Tuesday, August 30, 2016

BOMOABOMOA YALETA KIZAZAA MAILI MOJA KIBAHA


Na John Gagarini, Kibaha

WANANCHI wa eneo la Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wamelia na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani kuwa wawafikirie kwa kuwalipa fidia wakati wa zoezi la bomobomoa ambalo linatarajiwa kufanyika Novemba 23 mwaka huu.

Hataua hiyo imekuja baada ya TANROADS kutoa barua kwa watu waliojenga kwenye eneo la hifadhi ya barabara inayomilikiwa na wakala hiyo kwa wale waliojenga umbali wa mita 120 kwa kila upande wa barabara kuu ya Dar es Salaam Morogoro kuanzia Kiluvya hadi Tamco waanze kubomoa kabla ya zoezi hilo kwa kuwapa siku 90 kufanya hivyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwenyekiti wa chama cha ACT-Wazalendo mkoa wa Pwani Mrisho Swagala alisema kuwa mbali ya kuwtowlaipa fidia pia eneo linalopitiwa na zoezi hilo ni kubwa sana ikilinganishwa na maeneo mengine.

“Hatukati zoezi hilo kufanyika lakini wangeangalia namna ya kuwafidia wananchi kwani kuwabomolae bila ya kuwapa fidi itakuwa ni kitendo cha ukatili na kinakwenda kinyume cha haki za binaadamu kwani bomoa hiyo itawaacha watu wengi wakiwa hawana mahali pa kuishi na kwa wafanyabiashara hawatakuwa na sehemu ya kufanyia biashara,” alisema Swagala.

Alisema kuwa alisema kuwa sheria ya barabara iliyotungwa mwaka 1932 ambapo inadaiwa kuwa watu walilipwa fidia jambo ambalo kwa kipindi hicho fedha ilikuwa ni ndogo ukilinganisha hali halisi ya sasa hivyo kuna haja ya kuwafikiria.

Naye Ally Gonzi mwenyekiti wa ushirika wa wafanyabiashara wa soko la mkoa la Maili Moja alisema kuwa wao kama wafanyabiashara wansikitishwa na hatua hiyo kwani hadi sasa hawajui watakwenda kufanyia biashara wapi.

Gonzi alisema kuwa waliahidiwa kuwa watajengewa soko la kisasa lakini hadi sasa soko halijajengwa ambapo wao wako hapo kwa zaidi ya miaka 35 na Halmashauri ambao wao wako chini yao.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Mtaa wa Maili Moja Athuma Mkongota alisema kuwa wananchi wengi wamekwenda ofisini kwake kwenda kulalamika juu ya zoezi hilo ambalo litawakumba watu wengi ambao wako katikati ya mji huo.

Mkongota alisema kuwa ubomoaji huo umekuja baada ya kuisha kwa kesi iliyofunguliwa na wananchi kupinga hatua hiyo lakini walishindwa hata hivyo alisema kuwa hukumu ya kesi hiyo bado hajaipata.

Awali mkaguzi wa barabara wa mamlaka hiyo Livingston Urio alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na zoezi la kutoa barua ambapo idadi kamili ya nyumba na vibanda vya biashara vitakavyobomolewa itajulikana.

Urio alisema kuwa ilikuwa ifanyike mwezi Agosti lakini waliongeza hadi Novemba lakini miaka ya nyuma tayari walishawawekea alama ya X mwaka 2004 lakini zoezi hilo halikufanyika lakini kwa sasa zoezi hilo linafanyika.

Alisema kuwa wananchi walipoenda mahakamani walishinda na kuonekana kuwa eneo hilo ni mali ya mamlaka hiyo na kuwa eneo hilo magari yanakwenda taratibu hivyo barabara kuharibika na baada ya bomoa hiyo eneo hilo litawekwa stendi kubwa na patapangwa vizuri ili mji uonekane vizuri.

“Kulingana na sheria ya barabara ya mwaka 1932 na kufanyiwa marekebisho 1958 kifunga na 52 na marekebisho ya sheria ya barabara na 13 ya mwaka 2007 sambamba na taratibu za sheria za usimamizi wa barabara kifungu na 30 (b) eneo la hifadhi ya barabara sehemu iliyotajwa hapo juu ni mita 120 sawa na futi 400 kwenda kila upande kutoka katikati ya barabara ni marufuku kufanya maendelezo yoyote katika eneo hilo,” alisema Urio.


Mwisho.  

MBUNGE AITAKA DAWASCO KUUNGANISHA MAJI BILA YA UPENDELEO WA FEDHA


Na John Gagarini, Kibaha

MAMLAKA ya Maji Safi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imetakiwa kuwaunganishia maji wananchi wa Mlandizi bila ya kujali uwezo wa mtu ili kila mtu aweze kunufaika na mradi wa maji kwenye Kitongoji cha Janga.
Hayo yalisemwa na mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijni Hamoud Jumaa wakati alipofanya ziara kutembelea mradi wa maji wa ya mkopo kwenye kitongoji cha Janga kata ya Janga wilayanai Kibaha.

Mbunge huyo alitoa wito huo kufuatia mwenyekiti wa kitongoji hicho Josephine Maendaenda kudai kuwa baadhi ya wananchi wanalalamika kuwa watu wanaotoa fedha taslimu ndiyo wanaounganishiwa maji huku wale wanaokopa kutakiwa kusubiri.

“Kwanza nawapongeza wananchi kwa kuchimba mitaro ya kulaza mabomba hivyo thamani ya nguvu zao lazima zithaminiwe sawa na wale wanaotoa fedha taslimu kwani mitaro hiyo isingechimbwa na wananchi hao maji yasingeweza kufika kwenye maeneo ya watu,” alisema Jumaa.

Alisema kuwa thamani ya watu iko palepale lakini haiwezi kwani wanaotoa fedha na wale waliotumia nguvu zao kuchimba mitaro wamefanya kazi kubwa ambayo inapaswa kuungwa mkono na siyo ya kubezwa.

“Wananchi hawa wameonyesha uzalendo wa hali ya juu kwa kufanyakazi ya kujitolea na ndiyo tunataka utamaduni huu ufanyike kwenye kila jambo na si kusubiri serikali iwafanyie wananchi kila kitu kwani hata kwenye mikoa iliyoendelea kama Moshi na Arusha imefanikiwa kwa wananchi kujitolea kama huku,” alisema Jumaa.

Kwa upande wake meneja wa Dawasco wilaya ya Kibaha Erasto Emanuel alisema kuwa suala hilo watalifanyia kazi kwa kuwaunganishia wananchi bila ya kujali kama ni malipo ya moja kwa moja au mkopo.

Emanuel alisema kuwa hadi sasa wameweza kuwaunganishaia maji wananchi 40 huku wakitarajia kuwafikia wateja 300 katika hatua ya pili huku wakitarajia maji kuanza kutoka mwezi Oktoba na kuwafikia wateja 600.

Alisema kuwa mradi huo ulikumbwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vifaa jambo ambalo lililalamikiwa na wananchi lakini yote hiyo ilitokana na kila mwaka kuwa na zoezi la kufunga mwaka ambalo huambatana na uhakiki wa vifaa.

Naye mwenyekiti wa Kitongoji cha Janga Josephine Maendaenda alisema kuwa changamoto ya maji ni kubwa kwenye kitongoji hicho na wananchi wamekuwa wakilalamika kiu yao kubwa ikiwa ni kupata maji ambapo wamekuwa wakienda mwendo mrefu kufuata maji ambapo huuziwa dumu la lita 20 kwa shilingi 500.

Mwisho. 

KAMPUNI YA UUNGANISHAJI MAGARI YAZIMAMOTO MBIONI KUANZA USZALISHAJI

Na John Gagarini, Kibaha

KAMPUNI ya Equator Suma Jkt inatarajia kuanza kuunganisha magari ya zimamoto na matrekata mwishoni mwa mwaka huu ikiwa ni moja ya njia ya kukabiliana na majanga ya moto pamoja na kuinua kilimo cha Tanzania ambacho ni uti wa mgongo wa uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari ambao walitembelea kiwanda hicho kilichopo Ruvu Mlandizi wilayani Kibaha mkurugenzi Robert Mangazeni alisema kuwa kwa sasa kiwanda hicho kiko kwenye hatua za mwishi ikiwa ni pamoja na uunganishaji wa mitambo na mashine.

Mangazeni alisema kuwa teknolojia ya uunganishaji wa magari ya zimamoto ambapo watatumia magari ya kawaida kwa kuyabadilisha na kuwa ya zimamoto wameitoa nchi ya Urusi kutoka kwenye makampuni ya St Auto na Ural huku ile ya matekta wakiitoa kwenye kampuni za Escort kutoka nchini India na Farmtrac kutoka nchini Poland.

“Tukizungumzia kuhusu uunganishaji wa magari ya zimamoto ni teknolojia ambayo imeboreshwa na kuwa ya kisasa zaidi ambapo tutakuwa na uwezo wa kuunganisha magari ya aina mbalimbali kutegemeana na mteja anavyotaka ambayo yatakuwa na ujazo wa aina tofauti tofauti kuanzia magari makubwa hadi madogo siyo lazima yawe makubwa kama tulivyozoea hivyo hata majanga haya ambayo yamezikumba shule sasa taasisi zitaweza kudhibiti moto,” alisema Mangazeni.

Alisema kuwa ujazo huo utaanzia lita za maji 300 hadi 10,000 kutegemea na ukubwa hivyo kulinagana na miuondombinu ya barabara za mitaani wataunganisha hata magari madogo ili yaweze kufika kwenye eneo lililopata maafa ya moto.

“Ikumbukwe Tanzania itakuwa nchi ya pili kuwa na teknolojia hii ya uunganishaji wa magari ya zimamoto baada ya Afrika Kusini ambapo kwa nchi za Maziwa Makuu itakuwa ni ya kwanza na itaweza kuokoa asilimia 30 ya gharama ya kununua gari jipya la zimamoto pia watakuwa na uwezo wa kuyatengeneza magari hayo badala ya kuagiza wataalamu toka nje ya nchi mara yanapoharibika,”alisema Mangazeni.

Aidha alisema kuwa kwa upande wa matrekta wataweza kuyaunganisha ambapo kwa miaka ijayo watakuwa na uwezo wa kutengeneza trekta ambalo litakuwa ni zao la Tanzania tofauti na ilivyo sasa kuagizwa toka nje ya nchi.

“Miaka ijayo tutatengenza trekta la kwetu ambapo kwa sasa vitakuwa vinakuja vifaa vyake na kuunganishiwa hapa na tatizo la matrekta kufa haraka litakwisha kwani mafundi wa matrekta watazalishwa hapa na yatadumu kwani wengi hawana utaalamu wautengenzaji bali wanatumia uzoefu tu,” alisema Mangazeni.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho umekuja wakati mwafaka kwa upande wa janga la moto na kilimo bora.

Mshama alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitafanya shghuli hizo kwa pamoja itakuwa mwarobaini wa changamoto hizo ambazo ni kubwa na pia ni kutekeleza sera ya Rais John Magufuli ya kutaka Tanzania kuwa nchi ya viwanda ili baada ya miaka ijayo nchi kuwa na uchumi wa kati.

Ujenzi wa kiwanda hicho ulianza ulianza 2011 ambacho hadi kukamilika kwake kitakuwa na thamani ya shilingi bilioni tatu kitaajiri wafanyakazi 100 na kamapuni hiyo imeingia ubia na Suma Jkt na inaundwa na wanajeshi wastaafu.
 

Mwisho. 

WAILILIA HALMASHAURI KUWAJENGEA SOKO BAADA YA SOKO KUTAKIWA KUVUNJWA

Na John Gagarini, Kibaha
USHIRIKA wa Wafanyabiashara wa Soko la mkoa la Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwapatia eneo lingine la kufanyia biashara baada ya eneo wanalofanyia shughuli zao ambalo liko chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa kuvunjwa baada ya miezi mitatu kuanzia mwezi Agosti.

Akizungumza mara baada ya mkutano mkuu wa wanachama uliofanyika mjini Kibaha mwenyekiti wa ushirika huo Ally Gonzi alisema kuwa hadi sasa hawajui hatma yao mara zoezi hilo litakapofanyika.

Gonzi tunaiomba Halmashauri kutujengea soko au kama hawataweza kujenga ndani ya muda huo wa miezi mitatu ni vema wakaiomba wakala hao kutuongezea muda wa kuwa hapa hadi pale tutakapokuwa tumejengewa soko jipya.

“Tunamwomba Rais John Magufuli kutuangalia kwani hapa tuko zaidi ya miaka 30 na hadi sasa Halmashauri bado haijatujengea soko ambalo waliahidi kutujengea kutokana na eneo hilo kutokuwa la halmashauri,” alisema Gonzi.

Alisema kuwa kwa kipindi kirefu Halmashauri hiyo imekuwa ikiahidi kuwajengea soko la kisasa kwenye kitovu cha mji lakini hadi wanapewa barua za kutakiwa kuondoka kwenye eneo hilo na Tanroads hadi sasa hawajajengewa soko.

“Tunachoona kwa sasa kwa kuwa soko bado halijajengwa ni vema wakatuongezea muda hata wa miaka miwili kwani Halmashauri ilisema itakuwa imejenga soko ndani ya miezi 18 hivyo kwa kipindi hicho ni bora tungebaki hapa kwanza lakini vinginevyo hatujui tutakwenda wapi,” alisema Gonzi.

Aidha alisema kuwa mbali ya wao kutokuwa na mahali pa kufanyia biashara pia Halmashauri itakosa mapato kwnai soko hilo ni moja ya vyanzo vikuu vya mapato pia wao walikuwa wakitegemea hapo kwa ajili ya kujipoatia kipato chao na familia zao.


Mwisho. 

UVUNJAJI SHERIA WASABABISHA MIGOGORO YA ARDHI

Na John Gagarini, Rufiji

IMEELEZWA kuwa kuwepo kwa migogoro ya ya wakulima na wafugaji  katika Halmashauri ya Rufiji mkoani Pwani kunatokana na  baadhi ya wafugaji kuvunja sheria na taratibu zilizowekwa na   kwenda kulisha mifugo yao katika maeneo yaliyotengwa maalumu kwa ajili ya shughuli mbali mbali za kilimo.

Hayo yalisemwa na Mbunge  wa Jimbo la Rufiji Mkoani humo Mohamed Mchengerwa alipokuwa akizungumza na viongozi wa Halmashauri Mpya ya Rufiji ambapo ameahidi kulivalia njuga suala la migogoro ya ardhi inayotokana na jamii ya wafugaji na wakulima ambao wamekuwa wakigombania maeneo ya mashamba na kusababisha kutokea kwa mapigano ambayo wakati mwingine yanapelekea uvunjifu wa amani.

Mchengerwa alisema kuwa hawezi kuwavumilia wale wote ambao wataonekana wanakwenda kinyume cha sheria za nchi, na kuhakikisha kila mfugaji na mkulima anatengewa maeneo yao rasmi kwa ajili ya kufanyia shughuli zake ili kuepukana na migogoro na  mapigano ambayo yamekuwa yakijitokeza kutokana na kugombania ardhi.

“Nitaweka mikakati kabambe ambayo itaweza kuwawasaidia wananchi wakiwemo wafugaji na wakulima kwa kushirikina na viongozi wa halmashauri katika kuwatenge maeneo yao maalumu ambayo yataweza kusaidia kuepukana na migogoro hiyo ya ardhi,” alisema Mchengerwa.

Alisema kuwa anatambua kuwepo kwa changamoto kubwa na  migogoro kati ya wakulima na wafugaji, lakini dhamira yake kubwa anataka kuona wanachi wake wa jimbo la rufiji wanakaa kwa amani bila ya kuwepo kwa mapigano yoyote na kuhakikisha kwamba sula la amani na utulivu linakuwepo.

“Natambua wananchi wengi wa Jimbo la Rufiji wanategemea sana shughuli za kilimo hivyo kwa sasa wameshaweka utaratibu wa kutenga maeneo ya wafugaji ili wasiweze kuingia katika mashamba ya wakulima na kupelekea vurugu za mara kwa mara kitu amabcho sio kizuri na kinarudisha nyuma maendeleo,” alisema Mchengerwa.

Naye Mwenyekiti mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji Saidina Malenda mara baada ya kushinda katika uchaguzi huo  alisema  atahakikisha anasharikina bega kwa bega na viongozi wenzake kwa lengo la kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kwa wananchi wa Rufiji.

Malenda alisema kuwa anawashukuru madiwani wenzake kwa kuweza kumchagua kuwaongoza na kubainisha kwamba atafanya kazi bidii zote na kwa kushirikina katika mambo mbali mbali ya kimaendeleo  bila ya kuwa na ubaguzi wa aina yoyote wa itikadi ya vyama  ili kuweza  kuwatumikia wananchi katika huduma mbali mbali wanazozihitaji.

Katika uchaguzi huo wa halmashauri mpya ya Wilaya ya Rufiji,uliofanyika utete nafasi ya Mwenyekiti ilikwenda kwa Saidani Malenda ambaye alipata kura 11 kati ya kura 19 zilizopigwa, ambapo nafasi ya Makamu mwenyekiti ilikwenda kwa Hawa Mtopa  ambaye aliyepata kura 10 katika ya kura 19 zilizopigwa.
     

MWISHO

PANGANI WALILIA ZAHANATI


Na John Gagarini, Kibaha

KATA ya Pangani wilayani Kibaha inatarajia kubadilisha ofisi za Mtaa wa Kidimu kuwa Zahanati ili kukabiliana na changamoto ya mtaa huo kutokuwa na zahanati hivyo kufanya huduma za matibabu kupatikana kwa ugumu.

Akizungumza na waandishi wa habari diwani wa kata hiyo Agustino Mdachi alisema kuwa gharama za kufuata matibabu kwa wakazi wa mtaa huo ni kubwa na kuwafanya wagonjwa kuwahatarini pale wanapokuwa wamepatwa au kuzidiwa na ugonjwa.

Mdachi alisema kuwa tegemeo kubwa ni hospitali ya wilaya ya Kibaha ya Mkoani ambayo iko umbali wa kilometa 18 na ile ya jirani ya Mpiji Magohe ambayo iko kata ya Mbezi wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam ambapo usafiri wa pikipiki ni shilingi 5,000.

“Mgonjwa anapotaka kwenda Mkoani humbidi kuwa na shilingi 50,000 hasa nyakati za usiku na mchana ni 40,000 au 30,000 gharama hizi kwa ajili ya kwenda kupata matibabu ni kubwa sana na kwa mwananchi wa kawaida kumudu ni ngumu sana,” alisema Mdachi.

Alisema kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo wameamua kuibadili ofisi hiyo na kuwa zahanati ya mtaa ambapo wananchi watapa huduma karibu.

“Kwa sasa tuko kwenye mchakato kwa kuwaomba Halmashauri ya Mji kuturuhusu na kuleta wataalamu wa afya ili waangalie namna ya kulifanya jengo hilo kuwa zahanati na tunaamini ombi letu litakubaliwa,” alisema Mdachi.

Aidha alisema kuwa kutokana na ukubwa wa jengo hilo la serikali ya mtaa kuwa vyumba vingi wanaamini kuwa litafaa kwa ajili ya kuanzia huduma za kiafya wakati wanafanya mipango ya kujenga sehemu nyingine.

“Kwa kuwa ya kata ina ofisi nyingi tunaweza kutoa chuma kimoja kwa ajili ya ofisi ya mtaa ili kufanikisha zoezi hilo ambalo litawafanya wananchi wa mtaa na kata hiyo kupata huduma za afya karibu,” alisema Mdachi.

Aliwataka wananchi kuunga mkono jitihada za serikali kwa kujitolea katika masuala mbalimbali ya maenedeleo ikiwa ni pamoja na kufanikisha zoezi hilo la ujenzi wa zahanati hiyo.


Mwisho.

MADARASA YAUNGUA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

MADARASA matatu na ofisi ya Mwalimu Mkuu shule ya Msingi Kongowe wilayani Kibaha mkoani Pwani zimeungua na moto ambao ulitokea juzi usiku na kusababisha hasara kubwa.

Akizungumza na Patapata mwenyekiti wa mtaa wa Kongowe Maimuna Jamhuri alisema kuwa moto huo ulitokea Agosti 28 majira ya saa nne usiku ambapo chanzo chake bado hakijafahamika mara moja.

Jamhuri alisema kuwa moto huo ulianzia kwenye ofisi hiyo ambayo ni ya mwalimu mkuu na kuenea kwenye madarasa pamoja na chumba cha kuhifadhia vitabu ambavyo navyo vimeteketea kwa moto huo ambao ulikuwa mkali.

“Moto huo ulizimwa na wananchi ambao walijitokeza kwa wingi ambapo gari la zimamoto lilifika kwa kuchelewa kutokana na kuwa kwenye harakati za kuzima moto sehemu nyingine”, alisema Jamhuri.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Kongowe Iddi Kanyalu alisema kuwa baada ya kutokea moto huo viongozi kadhaa walifika akiwemo mkurugenzi, Mwenyekiti na Injinia wa Halmashauri kwa ajili ya kuangalia athari za moto huo.

Kanyalu alisema kuwa kutokana na makisio ya harakaharaka zinahitajika zaidi ya milioni 50 kwa ajili ya kujenga upya madarasa hayo na ofisi kwani madarasa hayo yameharibika sana na hayafai kwa matumizi wala kufanyiwa ukarabati.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo leo kamati ya maenedeleo ya kata ina kaa kuangalia namna ya kukabiliana na tatizo hilo ambalo limewakumba wanafunzi 200 waliokuwa wanatumia madarasa hayo.

Naye mtendaji wa kata hiyo ya Kongowe Said Kayangu alisema kuwa mwalimu mkuu wa shule hiyo Beatus Lingumbuka alitapa athari kidogo kichwani na mikononi kwani alikuwa kwenye harakati za kujaribu kuokoa baadhi ya vitu wenye ofisi yake.

Kayangu alisema kuwa kutokana na jitihada za wananchi wameweza kuokoa madawati kwenye madarasa hayo ambayo yalikuwa hatarini kuungua lakini hata hivyo waliweza kuyatoa na hakuna dawati hata moja lililoungua

Mwisho.


WAAMUZI KIBAHA WAPATA VIONGOZI WAPYA

Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA cha Waamuzi wa Soka Tanzania (FRAT) mkoa wa Pwani kimemchagua  Jeremia Komba kuwa mwenyekiti wa chama hicho kwa kupata kura 15 huku mpinzani wake Kassim Safisha akipata kura tano.

Uchaguzi huo ambao ulifanyika mjini Kibaha na kusimamiwa na mwamuzi mkongwe Hussein Magoti na kuwashiriki waamuzi ambao ni wanachama wa chama hicho cha waamuzi.

Komba alikuwa akichuana na mwamuzi mwenzake Kassim Safisha nakumshinda kwa tofauti ya kura tano hivyo kumfanya Komba kuwa bosi wa waamuzi wilaya ya Kibaha.

Nafasi ya makamu mwenyekiti ilikwenda kwa Sayenda Lubisa ambaye hata hivyo hakuwa na mpinzani na kujipatia kura 17 huku tatu zikiharibika.

Upande wa katibu mkuu Endrew Kayuni alikuwa mshindi kwa kupata kura 15 huku Mohamed Juaji akipata kura tano, nafasi ya katibu msaidizi ilikwenda kwa Hamis Mpangwa ambaye alijinyakulia kura 11 akimshinda Mohamed Msengi aliyepata kura tisa.

Nafasi ya mweka hazina ilikwenda kwa Kassim Naroho aliyepata kura 16 akimshinda Nickson Haule aliyepata kura nne, kwa upande wa mwakilishi wa mkutano mkuu ilikuwa na mgombea mmoja Hamad Seif ambaye alipata kura 19..

Kwa upande wa kamati ya utendaji nafasi tatu walioshinda ni Kasule Ambogo kura 18, Leah Petro kura 16, Gabriel Kinyogoli kura 15 na Sultan Singa kura nane ambapo mwenyekiti mpya Komba aliwataka waamuzi kuwa na mshikamano.

Komba alisema kuwa jambo kubwa ili waweze kufikia malengo ni kuwa nidhamu na kuzingatia sheria kwa kuzitafsiri wawapo uwanjani ili kuondoa malalamiko dhidi yao kwani baadhi wamekuwa wakienda kinyume na sheria za mchezo huo.


Mwisho.



 

ATISHIA KUWABAKA WANAFUNZI


Na John Gagarini, Chalinze

MWENYEKITI wa Halmashauri ya mji wa Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Said Zikatimu ameutaka uongozi wa Kitongoji Cha Msanga kata ya Talawanda uhakikisha inamkamata mtu ambaye anatishia kuwabaka wanafunzi wa shule ya Msingi Msanga.

Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Talawanda wakati wa ziara yake kuangalia shughuli za maendeleo kwenye kata ya Talawanda alisema kuwa mtu huyo hapaswi kuachwa kwani anahatarisha afya za wanafunzi hao.

Zikatimu alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wakike wa shule hiyo tayari wameshatoa taarifa dhidi ya mtu huyo ambaye huwa anawakimbiza kwa nia ya kuwafanyia kitendo hicho na endapo hatakamatwa anaweza kutekeleza azma yake hiyo mbaya.

“Mtu huyo inasemekena yuko Kijijini hapa amekuwa akificha sura yake ili asifahamike amekuwa akijificha kwenye vichaka na kuwakimbiza wanafunzi kwa nia ya kutaka kuwabaka hivyo lazima viongozi muweke mtego ili mumkamate mtu huyo ambaye ni hatari,” alisema Zikatimu.

Alisema kuwa serikali haiwezi kukaa kimya kwa mtu wa namna hiyo ambaye ni hatari kwa wanafunzi na kuwafanya watoto wa kike wasisome kwa amani hivyo lazima hatua za haraka zichukuliwe ili kumdhibiti mapema.

“Lazima mfanye mpango wa kumkamata mtu huyo pia mnaweza kupiga kura ili kumbainisha mtu huyo ambaye baadhi ya watu wanamfahamu na wengine hawamfahamu ambapo kwa kutumia kura anaweza kufahamika kwa urahisi,” alisema Zikatimu.

Aidha alisema kuwa kamati za ulinzi na usalama ya Kijiji na Kitongoji zinapaswa kulishughulikia suala hilo na wananchi kutolifumbia macho kwani mtu huyo anaweza kufanya kweli endapo hatua hazitachukuliwa mapema.

Mwisho.

Thursday, August 11, 2016

MZEE WA BARAZA LA MAHAKAMA APANDISHWA KIZIMBANI KWA RUSHWA

Na John Gagarini, Kibaha

TAASISI ya Kuzuia na Kupamaba na Rushwa (TAKUKURU) Mkoani Pwani imemfikisha mahakamani Mzee wa Baraza la Mahakama ya Mwanzo Maili Moja Kibaha Francis Ndawanje kwa tuhuma za kuomba na kupokea Rushwa ya shilingi 100,000 ili kumsaidia mtuhumiwa kushinda kesi yake.

Mtuhumiwa alisomewa mashitaka kwenye mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha  mbele ya hakimu mkazi wa mahakama ya mkoa wa Pwani  Herieth Mwailolo ambapo kwa upande wa chini ya mwendesha mashitaka kutoka TAKUKURU Mkoa Pwani Sabina Weston.

Akisoma maelezo juu shitaka hilo Weston aliiambia Mahakama kuwa mtuhumiwa huyo anatuhumiwa kutenda makosa hayo mawili kati ya tarehe 3 na 4  Agosti mwaka huu ambapo.

Mahakama iliambiwa kuwa mtuhimwa aliomba rushwa Agosti 3 kwa Omary Hoza ili amsaidie mkewe Mariamu Hoza ambaye ana kesi namba 324 kwenye mahakama hiyo hivyo kumuomba rushwa ya shilingi 100,000.

Ikaelezwa kuwa mtuhumiwa alipokea rushwa siku iliyofuata Agosti 4 alipokea fedha hizo eneo la jirani na Kituo cha Polisi Tumbi jirani na barabara kuu ya Morogoro Maili Moja wilayani Kibaha.

Baada ya kusomwa mashtaka hayo mtuhumiwa alikana tuhuma hizo ambapo upande wa Taasisi hiyo ulisema kuwa hauna pingamizi na dhamana kwa mtuhumiwa ili mradi akamilishe masharti ya dhamana na yuko nje kwa dhamana ya shilingi 500,000 kwa wadhamini wawili kila mmoja.

Hakimu alisema kuwa wadhamini wanapaswa kuhakikisha mtuhumiwa anafika siku ya kesi hiyo ambayo imepangwa kufanyika Agosti 15 mwaka huu.

Mwisho.


MAJAMBAZI YAMUUA KWA KUMPIGA RISASI MWANAMKE ALIKWENDA DUKANI KUWEKA MUDA WA HEWANII

Na John Gagarini, Kibaha

MKAZI wa Mtaa wa Karabaka-Misugusugu kata ya Misugusugu wilayani Kibaha mkoani Pwani Zawadi Halfan (25) ameuwawa kwa kupigwa risasi na majambazi wakati akisubiri kuunganishiwa kifurushi cha muda wa maongezi kwenye simu yake.

 Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha kamanda wa Polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa marehemu alikuwa amekaa kwenye benchi kwenye kibanda cha huduma za fedha kwa mtandao mali ya Gaitano Joseph (30).

Mushongi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 9 majira ya saa 2:30 usiku kwenye mtaa huo ambapo marehemu alikuwa akisubiri huduma hiyo kabla ya mauti kumkuta.

“Marehemu hakuwa mlengwa bali walikuwa wamemlenga Yohana Koseja (24) ambaye ni mfanyakazi wa Mchungaji Raphael John ambaye ni mmiliki wa duka la M-Pesa ambapo majambazi hao baada ya kufika walimwamuru Yohana asimame baada ya kufunga duka hilo lakini alikimbia na kukaidi agizo la majambazi hayo ambayo yalikuwa matatu,” alisema Mushongi.

“Kutokana na Yohana kukimbia majambazi hayo yalianza kufyatua risasi ndipo moja ilimpata marehemu sehemu ya mgongoni upande wa mgongoni na kufariki papo hapo ambapo  walikuwa wakifyatua risasi hizo kwa Yohana wakimhisi kuwa alikimbia na fedha bada ya kufunga duka,” alisema Mushongi.

Alisema baada ya majambazi hao kutoka kwenye tukio la kwanza walivamia duka lingine la M-Pesa lililopo pamoja na duka la madawa ya binadamu linalomilikiwa na Renovatus Katabalo (29) mfanyabiashara na mkazi wa Kongowe ambapo duka lake lipo eneo hilohilo la Karabaka na kupora kiasi cha shilingi 300,000.

“Chanzo cha tukio hilo ni kuwania mali na msako unaendelea mkoa mzima ili kuwakamata watuhumiwa ili wafikishwe kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili za mauaji ambapo eneo la tukio maganda ya risasi aina ya SMG/SAR,” alisema Mushongi.  

Mwisho.


Monday, August 8, 2016

MWILI WAKUTWA VICHAKANI UKIWA UMEPIGWA RISASI KIDEVUNI


Na John Gagarini, Kibaha

MWILI wa mtu mmoja ambaye jina lake ambalo halikuweza kufahamika mara moja mwenye umri kati ya miaka (33) na (38) umeokotwa huku ukiwa umepigwa risasi chini ya kidevu na kutokea utosini.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwenyekiti wa mtaa wa Lulanzi kata ya Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani Thobias Shilole alisema kuwa marehemu aliuwawa na watu wasiofahamika.

Shilole alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 7 majira ya saa 3 asubuhi kwenye korongo lililopo kwenye shamba linalomilikiwa na Saeed Yeslam Saeed ambapo watoto waliokuwa wakichunga mbuzi ndiyo waliogundua mwili huo na kutoa taarifa kwa wazazi wao ambao walitoa taarifa kwa balozi wao na ndiye aliyemjulisha juu ya tukio hilo.

“Mwili huo ulikuwa na jeraha la risasi chini ya kidevu na kufumua kichwa na mtu huyo anahusishwa na tukio lililofanyika siku kama tatu zilizopita kwa kumpiga risasi kwenye makalio na kumpora fedha mtu aliyetambulika kwa jina la Beno Nyoni (36) mkazi wa Picha ya Ndege ambaye alikuwa akijenga nyumba yake eneo la mtaa wa Lulanzi,” alisema Shilole.

Shilole alisema kuwa watu hao wanaosadikiwa kuwa ni majambazi baada ya kumshambulia walikimbia na kusababisha majeruhi huyo kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani Tumbi lakini ilishindikana na kupelekwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi ambako hadi sasa anatibiwa baada ya kutolewa risasi iliyokuwa mwilini.

“Tunaiomba serikali kumlazimisha mmiliki kulifanyia usafi kwani pori kubwa ambalo limekuwa likitumiwa na wahalifu kwa ajili ya kujificha na kufanya wizi kisha kujificha huko kwani hata mwaka jana tulikuta mtu akiwa amejinyonga hivyo sehemu hiyo usalama wake ni mdogo hasa ikizingatiwa eneo hilo liko umbali wa kilometa 2 toka barabara kuu ya Morogoro,” alisema Shilole.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa baada ya kuangaliwa marehemu alikutwa na jeraha kidevuni na kichwani huku mwili wake ukianza kuharibika.

Msuhongi alisema kuwa pembeni yake kulikutwa kofia ya kuficha sura ganda la risasi aina ya SMG/SAR na nyaraka mbalimbali ambazo ni ramani za nyumba mbili, stakabadhi za kibali cha ujenzi, hati ya hukumu ya shauri la mgogoro wa ardhi.

Alisema vitu vingine vilivyokutwa ni kadi za biashara, kadi za benki za posta, NBC, Posta na CRDB, kadi ya kupigia kura na leseni ya udereva vyote vikiwa na majina ya Nyoni ambaye ni mfanyabiashara wa Picha ya Ndege.

“Vitu hivyo ni vya Majeruhi huyo aliyofanyiwa tukio hilo la unyanganyi wa kutumia silaha na kupora mali na walifika kwenye kwenye hilo kwa lengo la kugawana mali hizo lakini inaonyesha walihitilafiana ndipo walipompiga marehemu risasi na kumuua kisha walimpekekua kwani mifuko ya suruale yake ilkuwa iko nje na hakukutwa na kitambulisho chochote na mwili umehifadhiwa hospitali ya Tumbi,” alisema Mushongi.

