Saturday, February 15, 2025

WAANDISHI WA HABARI WAJENGEWA UWEZO JUU YA MALEZI MAKUZI MAENDELEO YA WATOTO

WAANDISHI wa Habari nchini wametakiwa kuleta mabadiliko chanya kwenye masuala ya malezi na makuzi ya watoto ili kuja kupata viongozi bora wa baadaye.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Osifa Programu kutoka Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) Victor Maleko ambaye alikuwa mwezeshaji wa mafunzo kuhusu uandishi wa habari zinazohusu Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM).

Maleko alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwa ukuaji wa watoto ambao wanatakiwa kupata huduma muhimu katika ukuaji wao ili wawe na makuzi mazuri.

WAANDISHI WATAKIWA KUANDIKA HABARI SAHIHI ZA UCHAGUZI

NAIBU Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Hamis Mwinjuma amevitaka vyombo vya habari kuandika habari sahihi kipindi cha uchaguzi ili kudumisha amani.

Ameyasema hayo Mjini Dodoma alipokuwa akifunga Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini.

Mwinjuma amesema kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kutoa taarifa sahihi ambazo zitawafanya wananchi kuchagua viongozi bora ambao watailetea nchi maendeleo.

"Kazi yenu kubwa ni kutoa taarifa sahihi kwa wananchi ambao wanaviamini vyombo vya habari kupata taarifa za ukweli na siyo za kupotosha ili kupata viongozi bora,"amesema Mwinjuma.

Kwa upande wake Mhandisi Endrew Kisaka ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) amesema kuwa vyombo vya habari vinapaswa kuandika habari za vyama vya siasa wakati wa uchaguzi bila ya upendeleo.

Kisaka amesema kuwa waandishi wazingatie kuandika sera na siyo majibizano au udini, ukabila na kutoingilia faragha za watu na kotoegemea upande wowote bali watoe nafasi kwa watu wote.

Naye katibu wa Mtandao wa Bloggers Tanzania (TBN) Khadija Kalili ameishukuru  TCRA na kuiomba kupunguza gharama za usajili ambapo kwa sasa ni shilingi 500,000 ambayo ni kubwa hivyo wengi kushindwa kulipia.

Kalili alisema kuwa TBN ilisajiliwa mwaka 2015 na ilianza na wanachama 100 hadi kufikia 300 ambapo baadhi walijitoa kutokana na kushindwa kusajili.

Mkutano huo wa mwaka ambao uliansaliwa na TCRA ulihusisha washiriki 528 ambao wanajihusisha na masuala ya utangazaji na watoaji maudhui mtandaoni nchini, waandishi wakongwe wa Redio Tanzania.

WAZIRI KABUDI ATAKA WATANGAZAJI KUACHA MBWEMBWE WATUMIE KISWAHILI SANIFU

WAZIRI wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Profesa Kabudi amewataka watangazaji kuacha mbwembwe na kubananga Kiswahili na kutumia Kiswahili Sanifu ili Tanzania iendelee kuwa nchi inayotumia Kiswahili fasaha.

Profesa Kabudi ameyasema hayo Mjini Dodoma wakati akifungua mkutano wa mwaka wa vyombo vya utangazaji nchini.

Amesema kuwa Tanzania ni nchi kinara wa lugha ya Kiswahili lakini endapo hakutakuwa na juhudi za makusudi za kukisimamia Kiswahili hatutakuwa vinara tena wa lugha hiyo.

"Watangazaji wanapaswa kutumia Kiswahili fasaha na sanifu kwani tuna utajiri wa misamiati hivyo tukitumie vizuri ili kuandaa vipindi vyenye tija kwa wasikilizaji,"amesema Kabudi.

Naye Mkurugenzi wa Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dk Jabiri Bakari amesema kuwa wamekuwa wakifanya utafiti juu ya maudhui ya mtandaoni ili kutoa taarifa sahihi na za umahiri.

Bakari amesema kuwa kuna utafiti umefanywa ambapo utakamilika mwezi huu lengo kuu likiwa ni kuboresha utoaji wa maudhui mitandaoni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui Saida Muki amesema kuwa watangazaji wa maudhui mitandaoni wanapaswa kuweka maslahi ya nchi mbele  na kujiepusha na maudhui yanayokiuka maadili.

 

Tuesday, February 11, 2025

WAANDIKISHAJI WASAIDIZI DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA HALMASHAURI YA MJI KIBAHA WAASWA





WAANDIKISHAJI wasaidizi wa zoezi la uboreshaji daftari la kudumu la wapiga kura Halmashauri ya Mji Kibaha wametakiwa kuwa waadilifu na waaminifu wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili kwa waandikishaji wasaidizi kwenye Halmashauri hiyo.

Shemwelekwa amesema kuwa waandikishaji hao wasaidizi wamepewa jukumu kubwa na wameaminiwa kwani zoezi hilo ni la Kitaifa hivyo wahakikishe wanalifanya kwa weledi ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza.

Amesema mafunzo hayo yawe chachu ya utendaji kazi wao kwenye zoezi la uboreshaji taarifa za wapiga kura na kuandikisha wapiga kura wapya litakuwa la siku saba kuanzia Februari 13 hadi 19.

Amewataka watumie lugha nzuri wakati wakiwahudumia wananchi ili iwe sehemu ya kuwavutia watu wengi wajitokeze kuboresha taarifa zao na kuandikisha wapiga kura wapya.

Jumla ya waandikishaji 262 wamepatiwa mafunzo hayo na kuna vituo 131 vitatumika kwenye zoezi hilo ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwaka huu.


Sunday, February 9, 2025

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA TAMISEMI YARIDHISHWA MIRADI YA ELIMU NA AFYA HALMASHAURI YA MJI KIBAHA





KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imekagua miradi ya ikiwemo ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Kibaha iliyogharimu kiasi cha shilingi bilioni 4.1.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Kibaha Catherine Saguti kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashari wakati akitoa taarifa juu ya ujenzi wa hospitali hiyo.

Dk Saguti amesema kuwa mapokezi ya fedha za mradi wa Ujenzi wa Hospitali na ununuzi wa vifaa tiba kutoka Serikali Kuu yalitolewa kwa awamu nne 
jumla ya shilingi bilioni 3.3 kwa ajli ya ujenzi na shilingi milioni 400  kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. 

"Fedha hizo zimepokelewa kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha 2019/2020, 2020/2021, 2021/2022 na 2024/25 na jumla ya majengo ambayo yamejengwa hadi sasa ni 14 na majengo 11 yamekamilika na yanatumika huku majengo matatu yanaendelea na utekelezaji katika hatua ya
ukamilishaji,"amesema Saguti.

Amesema kuwa Halmashauri imechangia jumla ya shilingi milioni 446.7 kwa ajili ya ukamilishaji wa
miundombinu na majengo ambayo hayakukamilika kwa fedha za Serikali Kuu.

Pia kamati hiyo imetembelea ujenzi wa kituo cha afya cha Kata ya Pangani kilichogharimu kiasi cha shilingi milioni 914 huku Halmashauri ya Mji Kibaha ikichangia kiasi cha shilingi milioni 189 kutokana na mapato ya ndani.

Wabunge hao wa Kamati ya Tamisemi walitembelea mradi wa shule mpya ya sekondari ya Kata ya Tangini iliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 528.9.

Ujenzi huo umetokana na mradi wa Uboreshaji wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP) ina uwezo wa kuchukua wanafunzi 398 wa kidato cha kwanza na cha pili wanawake 191 na wanaume 207.

Katika hatua nyingine kamati hiyo ya kudumu ya Bunge ya Tamisemi pia ilitembelea ujenzi wa Shule ya Msingi Mtakuja Kata ya Pangani ambayo ina mfumo wa Kiingereza ambayo imegharimu kiasi cha shilingi milioni 309.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Zainab Katimba amesema kuwa serikali ya awamu ya sita imewekeza fedha nyingi kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya afya na elimu.

Katimba amesema kuwa Serikali imewekeza kwenye miradi mingi ili kuwaletea wananchi huduma karibu na maendeleo ili kupunguza changamoto.

Amesema kuwa maagizo na maelekezo yaliyotolewa na kamati ili kuboresha miradi hiyo wataifanyia kazi ili iwe na ubora na kuwa na manufaa kwa wananchi.  

Akitoa majumuisho ya ziara ya Kamati Mwenyekiti wa kamati hiyo Justin Kamoga amesema wameridhishwa na ujenzi wa miradi hiyo kwani imejengwa kwa viwango vizuri.

Kamoga amesema licha ya miradi hiyo kujengwa vizuri lakini kuna baadhi ya changamoto ndogo ndogo ikiwa ni pamoja na kukamilisha baadhi ya maeneo yaliyobakia.

Friday, February 7, 2025

KITUO CHA AFYA VIGWAZA MBIONI KUKAMILIKA

KITUO cha afya cha Kata ya Vigwaza Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani kiko kwenye hatua za mwisho kukamilika ambapo kitatoa huduma mbalimbali zikiwemo za upasuaji hivyo kuwaondolea kero za akinamama za kujifungua.

Aidha serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 525 kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya kwenye Kata hiyo hivyo kuondoa changamoto hasa za mama wajawazito wakati wa kujifungua.
 
Diwani wa Kata ya Vigwaza Mussa Gama akizungumza Vigwaza wakati wa maadhimisho ya miaka 48 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amesema kwa sasa wananchi hususani wanawake waliokuwa wanashindwa kujifungulia kwenye Zahanati ya Vigwaza ambapo hawatapelekwa tena Mlandizi na Chalinze kupata huduma hizo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Lulu Rajabu kata ya Vigwaza amesema wanawake walikuwa wakikumbana na adha ya kutembea kilometa tisa na zaidi kipindi wanaposhindwa kujifungulia kwenye Zahanati.

Katika maadhimisho hayo wanachama wa CCM kutoka maeneo mbalimbali ya kata hiyo walioshiriki kupanda miti kwenye kituo hicho sambamba na kufanya harambee ya ujenzi wa ofisi ya chama ambapo zaidi ya milioni tatu zilichangwa 


Friday, January 31, 2025

TAKUKURU PWANI YAONGEZA MAPATO KUTOKA M 4.6 HADI M 12

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kuongeza makusanyo kutoka kiasi cha shilingi milioni 4.6 hadi 12 kwa wiki kwenye kizuizi cha Maliasili cha Wilaya ya Kibiti.

Aidha kutokana na kuongezeka kwa mapato hayo kwa mwaka mmoja kupitia kizuizi hicho Maliasi watakuwa na uwezo wa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 480 kwa mwaka.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Pwani Alli Sadiki alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya mafanikio yaliyopatikana kipindi cha miezi mitatu iliyopita kuanzia Oktoba hadi Disemba mwaka jana.

Sadiki amesema kuwa mafanikio ya makusanyo hayo yamefikiwa baada ya Takukuru kufanya uzuiaji katika mfumo wa ukusanyaji wa mapato kwa kutumia mashine ya Pos.

"Uzuiaji huo ulikuja baada ya taasisi hiyo kutoridhishwa na ukusanyaji mapato kwani yalikuwa ni madogo kulingana na uwezo mkubwa wa kizuizi hicho,"amesema Sadiki.

Amesema kuwa Takukuru ilisimamia ukusanyaji kuanzia Novemba 5 mwaka 2024 hadi Novemba 11 mwaka huo kwa saa 24 na kufanikiwa kukusanya kiasi hicho cha shilingi milioni 12  badala ya shilingi milioni 4.6 kwa wiki moja.

Aidha amesema kuwa walibaini kuwa baadhi ya wakusanyaji ushuru walipewa fedha na wenye mizigo ili wasitozwe malipo ya serikali, baadhi ya magari hayakukaguliwa hivyo kukwepa kulipa ushuru, baadhi ya wakusanyaji kupewa mwanya ukadiriaji wa chini wa malipo.

Pia katika kipindi hicho walifanya ufuatiliaji wa miradi 52 ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 12 ambapo hakukuwa na mapungufu huku mingine ikiwa inaendelea na utekelezaji.

Ameongeza kuwa miradi hiyo ni ya sekta za afya, elimu, maji, barabara na katika uelimishaji umma wamefanya semina, mikutano ya hadhara, vipindi vya redio, kuimarisha klabu za wapinga rushwa na Takukuru Rafiki ambapo wamezifikia kata 11.

"Katika kipindi hicho Takukuru ilifungua kesi 24 mahakamani ambapo washitakiwa 13 wametiwa hatiani na tulipokea malalamiko 60 kati ya hayo 37 yalihusu rushwa na yanafanyiwa kazi yakiwa kwenye hatua mbalimbali,"amesema Sadiki.

Ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa huo kuendelea kuunga mkono jitihada za mapambano dhidi ya rushwa kwa kuwafichua wale wanaoshiriki vitendo vya rushwa.