Tuesday, June 14, 2016

WATATU WASHIKILIWA KWA MAUAJI YA DEREVA WA NOAH

Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia watu watatu kwa tuhuma za mauaji ya dereva wa gari la abiria aina ya Toyota Noah Mohamed Ramadhan (21) mkazi wa Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha kamanda wa Polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao walimkodisha dereva huyo.
Mushongi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Juni 13 mwaka huu majira ya saa 19:45 usiku eneo la Vigwaza Tarafa ya Chalinze wilaya ya Bagamoyo.
“Watu hao walimuua dereva huyo kwa kumkaba shingoni kisha kupora gari hilo lenye namba za usajili T 119 DDM rangi nyeupe lililokuwa likitumiwa na marehemu baada ya kumkodi wakimataka awapeleke Kanisa la Pentekoste Vigwaza,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa watu hao kabla ya kumuua marehemu walimkaba wakiwa njiani ambapo alipiga kelele kuomba msaada na madereva bodaboda walizisikia na kuamua kufuatilia gari hilo barabara ya vumbi kwenye njia kuu ya umeme wa Tanesco.
“Watu wale walipoona taa za bodaboda waliamua kusimama na kutoka ndani ya gari na kuanza kukimbia kutokomea porini lakini mmoja wao alikamatwa palepale na walipoangalia ndani walikuta mwili wa marehemu ukiwa umewekwa kiti cha nyuma kwa lengo la kwenda kuutupa mwili huo porini ili kuondoka na gari hilo,” alisema Mushongi.
Aidha alisema kuwa juhudi za wananchi, dereva bodaboda na polisi zilifanikisha kukamatwa watuhumiwa wawili ambao majina ya watuhumiwa hao yamehifadhiwa ili kutoharibu upelelezi kwani watu hao ni mtandao wa majambazi ambao wengine wako Jijini Dar es Salaam.
Alibainisha kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa kwenye hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi kusubiri ndugu na uchunguzi wa daktari kwa ajili ya mazishi.
Aliwataka madereva wa vyombo vya moto hasa wale wanaofanya biashara za usafirishaji nyakati za usiku kuwa makini ili kujiepusha na matukio kama hayo ya wizi.
Mwisho.         

    

No comments:

Post a Comment