Sunday, June 5, 2016

WATAKA TAARIFA RASMI MRADI WA MIWA KUFUTWA

Na John Gagarini, Bagamoyo
HALMASHAURI ya Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani imetakiwa kutoa taarifa rasmi kwenye vijiji vilivyokuwa kwenye mradi wa kilimo cha miwa chini ya kampuni ya Eco Energy uliosimamishwa na serikali ili eneo hilo lisije kuchukuliwa na mtu mwingine ili hali wananchi hao hawajalipwa fidia.
Mradi huo ulisimamishwa kupitia majibu ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa anajibu swali la kiongozi wa kambi ya upinzani Bungeni Freeman Mbowe aliyetaka kujua ni kwanini serikali imeshindwa kuweka jitihada za makusudi ili mradi huo ukamilike ambao ulibainika kuwa ungetumia maji mengi ya Mto Wami na kuathiri usatawi wa wanyama kwenye Mbuga ya Saadani.
Akizungumza na waandishi wa Habari mjini Bagamoyo katibu wa kamati ya ardhi ya Asasi isiyokuwa ya kiserikali ya Mkombozi Bakari Salum alisema kuwa     kwa kuwa kauli ya Waziri Mkuu ni agizo ni vema Halmashauri ingetoa tangazo rasmi kwa wananchi husika.
“Kwa kuwa wakati anakuja mwekezaji kuchukua maeneo ya wananchi kwa ajili ya mradi huo kulikuwa na taarifa rasmi na wananchi walitoa maeneo yao kwa ajili ya kilimo hicho cha miwa ambacho baadaye kungejengwa kiwanda kwa ajili ya kuzalisha sukari hivyo baada ya kushindikana wangewajulisha wananchi,” alisema Salum
Kwa upande wake mjumbe wa kamati hiyo Jackson Mkango alisema kuwa eneo ambalo lilichukuliwa na mwekezaji ni hekari zaidi ya hekta 22,000 wananchi hao hawajalipwa fidia yoyote licha ya kuwa tathmini kufanyika mwaka 2011 hadi leo hawajalipwa.
Mkango alisema kuwa sheria inasema kuwa tathmini ikifanyika walengwa wanapaswa kulipwa ndani ya kipindi cha miezi sita lakini sasa imepita miaka mitano sasa.
“Tunaiomba Halmashauri kutoa tamko juu ya ardhi hiyo ya wananchi ambayo toka imechukuliwa wananchi hawakufanya chochote licha ya kuwa eneo hilo walikuwa wakitegemea kwa ajili ya kilimo na hawajui hatma yao kwani walitegemea wangelipwa fidia,” alisema Mkango.
Vijiji vilivyokuwa kwenye mpango huo ni Razaba, Matipwili, Kitame, Fukayosi, Makaani na Gongo ambapo kuna jumla ya wananchi zaidi ya 700 ambao walikuwa wakiishi kwenye maeneo hayo yaliyoingizwa kwenye mradi huo ambao ulikuwa na lengo la kukabiliana na upungufu wa sukari hapa nchini.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment