Sunday, August 13, 2017

PAKISTANI KUENDELEA KUSAIDIA MIRADI YA MAENDELEO NCHINI





















































Na John Gagarini, Chalinze

NCHI ya Pakistani imesema kuwa itaendelea kusaidia miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano wa nchi hiyo na Tanzania.

Hayo yalisemwa na Balozi wa Pakistani hapa nchini Amir Khan wakati wa sherehe za kupokea majengo ya madarasa ya Shule ya Msingi Pakistani Mtete yaliyokarabatiwa na marafiki wa Pakistani.

Khan alisema kuwa nchi yake imekuwa na miradi mbalimbali ya kimaendeleo hapa Tanzania na hiyo inatokana na urafiki uliopo baina ya nchi hizo.

“Tumekuwa na miradi mingi hapa Tanzania na tutaendelea kushirikiana kama walivyofanya wenzetu na kujitolea kukarabati shule hii,” alisema Khan.

Alisema kuwa miradi kama huo uliofanyika kwenye shule hiyo ni fedha ambazo walitoa marafiki wa Pakistani kwa ajili ya kuhakikisha sekta ya elimu inaboreka.

“Suala la elimu ni muhimu kwa watoto ambao baadaye tunatarajia watakuwa wataalamu wazuri hivyo lazima kuwawekea mazingira mazuri ya kusomea,” alisema Khan.

Aidha aliwataka wananchi kuwa walinzi wa miundombinu ya shule hiyo ili ukarabati uliofanyika uwe na maana hata mazingira yanaendelea kuwa mazuri.

“Kuhusu uzio kwenye shule hiyo alisema kuwa atapeleka ombi hilo kwa marafiki wa Pakistani ili walifanyie kazi kama ilivyoombwa na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete,” alisema Khan.

Naye Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete aliwapongeza Marafiki hao wa Pakistani kwa kuisaidia shule hiyo na kusema kuwa watahakikisha wanenzi ukarabati huo kwa kuitunza miundombinu ya shule.

Ridhiwani alisema kuwa jambo watakalolifanya ni kuhakikisha eneo hilo linapimwa na kuwekewa mipaka ili kukabiliana na wavamizi.

“Tutahakikisha linapimwa na kuwekewa mipaka yake kwani baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo yakiwemo yale ya taasisi,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa pia watahakikisha miundombinu mingine inatengenezwa ili kuifanya shule hiyo kuwa na mazingira mazuri ya utoaji elimu.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment