Wednesday, June 12, 2024

WATU WENYE ULEMAVU WATAKA KUTEULIWA NAFASI NGAZI ZA MAAMUZI

CHAMA Cha Watu Wenye UalbinoTanzania (TAS) kimeiomba serikali iwateue kwenye nafasi za ngazi za maamuzi.

Aidha ametaja nafasi hizo za maamuzi kama vile Uwaziri, Ukuu wa Mikoa na Ukuu wa Wilaya kwani nao wanauwezo kama walivyo watu wengine.

Hayo yamesemwa na Mjumbe wa Bodi ya chama hicho Thomas Diwani wakati akitoa salama za chama kwenye kongamano la kuongeza uelewa juu ya Ualbino lililofanyika kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere Kwa Mfipa Kibaha.

Naye Mkurugenzi kitengo cha huduma kwa watu wenye ulemavu Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Rasheed Maftah amesema kuwa serikali inaanda sera na miongozo mbalumbali kwa watu wenye ulemavu za kuweka usawa na haki.

Awali mwenyekiti wa Tas Godson Mollel amesema kuwa wanampongeza Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia Hospitali Rufaa ya KCMC kwa kuwapatia kiasi cha shilingi milioni 124 kwa ajili ya kuzalisha losheni zinazotumiwa na watu wenye ualbino.

Kwa upande wake kaimu mkuu wa mkoa wa Pwani Nickson John amesema kuwa watu wenye ualbino wapatao 368 wanapatiwa misaada mbalimbali na zimeundwa kamati za watu wenye ualbino.


MAHAKAMA YATAKIWA KUTOA ADHABU KALI WANAOWAFANYIA VITENDO VYA UKATILI WATU WENYE UALBINO



CHAMA cha watu wenye Ualbino Tanzania (TAS) kimeiomba Mahakama kutoa adhabu kali kwa watu wanaokutwa na hatia ya kuwakata viungo au kuwaua watu wenye Ualbino.

Hayo yamesemwa mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Taifa wa TAS Godson Mollel alipozungumza na waandishi wa habari wakati wa maadhimisho ya kitaifa ya siku kuongeza uelewa juu ya Ualbino (IAAD) duniani.

Mollel amesema kuwa Mahakama ikotoa hukumu kali kwa wahusika hao itakuwa fundisho kwa watu wanaojihusisha na vitendo hivyo kuacha kuwadhuru watu wenye Ualbino.

Naye ofisa ustawi mkuu toka Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana na Watu wenye ulemavu Joy Maongezi amesema kuwa sheria namba 9 ya mwaka 2010 inataka kuwa na haki kwa watu wenye ulemavu ambapo watu wenye Ualbino ni sehemu yao.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Shangwe Twamala amesema kuwa wakati wa maadhimisho hayo huduma mbalimbali zinatolewa ikiwa ni pamoja na upimaji saratani ya ngozi, utoaji miwani, kofia na losheni ya kuzuia ngozi kuathirika, upimaji wa tezi dume na kansa ya kizazi.

Maadhimisho hayo hufanyika kila mwaka duniani ambapo kilele huwa tarehe 13 Juni kila mwaka na kwa mwaka huu kitaifa yanafanyika Kibaha Mkoani Pwani.


Monday, June 10, 2024

KAMPUNI YA REFUELLING TANZANIA LIMITED YATOA MABATI 72 KWA KIKUNDI CHA KUKAYA MIONO

KAMPUNI ya Refuelling Tanzania Ltd imekipatia mabati 72 kikundi cha KUKAYA-Miono Chalinze Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa ya shule ya msingi Miono.

Akipokea mabati hayo kwa niaba ya kikundi cha KUKAYA MIONO ,Mwenyekiti Omary Mtiga ameishukuru kampuni ya Refuelling kwa msaada huo.

Alieleza ujenzi una miezi sita kwa nguvu zao wananchi ,wameshapokea milioni 13.5 kutoka kwa wadau, lengo lilikuwa kujenga kuongeza darasa moja lakini wamefanikiwa kujenga madarasa mawili.

