Sunday, June 5, 2016

JUMUIYA YA WAZAZI YASISITIZA UBORA WA ELIMU CHUO CHA KILIMO NA MIFUGO

Na John Gagarini, Chalinze
JUMUIYA ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kimesema kuwa kitashirikiana na uongozi wa Chuo Cha Kilimo na Mifugo cha Kaole ili kuhakikisha elimu inayotolewa ina kuwa na manufaa kwa nchi.
Hayo yalisemwa Lugoba wilayani humo na mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Abdul Sharifu wakati wa baraza la Wazazi na kusema kusema kuwa chuo hicho ambacho kinamilikiwa na jumuiya kitaboreshwa masomo yanayotolewa chuoni hapo ili wahitimu wake wabadilishe sekta hiyo na kuleta faida kwa wafugaji na wakulima nchini.
Sharifu alisema kuwa chuo hicho kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo watahakikisha wanaziondoa kwa kushirikiana na makao makuu ya Jumiya hiyo ili kiweze kutoa elimu bora ambayo itasaidia kuboresha ufugaji na kuwa wa kisasa na wenye tija.
“Chuo kinakabiliwa na changamoto lakini tutazikabili kadiri ya uwezo wetu ili tuboreshe elimu inayotolewa chuoni hapo hasa tukizingatia ufugaji ni moja ya chanzo kikubwa cha pato la Taifa na kilimo kwa ajili ya chakula,” alisema Sharifu.
Alisema kuwa chuo hicho kinajijenga upya baada ya awali kubadilishwa na kuwa shule ya sekondari lakini sasa kimerudishwa mikononi mwao hivyo watahakikisha kinakuwa moja ya vyuo bora hapa nchini kwa kutoa elimu inayokubalika.
“Tunaomba wadau mbalimbali kujitokeza kukisaidia chuo chetu ili kiweze kuboresha wasomi ambao watakubalika kule watakakopangiwa hasa ikizingatiwa wahitimu hao watakuwa ni maofisa ugani wataboresha kilimo na ufugaji,” alisema Sharifu.
Kwa upande wake mjumbe wa baraza la jumuiya hiyo Yahaya Msonde alisema kuwa lengo lao ni kutoa elimu itakayokidhi mahitaji ya wakulima na wafugaji ili waboreshe shughuli zao.
Msonde alisema kuwa kilimo ni uti wa mgongo hivyo lazima kiwekewe mikakati ya kuinuliwa kwa kuzalisha wataalamu wenye uweze na mbinu za kisasa na kwa wafugaji nao waweze kukabiliana na ufugaji usiokuwa na tija.

Mwisho.   

No comments:

Post a Comment