Saturday, June 25, 2016

ZEGERENI KUJENGA SHULE YA MSINGI

Na John Gagarini, Kibaha

MTAA wa Zegereni wilayani Kibaha umefayatua matufali 2,500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa shule ya Msingi katika mtaa huo ambao unategemea mtaa wa Visiga kuwapeleka watoto wao umbali wa kilometa nane.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake wakati wa zoezi la kuwapa zawadi wanafunzi wa darasa la saba ambao wamefanya vizuri na kuwa kwenye 10 bora mwenyekiti wa mtaa huo Rashid Likunja amesema kuwa wanatarajia kuanza ujenzi wa shule hiyo kuanzia Julai Mwaka huu ili ifikapo mwakani watoto wao waanze kusoma kwenye shule hiyo.

Likunja amesema kuwa fedha za kununulia kiwanja chenye ukubwa wa hekari sita zimetokana na mchango wa shilingi 5,000 kila kaya ambapo hatua ya ujenzi itaanza kwa kutumia tofaali hizo huku wakiwa na mifuko 12 ya simenti wakianza na madarasa mawili, ofisi na matundu manne ya vyoo.

Amesema kuwa kwa sasa wako kwenye harakati za kupata kibali cha ujenzi pamoja na ramani toka Halmashauri ya Mji ili waweze kuanza ujenzi huo na utawapunguzia watoto wao kwenda kusoma mbali pia huwabidi kuvuka barabara ya Morogoro ambapo ni hatari kwao kwani wengine ni wadogo sana.

Aidha amewataka wadau mbalimbali kujitokeza kuwasaidia ili waweze kutekeleza azma yao ya ujenzi wa shule hiyo ambayo itakuwa mkombozi kwa watoto wanaotoka mtaa huo ambao wanafikia zaidi ya 200 wanaosoma madarasa mbalimbali kutoka mtaa huo ambao wanasoma shule jirani ya Visiga.


Mwisho.   

No comments:

Post a Comment