Friday, February 22, 2013


Na Mwandishi Wetu, Kibaha
ASKARI wa Jeshi la Polisi kituo kidogo Cha Kwa Mathiasi Wilyani Kibaha mkoani Pwani Pc Ramadhan amelazwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kujeruhiwa na wananchi waliovamia kituo hicho kutaka kuwatoa watu waliowatuhumu kuwa wameiba simu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake kamanda wa polisi mkoani humo Ulrich Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 21 mwaka huu majira ya saa 1 usiku baada ya wananchi hao kutaka kuwatoa watu waliodai kuwa wameiba simu na kutaka kuwaua.
Kamanda Matei alisema kuwa chanzo cha tukio hilo kilianza kwenye uwanja wa mpira wa miguu baina ya timu za Palasupalasu na Kigogo ya Jijini Dar es Salaam, ambapo mchezo huo uliokuwa ukichezwa kwenye uwanja wa Mwendapole kulivunjika kutokana na vurugu zilizojitokeza.
“Baada ya mchezo huo kuvunjika washabiki wa timu hizo walianza kushambuliana na ndipo watu waliotuhumiwa ambao ni Michael Mathias (30) na Hashim Noah (19) ambaye ni mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Mwanagati Jijini Dar es Salaam kukimbia kwa kutumia pikipiki na walipoona wmezidiwa waliiacha pikipiki kisha kuingia kwenye msikiti wa Tanita,” alisema Kamanda Matei.
Aidha alisema kuwa baada ya kuingia ndani ya msikiti huo wananchi hao waliuzunguka msikiti huo kisha kutaka kuwatoa watu hao ili wawaue ndipo polisi walipofika na kuwatawanya wananchi hao lakini waligoma na kuanza kuwarushia mawe polisi ndipo polisi walipopiga risasi kuwatawanya wananchi hao.
“Katika vurugu hizo Maria Stamford alipigwa risasi ya ziwa na Idd Shukuru alipigwa mguu wa kulia kisha waliwachukuwa watu hao na pikipiki yao ndipo wanannchi hao walikwenda hadi kwenye kituo hicho wakidhani kuwa watu hao wako pale kwani waliiona ile pikipiki nje ya kituo hicho,” alisema KamandaMatei.
Aliendelea kusema kuwa walikivamia kituo hicho na kumpiga askari huyo ambaye alikuwa amevaa sare na askari mwingine Bonventura kisha kuvunja mlango na kuwaangalia watu wale lakini hawakuwakuta na kuharibu vitu mbalimbali.
“Uchunguzi ulibaini kuwa watu wale hawakuwa wezi bali walikuwa ni mashabiki wa timu mojawapo ambao walizushiwa kuwa wezi jambo ambalo si la kweli majeruhi wanaendelea vyema na matibabu na kwa sasa tayari wameunda tume ndogo kufuatilia tukio hilo na hakuna mtu aliyekamtwa kuhusiana na tukio hilo,” alisema Kamanda Matei .
Mwisho. 
  

Thursday, February 21, 2013

MISITU


Na John Gagarini, Kibaha

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wametakiwa kutoa elimu zaidi kwa wananchi juu ya upandaji miti kuliko kuvuna ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi ambayo yanapelekea uoto wa asili kutoweka.

Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Katibu Tawala mkoa wa Pwani Bi Betha Swai wakati akifungua mkutano wa wataalamu wa sekta ya misitu kuweka mikakati mbalimbali juu ya kuboresha misitu kwenye mkoa huo.

Bi Swai alisema kuwa ukatiji wa miti ni mkubwa tofauti na miti inayopandwa jambo ambalo litaipelekea nchi kukumbwa na majanga yanayotokana na uharibifu wa mazingira ikiwemo ukame, mmomonyoko wa ardhi na ukosefu wa vyanzo vya maji.

“Ni vema mkatoa elimu kwa wananchi kwa kiwango kikubwa ili wananchi wakawa na uelewa juu ya uharibifu wa mazingira na umuhimu wa kutunza misitu kwani wengi wao hawaoni umuhimu wake licha ya kuwa wanatumia zao la miti katika kujipatia kipato,” alisema Bi Swai.

Aidha alisema kuwa halmashauri na serikali nazo zijikite kwenye utoaji elimu hiyo na si kutaka tu ushuru huku misitu ikiendelea kuteketea huku mikakati ya kupanda miti ikiwa si mizuri.

“Tuachane na kusema kuwa tumegawa miti sehemu Fulani kwa ajili ya kupanda kwa sasa tuwe na mkakati wa kupanda baadhi ya maeneo mfano kwenye mabonde au sehemu ambako kumefanyika uharibifu mkubwa ili tuonyeshe na si kusema kwa maneno tu,” alisema Bi Swai.

Kwa upande wake Bakari Mohamed alisema kuwa  lengo la kuanzishwa wakala hao amabo ni wapya ni kwa ajili ya kuondoa urasimu na mfumo wa kiutendaji katika utekelezaji wa majukumu ya misitu ili kuleta ufanisi.

Bw Mohamed alisema kuwa moja ya kazi za wakala ni kuihamasisha jamii kuanzisha misitu yao na kuilinda ile iliyopo pia kuwa na vikundi vya uzalishaji nyuki kwa kutumia rasilimali ya misitu.

Mwisho.      




Monday, February 18, 2013

Na John Gagarini, Kibaha
DIWANI wa kata ya Maili Moja Bw Andrew Lugano amesikitishwa na mamalaka ya maji safi na majitaka (DAWASCO) kushindwa kuwahudumia wananchi hali inayosababisha kukosa maji kwa zaidi ya mwezi sasa.
Akizungumza mara baad aya kufanya ziara kwenye kata hiyo kuangalia maeneo ambayo yamekuwa yakikosa maji kwa muda mrefu, huku akiwa ameambatana na meneja wa DAWASCO Bw Robert Mugabe alisema kuwa hakuna sababu ya wananchi kukosa maji kwa muda wote huo na uongozi upo.
Bw Lugano alisema kuwa amekuwa akipata kero hiyo ya maji toka kwa wananchi na jitihada zake za kufuatilia zimekuwa zikigonga mwamba hali iliyomlazimu kumtoa meneja huyo ofisini kwake Jumamosi na kumwonyesha jinsi gani wananchi wanavyotaabika kwa kukosa maji.
“Siwezi kukubali kuona wananchi wakihangaika kutafuta maji huku chanzo cha maji kikiwa jirani hivyo lazima kampuni hiyo ijali wananchi ili waondokane na kero hiyo,” alisema Bw Lugano.
Moja ya wakazi wa kata hiyo ambaye anakaa mtaa wa Mzimuni Bw Mohamed Atiki alisema kuwa wamekuwa wakipata tabu kubwa ya kupata maji hali inayowasababisha kununua maji kwa bei ya shilingi 500 kwa dumu la lita 20.
“Tumekuwa tukihangaika kwa kipindi kirefu licha ya kutoa taarifa ya ukosefu wa maji kwenye kampuni hii ya maji hivyo lazima wabadili utendaji kazi wao,” alisema Bw Atiki.
Kwa upande wake meneja wa DAWASCO Kibaha Bw Robert Mugabe alisema kuwa tatizo kubwa lililosababisha wananchi kukosa maji ni kutokana na ujenzi wa barabara katika kata hiyo.
“Mabomba mengi yamekatwa kutokana na ujenzi wa barabara lakini hata hivyo tayari tumewasiliana na mkandarasi ili kuangalia namana ya kuweza kurekebisha hali hiyo,” alisema Bw Mugabe.
Bw Mugabe alisema kuwa tayari wameshafanya tathmini ya uharibifu uliofanyika na wakati wowote wataanza kufunga mabomba yaliyokatwa ili wananchi hao waendelee kupata maji kama kawaida.
Mwisho.
Diwani wa kata ya Maili Moja Kibaha kushoto Andrew Lugano akizungumza na meneja wa DAWASCO Kibaha kulia Robert Mugabe, kuhusiana na kata hiyo kuwa na tatizo kubwa la ukosefu wa maji (Picha na John Gagarini)


Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MWANAFUNZI wa darasa la kwanza wa  shule ya Msingi Mbaya, Geuza Patrick (12) amekufa kwa kujinyonga kwa kamba ya katani.
Kwa mujibu wa kaimu kamanda wa Polisi mkoani Pwani Gregory Mushi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 13 mwaka huu majira ya saa 12 jioni huko kitongoji cha Msufini tarafa ya Chalinze wilayani Bagamoyo.
Kamanda Mushi alisema kuwa mwanafunzi huyo alijinyonga kwenye Mti wa Mwembe nyumbani kwao.
Alisema kuwa chanzo cha kujinyonga bado hakijafahamika na polisi wanaendelea na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo.
Aidha alisema mwili wa marehemu ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
Mwisho.
Na Mwandishi Wetu, Kibaha
SHULE ya Sekondari ya Bundikani ya Kata ya Maili Moja wilayani Kibaha imeanza kuchukua hatua kali kwa wanafunzi wanaovaa suruali za kubana maarufu kama modo kwa kuzichana.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwalimu mkuu wa shule hiyo Flora Chibululu alisema kuwa juzi walichana suruali za wanafunzi watatu kutokana na kwenda shuleni na suruali hizo kinyume cha sheria.
Alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wamekuwa na tabia ya kuzirekebisha  kwa kuzibana suruali hizo licha ya kuwa zinashonwa kawaida na kukiuka taratibu za shule.
“Suruali hizo za shule hushonwa vizuri lakini wao huzipeleka kwa fundi na kuzibana sawa na miili yao maarufu kama modo, tulishawapiga marufuku kuzibadili nguo hizo lakini wanakaidi hali iliyotufanya tuchukue hatua hiyo ili kuleta nidhamu shuleni,” alisema Chibululu.
Chibululu alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakikiuka taratibu za shuleni na kuiga tabia ambazo zinashusha taaluma hivyo shule itakabiliana na vitendo kinyume cha taratibu za shule.
Aidha alisema wataendelea kuzichana suruali hizo kwa mwanafunzi atakaye vaa kinyume cha sheria za shule kwani huo ni utovu wa nidhamu na lazima wanafunzi wafuate taratibu za shule.
Mwisho.  
Na Mwanidshi Wetu, Kibaha
WAFANYABIASHARA kwenye kata ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kupima afya zao kwa mujibu wa sheria ili waweze kuhudumia wateja wao wakiwa na afya njema vinginevyo watapelekwa mahakamani kwa kukiuka kanuni za afya.
Hayo yalisemwa na ofisa afya wa kata hiyo Ally Shah, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha na kusema kuwa watakaokataa kupima afya zao watapelekwa mahakamani.
Shah alisema kuwa hivi karibuni baadhi ya wafanyabiashara waligoma kwenda kupima afya zao wakidai kuwa kiwango cha kupima ni shilingi 5,000 ambayo ilipangwa na halmashauri wakidai kuwa ni kubwa.
“Wafanyabiashara wanatakiwa kupima afya ili kutoa huduma wakiwa na afya njema ili kuepuka maambukizi ya magonjwa mbalimbali kama vile kifua kikuu na magonjwa ambayo yanaambukiza kwa haraka,” alisema Shah.
Alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hao wamekuwa na hofu ya kupima afya kuwa wataonekana na maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI jambo ambalo alisema kuwa upimaji huo hauhusiani na kupima vipimo vya ugonjwa huo.
“Wasihofie kupima afya kwani magonjwa yanayopimwa hayahusiani na ugonjwa wa UKIMWI na kama mtu anataka kupima ugonjwa huo ni hiyari yake mwenyewe na si kwa lazima kama sheria inavyoelekeza,” alisema Shah.
Aidha alisema kuwa magonjwa yanayopimwa ni pamoja na magonjwa ya zinaa, kifua kikuu na haja kubwa hivyo wafanyabiashara wapime afya zao kwani ni kwa faida yao na wateja wanaowahudumia.
Katika hatua nyingine alisema kwa sasa wanaendelea na kuboresha usafi wa mazingira ambapo vimeundwa vikundi mbalimbali vya usafi kwa ajili ya kuhakikisha mazingira ya Mji wa Kibaha ambapo sheria ndogondogo ya halmashauri inawatoza kiasi cha shilingi 50,000 kwa mtu atakayechafua mazingira.
Mwisho.

Saturday, February 16, 2013

STORY PWANI



Na John Gagarini, Mkuranga
IMEELEZWA kuwa kuishi mbali na vituo vyao vya kazi kwa baadhi ya maofisa
ugani kwenye vijiji wilayani Mkuranga mkoa wa Pwani kumechangia kudumaza
shughuli za kilimo wilayani humo.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa mafunzo kwenye kijiji cha
Msufini kata ya Mbezi, mratibu wa mradi wa Wajibu wa Jamii Katika Usimamizi
wa Rasilimali za Umma za Sekta ya Kilimo wilaya hiyo (POCUSO), Bw Said
Gwaja alisema kuwa maofisa hao wamekuwa hawafiki kwenye vijiji
walivyopangiwa.

Bw Gwaja alisema kuwa kutokana na kuishi mbali na vituo vyao vya kazi
wamekuwa wakiishia ofisini na kushindwa kwenda kwenye maoeneo waliyopangiwa
hasa yale ya vijijini.

“Ni vema wangekaa kwenye maeneo yao ya kazi ili iwe rahisi kwao kutoa
huduma kwa wakulima ambao wanakosa fursa nyingi kutokana na kutofahamishwa
namna ya kuweza kuzipata,” alisema Bw Gwaja.

Alisema kuwa fursa ambazo wakulima walipaswa kuzijua zinashindwa kuwafikia
kwani wanazipata wakati muda wa kilimo unakuwa umepita hivyo kushindwa kupata pembejeo za ruzuku kwa wakati muafaka.
Aidha alisema kuwa endapo wangekuwa wanafanya kazi kwenye maeneo waliyopangiwa hususani vijijini ingekuwa raisi kwao kujua chanagamoto zinazo wakabili wakulima hivyo ingekuwa rahisi kuwasaidia kuliko ilivyosasa.
Aliwataka wakulima kujitokeza kwenye mafunzo yanayoandaliwa na shirika lake ili waweze kujua namna ya kufuatilia matumizi ya rasilimali za wananchi zikiwemo zile za kilimo ambazo nyingine zinawalenga wao moja kwa moja.
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

WATANZANIA wametakiwa kuwekeza kwenye hisa za makampuni na taasisi za fedha nchini badala ya kuwaachia wageni pekee ili  nao wamiliki makampuni na taasisi hizo.
Hayo yamesemwa na mjumbe wa bodi ya soko la hisa Dar es Salaam  Bw Arphaxad Masambu  wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha.

Bw Masambu alisema Watanzania wengi hawana tabia ya kuwekeza katika hisa za makampuni mbalimbali na kusababisha makampuni mengi na taasisi nyingi nchini kumilikiwa na wageni kutoka katika mataifa ya nje na kuwaacha wazawa wakiwa masikini wa kipato.

“Faida ya kununua na kumiliki hisa kuwa si kwa mnunuzi wa hisa pekee bali ni pamoja na vizazi yaani watoto wajukuu, vitukuu kunufaika na hisa hizo,” alisema Bw Masambu.

Alisema kuwa uuzaji wa hisa za makampuni na taasisi ni kwaajili ya kuonfgeza nguvu ya pamoja katika kuendesha na kusimamia kampuni hizo na taasisi hizo ili kuzalisha na kutoa faida yenye tija kwa wengi zaidi.

Naye Mwenyekiti wa chemba ya wafanyabiashara (TCCIA) mkoa wa Pwani Bi Kasa Mlonja aliwataka wananchi, wakulima na wafanyabiashara kuwekeza katika hisa mbalimbali zinazouzwa katika taasisi za fedha na makampuni ilikuwa na madaraka kamili ya hizo kampuni na taasisi kwa lengo la kuendeleza nchi yetu.

Mwisho.   
Na John Gagarini, Kibaha
DIWANI wa kata ya Maili Moja Bw Andrew Lugano amesikitishwa na mamalaka ya maji safi na majitaka (DAWASCO) kushindwa kuwahudumia wananchi hali inayosababisha kukosa maji kwa zaidi ya mwezi sasa.
Akizungumza mara baad aya kufanya ziara kwenye kata hiyo kuangalia maeneo ambayo yamekuwa yakikosa maji kwa muda mrefu, huku akiwa ameambatana na meneja wa DAWASCO Bw Robert Mugabe alisema kuwa hakuna sababu ya wananchi kukosa maji kwa muda wote huo na uongozi upo.
Bw Lugano alisema kuwa amekuwa akipata kero hiyo ya maji toka kwa wananchi na jitihada zake za kufuatilia zimekuwa zikigonga mwamba hali iliyomlazimu kumtoa meneja huyo ofisini kwake Jumamosi na kumwonyesha jinsi gani wananchi wanavyotaabika kwa kukosa maji.
“Siwezi kukubali kuona wananchi wakihangaika kutafuta maji huku chanzo cha maji kikiwa jirani hivyo lazima kampuni hiyo ijali wananchi ili waondokane na kero hiyo,” alisema Bw Lugano.
Moja ya wakazi wa kata hiyo ambaye anakaa mtaa wa Mzimuni Bw Mohamed Atiki alisema kuwa wamekuwa wakipata tabu kubwa ya kupata maji hali inayowasababisha kununua maji kwa bei ya shilingi 500 kwa dumu la lita 20.
“Tumekuwa tukihangaika kwa kipindi kirefu licha ya kutoa taarifa ya ukosefu wa maji kwenye kampuni hii ya maji hivyo lazima wabadili utendaji kazi wao,” alisema Bw Atiki.
Kwa upande wake meneja wa DAWASCO Kibaha Bw Robert Mugabe alisema kuwa tatizo kubwa lililosababisha wananchi kukosa maji ni kutokana na ujenzi wa barabara katika kata hiyo.
“Mabomba mengi yamekatwa kutokana na ujenzi wa barabara lakini hata hivyo tayari tumewasiliana na mkandarasi ili kuangalia namana ya kuweza kurekebisha hali hiyo,” alisema Bw Mugabe.
Bw Mugabe alisema kuwa tayari wameshafanya tathmini ya uharibifu uliofanyika na wakati wowote wataanza kufunga mabomba yaliyokatwa ili wananchi hao waendelee kupata maji kama kawaida.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kisarawe
IMEELEZWA ukosefu wa vifaa kwa watoto wenye ulemavu 89 wilayani Kisarawe mkoani Pwani wameshindwa kuanza masomo kutokana na kukosa vifaa vya kusomea.
Hayo yalisemwa na katibu wa chama cha watu wenye ulemavu wilayani Kisarawe Bw Ibrahim Tully alisema kuwa jumla ya watoto wenye ulemavu katika wilaya hiyo ni 218.
Bw Tully alisema alisema kuwa kati ya watoto hao ni 34 hivyo kuwafanya watoto hao kushindwa kuanza shule hadi kufikia umri wa miaka 12 na kuendelea.
“Tatizo hilo linasababishwa na uhaba wa fedha wa kununua vifaa hivyo kutoka kwa wazazi na kukosekana kwa wafadhili wa kudumu kusaidia hali hiyo,” alisema Bw Tully.
Aidha alisema mbali ya hayo ,tatizo jingine kubwa ni baadhi ya wazazi na walezi kuwanyanyapaa watoto wenye ulemavu wanaoishi nao kwa kuona aibu kuwaanzisha shule jambo linalowanyima haki yao msingi.   
“Tunakabiliana na hali hiyo kwa kutafuta wafadhili ili kusaidia upatikanaji wa baiskeli maalum kwa ajili ya watoto hao waweze kwenda shule,” alisema Bw Tully.
Bw Tully alisema katika jitihada hizo tayari wamepata baiskeli  50 za aina hiyo na kati ya hizo 10 wamezigawa kwa watoto wa Tarafa ya Chole na nyingine 40 zilizobaki watazigawa kwa watoto wenye ulemavu katika kata zilizopo wilayani kisarawe.
Pia wilaya hiyo ina changamoto ya ukosefu wa shule maalum ya watoto wenye ulemavu ikiwemo wenye ulemavu wa akili ambao  hawawezi kuchanganywa na watoto wengine kwasababu ya mahitaji yao kuhitajika kuwa rafiki zaidi.
Hata hivyo alisema kufuatia tatizo hilo jitihada za hali na mali zinafanyika kujenga shule hiyo mwaka huu ambapo wameshapata eneo lenye heka 100 katika kijiji cha Kidugalo  kata ya Mzenga na mchakato wa kupata hati unaendelea.
Mwisho                                                                                     
Na John Gagarini, Bagamoyo
VIONGOZI wa vikundi vya ujasiriamali kwenye kata ya Msata wilayani Bagamoyo wametakiwa kutumia fedha wanazopewa na sereikali na wafadhili mbalimbali kuzitumia kwa mipango waliojiwekea ili waweze kujikwamua na hali ngumu ya kiuchumi.
Hayo yalisemwa na Ofisa Mtendaji Kata ya Msata Bw Edgar Nazar wakati
akizungumza na kikundi cha Lulenga kinachojihusisha na ufugaji
nyuki na mazingira ambacho kimepatiwa zaidi ya sh. Mililioni nne  kwa ajili ya
utoaji wa elimu inayohusiana na sekta ya nyuki.

Bw Nazar alisema kuwa serikali na wadau mbalimbali wa maenedeleo wamekuwa wakitoa fedha nyingi kwa ajili ya kufadhili miradi ya maendeleo kupitia vikundi hivyo lazima zitumike kwa malengo husika.
“Serikali  imekuwa ikielekeza masuala mbalimbali yanayohusiana na ujasiliamali na
ushahidi huo ni huu wa Wizara ya Misitu kutoa kiasi hiki cha fedha kwa
ajili ya kuendeleza ufugaji nyuki na mazingira, niwaombe fedha hizi
zitumike kama zilivyolengwa,” alisema Bw Nazar.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kikundi hicho Bw Douglas Kilomo alisema kuwa kwa msimu wa mwaka uliopita kulikuwepo na mgongano kati yao na
wafugaji jamii ya wamasai hali iliyosababisha kusimama kwa shughuli
zetu kutokana na mgongano huo,” ilieleza sehemu ya taarifa.

Bw Kilomo alisema uwa zoezi la ufugaji nyuki linaendana na sanjali na utunzaji wa
mazingira hivyo amewaasa kuzingatia hayo ili kujiletea mafanikio katika zao la asali ambalo kwa sasa lina soko kubwa.

“Ufugaji nyuki ni sekta ambayo haihitaji mtaji mkubwa kama ilivyo
miradi mingine, unapokuwa na mzinga tu unasubiri mazao ambapo kwa
mwaka unavuna mara tatu sawa na sh. Laki 9 hivyo niwaombe muwe makini
kwa hilo,” alisema Bw Kilomo.

Naye mmoja wa wanakikundi Bw Mohamed Mrisho ameeleza kuwa mafunzo hayo anaimani yatawaongezea ufanisi wa shughuli zao na kujiongezea kipato chao.

MWISHO.

Friday, February 15, 2013

MWANAFUNZI AJINYONGA


Na John Gagarini, Kibaha
MWANAFUNZI wa darasa la kwanza wa  shule ya Msingi Mbaya, Geuza Patrick (12) amekufa kwa kujinyonga kwa kamba ya katani.
Kwa mujibu wa kaimu kamanda wa Polisi mkoani Pwani Gregory Mushi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 13 mwaka huu majira ya saa 12 jioni huko kitongoji cha Msufini tarafa ya Chalinze wilayani Bagamoyo.
Bw Mushi alisema kuwa mwanafunzi huyo alijinyonga kwenye Mti wa Mwembe nyumbani kwao.
Alisema kuwa chanzo cha kujinyonga bado hakijafahamika na polisi wanaendelea na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo.
Aidha alisema mwili wa marehemu ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SHULE ya Sekondari ya Bundikani ya Kata ya Maili Moja wilayani Kibaha imeanza kuchukua hatua kali kwa wanafunzi wanaovaa suruali za kubana maarufu kama modo kwa kuzichana.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwalimu mkuu wa shule hiyo Bi Flora Chibululu alisema kuwa juzi walichana suruali za wanafunzi watatu kutokana na kwenda shuleni na suruali hizo kinyume cha sheria.
Alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wamekuwa na tabia ya kuzirekebisha  kwa kuzibana suruali hizo licha ya kuwa zinashonwa kawaida na kukiuka taratibu za shule.
“Suruali hizo za shule hushonwa vizuri lakini wao huzipeleka kwa fundi na kuzibana sawa na miili yao maarufu kama modo, tulishawapiga marufuku kuzibadili nguo hizo lakini wanakaidi hali iliyotufanya tuchukue hatua hiyo ili kuleta nidhamu shuleni,” alisema Bi Chibululu.
Bi Chibululu alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakikiuka taratibu za shuleni na kuiga tabia ambazo zinashusha taaluma hivyo shule itakabiliana na vitendo kinyume cha taratibu za shule.
Aidha alisema wataendelea kuzichana suruali hizo kwa mwanafunzi atakaye vaa kinyume cha sheria za shule kwani huo ni utovu wa nidhamu na lazima wanafunzi wafuate taratibu za shule.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
AKINA Mama Lishe na Baba Lishe kwenye kata ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kupima afya zao kwa mujibu wa sheria ili waweze kuhudumia wateja wao wakiwa na afya njema vinginevyo watapelekwa mahakamani kwa kukiuka kanuni za afya.
Hayo yalisemwa na ofisa afya wa kata hiyo Bw Ally Shah, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha na kusema kuwa watakao kataa kupima afya watapelekwa mahakamani.
Bw Shah alisema kuwa hivi karibuni baadhi ya wahusika waligoma kwenda kupima afya zao wakidai kuwa kiwango cha kupima ambayo ni shilingi 5,000 ambayo ilipangwa na halmashauri kuwa ni kubwa.
“Makundi hayo yanatakiwa kupima afya ili kutoa huduma wakiwa na afya njema ili kuepuka maambukizi ya magonjwa mbalimbali kama vile kifua kikuu na magonjwa ambayo yanaambukizwa kwa haraka,” alisema Bw Shah.
Alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hao wamekuwa na hofu ya kupima afya kuwa wataonekana na maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI jambo ambalo alisema kuwa upimaji huo hauhusiani na kupima vipimo vya ugonjwa huo.
“Wasihofie kupima afya kwani magonjwa yanayopimwa hayahusiani na ugonjwa huo na kama mtu anataka kupima ugonjwa huo ni hiyari yao wenyewe na si kwa lazima kama sheria inavyoelekeza,” alisema Bw Shah.
Aidha alisema kuwa magonjwa yanayopimwa ni pamoja na magonjwa ya zinaa, kifua kikuu na haja kubwa hivyo wafanyabiashara wapime kwani ni kwa faida yao na wateja wanaowahudumia.
Katika hatua nyingine alisema kwa sasa wanaendelea na kuboresha usafi wa mazingira ambapo vimeundwa vikundi mbalimbali vya usafi kwa ajili ya kuhakikisha mazingira ya Mji wa Kibaha ambapo sheria ndogondogo ya halmashauri inawatoza kiasi cha shilingi 50,000 kwa mtu atakayetupa uchafu kiholela.
Mwisho.