Mtiga alifafanua, kwasasa bado kuna mahitaji ya mabati 34 ,malori sita ya mchanga ,maroli manne ya kokoto na mifuko ya saruji 60 ili kukamilisha ujenzi huo.

"Tunashukuru uongozi wa kampuni hii, chini ya Mkurugenzi Mohsin Bharwani ambae ameguswa na jambo hili, Mohsin amekuwa akijitoa katika masuala ya kijamii kwenye maeneo mengi ndio na sisi tuliamua kumuomba msaada na tunashukuru kutusaidia "

Aidha Mtiga alitoa wito kwa makampuni na wadau wengine kuendelea kujitolea kwani bado kuna uhitaji.

Aliiomba jamii Miono kuendelea kushirikiana katika masuala ya maendeleo ili kujiinua kimaendeleo ikiwemo kuboresha sekta ya elimu.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa kampuni ya Refuelling Tanzania limited, Mohsin Bharwani, Meneja wa kampuni hiyo Renatus Kabeyo alisema wamekabidhi mabati 72 na kusafirisha jumla milioni mbili (mil.2).

Alifafanua kuwa, kampuni hiyo inashirikiana na jamii kwa kila jambo kulingana na uwezo wao.

"Nimeona kuna madarasa tunaona mnajenga ,vyoo ,niweze kuahidi tutajenga hoja ,pamoja na misaada inayokuja nikuombe ofisa elimu kata andika andiko ,ili mpate misaada mikubwa kutoka kwa wadau mbalimbali" alieleza Kabeyo.

Kabeyo alisema wanafunzi wanasoma ila wanatakiwa kusoma kwenye mazingira bora.

Sunday, June 9, 2024

375 WAFAULU BUNDIKANI SEC YAFUTA ZIRO

SHULE ya Sekondari ya Kata ya Maili Moja Bundikani Halmashauri ya Mji Kibaha imefanikiwa kufaulisha wanafunzi wote wa kidato cha nne 375 kufaulu na kuondoa daraja sifuri.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Bernard Muyenjwa alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.

Muyenjwa alisema kuwa ufaulu huo ni asilimia 100 ya wanafunzi waliofanya mtihani wa kidato cha nne waliofanya mitihani yao mwaka jana.

"Wanafunzi 234 wamefaulu kwenda kidato cha tano na vyuo mbalimbali vya kati ambapi ufaulu huo ni sawa na asilimia 65 huku wengine wakisubiri uteuzi wa awamu ya pili,"alisema Muyenjwa.

Alisema kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani walikuwa 375 wasichana wakiwa 218 wavulana 157 ambapo daraja la kwanza walikuwa 22 wasichana tisa wavulana 13.

"Daraja la pili 79 wasichana 53 wavulana 26 daraja la tatu 144 wasichana 73 wavulana 71 na daraja la nne ni 130 wasichana 83 wavulana 47 huku daraja sifuri kukiwa hakuna hata mmoja,"alisema Muyenjwa.

Aidha alisema kuwa mafanikio hayo yalitokana na mshikamano walionao walimu na kujitolea, kusimamia vizuri mipango iliyowekwa ya kufikia ufaulu.

"Ushirikiano kati ya shule, wazazi na bodi, kusimamia nidhamu kwa wanafunzi na kuhimiza walimu kufundisha kwa kasi na mazoezi ya mara kwa mara na ufuatiliaji, ufanyaji wa mitihani kila Jumamosi,"alisema Muyenjwa.

Aliongeza kuwa upande wa nidhamu ni kuweka uzio na walinzi ili kudhiti wanafunzi kutoka bila ya sababu zisizokuwa na msingi bali iwe ya msingi ndipo atoke au muda wa kuingia shuleni.

"Malengo ni kuhakikisha tunapunguza wanafunzi wanaopata daraja la nne na kuongeza ufaulu wa daraja la kwanza wafikie angala 60 au 70 na hilo linawezekana,"alisema Muyenjwa.

Alibainisha kuwa shule yao ambayo ni kinara kwa shule za Kata kwa kufaulisha kwenye Halmashauri ya Mji Kibaha ikiwa inazidiwa na shule ya Tumbi na Kibaha wasichana ambazo ziko chini ya Shirika la Elimu Kibaha.

"Tunaishukuru Serikali kwa kutoa kiasi cha shilingi milioni 120 kwa ujenzi wa vyumba vya madarasa vinne na changamoto zilizopo ni ndogondogo ambazo ziko ndani ya uwezo wetu walimu wapo wa kutosha zaidi ya 100,"alisema Muyenjwa.

Aliwaomba wazazi na wadau kuendelea kutoa ushirikiano ili shule hiyo iendelee kufanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha nne na kufikia malengo ya kuwa na kidato cha tano na sita.

Saturday, June 8, 2024

LAMI KUWEKWA SHELI MAILI MOJA






WANANCHI wanaopitiwa na mradi wa ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya BP Sheli-Maili Moja yenye urefu wa kilometa nne wametakiwa watoe ushirikiano ili kufanikisha ujenzi huo.
Hayo yamesemwa na Diwani wa Kata ya Maili Moja Ramadhan Lutambi alipokuwa akizungumza na wananchi wakati wa utoaji elimu juu ya mradi huo ambao kwa sasa uko kwenye hatua ya usanifu.

Lutambi amesema kuwa mradi huo unatekelezwa na benki ya dunia umeanza kwa kufanya usanifu hivyo wananchi wasiweke vikwazo ili hatua hiyo ambayo ni ya miezi nane iweze kwenda vizuri bila ya kikwazo chochote.

"Tunawaomba wananchi muonyeshe ushirikiano kwani kujengwa lami kwa barabara hii ni mkombozi kwa Kata yetu na italeta maendeleo na kurahisisha shughuli mbalimbali hasa za usafirishaji,"amesema Lutambi.

Amesema kuwa katika kutekeleza mradi huo hakutakuwa na fidia kwa sehemu ambazo nyumba zimejengwa barabarani itakapopita barabara hiyo ambayo inaanzia barabara kuu ya Dar es Salaam-Morogoro.

"Tusije tukakwamisha mradi ukikwama mradi utahamishiwa sehemu nyingine hivyo hii ni fursa kwetu tusiiache kwani kukwamisha ni kushindwa kujiletea maendekeo kwani barabara ni maendeleo na fursa zitajitokeza kwa wingi kupitia barabara,"amesema Lutambi. 

Kwa upande wake mwakilishi wa Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini TARURA Mhandisi Fredrick Nzogela amesema kuwa hatua ya usanifu itakamilika mwezi wa tisa ambapo mkandarasi atakabidhi taarifa ambayo itaonyesha baadhi ya maeneo yatakayo athirika.

Nzogela amesema kuwa barabara hiyo itakuwa na upana wa mita 8.5 na itakuwa na mitaro pande zote pamoja na kuwekwa taa na alama mbalimbali na matuta sehemu ambazo ni hatarishi hususani kwenye eneo la shule.

Kaimu Mtendaji wa Kata ya Maili Moja  Mwanawetu Said amewataka wananchi wasiwe na hofu kwani athari hazitakuwa kubwa kama wanavyofikiri na sehemu zitakazo athirika ni kidogo sana.

Said amesema kuwa sehemu zitakazo athirika wahusika wasikwamishe kufanyika kwa ujenzi huo kwani kuukwamisha ni kuyakataa maendeleo ndani ya maeneo yao.

Naye Mhandisi Kiza Mwesigwa ambaye anasimamia ujenzi wa barabara hiyo kwa ujenzi wa changarawe kabla ya kuwekwa lami amesema ujenzi wake utakuwa kuchonga na kuweka kifusi na kushindilia itakuwa na urrefu wa kilometa .

Mwesigwa amesema kuwa mradi huo utaanza mwezi huu kuanzia wiki ijayo na utakuwa wa miezi sita hadi mwezi Novemba itakuwa na urefu wa kilometa moja na mita 800.

Nao baadhi ya wananchi waliohudhuria mkutano huo wa elimu juu ya mradi huo waliitaka Halmashauri kutoa elimu ya kutosha juu ya utekelezaji mradi huo.

Wamesema wako tayari kutoa ushirikiano ili kufanikisha ujenzi wa barabara hiyo na kuwaweka wazi ili wajue maeneo ambayo yameonekana kuzidi ili waweze kuhamisha vitu vyao mapema.





Monday, June 3, 2024

WANAWAKE WA NDUMBWI WAASWA KUWAENZI WANAWAKE VINARA WAZALENDO







Ndugu Omary Abdul Punzi Afisa Mahusino wa Mradi wa Mazingira wa RAMATA (Rafiki wa Mazingira Tanzania) kutoka GBCF nchini Tanzania Tarehe 1.6.2024 awafunda wakina mama wa UWT tawi la Ndumbwi Mbezi Juu Kata ya Mbezi juu Wilaya ya Ubungo Jijini  Dar es Salaam.

Ndugu Omary Punzi aliwaelekeza kuwa Taifa hili limejengwa katika Misingi ya Kizalendo na walioitengeneza hii nchi ni wakina mama mfano Mwenyekiti wa kwanza Taifa wa Uwt  Sofia Kawawa na  Mwanasiasa Mashuhuri Bibi Titi Mohammed aliyejitoa kuchangia Mchango wake katika nchi hii.

Aliwaomba wanawake wamuunge mkono Mhe Dr Samia Suluhu Hassani Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sekta ya kutunza Mazingira na sekta nyingine za Kiuchumi.

Kwa kuzifuata hizi Falsa za TA TE TI TO TU
TA = Tangaza nchi yako bila uoga
TE= Tetea nchi yako bila uoga tusikubali idhalilike
TI= Timiza wajibu wako kwa kila hali
TO= Toa Ushauri kwa hali na Mali
TU= Tubu pale unapokosea

Pia aliwakumbisha sifa kuu ya kiongozi ni Kulalamikiwa na kuwa na Kiherehere chenye Manufaa kwa nchi yake

Naye Wakili msomi Godfrey Kizito Chambi alitoa mada ya Umuhimu wa wanawake katika kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mtaa wa mwaka 2024 na wasisite kwenda kujiandikisha katika Daftari la kudumu la kupiga kula  zoezi hilo  la kupata kitambulisho kwa ajili ya uchaguzi litakalo anza tarehe 1.7.2024 alisisitiza kuwa wasijitokeze kupokea au kutoa rushwa katika mchakato wa Uchaguzi utarudisha nyuma na kuwapata wagombea siyo sahihi na aliendelea kuwakumbusha wanawake hao juu ya Umuhimu wa kutunza Mazingira kwa kutumia rasilimali rafiki ili mazingira yetu yawe rafiki alisema shughuli za binadamu zinaongoza kuchochea kuharibu Mazingira.

Kwa upande Rehema Muya Mwenyekiti wa UWT Kata ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika Mkutano huo alimwaga sifa kwa Mwenyekiti  na katibu wa tawi la ndumbwi kwa kufanya jambo kubwa la kuandaa mada hizo na kuwakusanya Wanawake wa UWT hii inaonesha kuwa sasa CCM inakwenda kupata Ushindi wa Kishindo kwa Mhe Dkt Samia Suluhu Hassani Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika uchaguzi wa 2024 na 2025

Naye Mhe Anna lukindo Diwani wa kata ya Mbezi Juu alisema kuwa Serikali Mhe Dk  Samia Suluhu Hassani imewasaidia wananchi wa Mbezi Juu kujenga Daraja Mito Miwili lengo kutatua kero ya muda mrefu ya kupita hapo Daraja  hilo likikamilika litakuwa chachu ya Maendeleo kutokana na Kasi inayofanywa na Mhe Josephat Gwajima na Timu nzima ya Viongozi wa Kinondoni sambamba na hilo alivutiwa na Mada za mkutano huo.

