Monday, June 20, 2016

SIDO YATUMIA DOLA MILIONI 2

Na John Gagarini, Kibaha

SHIRIKA la Kuendeleza  Viwanda Vidogo Vidogo (SIDO) kwa kushirikiana na wafadhili wake limetumia kiasi cha dola milioni mbili za Kimarekani kwa ajili ya kutoa mafunzo ya uzalishaji bidha za vyakula zisizo na madhara kwa wajasiriamali zaidi ya 700.

Mratibu wa mafunzo hayo Happines Mchomvu alisema kuwa mafunzo hayo ambayo yametolewa kwa kipindi cha miaka miwili kwa lengo la kuhakikisha bidhaa wanazozalisha zinakuwa hazina madhara kwa watumiaji zinakuwa na usalama.

Mchomvu alisema kuwa mbali ya kuwa na usalama pia zinakuwa na viwango vya wa ubora wa kimataifa ili viweze kuuzwa sehemu yoyote ile duniani.

“Mafunzo hayo yalikuwa na malengo ya kuboresha bidhaa za maembe, viungo na asali ambapo wameweza kuwajengea uwezo wajasiriamali hao kutoka mikoa ya Tabora, Singida, Shinyanga, Morogoro, Pwani na Dar es Salaam,” alisema Mchomvu.

Aidha alisema lengo ni kuhakikisha wajasiriamali kote nchini kuanzia ngazi ya mikoa hadi kwenye mitaa wanazalisha bidhaa zenye ubora na viwango kwa lengo la kuwa na soko la uhakikka la ndani na nje ya nchi ambapo bidhaa za Tanzania zinapendwa kutokana na uhalisia wake.

Kwa upande wake ofisa udhibiti wa ubora kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Magdalena Sademaki alisema kuwa kupitia mafunzo hayo wajasiriamali hao wameweza kutengeneza mifumo yao kimataifa kwa kupambana na vihatarishi ili visiweze kuingia kwenye vyakula.
Sademaki alisema kuwa katika kuhakikisha wajasiriamali hao wanatengeneza bidhaa zenye viwango wanashirikiana na SIDO kuwatambua ili waweze kufikia viwango vya uzalishaji wa bidhaa bora ili ziendane na viwango vya kimataifa.

Na mmoja wa wajasiriamli ambaye amehudhuria mafunzo hayo Zaloki Mohamed ameishukuru SIDO kwa kuwapatia elimu juu ya viwango vya bidhaa  wanazozalisha kwa kuzingatia  utaratibu wa viwango vya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Shirika la Viwango la Kimataifa (ISO).

Mohamed  ameiomba serikali iwapunguzie tozo zinazotozwa kwa wajasiriamali ili wapate hati ya viwango ya bidhaa wanazozalisha na kuweza kufikia malengo  ya Tanzania ya kuwa na viwanda.

Mafunzo hayo yameendeshwa kwa ufadhili wa Shirika la Biashara la Kimataifa (ITC) kupitia mpango wa kuendesha biashara wa shirika la World Trade Organisation (WTO) kwa kushirikiana na SIDO.

Mwisho. 





 

   




No comments:

Post a Comment