Friday, October 27, 2017

MIILI MIWILI YA WATU WALIOSOMBWA NA MAJI YAPATIKANA


Na John Gagarini, Kibaha

WATU wawili wamefariki dunia kufutaia mvua iliyonyesha juzi mkoani Pwani ambapo miili yao imeweza kugundulika baada ya maji kupungua kwenye mto Mpiji unaotenganisha mikoa ya Pwani na Dar es Salaam.

Akithibitisha kuokotwa kwa miili hiyo kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Pwani Blasius Chatanda alisema kuwa miili hiyo ilikutwa kando kando ya mto huo ambao ulikuwa umejaa kutokana na mvua kubwa zilizonyesha maeneo mbalimbali ya nchi.

Chatanda alisema kuwa miili hiyo ilokotwa maeneo tofauti ambapo mwili wa kwanza ulipatikana majira ya saa 2:30 eneo la Muheza kata ya Pangani alitambuliwa kwa jina la Simon Ramadhan mwenye umri kati ya miaka (25) na (30) uliokotwa eneo la mto Mpiji na marehemu alikufa alipokuwa akijaribu kuvuka.

“Mwili wa pili wa Issa Ally (28) ambaye ni mgambo uliokotwa eneo la Kiluvya na inadaiwa kuwa marehemu alisombwa na maji alipokuwa akijaribu kumwokoa mtoto aliyetaka kusombwa na maji na kukutwa kilometa nne toka sehemu aliyozama,” alisema Chatanda.

Alisema kuwa miili yote ya marehemu imehifadhiwa kwenye hospitali ya Rufaa ya Tumbi kwa ajili ya kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi.

“Nawaomba wananchi kuwa makini wakati wa kuvuka kwenye mito kuwa na subira ili maji yapungue waweze kuvuka na kuendelea na safari zao kwani wasidaharu maji kama ni madogo ambapo yanaweza kuwaletea madhara,” alisema Chatanda.

Mwisho.   
  


SABA WASOMBWA NA MAJI WANUSURIKA


Daraja linalounganisha mikoa ya Pwani na Dar es Salaam likiwa limejaa maji

 Baadhi ya wananchi wakifuatilia zoezi la uokoaji watu waliosombwa na maji ambao walipanda kwenye miti

 Moja ya kijana aliyenusurika Silas Moshi baada ya kusombwa na maji mara baada ya kuokolowa

 Dada ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja baada ya kuokolewa akiwa amepoteza fahamu akipakiwa kwenye gari la polisi kwa ajili ya huduma ya kwanza.



 Kijana Mohamed Kitindi aliyenusurika baada ya kusombwa na maji 

 Furaha Mwaipopo moja ya watu walionusurika baada ya kusombwa na maji na kupanda kwenye mti


 Moja ya watu walionusurika akihojiwa na polisi baada ya kunusurika 

 Kened Meshaki ambaye alishika nguzo ya bango huku mwili wake ukiwa ndani ya maji kwa zaidi ya masaa matatu akiwa ameshikwa mkono na polisi kwa ajili ya kwenda kupatiwa huduma ya kwanza


Na John Gagarini,Kibaha

WATU saba wamenusurika kifo baada ya kusombwa na maji walipokuwa wakijaribu kuvuka huku wakiwa wameshikana mikono ambapo walijinusuru kwa kupanda kwenye miti kabla ya kuokolewa na kikosi cha Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani.

Aidha kati ya watu hao mmoja alikuwa akininginia kwa kujishika kwenye bomba la bango la matangazo huku mwili wake ukiwa ndani ya maji kwa masaa zaidi ya huku akiwa anaomba msaada wa kuokolewa bila mafanikio.

Watu walionusurika ni pamoja na Kened Meshaki, Mohamed Kitindi, Silas Moshi Henry Francis na mwanamke mmoj ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja ambao wote walikimbizwa hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Pwani.

Tukio hilo lilitokea jana eneo la Maili Moja wilayani Kibaha kwenye daraja linalotenganisha kati ya mkoa wa Dar es Salaam na mkoa wa Pwani na kusababisha daraja kujaa maji na kusababisha magari na watu kushindwa kuvuka upande wa pili.

Daraja hilo ambalo linapita kwenye mto Mpiji lilikuwa halipitiki na kusababisha watu na abiria kushindwa kuvuka upande wa pili kutoka Maili Moja wilayani Kibaha na upande mwingine Kiluvya wilaya ya Ubungo.

Kutokana na daraja hilo kushindwa kupitika abiria wa mabasi wameshindwa kuendelea na safari zao za kwenda mikoani na maeneo mengine yanayopita kwenye barabara ya Morogoro.

Akizungumza na gazeti hili kwenye eneo la tukio hilo ofisa habari na uhusiano wa Jeshi la uokoaji Harison Mkonyi alisema kuwa zoezi la ukoaji limefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani wameweza kuwaokoa watu hao wakiwa salama.

Mkonyi alisema kuwa wamefanikiwa kuwaokoa watu hao kwa kushirikiana na wadau wengine ambao walijitosa kwenye maji hayo ambayo yalikuwa mengi na kulifunika kabisa daraja hilo na kusababisha kushindwa kupitika.

“Tunawashukuru wadau mbalimbali vikiwemo vikosi vya majeshi ya Polisi, Magereza, JWTZ na wananchi ambao walionyesha ushirikiano wa hali ya juu kuwanusuru watu hao akiwemo mwanamke mmoja,” alisema Mkonyi.

Mwisho.

Thursday, October 19, 2017

MBUNGE KIBAHA MJINI AKABIDHI VYEREHANI KWA WATU WENYE ULEMAVU


Na John Gagarini, Kibaha

MBUNGE wa Jimbo la Kibaha mkoani Pwani Silvestry Koka ametoa vyerehani vinnne kwa Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) wilaya ya Kibaha kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za ujasiriamali.

Akikabidhi vyerehani hivyo kwa uongozi wa shirikisho hilo Katibbu wa Mbunge huyo Method Mselewa alisema kuwa mbunge huyo katoa vyerehani hivyo kufuatia ombi lao.

Mselewa alisema kuwa watu wenye ulemavu nao wanapaswa kusaidiwa kama wanavyosaidiwa watu wa makundi mengine yanavyosaidiwa ili kujiendeleza kiuchumi.

“Kuwa na ulemavu siyo mwisho wa maisha kwani nguvu mnazo na mnauwezo kama watu wasiokuwa na ulemavu na tutaendelea kuwasaidia ili nanyi mjikwamue kwa kujiongezea kipato chenu na cha familia zenu,” alisema Mselewa.

Alisema kuwa kutokana na kuungana kwao kutasaidia kuwafikia kwa urahisi kuliko kila mtu angekuwa anaomba peke yake ingekuwa ngumu lakini kwa kuwa pamoja imekuwa rahisi.

“Hizi mashine mnapaswa kuzitunza kwani mbali ya kuwapatia ujuzi kia zitawapatia kipato ambacho kitaweza kuwafanya muwe na mapato kuliko kuomba jambo ambalo halifurahishi,” alisema Mselewa.

Kwa upande wake mwenyekiti wa SHIVYAWATA Ally Mlanga alisema kuwa wanshukuru msaada huo kwani kwao huo ni kama mtaji ambao watahakikisha wnaauendeleza.

Mlanga alisema kuwa wao hawataki fedha ila wanachotaka ni kupewa vitu ambavyo vitawasaidia kuliko fedha ambazo zinaweza kupotea kwa urahisi.

Naye ofisa Maendeleo wa Kata ya Kibaha Regina Lazaro alisema kuwa kupatiwa vyerehani hivyo vitawasaidia kujiongezea kipato kwani moja ya shughuli zake ni kuhamasisha ujasiriamali.

Lazaro alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana na shirikisho hilo ikiwa ni njia mojawapo ya kuwasaidia kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na serikali au wadau toka sekta binafsi.


Mwisho.

WAWILI WASHIKILIWA NA POLISI KWA KUKUTWA NA MAGUNIA SABA YA BHANGI



Na John Gagarini, Kibaha


WATU wawili wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Pwani kwa tuhuma za kukutwa na magunia saba ya dawa za kulevya aina ya bhangi yenye uzito wa kilogramu 7,500.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha kamanda wa Polisi mkoani humo Jonathan Shana alisema kuwa watuhumiwa hao waligundulika baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali.

Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea huko Kwa Mathias wilaya ya Kibaha baada ya askari waliokuwa doria kupata taarifa juu ya ajali ya gari.

“Watuhumiwa hao walikuwa kwenye gari namba T847DHT aina ya IST ambalo lilipata ajali kwenye eneo hilo na baada ya kufika walianza kuwaokoa na ndipo walipokuta na gunia saba za bhangi hiyo ikiwa kwenye hilo gari ikiwa imehifadhiwa kwenye magunia ya salfeti,” alisema Shana.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Kundaeli Mbowe (24) ambaye ni dereva wa gari hilo na mkazi wa Kiwalani Jijini Dar es Salaam na Ally Mtena (28) mfanyabiashara na makazi wa Gongolamboto.

Aidha alisema kuwa watuhumiwa hao wanashikiliwa ili kuweza kuchukuliwa hatua za kisheria na kujua bhangi hiyo waliitowa wapi na walikuwa wakiipeleka wapi.


Mwisho.

AMUUA MWENZAKE KWA KUMCHONA NA VISU


Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi Mkoani Pwani linamsaka Niniyay Silongoy kwa tuhuma za kumwua kwa kumchoma kisu Lemandra Kishwakwi (35) wote wa Kijiji cha Chamakweza wilaya ya Kipolisi Chalinze-Bagamoyo.
Kwa mujibu wa kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani Jonathan Shana alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikimbia kusikojulikana baada ya tukio hilo.

Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 18 mwaka huu majira ya saa 11:30 jioni Kijijini hapo baada ya kuchomwa kisu hicho kwenye kwapa la kushoto na mtuhumiwa.

 “Mbali ya kuchomwa kwapani pia mtuhumiwa alimchoma kisu shingoni na mkono wa kulia na mtuhumiwa baada ya kutekeleza azma yake alikimbia na anatafutwa na jeshi hilo kufuatia tukio hilo,” alisema Shana.

Alisema kuwa chanzo cha mauaji hayo ni ulevi ndipo mtuhumiwa alipofanya mauaji hayo ya kusikitisha ambayo haikujulikana kwanini mtuhumiwa alifikia hatua hiyo ya kumchoma mwenzake kisu.

Aidha alisema kuwa mwili wa marehemu ulikabidhiwa ndugu kwa ajili ya mazishi baada ya uchunguzi wa daktari huku juhudi za kumtafuta mtuhumiwa zikiendelea.

Mwisho.

Thursday, October 12, 2017

ULEGA AMWAGA CHECHE

NAIBU Waziri mpya  wa wizara ya  Mifugo na Uvuvi Abdalah  Ulega amesema hawezi kulifumbia macho hata kidogo suala la baadhi ya viongozi na watendaji ambao wamekuwa na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea kwa kukaa tu ofisini bila ya kutimiza majukumu yao   ipasavyo na kuwaagiza kuchapa kazi kwa bidii bila ya kutegeana kwa kuvitembelea vikundi  vyote vya  uvuvi na ufuga   ili kuweza kusikiliza kero na kubaini  changamoto  zinazowakabili katika kutekeleza majukumu yao.

Ulega alitoa  kauli hiyo wakati alipofanya ziara yake ya kikazi ya siku moja kwa viongozi  mbali mbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, ambapo  amesema kuna baadhi ya watumishi wengine  wamekuwa ni wazembe na kusababisha kukwamisha juhudi za serikali katika kuleta  chachu ya maendeleo  hivyo ameahidi kulivalia njuga suala hilo kwa lengo la kuweza kuboresha sekta ya uvuvi na ufugaji.

Aidha Naibu Waziri huyo aliwataka maafisa uvuvi na mifugo  kuwa wazalendo na nchi yao na kuhakikisha wanazilinda  na kuzitunza rasilimali zilizopo  pamoja na   kuweka mipango  endelevu ya kutenga maeneo  maalumu kwa ajili  ya kufanyia kazi zao sambamba na kuviwezesha vikundi hivyo  katika mambo mbali mbali ikiwemo kujenga,malambo, majosho pamoja  na kuwapatia vitendea kazi.

Pia Ulega alisema kwamba  kwa sasa kipaumbele chake kikubwa ni kuhakikisha kwamba anavisaidia kwa hali na mali  kwa kuviwezesha vikundi mbali mbali  vya wafugaji na uvuvi  pamoja na kuweka mipango madhubuti ambayo itaweza kusaidia kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo katika sekta hiyo aliyopewa dhamana na Rais Dk. John Pombe Magufuli.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Filbeto Sanga akizungumzia kuhusiana na suala la ardhi alisema kuwa kumeibuka kikundi cha baadhi ya  madalali ambao ni matapeli wanachukua hela za watu na kuamua kuuza  maeneo ya mashamba  ambayo tayari yana hati miliki  bila ya kufuata taratibu zozote na  kupelekea  wananchi  wenyewe  kujikuta wanakosa maeneo  kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao za kimaendeleo.

Katika hatua nyingine Mkugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Mkurunga Mshamu Munde akizungumza katika kikao cha dharura na waandishi wa habari ofisini kwake amekanusha uvumi wa taarifa zinazotolewa na  wananchi kuhusiana na shamba  linalomilikiwa na  mwekezaji wa kampuni ya Soap Allied Industry .

Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa  eneo hilo  ambalo linalalamikiwa na wananchi hao lina ukumbwa wa hekari 1750 na kuongeza kuwa kwa sasa linamilikiwa kihalali na mwekezaji huo  tangu mwaka 1988, na kupiga marufuku  wananchi wanaovamia maeneo  ya watu kiholela bila ya kuzingatia taratibu.

“Mimi kwa kweli nina shangaa sana  huu uvumi unaotokwa kwa baadhi ya wananchi kuhusiana na eneo hili, ndugu zangu waandishi eneo hili linamilikiwa kihalali, hivyo mimi ninachowaomba watu wanaolalamika kufika ofisi za mkurugenzi ili niwape ufafanuzi zaidi na sio kuanza kusababisha migogoro ambayo haina faida  hata kidogo katika Wilaya yetu ya Mkuranga nah ii tabia kwa kweli mimi siwezi kuivumilia hata kigogo nitahakikisha kwamba maeneo yote yanatolewa kwa utaratibu unaotakiwa,”alisema Mkurugenzi huyo.

Pia Mkurugenzi huyo alisema  katikia kumuunga juhudi mkono Rais wa awamu ya tano Dk. John Pombe Magufuli katika kuwa na Tanzania yenye uchumi wa viwanda wameshatenga maeneo mbali mbali kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda ambavyo vitaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kukuza sekta ya viwanda na kuleta maendeleo kwa wananchi pamoja na upatikanaji wa fursa za ajira kwa vijana.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri hiyo ya Mkuranga Juma Abed na Diwani wa kata ya Makamba  Hssan Dunda hapa wanazungumzia kuhusiana na sakata hilo la mgogoro wa shamba la mwekezaji huo na  malalamiko yanayotolewa na wananchi.

Walisema kuwa kwa sasa shamba hilo linamilikiwa kihalali na mwekezaji huyo kwani alishakabidhiwa na halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga baada ya kufuata taratibu zote zinazostahili hivyo wananchi wanatakiwa kuachana na tabia ya kuvamia maeneo mengine ambayo sio yao.

VITENDO vya uvamizi wa maeneo ya mashamba pamoja na viwanja  vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wa  na wenyeviti wa vijiji kwa kushirikiana na madalali ambao ni matapeli kwa kuvamia maeneo ambayo sio yao na kuamua kuuza  kinyemela kinyume na taratibu katika Wilaya ya Mkuranga Mkoani Pwani vinachangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa migogoro kila kukicha.
      MWISHO

Wednesday, October 11, 2017

MAMA SALMA KIKWETE AITAKA JAMII KUMSAIDIA MTOTO WA KIKE KUPATA ELIMU











Na John Gagarin, Kibaha

MKE wa Rais Mstaafu wa awamu ya nne Mama Salma Kikwete amesema kuwa kuna haja ya kuondoa mila na desturi zinazomkwamisha mtoto wa kike kukosa elimu.

Ambapo jamii nzima inapaswa kumlinda mtoto wa kike ili aweze kufikia malengo yake kwa ukimsomesha umeisomesha jamii nzima na nchi itapata maendeleo.

Aidha alisema kuwa mkoa wa Pwani uko ndani ya mikoa 10 yenye matatizo ya mimba za utotoni ikiwa na asilimia 30 huku mkoa wa Katavi ukiwa ni wa kwanza kwa kuwa na asilimia 45 jambo ambalo halikubaliki kwa jamii kupinga masuala haya.

Ameyasema  wakati wa sherehe za siku ya mtoto kike Duniani zilizoandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la Room To Read ambapo kimkoa zilifanyika Kibaha na kusema kuwa Pwani inapaswa kuongoza kwenye mambo ya maendeleo na si kuongoza kwa mambo mabaya.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama ambaye alimwakilisha mkuu wa mkoa wa Pwani amesema kuwa licha ya sheria kali kuwekwa lakini baadhi ya changamoto zimekuwa zikimkwamisha mtoto wakike kupata elimu.

Naye mkurugenzi wa Room To Read amesema kuwa wameanzisha mradi wa mtoto wa kike wa stadi za maisha ili aweze kujitambua na kuwa na maamuzi sahihi na kujiepusha na vishawishi ambavyo ni vikwazo vya kushindwa kupata elimu.

Kwa upande wake Ofisa elimu Mkoa wa Pwani Germana Sondoka amesema kuwa changamoto zinazochangia mtoto wa kike kupata elimu ni nyingi lakini wamekuwa wakijatihidi kushirikiana na wadau kuzikabili.


Mwisho.

Monday, October 9, 2017

SIMBA WAKIWA WAMEPOZI

ATAKA WATHAMINI RAIS KUREJESHA RASILIMALI ZA NCHI




Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama amesema anasikitishwa na watu wanaomsema vibaya Rais Dk John Magufuli kwa kutothamini kile anachokifanya katika kurejesha rasilimali za umma.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha alisema kuwa kazi inayofanywa na Rais inapaswa kuungwa mkono na kila Mtanzania yoyote anayeitakia mema nchi yake.
Mshama alisema kuwa kutokana na jitihada anazozifanya wananchi wanapaswa kumuunga mkono kwa kubainisha wale ambao hawana uzalendo na nchi yao.
“Rais kasikia kero nyingi na sasa ameanza kutekeleza kwa vitendo mfano masuala ya usafiri, upatikanaji wa dawa, suala la madini, reli na masuala ya viwanda iweje watu waanze kumsemea vibaya na kumwita majina yasiyofaa jambo hili halikubaliki,” alisema Mashama.
Alisema kuwa kuna njia nzuri za kumfikishia ujumbe hata kama unaona anakosea lakini siyo kumwambia maneno mabaya yasiyofaa ni vema kutumia njia nzuri.
“Hata vitabu vya dini vinatuelekeza kutii mamlaka iliyopo na mamlaka yoyote imewekwa na Mungu hivyo lazima watu wanapaswa kuheshimu mamlaka,” alisema Mshama.
Aidha alisema anatoa pole kwa Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lisu kwa kujeruhiwa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana hivi karibuni mkoani Dodoma.
“Tunampa pole Tundu Lisu kwa kujeruhiwa na tunaamini watu waliohusika na tukio hilo watakamatwa tu na wananchi ndiyo watakaojua wafanywe nini watu hao,” alisema Mshama.
Alibainisha kuwa kwa sasa nchi imeingia kwenye matukio ambayo si ya kawaida ikiwa ni pamoja na watoto kutekwa watu kujeruhiwa kwa silaha utamaduni ambao si Wawatanzania na haupswi kuungwa mkono.
“Matukio kama haya na mengine ya ukatili kama yaliyokuwa yakitokea wilaya ya Kibiti ya kuwaua watu wasio na hatia ni mambyo mabaya na serikali imedhamiria kupambana nayo kwa nguvu zote,” alisema Mshama.
Aliwataka Watanzania kuendelea kuiombea nchi imani ili iendelee kuwa Kisiwa cha amani na kuachana na watu wanaotaka kuichafua nchi ili ionekane ina matatizo.
Mwisho.
John Gagarini, Kibaha
WATUMISHI wa Umma ambao wanaotumia vyeti vya kughushi wametakiwa kujiondoa wenyewe kwani endapo watabainika watapelekwa kwenye vyombo vya sheria ikiwa ni pamoja na kurudisha fedha wanazojipatia kupitia mishahara.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Angela Kairuki wakati akizungumza na watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa, watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha na Halmashauri ya Mji Kibaha.
Kairuki alisema kuwa watumishi wa umma nchini wanaotumia vyeti vya kughushi au visivyo vyao wajiondoe wenyewe mara moja katika utumishi wa umma kwani wakiendelea kukaa itawagharimu na endapo watabainika watatakiwa kurejesha mishahara ya miezi yote waliyoiibia serikali.
“Hata kwa upande wa watumishi ambao hawajahakikiwa kwenye zoezi la uhakiki wa vyeti kwa watumishi nao wanatakiwa wajiondoe kwani wakibainika hatua kali zitachukuliwa dhidi yao na fedha wanazolipwa kupitia mshahara watazirudisha,” alisema Kairuki.
Alisema kuwa makatibu tawala wa mikoa wanapaswa kuangalia na kujiridhisha na majina ya watumishi kwenye orodha ya malipo ya mishahara ya watumishi wa umma na ya kwenye zoezi la uhakiki kama yanafanana.
“Majina yalioonekana kwenye zoezi la uhakiki ndiyo yanayopaswa kuonekana kwenye orodha ya ya malipo ya mishahara na kama kuna mtumishi hajahakikiwa anatakiwa aondolewe kwenye malipo ya mshahara,” alisema Kairuki.
Aidha alisema kuwa serikali itaendelea na zoezi kuhakikiwa watumishi hadi itakapojiridhisha kuwa hakuna watumishi ambao hawana sifa kwenye utumishi wa umma.

Mwisho.

Sunday, October 8, 2017

UJENZI WA BANDARI KAVU KWALA KIBAHA KUPUNGUMZA MSONGAMANO



Na John Gagarini, Kibaha

IMEELEZWA kuwa ukamilikaji wa Bandari Kavu ya Kwala wilayani Kibaha mkoani Pwani itasaidia kupunguza msongamao wa malori Jijini Dar es Salaam kwani makontena yote yanayoingia nchini hayatashushwa kwenye Bandari ya Dar es Salaam badala yake yatashushwa kwenye bandari mpya ya Kwala.

Kutokana na ujenzi huo wa Bandari Kavu ya Kwala mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha kupanga mipango mji kwenye Kijiji hicho cha Kwala kwani sasa inaenda kuwa Mji.

Ndikilo aliyasema hayo alipotembelea mradi huo ambao ulianza mwezi Machi mwaka huu ukiwa na thamani ya shilingi bilioni 7.2 ukijengwa na kampuni ya kizalendo ya Suma JKT chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA).

“Halmashauri mnapaswa kuhakikisha mnaweka mipango miji kwenye eneo hilo ili kusiwe na ujenzi holela pia kuwe na huduma zote kuanzia mahoteli sehemu ya magari kusubiria siyo zije kujengwa na watu binafsi, polisi, mabenki na huduma nyingine muhimu,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa Hlmashauri isisubiri hadi mradi uishe ndiyo ianze kuweka mipangomiji kwani wanatakiwa kwenda sambamba na ujenzi wa mradi ili kuwe na mpangilio mzuri.

“Hichi kitakuwa kitovu cha biashara na kutakuwa na shughuli nyingi hivyo lazima kuwe na mpangilio mzuri wa ujenzi kwani hata barabara ya kuja huku ni mbaya lazima mamlaka zinazohusika zianze kuboresha mazingira na mara kazi zitakapoanza mwakani serikali ijipatie mapato,” alisema Ndikilo.

Naye Meneja mradi Mhandisi Raymond Kweka alisema kuwa wanatarajia kukamilisha Novemba 30 mwaka huu kwa awamu ya kwanza ujenzi huo ambao unaendelea vizuri ukiwa umefikia asilimia 85 kwenye eneo la mradi lenye ukubwa wa hekta zaidi ya 150.

Kweka alisema kuwa baadhi ya changamoto kubwa ni mvua baada ya barabara ya Vigwaza Kwala kukatika na maji kujaa kwenye eneo la mradi, maji yanatoka mbali ambapo mwanzo walitegemea bwawa jirani na mradi ambao limeendelea kukauka na kukosa maji.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmshauri ya wilaya ya Kibaha Beda Mbaga alisema kuwa wanatarajia kuanza kupitia maeneo yanayozunguka mradi huo ili kuweka mipangomiji kuanzia wiki hii kwa 


Mwisho.

WAANDISHI WA HABARI NCHINI WAASWA










Na John Gagarini, Kibaha

WAANDISHI wa Habari mkoani Pwani na hapa nchini wametakiwa kutotumia vibaya kalamu zao ili kulinda amani ya nchi kwani maneno yao endapo yatatumika vibaya ni hatari zaidi ya bunduki.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama wakati akifungua kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Pwani mafunzo juu ya Haki za Binaadamu Utawala Bora na Amani nchini kwa Viongozi na watumishi wa serikali za mitaa mkoa wa Pwani yaliyoandaliwa na Alpha And Omega Reconciliation And Peace Building (AREPEB).

Mshama alisema kuwa waandishi wana nafasi kubwa ya kudumisha amani iliyopo kwa kutumia vyema kalamu zao katika kuleta mshikamano na kuepusha utengano.

“Nyie ndiyo mnanafasi kubwa ya kuifanya nchi iendelee kuwa na amani au mnaweza kuifanya nchi ikaingia kwenye machafuko hivyo mnatakiwa kutumia vizuri kalamu zenu kwa kutotumia vibaya kalamu zenu,” alisema Mshama.

Alisema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia viongozi hao kuwahamasisha wananchi kulinda amani ya nchi na kutokubali kuingia kwenye migogoro ambayo itasababisha amani kuvunjika.

“Tanzania bado tuna amani kubwa na ya kutosha hatuna sababu ya kuleta vurugu kwani nchi inatawaliwa kwa utawala wa sheria lakini kuna baadhi ya watu wanataka kutuingiza kwenye matatizo,” alisema Mshama.

Naye mkurugenzi wa  (AREPEB) Francis Luziga alisema kuwa lengo lao kubwa ni kujenga amani hapa nchini kwa kubadilishana uzoefu na viongozi na watendaji wa serikali za mitaa na wasimamizi wa watekelezaji wa sheria katika masuala ya haki za binadamu na utawala bora.

Luziga alisema kuwa pia mafunzo hayo yameambatana na uzinduzi wa mfumo wa kieletroniki wa kupokea maoni na malalamiko dhidi ya masuala mazima ya haki za binadamu.


Mwisho. 

MKUU WA WILAYA KIBAHA ATOA MAAGIZO MAZITO KWA WATENDAJI




Na John Gagarini, Kibaha

MKUU wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama amesema kuwa serikali inawafanyia tathmini watendaji wa mitaa vijiji na vitongoji na wale ambao watashindwa kufikia vigezo wataondolewa ili kupisha wale wenye weledi wafanyekazi ili kuwaletea maendeleo wananchi.

Ameyasema hayo mjini Kibaha wakati wa mkutano na viongozi hapo pamoja na wenyeviti kwenye Halmashauri za Mji na wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha na kusema baadhi ya watendaji wamekuwa hawawajibiki ipasavyo.

Nao baadhi ya wenyeviti walielezea changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili kwenye maeneo yao.

Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Marco Njau alikiri kuwepo kwa baadhi ya changamoto.

Naye kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Beda Mbaga amesema kuwa watakabili changamoto zilizo kwenye eneo lao ili kuleta maenedeleo kwa wananchi.

Naye Ernest Shalua ambaye ni mwakilishi wa Kamanda wa Polisi wilaya ya Kibaha amesema kuwa ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa watuhumiwa lazima viongozi na wananchi watoe tushahidi kwenye matukio mbalimbali.

mwisho.