Thursday, April 4, 2024

MKUU WA MKOA DODOMA ROSEMARY SENYAMULE AKAGUA MIRADI YA MAENDELEO

Ziara ya kikazi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, imeendelea Wilayani Kondoa April 3/ 2024 ambapo amefanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa wilayani humo ikiwemo Ujenzi wa Wodi ya wazazi, jengo la Mochwari na jengo la upasuaji katika hospitali ya wilaya ya kondoa.

Aidha amekagua ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya sekondari  ya wasichana Kondoa pamoja ukaguzi wa nyumba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya kondoa mji ambapo ujenzi unaendelea na unatarajia kukamilika muda wowote kwani umefika hatua za umaliziaji ( Finishing).

Hatahivyo Mhe. Senyamule ameendelea kuwahimiza watumishi wa sekta ya afya kuendelea kutunza mazingira yanayozunguka katika vituo vyao ili kuendelea kuweka mazingira safi na ya kuvutia siku zote ikiwemo kupanda miti kwa mpangilio unaofaa.

SIDO YAWATAMBUA WAJASIRIAMALI WATAKIWA KUZALISHA BIDHAA BORA KUKUZA UCHUMI

KATIBU Tawala Mkoa wa Pwani Rashid Mchatta amewataka wajasiriamali  watakiwa kuzingatia uzalishaji wa bidhaa zao kitaalam ili kukuza uchumi wa mkoa huo.

Mchatta ameyasema hayo wakati akikabidhi vyeti vya kwa wajasiriamali wenye viwanda vidogo na vidogo kabisa wa mkoa huo ambao wametambuliwa na Shirika la Viwanda Vidogo Vidogo (SIDO) Mkoa wa Pwani.

Amesema kuwa wajasiamali hao wanapaswa kuzingatia ubora na viwango pia kushirikiana na taasisi zinazothibitisha viwango vya bidhaa ili ipate soko ndani na nje ya nchi.

Aidha ameipongeza SIDO kwa jitihada za kuwawezesha wajasiriamali ambapo Mkoa huo una jumla ya viwanda 1,533 vikubwa 122 vya kati 120 vidogo 274 na vidogo sana 1,117.

Naye Meneja wa SIDO Mkoa wa Pwani Beata Minga amesema kuwa unatambua jitihada za wajasiriamali ambao wameanzisha viwanda ambavyo vitaongeza ajira na kuongeza pato la mwananchi mkoa na Taifa.

Minga amesema kuwa vyeti hivyo vya kuwatambua vitawasaidia pale wanapohitaji kutambuliwa na taasisi nyingine ambazo ni za uwezeshaji na zoezi hilo litakuwa endelevu ambapo jumla ya wajasiriamali 65 wametambuliwa 

Wednesday, April 3, 2024

*MTOTO* *ATOLEWA* *SARAFU KOONI*

Wataalamu katika Idara ya ENT ya Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) wamefanikiwa kuitoa sarafu iliyokuwa imekwama kwenye koo la mtoto mdogo kwa siku sita.

Daktari Bingwa wa Masikio, Pua na Koo wa BMH, Emmerenceana Mahulu, amesema BMH imempokea  mtoto huyo wa miaka miwili siku ya Alhamisi ya tarehe 26, Machi.

"Tumefanikiwa kuitoa sarafu iliyokuwa imekwama kwenye koo la mtoto kwa siku sita kwa kutumia kifaa tiba kinachoitwa _esophagoscopy_," amesema Daktari huyo Bingwa ambaye pia Kaimu Mkuu wa Idara ya ENT ya BMH.

Dkt Mahulu amefafanua kuwa sehemu ya koo ilipokuwa imekwama sarafu  ilisabisha uvimbe, akiongeza kuwa ilikuwa imeacha uwazi kidogo ambayo ilikuwa ikiruhusu vimiminika kama uji, maji juisi kupita.

"Mtoto anaendelea vizuri baada ya matibabu na anaweza kula vizuri kwa sasa. Tumeishamruhusu na tutamuona tena baada ya wiki moja ili kuona maendeleo yake," amesema. 

Kwa mujibu wa mama wa mtoto, Juliana Yuda, mkazi wa kijiji cha Mkoka, Kongwa, Dodoma, mtoto wake, ambaye alitoka kucheza na wenzake siku ya Jumamosi ya  tarehe 20, Machi, alirudi nyumbani muda wa mchana akiwa analia.

"Mtoto alikuwa hawezi kula kwa muda wa siku sita, alikuwa anashindia uji, juisi na maji tu. Hali yake ilizidi kuwa mbaya Siku ya Alhamisi," anasema.

Anaongeza kuwa Alhamisi ya tarehe 26, Machi alimpeleka mtoto Hospitali ya Wilaya ya Kongwa ambapo alipewa rufaa kuja BMH baada ya kupigwa picha ya x-ray na kubaini sarafu imekwama kwenye koo.

Tuesday, April 2, 2024

WAFANYAKAZI OFISI YA RAIS FEDHA MIPANGO ZANZIBAR NA WAFANYAKAZI WIZARA YA FEDHA WASAIDIA WATU MAHITAJI MAALUM




Na Wellu Mtaki, Dodoma

Wafanyakazi Ofisi ya Rais fedha na Mipango Visiwani Zanzibar wakishirikiana na wafanyakazi wa wizara ya fedha wametembelea vituo vinne vya watu wenye mahitaji Maalum.

Vituo hivyo ni kituo cha Safina Street Network, Asmaa Bint Shams, kituo Cha  wasioona watu wazima Buigiri na Shule ya Msingi ya watoto wenye mahitaji maalum Buigiri ikiwa ni muendelezo wa ziara yao kila mwaka kutembelea vituo vya watu wenye maitaji Maalum na kutoa misaada ya chakula na fedha.

Hayo yamesemwa na ofisa Uendeshaji Ofisi ya Rais fedha na mipango Zanzibar Rajab Uweje wakati akizungumza na vyombo vya habari Jijini Dodoma mara baada ya ziara wameweza kutambua  mahitaji mengine ya vituo hivyo na ametoa ahadi awamu zijazo watajitaidi kuhakikisha wanatatua changamoto zao.

"Tumetoa ahadi katika vituo hivi tumechukua changamoto zao tuone awamu ijayo tuje kutatua changamoto tunaondoka hapa tukiwa tunaenda kuongea na viongozi wetu kuwaeleza hali iliyopo huku ili awamu ingine tuje tusaidie kutatua changamoto,"amesema  Uweje.

Pia ametoa wito kwa walezi wa vituo hivyo kuendelea kuwatunza watoto hao  na kuwasimamia  vizuri ili kujenga Taifa  lenye raia wema.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Hazina Sports Club Mugusi Musita amesema kuwa upo muhuhimu wa jamii kutambua kusaidia watu wenye maitaji maalum kutokana ha changamoto zilizopo kwenye jamii zao hivyo anaiomba jamii kiujumla kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele kusaidia watoto kwani watoto ndiyo Taifa la kesho.

"Vituo vinamahitaji mengi na makubwa sana   kama viongozi  watambue watoto hawa wanamaitaji sana tumekuja kuwapa chochote ila naona kama havitoshi pia tutachuka nafasi hii kupeleka taarifa za cha changamoto hizi katika Halmashauri ya Chamwino nao waone namna ya kusaidia," amesema Musita.

Naye Mratibu wa  Shirika la Safina Street Network Dodoma Ebeneza Ayo ameiomba jamii kuacha kutoa hela kwa watoto wa mitaani ndiyo inasababisha watoto hao kuendelea  kukaa mitaani kuombaomba bali jamii iendelee kuwapa msaada kwa kuwasidi kuwapekeka katika vituo vya kulelewa ili waweze kupata msaada pamoja na elimu Ili kusaidia kutengeneza Taifa lenye nguvu kazi.

"Tuwapende hao watoto wanaotoka katika manzingira hatarishi tuwe  tayari kuwasaidia kwa mambo  mbalimbali tunavyokutana nao mitaani tujaribu kuwasaidia  waweze kwenda kwenye vituo au ofisi ustawi wa jamii na sio kuwapa hela kwani ukiwapa hela ndiyo wanazidi kukaa mitaani , lakini pia hata sisi wenye mashirika ya kuwasaidia watoto tunachangamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa maji katika kituo chetu hivyo tunaomba jamii iweze kutusaidia,"amesema Ayo.

