa imehitimisha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili matukio kwa Mkoani wa Pwani yamepungu kutoka matukio 8,573 mwaka 2023 na kufikia matukio 6,916 mwaka huu sawa na asilimia 19.3.

Hayo yamesemwa na Edna Kataraiya kutoka Ofisi ya Mipango na Uratibu Mkoa wa Pwani wakati wa kuhitimisha siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili kimkoa zilifanyika Kwa Mbonde Wilayani Kibaha.

Kataraiya amesema kuwa ofisi yake inashughulikia matukio yanayohusiana na matukio hayo kwa asilimia 40 huku matukio mengine asilimia 60 yanashughulikiwa na idara ya afya.

Kwa upande wake Polisi Kata ya ya Picha ya Ndege Ibrahim Makaruti amesema kuwa moja ya changamoto inayojitokeza ni baadhi ya wazazi kumalizana nyumbani pasipo kuyapeleka kwenye vyombo vya sheria.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Watu Wenye Ulamavu Tanzania (SHIVYAWATA) Kibaha Mjni Jabir Makasala alisema kuwa kutungwe sera ya kuwakopesha wazazi wenye watoto wenye ulemavu ili wafanye shughuli za ujasiriamali kwani wazazi hao hawana kipato chochote.

Naye Mkurugenzi wa African Talent Forum (ATF) Rosemery Bujash amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu ya kupinga vitendo vya ukatili kwa vijana wa makundi mbalimbali kupitia sanaa na michezo.

Akitoa salamu za taasisi ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Mariam Mnengwah amesema kuwa wao walitoa elimu iliyosaidia kuibua vitendo vya ukatili na kutoa msaada wa kisheria na msaada wa matibabu.





  

CATHERINE MWENYEKITI MTAA WA SOFU NA MKAKATI WA KUJENGA OFISI SERIKALI YA MTAA.


**Catherine baada ya kumshinda Mwenyekiti mwanaume aliyeongoza kwa miaka 10 na kuambiwa Mtaa hauwezi kuongozwa na Mwanamke aondoa mawazo hayo, lengo lake ni kujenga ofisi ya Serikali ya Mtaa**

MWENYEKITI wa Mtaa wa Sofu kata ya Sofu wilaya ya Kibaha Catherine Lyimo ameweka mikakati ya kuhakikisha mtaa huo unakuwa na ofisi yake badala ya kupanga.

Lyimo akizungumza na mwandishi wa habari hizi amesema kuwa hilo ndiyo jambo ambalo ni kipaumbele chake mara baada ya kuchguliwa kwenye uchaguzi wa serikali za mita uliofanyika hivi karibuni na yeye kushinda nafasi hiyo.

Amesema kuwa eneo tayari wanalo wanachofanya ni kuwaandikia wadau wa maendeleo kwenye mtaa huo kwa kushirikiana na wananchi kufanya ujenzi huo ambao ni ndoto yake kuhakikisha mkakati wa kuwa na ofisi unafanikiwa.

“Mpango mkakati wa mtaa kwa sasa ni kuwa na ofisi yake badala ya kutumia ofisi za watu wengine tunataka tuwe na ofisi yetu wenyewe ili tufanye kazi kwa uhuru badala ya kutegemea wengine kwani kutumia ofisi za watu wengine kuna changamoto zake,”amesema Lyimo.

Aidha amesema kuwa anamatumaini ofisi itajengwa kutokana na ushirikiano anaoupata kutoka kwa wananchi na wadau wa maendeleo kwani anaamini ushirikiano huo utafanikisha kupatikana kwa ofisi ya mtaa huo.

“Nataka kwa kushirikiana wananchi na wadau kuhakikisha tunaacha alama ya uongozi kwa kujenga ofisi yetu kwani tukiwa na ofisi yetu tutakuwa na uhuru na tutajenga kutokana na mahitaji ya mtaa wetu ambapo itakuwa na vyumba kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi,”amesema Lyimo.

Amebainisha kuwa jambo lingine ambalo atahakikisha linafanyika ni kuwagawia wananchi eneo la kufanyiabiashara kwa ananchi wa mtaa huo ili waweze kupata huduma ya soko karibu kwani wanataka liwe soko dogo ili kuwaongezea wananchi kipato na kutoa huduma.

“Tunahitaji tuwe na eneo ambalo litakuwa kama soko ambapo wananchi watauza bidhaa zao badala ya kwenda mbali kufuata mahitaji yao nyumbani tunataka wapate hapa jirani na pia itakuwa ni sehemu ya kujiongezea kipato,”amesema Lyimo.

Lyimo alifanikiwa kushinda nafasi hiyo baada ya kumshinda aliyekuwa mwenyekiti wa Mtaa huo Lazaro Joseph ambaye aliongoza kwa vipindi viwili vya miaka 10 huku yeye akiwa ni mjumbe wa serikali ya mtaa huo ambapo alishindwa kwenye nasafi hiyo na mtangulizi wake mwaka 2019 na alikuwa ni mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania Kata ya Sofu na Mjumbe wa mtaa.

Friday, December 13, 2024

MBONI MWANAMKE WA SHOKA AWEKA MIKAKATI YA UJENZI WA MATUNDU YA VYOO VYA SEKONDARI BAMBA


**Licha ya kuwa Mjane haukumzuia kupambana kutoka ujumbe hadi Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa ndoto yake kujenga Sekondari  ndani ya Mtaa anaoungoza kuwapunguzia watoto umbali kwenda shule** 

WAKAZI wa Mtaa wa Bamba Wilaya ya Kibaha wamejipanga kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa vyoo vya shule ya sekondari Bamba inakamilika ili ikifika Januari mwaka 2025 ifunguliwe na kupokea wanafunzi zaidi ya 100 wa mtaa huo ambao wanasoma shule za sekondari za mbali ambapo hutembea umbali wa kilometa sita kwenda na kurudi shuleni. 

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake Mwenyekiti wa Mtaa huo Mboni Mkomwa amesema kuwa shule hiyo shule hiyo ina madarasa manne yamekamilika isipokuwa wana mahitaji ya matundu nane ili ikamilke na kuanza masomo kwa wanafunzi wanaotoka mtaa huo.

Mkomwa amesema kuwa kwa sasa anaandaa mpango wa kukutana na wadau wa maendeleo wa mtaa huo ili kufanya harambee ya kuchangia kukamilisha ujenzi wa vyoo hivyo kabla ya mwaka huu kwisha ili hadi Januari viwe vimekamilika na wanafunzi kuanza kusoma.

“Wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa huu wanasoma shule za sekondari za Mwambisi na Miembe Saba ambako ni mbali hivyo baada ya kuona changamoto hiyo tulikaa na wananchi na kukubaliana kujenga madarasa ambapo manne yamekamilika kilichobaki ni vyoo  matundu nane yakikamilika hayo shule inaanza,”amesema Mkomwa.

Amesema kuwa wanaishukuru serikali ambayo ilitoa kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi huo pia wananchi nao walichangia kila kaya 2,000 na kufanikisha ujenzi huo kufikia hapo na kubaki hatua ndogo ili ianze.

“Tuliomba tena fedha ila walituambia kuwa wasubiri hadi kipindi cha bajeti ambapo malengo yetu hayatafikia kwani bajeti ni katikati ya mwaka ambapo mwanzo wa mwaka tunataka wanafunzi wanaotoka kwenye mtaa wetu waanze kusoma hapo pia itasaidia maeneo ya mitaa jirani ambao nao watanufaika,”amesema Mkomwa.

Aidha amesema kuwa changamoto nyingine ambayo iko kwenye mipango yake katika kuitatua ni baadhi ya wakazi wa mtaa wake wapatao 23 hawana huduma ya maji kabisa hali ambayo inawasababisha kupata shida ya kupata maji kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya kawaida.

“Wakazi hao waliandika barua baada ya kukaa kikao lakini wakifika Dawasa wanaambia watoe milioni mbili au wasubiri mradi upite maeneo yao jambo ambalo kwao bado ni mtihani na wanahitaji bomba kubwa la nchi sita ili wananchi waweze kuvuta maji kwa urahisi ambapo kwa sasa wanapotaka kuvuta maji kwa majirani huwabidi kuwalipa na kuilipa Daawasa hivyo kujikuta wakilipa mara mbili,”amesema Mkomwa.

Mkomwa alishinda kwenye uchaguzi wa wenyeviti uliofanyika hivi karibuni na alichaguliwa akiwa anatoka kuwa mjumbe wa mtaa huo kwa kipindi cha miaka mitano pia alikuwa mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) tawi la Bamba ambapo mtaa huo una jumla ya wananchi 7,546 yeye ni mjane akiwa na watoto watatu na alifiwa na mume wake mwaka 2015 na ni mjasiriamali.  



Thursday, December 12, 2024

NMB YAKABIDHI VIFAA VYA KUJIFUNGULIA NA MASHUKA HOSPITALI YA WILAYA YA RUFIJI UTETE

BENKI ya NMB imetoa vifaa vya kujifungulia mama wajawazito seti 300 na mashuka 300 kwenye Hospitali ya Wilaya ya Rufiji Utete vyenye thamani ya shilingi milioni 12.3.

Aidha benki hiyo imetoa msaada huo ikiwa ni sehemu ya kumkumbuka mpigania Uhuru wa Tanzania Bibi Titi Mohamed kupitia tamasha la (Bibi Titi Mohamed Festival) linalofanyika kila mwaka.

Akipokea vifaa hivyo hospitalini hapo Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Mbunge wa Jimbo la Rufiji Mohamed Mchengerwa ameishukuru benki hiyo kwa kutoa msaada huo.

Mchengerwa amesema kuwa benki hiyo imemuenzi mwasisi huyo ambaye pia ni Mbunge wa kwanza wa Rufiji na imeonyesha uzalendo kwa kuwasaidia wakinamama wajawazito kwenye hospitali hiyo ya Wilaya ya Utete.

Sunday, December 8, 2024

MAFUNZO KWA VIONGOZI VIJANA KUTAIMARISHA VYAMA





ILI kuwa na vyama vya siasa imara na kuwa na serikali imara vyama hivyo vimetakiwa kuwa na mafunzo kwa viongozi vijana ili waendeleze maono ya waasisi wa vyama vya ukombozi Kusini mwa Afrika.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar Dk Mohammed  Said  Mohammed  wakati wa akifunga Mafunzo ya 13 ya uongozi vijana kutoka vyama sita vya ukombozi Kusini mwa Afrika kuhusu masuala ya maendeleo kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere Kibaha.

Mohamed amesema kuwa kuwekeza kwenye mafunzo kwa vijana itakuwa na vyama imara ambavyo vitajenga serikali zenye uwezo.

"Historia ya vyama hivi sita ni kuwa vinamshikamano wa kweli tangu enzi hizo kujenga ukombozi wa siasa kwa maono ya waasisi hivyo vijana hawa wanapaswa kurithishwa ili wawe viongozi bora,"amesema Mohamed.

Amesema kuwa ili kuleta ufanisi wa vyama na nchi yapaswa kuwekeza elimu na mafunzo kwa vijana ili kuleta mafanikio na yanategemea kwa kuwa na maono ya waasisi wa mataifa hayo.

"Mafunzo haya ni bora kwani yamezidi kuwandaa vijana kuwa viongozi bora wa baadaye kwa mustkbali wa vyama na nchi kwa ujumla,"amesema Mohamed.

Aidha amesema kuwa wanaishukuru nchi ya China kupitia Chama Cha Kikomunisti cha CPC ambacho kimekuwa kikivisaidia vyama hivyo sita rafiki na  imesaidia Afrika kwenye sekta za afya usafiri, na viwanda.

"Wahitimu muwe kigezo cha kujenga masoko ya pamoja na masoko na nchi ya China ni muhimu sana kwani ushirikiano wa kibiashara kati ya nchi hizo ni kubwa pia tunashukuru chama cha CPC kwa kufadhili wa mafunzo haya,"amesema Mohamed.

Kwa upande wake Mkuu wa Shule hiyo ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere Profesa Marcelina Chijoriga amesema kuwa mafunzo mbalimbali ya uongozi yamekuwa yakitolewa kwa vijana kupitia vyama hivyo.

Chijoriga amesema kuwa mafunzo hayo ni kuwaandaa vijana ili kuwa viongozi bora wa baadaye ambapo wanafundishwa juu ya masuala ya maendeleo na kujifunza maono ya viongozi ambao ni waasisi wa mataifa hayo kwa kushirikiana na CPC.

Mafunzo hayo siku 10 yaliwashirikisha viongozi vijana zaidi ya 100 kutoka vyama vya ANC-Afrika Kusini, CCM-Tanzania, FRELIMO-Msumbiji, MPLA-Angola, SWAPO-Namibia na ZANU-PF-Zimbabwe.


KIBAHA SHOPPING MALL YAZINDULIWA DC AWATAKA WANANCHI WASIENDE DAR ES SALAAM KILA KITU KIPO

MKUU wa Wilaya ya Kibaha Nickson John amezindua soko la kisasa (Kibaha Shopping Mall) lenye thamani ya shilingi milioni 8 ambalo litakuwa likiingizia Halmashauri ya Mji Kibaha kiasi cha shilingi milioni 660.7 kwa mwaka.

John amezindua soko hilo ambalo linamilikiwa na Halmashauri ya Mji Kibaha lipo kwenye eneo la kitovu cha Mji (CBD) amesema kuwa huo ni mradi wa kimkakati ambapo fedha za ujenzi zimetokana na fedha kutoka serikali kuu.

Amesema kuwa soko hilo ni mkombozi kwa wananchi wa Kibaha ambapo haitawalazimu kwenda Jijini Dar es Salaam kufuata bidhaa lakini bidhaa hizo zitakuwazikipatikana kwenye soko hilo ambalo limejengwa kwa miundombinu ya kisasa.

"Kuanzia sasa mtakuwa mnanunua hapa na hamtahitajika kufuata bidhaa Jijni Dar es Salaam hivyo mtapunguzagharama za nauli pamoja na muda ambao mneutumia kufuata bidhaa ambapo hapa zitapatikana kwa bei ya jumla na   rejereja",amesema John.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa amesema kuwa mradi huo umeshakamilika na umeanza kazi ambapo kwa sasa uko kwenye kipindi cha matazamio.

Shemwelekwa amesema kuwa soko hilo lina sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja maduka 63, super market moja, kumbi za benki mbili, Atm mbili, eneo la kuchezea moja ni ya chakula mawili, eneo la kuangalia michezo moja, ukumbi wa mikutano mmoja, maegesho ya pikipiki 50, taxi 10, magari 100 na bajaji 30.


mwisho.