Thursday, June 9, 2016

WAWEKEZAJI WATAKIWA KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUDUMISHA AMANI YA NCHI

Na John Gagarini, Mafia
MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewataka wawekezaji kwenye Visiwa vilivyopo Wilayani Mafia kushirikiana na serikali ili kudhibiti usalama wa nchi kukabiliana na wageni wasio waaminifu ambao wanaoweza kuvitumia visiwa hivyo kuhatarisha amani ya nchi.
Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa ilipotembelea Kisiwa cha Shungimbili kwenye Hoteli ya Thanda ambayo inamilikiwa na raia wa kigeni na kusema kuwa kuna haja ya kuwa na kituo cha kufuatilia wageni wanaoingia na kutoka.
Ndikilo alisema kuwa kutokana na hali ya sasa kuwa mbaya kiusalama kutokana na matukio ya mauaji ya kutisha ambayo yanatokea hapa nchini ni vema ulinzi ukaimarishwa.
“Kuna haja ya kuwa na ushirikiano na baina ya wawekezaji na serfikali ili kukabiliana na wahalifu ambao wanaweza kutumia visiwa kujiingiza hapa nchini na kufanya uhalifu ikiwa ni pamoja na mauaji,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa dunia ya sasa imebadilika na baadhi ya watu wamekuwa wakitumia njia ya Bahari kupitisha wahamiaji haramu, dawa za kulevya pamoja na uingizwaji wa silaha.
“Serikali haina nia mbaya ya kutaka kujua mambo yanayofanywa na wawekezaji kwa kujua wageni wanaoingia na kutoka na wameleta nini wanatoka na nini na hapa kutakuwa na kituo cha ukaguzi ambacho kitakuwa na polisi kwa ajili ya kulinda eneo la Kisiwa kwani wageni watakuwa wanafika kwa wingi,” alisema Ndikilo
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa Thanda Island Tanzania Ltd Oscar Pucci alisema kuwa hana tatizo na ushirikiano na serikali kwani anashirikiana vizuri na Halmashauri.
Pucci alisema kuwa wamekuwa wakisaidia shughuli za maendeleo kama kuchangia kwenye Hospitali ya wilaya na hata wavuvi wanaovua jirani na hoteli yao.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment