Sunday, August 20, 2023

COREFA YAZINDUA KITUO CHA SOKA KWA VIJANA KIBAHA


CHAMA Cha Soka Mkoa wa Pwani (COREFA) kimezindua kituo cha michezo kwa vijana chini ya miaka 17 kikiwa na lengo la kuibua na kukuza vipaji vya vijana ndani ya mkoa huo.

Akizindua kituo hicho kwa Kanda ya Kaskazini kaimu mkuu wa wilaya ya Kibaha Moses Magogwa ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema kuwa uwekezaji kwa vijana kutasaidia kuwa na timu bora za baadaye.

Magogwa ambaye ni katibu tawala wa wilaya (DAS) na mwenyekiti wa kamati ya michezo wa wilaya alisema kuwa serikali inaunga mkono suala la michezo kwani ni sehemu ya kutoa ajira kwa vijana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha soka mkoa wa Pwani Robert Munisi alisema kuwa malengo ya kuanzisha kituo hicho na vingine kwenye kila wilaya itakuwa na vituo vitatu ambapo kutakuwa na vituo 21 kwa mkoa mzima ni kuibua vipaji na kuviendeleza.

Naye mratibu wa kituo hicho Abdulakarimu Alawi alisema kuwa jumla ya vijana 500 wa shule za msingi na sekondari ambapo vijana wanacheza kutegemeana na umri wao.

JAMII IMETAKIWA KUPANDA MITI KWENYE MIRADI ILI KUHIFADHI MAZINGIRA

 

Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Switbert Mkama ameitaka jamii kupanda miti kuzunguka maeneo yenye miradi ili kuhifadhi mazingira na kuifanya kuwa endelevu.

Amesema hayo alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi ya Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa Kutumia Mfumo Mfumo Ikolojia Vijijini (EBARR) katika Wilaya ya Kaskazini ‘A‘ Mkoa wa Kaskazini, Unguja - Zanzibar.

Akikagua visima, ujenzi wa majengo ya vituo vya wajasiriamali wa ufugaji, ushonaji, utengenezaji wa sabuni pamoja na vitalu nyumba katika Shehia za Jugakuu, Mbuyutende na Kijini, Dkt. Mkama amesema ameridhishwa hatua iliyofikiwa.

Aidha, aliwahimiza viongozi wakiwemo masheha wa shehia hizo ambazo zimefaidika na miradi ya visima kuwasimamia wananchi kupanda miti na kuimwagilia.

“Binafsi nimeridhishwa na namna mnavyosimamia miradi hii na nawapongeza masheha kwa kuisimamia na wananchi kwa kuipokea na kushiriki kikamilkfu katika kuitekeleza, niwaombe mhakikishe inaendelea kuwa na ubora ule ule,“ amesisitiza.

Kwa vile ujenzi wa majengo ya wajasiriamali wa ushonaji na uzalishaji wa sabuni utahusisha mashine na vifaa, Dkt. Mkama alisema ni muhimu kuwepo na mpango mkakati ili mradi uwe endelevu hata pale utakapokwisha muda wake.

Alisema vyerehani vitakavyotolewa pamoja na vifaa vingine vikiwemo taa na mabomba ya maji vitahitaji matengenezo madogo madogo na kulipiwa umeme hivyo wanajamii waangalie namna ya kuuhudumia bila kusubiri serikali.

Saturday, August 19, 2023

NYERERE SUPER CUP KUFANYIKA KIBITI NA RUFIJI KUANZA SEPT 23 MWAKA HUU

Katika kuelekea kumbukizi ya Miaka 23 ya kifo Cha Mwalimu Julius kambarage Nyerere na kuenzi FIKRA zake kwa vitendo Taasisi ya kumbukumbu ya mwalimu Julius Kambarage Nyerere Tarehe 19.8.2023 imefanya kikao cha maandalizi ya NYERERE SUPER CUP.

Wilaya ya Kibiti itashirikisha timu 6 Bungu Jaribu, Mtawanya, Kibiti, Mchukwi, na Dimani na Wilaya ya Rufiji timu 6 Ngorongo, Utete, Mgomba, Muhoro, Umwe na Mkongo.

Mashindano hayo yanatarajiwa kunaza Tarehe 23.9.2023 na kwisha 12.10.2023 tunashukuru 1.Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani 2.Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Kibiti 3.Ofisi ya Mkuu wa Mkuu wa wilaya ya Rufiji 4.Ofisi ya Mbunge wa Kibiti na Rufiji 6.Madiwani wa Rufiji na Kibiti 7.Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani COREFA 8.Chama Cha Mpira wa Miguu Kibiti na Rufiji 9.Chuo Cha Afya St David college kimara 10. Mfuko wa NSSF Temboni na wadau wote kufanikisha Safari hii UZALENDO NI KULIPENDA TAIFA LAKO MITANO TENA

MNEC HAMOUD JUMAA ATAKA SUALA LA BANDARI RAIS ASISEMWE VIBAYA





MJUMBE wa Halmashauri Kuu Taifa (NEC) Hamoud Jumaa amevitaka baadhi ya vyama vya upinzani nchi kuacha kumsema vibaya Rais Dk Samia Suluhu Hassan kuhusu suala la mkataba wa Bandari badala yake watoe ushauri.

Jumaa aliyasema hayo Kata ya Mtambani Mlandizi Kibaha alipokuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa operesheni ya kuanza maandalizi ya uchaguzi ngazi ya serikali za vijini yenye kauli mbiu ya Simika Bendera.

Alisema kuwa anawashangaa wapinzani kutoa maneno mabaya kwa Rais kuhusu mkataba wa Bandari ambapo walipaswa kutoa ushauri na si kumsema vibaya.

"Suala la mkataba wa bandari ni jambo la msingi na Rais yuko makini na mkataba huo ili kuongeza mapato ya nchi na kama wao wanaona kuna jambo basi washauri na siyo kutoa maneno yasiyofaa,"alisema Jumaa.

Aidha alisema kuwa wanamshukuru Rais kwani ameonyesha uvumilivu mkubwa licha ya kusakamwa kuhusu suala la bandari ambalo mchakato wake bado unaendelea.

"Tumechoka kusikia Rais anasemwa vibaya yule ni kiongozi hivyo lazima aheshimiwe ila tunampongeza kwa ustaamilivu anaouonyesha kwani hawajibu licha ya kusemwa vibaya,"alisema Jumaa.

Aliwataka viongozi kuwajali viongozi wa ngazi za chini hususani mabalozi na viongozi wa mashina kwani wao ndiyo wako karibu na wanachama kwani ili kushinda uchaguzi kwani ndiyo malengo ya chama chochote.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Said Kanusu alisema kuwa anashangazwa na watu kutoa maneno kuwa eti bandari imeuzwa wapinzani wameishiwa hoja.

Kanusu alisema kuwa wananchi wawe na imani na wasikatishwe tamaa na wanaoleta hoja zisizo na msingi ajenda ya nchi ni kuleta maendeleo na miradi.

Naye Diwani wa Kata ya Mtambani Godfrey Mwafulilwa alisema kuwa kauli mbiu hiyo ni kuimarisha ngazi ya chini ya mabalozi kuwapa nguvu kwani wanakazi kubwa kukiimairisha chama.

Mwafulilwa alisema kuwa ngazi ya msingi sana ni balozi ambapo chama kinarudi chini ambako huko ndiko kwenye wanachama na hoja za wanachama na wananchi.

Alisema kuwa Rais ni mvumilivu na hawavutiwi na tabia inayofanywa na watu wanamchafua wao wanapaswa kuja na hoja na ushauri ila siyo kumchafua.

JUKWAA LA WAZALENDO HURU TANZANIA KUUNGA MKONO ROYAL TOUR


JUKWAA la Wazalendo Huru Tanzania Mkoa wa Pwani katika kuunga jitihada za Rais Dk Samia Suluhu Hassan kutangaza utalii inatarajia kufanya ziara Visiwani Zanzibar kutembelea vivutio vya utalii.

Akizungumza na waandishi wa Habari Mjini Kibaha mwenyekiti wa Taasisi hiyo Hadija Juma alisema kuwa hiyo ni sehemu mojawapo ya kuunga mkono jitihada za serikali kwa vitendo.

Juma alisema kuwa utalii ni moja ya vyanzo vikuu vya pato la Taifa hivyo wameona waihamasishe jamii kutembelea vivutio vilivyopo ikiwa ni utalii wa ndani.

Kwa upande wake katibu wa taasisi hiyo Hawa Cheka alisema kuwa lengo lao ni kuelezea mafanikio ya serikali kwenye nyanja mbalimbali za kiafya, kielimu, kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Cheka alisema kuwa mbali ya malengo hayo pia ni kuwafanya Watanzania kuwa Wazalendo, kuwa waadilifu, kuheshimu mila na desturi na kujitolea kwenye shughuli za maendeleo.

Friday, August 18, 2023

SERIKALI YATOA BILIONI 12 UJENZI VITUO VIDOGO KUSAMBAZA BIDHAA ZA PETROLI NA DIZELI VIJIJINI

 

Serikali imetoa billion 12 kwa ajili ya mradi wa kuwezesha ujenzi wa vituo vidogo vya kusambaza bidhaa za Petroli na Diseli vijijini Tanzania bara kwa lengo la kulinda Mazingira na Afya ya watumiaji na kuboresha upatikanaji na Usambazaji wa Mafuta vijijini.

Mkurugenzi Mkuu Wa Wakala wa Nishati Vijiini REA Mhandisi Hassan Said amesema hayo leo Jijini Dodoma katika Mkutano na waandishi wa habari akisema usambazaji wa mradi huo  unahusu kuwekeza ujenzi wa vituo vidogo vya mafuta katika maeneo mbalimbali Vijiini.

Said amesema kuwa moja ya changamoto inayosababisha wananchi wasitumie nishati safi na kuendelea kutumia nishati ya asili yaani mkaa na kuni ni pamoja na upatikanaji wake kwani nishati asilia zimekua zikipatikana kwa urahisi.

Aidha amesema Wakala umeanza kutekeleza Mradi wa kusambaza mitungi ya gesi ya kupikia kwa utaratibu wa utoaji ruzuku kuwezesha usambazaji wa mitungi ya gesi ya kupikia (LPG) 71,000  yenye thamani ya shilingi bilioni 3 pamoja na majiko banifu 200,000  (laki mbili) katika maeneo ya vijijini huku kwa mwaka wa fedha 2023/24 jumla ya fedha  takribani bilioni 10 zimetengwa kwaajili ya kufanikisha mradi huo.

Pia ametoa rai kwa Watanzania kutumia mafundi wanaotambulika na Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO) kuondoa lawama zinazotolewa na wananchi dhidi ya Serikali zinazosababishwa vishoka wanaofanya uunganishaji wa umeme kinyume cha sheria.

Serikali imetoa jumla ya shilingi trillioni 1.7 kwa Wakala wa Nishati Vijiini (REA) kwaajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali  ya nishati nchini.

Kadhalika Serikali kupitia REA kwa kushirikiana na Benki ya Dunia (WB) imetenga Dola za Kimarekani milioni 6 kwa ajili ya mradi wa usambazaji wa majiko banifu ya kupikia.

DKT KIJAJI AWATAKA WAFANYABIASHARA KUJENGA MIUNDOMBINU YA UWEKEZAJI

 


Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji amewataka wafanyabiashara wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa zinazojitokeza kwa kujenga miundombinu wezeshi kwa wawekezaji na wageni  kwani baada ya Serikali kuhamia Jijini Dodoma kumekuwa na ongezeko la wageni kutoka sehemu mbalimbali Duniani.

Kijaji ameyasema hayo leo Agosti 17, 2023 wakati wa Kikao kazi na wafanyabiashara wa Jiji la Dodoma katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Jengo la Mkapa ambapo kikao hicho kimewahusisha wajasiriamali na wafanyabiashara pamoja na majukwaa yanayojihusisha na ujasiriamali. 

Waziri Kijaji amesema uchumi imara wa Taifa upo mikononi wa sekta binafsi hivyo amewahimiza wafanyabiashara hao kutumia fursa zote zinazojitokeza  iwe ni sekta binafsi au kutoka serikalini ili kuendelea kukuza uchumi wa nchi. 

Waziri Kijaji amewahimiza wajasiriamali kuwa waaminifu na Fedha zinazotolewa na Serikali kama sehemu ya mtaji ili kuwawezesha na wengine kupata hiyo fursa. 

"Lazima tukubaliane na utaratibu uliowekwa uadilifu wetu, uaminifu wetu ni muhimu hakuna fedha za bure sehemu yeyote lazima uwe na uhakika wa fedha kurudi  na mtu unae mpatia fedha hivyo tunatakiwa kumthibitishia Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama alivyo mtetezi wetu namba moja "ameeleza Kijaji

Kwa Upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule akitoa salamu za Mkoa amempongeza Waziri huyo kwa kukutana na kuzungumza na wafanyabiashara hao pamoja na kutatua changamoto na kero  zilizokuwa kikwazo katika utekelezaji wa biashara zao.

Senyamule amesema Mkoa wa Dodoma upo tayari kupokea wawekezaji na kuongeza idadi ya viwanda ili kuongeza na kukuza mapato ya Serikali na uchumi wa nchi ya Tanzania.