Katibu wa Tawi la Ndumbwi ndugu Witnes Ngowi alisema kuwa UWT katika Tawi hilo wamejipanga na kuhakikisha kuwa watashinda kwa kishindo katika Uchaguzi wa 2024 na  2025.

Kwa upande wa Catherine Mpangala Mwenyekiti wa Tawi la Ndumbwi alisema wameanda Mkutano huo   kwa lengo la kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi na kuwakumbusha watanzania kuwa mwaka 2024 kutakuwa na Uchaguzi wa serikali ya Mitaa hivyo wasisite kujitokeza kwa wingi katika zoezi la kujiandikisha katia Daftari la Kupiga kula litakalo anza Julai Mosi.

Aliwashukuru Bank ya NMB kuja kutoa Elimu ya Mikopo kwa wakina mama na na watoa mada ya Ujasiliamali kutoka kwa Estar Muhanga ,Mada Itifaki na Uzalendo iliyotolewa na ndugu Omary Punzi  na ile mada ya Utunzaji wa Mazingira na Umuhimu wa kushiriki Uchaguzi wa serikali za mita iliyotolewa na wakili Msomi Geoffrey Kizito 

Ndugu Catherine aliwawapongeza wanachama wa UWT kufika kwa wingi Sambamba na viongozi wa Chama kutoka Wilaya na kata kuja kushiriki Mkutano huo.

Sunday, June 2, 2024

CHAURU YACHAGUA VIONGOZI WAKE








CHAMA Cha Ushirika wa Umwagiliaji Mpunga Ruvu (CHAURU) cha Halmashauri ya Chalinze Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani kimefanikiwa kumchagua Mchujuko Mchujuko kuwa mwenyekiti atakayeongoza kwa kipindi cha miaka mitano.

Kwenye uchaguzi huo ambao ulisimamiwa na Ofisa Ushirika Halmashauri ya Chalinze alimtangaza Mchujuko aliyepata jumla ya kura 214 sawa na asilimia 91.8 kati ya kura 1,165 halali zikiwa 1,162 na kura zilizoharibika ni tatu ambapo mshindi alipaswa kupata angalau asilimia 50 ya kura.

Akitangaza washindi wa uchaguzi huo msimamizi huyo Raphael Kajale amemtangaza makamu wa mwenyekiti ni Otnel Mbura aliyepata kura 186 sawa na asilimia 79.8.

Kajale amewataja wagombea wengine kuwa ni Sade Mwakitalu alipata kura 173 sawa na asilimia 74, Renatha Mwaipopo alipata kura 171 sawa na asilimia 73.3 na Shea Bilali aliyepata kura 154 sawa na asilimia 67 hawa wote wataunda bodi ya ushirika huo.

Amewataja wajumbe wa kamati ya maadili waliochaguliwa ni Moses Polepole, Rajab Mfyome, Theresia Shayo, James Ole Njolay na Zuhura Matimbwa.

Akiwashukuru wajumbe wa mkutano huo mkuu wa uchaguzi uliompa ushindi mwenyekiti mpya Mchujuko amesema kuwa kikubwa atakachokifanya ni kuhakikisha wanaongeza uzalishaji kutoka tani tano za sasa hadi saba mpaka 10 na kukarabati miundombinu.

Awali mwenyekiti aliyemaliza muda wake Chacha Sadala akishukuru amesema pia wamefanikiwa kununua trekta na jembe lake ukarabati wa pampu nne kukarabati mashine mbili za kukoboa mpunga na tayari hekari 800 zimepandwa kati ya hekari 1,800 na hadi itakapofika Juni 30 wakulima wote watakuwa wamepanda mashamba yao.