Mwenyekiti wa Makazi ya watu wasioona Buigiri  Yaledi Daudi ameiomba serikali kuwasaidia kujenga maeneo yao ya Makazi kutokana na nyumba zao kuwa chakavu ili waweze kuishi maisha bora.

"Kwa upande wa serikali tunamshukuru  sana Rais Samia kwa kazi nzuri anayofanya na natoa wito kwa serikali kuwa nyumba zetu tunazoishi zimekuwa chakavu tunaomba serikali itujengee nyumba ili kuwa na maisha bora,"amesema Daudi

Ikumbukwe kuwa ziara hizi hufanyika kila mwaka ikiwa na lengo la kuwasaidia watu waishio manzingira magumu pamoja na watu wenye uhitaji mbalimbali, ziara hizi ufanyika katika maeneo ya visiwani Zanzibar na Bara kwa awamu tofauti tofauti.

Sunday, March 31, 2024

KANISA LATAKIWA KUWEKEZA KWA WANAWAKE





Na Wellu Mtaki,Dodoma.

Askofu wa Kanisa Anglikana Dayosisi ya Central Tanganyika Dodoma Dr. Dickson Chilongani  amewataka wahumini wa kanisa hilo kuwekeza nguvu kazi kwa wanawake kwani ukiwekeza kwa mwanamke unakuwa umenufaika.

Kauli hiyo ameitoa Leo Tarehe 31 March 2024 Katika kanisa la Dayosisi Central Tanganyika Dodoma wakati akilihubiria kanisa  kuhusu habari za yesu kristo Mleta Mageuzi pamoja na kueleza habari za kuwekeza Mwanamke kuharakisha Maendeleo.

Amesema kuwa lazima mkubali kwamba ukiwekeza kwa mwanamke mwisho wa yote inalipa ila kwa wanaume inaweza isikulipe na ifikiapo wakati unawaitaji wanaweza usiwaone kwenye itaji lako.

"Wekeza kwa wanawake: Harakisha maendeleo.” Kwa kauli mbiu hii wanawake walitaka watambuliwe na waaminiwe zaidi kuwa wanaweza. Na hapa tena siku ya pasaka tunawaona wanawake wakiwa mstari wa mbele. Saa 12 Alfajiri wakati wanaume bado wanachapa usingizi, Mariamu Magdalene, Mariamu mamaye Yakobo na Salome wanakwenda kaburini na manukato ya thamani ili kuupaka mwili wa Yesu. Wanafanya hivi kwavile Yesu aliposulubiwa, sabato ilikuwa inakaribia na kwahiyo mazishi yalikuwa ni ya haraka haraka, hawakuwa na muda wa kuuandaa mwili wake kwa maziko" Amesema Chilongani.

"Kwahiyo saa 9 mchana Yesu anapokata roho, wanaoshuhudia kifo chake ni wanawake. Inapofika jioni, Yesu anapozikwa, wanaoshuhudia kaburi na mazishi yake ni wanawake. Wanaume wameingia mitini" amesema Chilongani

Aidha amehisihi jamii kuwe na usawa ambao utasaidia kumuwesesha mwanamke kujiamini Katika kujikomboa  kimaisha kwani kumekuwa na mageuzi makubwa sana kwa wanawake na hii ndio inahashiria wanawake wanaweza kuongoza .

"Haya ni mageuzi makubwa sana, kwavile wakati huu wa Yesu Israeli ilikuwa ni nchi yenye mfumo dume na ukilitimba uliokithiri kwelikweli dhidi ya wanawake. Mwanamke alikuwa si kitu. Ndio sababu hata katika Yohana 6 tunasoma kwamba Yesu alilisha watu 5000 kwa samaki 2 na mikate 5. Lakini waliohesabiwa walikuwa ni wanaume peke yao, wanawake hawakuhesabiwa. Ni kana kwamba walikuwa si binadamu. " Amesema Chilongani

Pia amesisitiza wahumini wa kanisa hilo watambue kuwa mwanamke ni mtekekezaji mzuri wa majukumu na hanahakikisha anafanya kazi kwa weledi bali wapo watu ambao awana imani naye na hao ndio wanapelekea kushusha uchumi wa mwanamke kiujumla.

"Na hata katika mahakama za Israeli ushahidi wa mwanamke kisheria ulikuwa haukubaliki. Lakini bado Yesu anawafanya wanawake kuwa mashahidi wa kufufuka kwake na anawatuma wawaambie wanafunzi wake waende Galilaya watamkuta" amesema Chilongani.

Aidha amewataka wahumini wamtangulize Mungu Katika maitaji ya maombi Yao na waachane na tabia ya kupanga aina ya maitaji wanayoyataka kwa Mungu Bali wamwache Mungu atatenda mwenyewe.

"Ni lazima tujifunze kumtanguliza Yesu Kristo na siyo kumtangulia. Askofu Mkuu mstaafu marehemu John Ramadhani aliwahi kusema: “Wakristo wengi badala ya kumtanguliza Roho Mtakatifu wanamtangulia”. Mtu badala ya kumwomba Mungu ampe mke mwema, anampa Mungu masharti kwamba anataka mke mweupe tena mwenye mwanya. Huko ni kumtangulia Mungu. Badala ya kuomba gari, anaomba Scania, wakati hata baiskeli yenyewe hana. Huko ni kumtangulia Mungu. Kumtanguliza Mungu ni kumwomba mke au gari na kuacha mapenzi yake mema yatimizwe" amesema Chilongani 

Pia  hamewahimiza wanawake kuwania nafasi mbalimbali za uongozi Katika ngazi ya kanisa na serikali kwa ujumla na kuzingatia usawa wa kijinsia.

"Somo linatutaka tuwaamini wanawake na tuthamini mchango wao katika kanisa na jamii. Katika kanisa mwaka huu Dayosisi yetu ina mkutano mkuu (sinodi), na tumeanza chaguzi mbalimbali katika ngazi zote. Ningeomba sana kuwe na usawa. Zisiwepo nafasi za wanaume peke yao na za wanawake peke yao" amesema Chilongani 

"Katika taifa, chaguzi pia zimeanza kufanyika kuelekea kwenye uchaguzi mkuu. Ni vyema kuwe na usawa, tuwaamini wanawake. Kubwa zaidi, kumekuweko na baadhi ya wanaume wanaomzodoa Rais Samia kana kwamba hawezi lolote kwasababu tu ni mwanamke. Ni kana kwamba hawaoni kazi ambazo Rais wetu amezifanya katika kipindi chake hiki kifupi cha uongozi. Watu wa jinsi hii ni wabinafsi na hawatufai katika jamii" amesema Chilongani 

Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu ni kanisa la Kiuaskofu katika Dayosisi ya Central Tanganyika. Dayosisi ya Central Tanganyika ilianzishwa mwaka 1927. Ilikatwa kutoka Dayosisi ya Mombasa. Kabla ya hapo Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Burundi na DRC Congoeneo lote hili lilikuwa chini ya umisheni wa CMS Afrika na kujulikana kama Dayosisi ya Eastern Equatorial Africa na Askofu wa kwanza alikuwa James Hannington (1884 – 1885). Huyu alikuwa shahidi wa kwanza baada ya kuuwawa na Kabaka Mwanga katika eneo la Busuga nchini Uganda 29/10/1885.

BONANZA LA WIZARA YA FEDHA BARA NA VISIWANI LAFANA





Na Wellu Mtaki, Dodoma

Bonanza la mpira wa miguu, kuvuta kamba na mpira mikono limefanyika leo Jijini Dodoma likiwashirikisha watumishi mbalimbali wa Wizara ya Fedha kutoka Bara na Visiwani.

Mkurugenzi wa Idara ya Utawala rasilimali watu Wizara ya Fedha Lusius Mwenda amesema kuwa lengo la bonanza hilo ni kudumisha ushirikiano na undugu kati yao.

Na kusema kuwa kuna tija inayopatikana ikiwemo kuimarisha urafiki wa pande zote mbili, kufahamiana na kuimarisha afya za Watumishi.

"Lengo kubwa katika mashindano ni Ushirikiano kati yetu,sisi huku Tanzania  Bara na wenzetu wa Zanzibar".

"Tija kubwa ambayo inapatikana ni pamoja na watumishi kuimarisha afya, kufahamiana  na kuwa na urafiki wa pande zote mbili, kwa mfano kwa sisi kwenda kule Zanzibar na wao kuja huku kama ambavyo tumekuwa tukifanya".

Akizungumza Mwakilishi kutoka Zanzibar Bwana Rajab Uweje ofisa Uendeshaji Ofisi ya Raisi fedha na mipango Zanzibar amesema kuwa  Tamasha hilo ni ishara nzuri tumelikuta na hivyo tuliendeleze.

"Kwanza bonanza hili tunajenga uhusiano baina yetu nichukue nafasi hii kuzishukuru Taasisi zetu mbili kutudhamini katika Tamasha hili na hiki ni kitu chema sana tumekikuta na hivyo kwahiyo tukiendeleze kwa vizazi vyetu".

Mwenyekiti wa Hazina Sports Club Mugusi Musita amezungumzia suala la mikakati ya uboreshaji wa Tamasha hili kwa muda mrefu ikiwemo kuongeza wigo wa timu shiriki katika Tamasha hili ambapo kwa mwaka huu wamefaniki na kuweza kuongeza timu mpaka kufika sita.

"Kawaida huwa tunacheza Hazina ya Tanzania Bara na Zanzibar lakini mwaka huu tumekuwa na timu sita kwa hiyo mikakati tuliyoiweka ni kuboresha kama kuongeza timu umeona kama polisi walikuwepo hapa lakini kujenga mahusiano mazuri na wenzetu sisi kama Wizara za Kimuungano wenzetu wa visiwani tunafanya kazi moja na ndo tunaboresha mahusiano na kuboresha afya".

Tamasha hili la Pasaka limekuwa likifanyika kwa zaidi ya miaka ishirini mpaka sasa.

Saturday, March 30, 2024

VIONGOZI WAASWA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI WAO - RAS MMUYA.


Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Kaspar Mmuya ameendelea na ziara yake ya kikazi ya ukaguzi wa miradi na kuongea na watumishi kwa lengo la kujitambulisha Katika Halmashauri za Mkoa wa Dodoma ambapo Leo Machi 28, 2024 ametembelea Halmashauri ya Wilaya ya Dodoma Mjini.

Kufuatia uzinduzi wa kampeni ya "Kero yako wajibu wangu", Mmuya ameendelea kuwa sisitiza watumishi kuwa na wajibu wa kusikilza na kutatua kero za wananchi kwa nafasi zao. Hayo ameyasema katika Kikao chake na watumishi wa Halmashauri hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Umonga Jijini Dodoma.

“Ni vyema kujua vipaumbele na  wajibu wako wa Kusikiliza Kero za wananchi wanaotuzunguka tukiwa wawakilishi wao na uongozi mliopewa una jukumu la kutatua kero za wananchi katika Mitaa yetu na dhana ya kuwajibika inaenda Sabamba na utaratibu na kuipa ubora kazi yako.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anawajibika ipasavyo kwa kuleta fedha za miradi katika jamii na kama Msimamizi wa hizo fedha unapaswa kuzingatia ubora wa majengo yanayojengwa na kama kiongozi wajibu wako ni kuhakikisha hizo fedha zinatumika vizuri kama ilivyoelekezwa na usiwe chanzo cha kuwa kero kwa wengine," Amesema. Mmuya.

Vilevile, ametilia mkazo suala la kuongeza ufaulu mashuleni, kuondoa utoro kwa wanafunzi, upandaji na utunzaji miti, mahusiano bora mahala pa kazi, uwajibikaji katika kila ngazi aliyonayo mtu.

Aidha, Katibu Tawala Mkoa amekagua mradi wa ujenzi wa Madarasa 08 na matundu 10 ya vyoo kwa ajili ya wanafunzi wa Kidato cha tano katika shule ya Sekondari Mtumba iliyopo kwenye kata ya Mtumba ambayo ilipokea fedha kiasi cha shilingi Milioni 201.

Mradi mwingine ni ujenzi wa vyumba 08 vya madarasa na matundu 10 ya choo katika shule ya Sekondari Zulu iliyopokea kiasi cha shilingi Milioni 201 na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya iliyopokea shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Maabara, jengo la wagonjwa wa nje ( OPD), jengo la mama na mtoto, Jengo la Mionzi, Jengo la Dawa, jengo la kuhifadhia maiti na kichomea taka.