Naye diwani wa kata hiyo Robert Machumbe alisema kuwa shamba hilo lilikofanyika tukio hilo lina pori kubwa sana hivyo ni vema Halmashauri likafanya utaratibu kama mmiliki kashindwa litolewe kwa mtaa ili kuweza kujengwa huduma za jamii kama shule, zahanati na huduma nyingine kwani kwa sasa limekuwa hatari kwa wananchi.

Mwisho.       


  



  




WATU ZAIDI 20 WANUSURIKA KUUNGUA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

FAMILIA nane zenye watu zaidi ya 20 kwenye mtaa wa Mharakani kata ya Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani zimenusurika kufa baada ya moto kutokea wakati wamelala.

Wakizungumza na mwandishi habari hizi wahanga wa tukio hilo la moto huo ambao ulitokea Agosti 7 usiku kuamkia Agosti 8 majira ya saa 6;30 usiku walisema kuwa watu waliokuwa jirani na nyumba yao ndiyo waliowafahamisha juu ya moto huo ambao unasadikiwa ulianzia kwenye moja ya maduka yaliyo kwenye nyumba hiyo.

Emanuel Mhina alisema kuwa wao walikuwa wamelala na ilipofika majira ya saa saba kasoro waliamshwa na watu na walipoamka walikutana na moto mkubwa ambao hawakujua ulianza saa ngapi ndipo walipoanza kujiokoa.

“Tunamshukuru mungu tumenusurika licha ya mali zetu zote kuteketea kwa moto ambao ulianzia kwenye moja ya maduka ambayo yameungana na nyumba hii ambayo tulikuwa tunaishi,” alisema Mhina.

Naye Said Juma alisema kuwa moto huo umewapa hasara kubwa kwani amepoteza vitu karibu vyote na kufanikiwa kuokoa vichache hali ambayo inamfanya aanze upya maisha.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Yahaya Abdala alisema kuwa wananchi, Zimamoto pamoja Jeshi la polisi walifanikisha kuzimwa moto huo ambao ulisababisha vitu vote kuteketea lakini hakuna mtu aliyedhuriwa na moto huo zaidi.

Naye diwani wa kata ya Picha ya Ndege Robert Machumbe alisema kuwa wahanga hao hawakuweza kuokoa kitu kwani vitu vyote viliteketea kwa moto huo uliokuwa mkali.

Machumbe alisema kuwa baada ya tukio hilo walichangisha kwa majirani na kupata kiasi cha shilingi 80,000 ambazo ziligawanywa kwa wahanaga hao angalau wapate fedha kwa ajili ya chakula na wahanga hao wamehamia kwa ndugu jamaa na marafiki zao wakiangalia namna ya kutafuta nyumba nyingine.

Katika hatua nyingine mtoto mwenye umri kati ya miaka minne na nusu amenusurika kufa baada ya mama yake kumwacha kwenye nyumba huku akiwa amemfungia ndani na yeye kwenda kusikojulikana ambapo kati ya majirani waliounguliwa nyumba ambaye ni mwanajeshi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) alijitosa na kumwokoa mtoto huyo.

Mwisho.   

DC ASHANGAA WATU KUFANYA NGONO KWENYE MAKABURI

Na John Gagarini, Kibaha

MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Asumter Mshama amesikitrishwa na baadhi ya wakazi wa mtaa wa Mwanalugali kata ya Tumbi wanaoshiriki kwenye vitendo vya kishirikina kwa kufanya ngono kwenye makaburi ya Air Msae yaliyopo katika mtaa huo na kusema kuwa serikali haitatoa fedha kwa ajili ya kuweka uzio kwenye makaburi hayo ili kuzuia vitendo hivyo.

Makaburi hayo ambayo yalianzishwa na halmashauri ya Mji wa Kibaha baada ya basi la Air Msae kupata ajali kwenye barabara kuu ya Morogoro ambapo ili ua watu wengi na maiti nyingi zilizikwa hapo baada ya kukosa ndugu.

Akizungumza na wakazi wa mtaa huo alisema kuwa inasikitisha kuona watu wanafanya vitendo hivyo juu ya makaburi kwani hiyo ni laana kwa watu wanaojihusisha na vietendo hivyo na serikali haitapeleka fedha kwa ajili ya kuweka uzio badala yake fedha hizo ni afadhali zipelekwe kwenye shughuli za maendeleo.

Mshama alitoa kauli hiyo kufuatia uongozi wa kata hiyo ambapo mtendaji wa kata hiyo Msemakweli Karia akisoma risala alisema kuwa moja ya changamoto zilizopo kwenye kata ni baadhi ya watu kujihuisha na uovu huo nyakati za usiku juu ya makaburi hayo pamoja na vitendo vingine viouvu ikiwa ni pamoja na uvuitaji wa bangi hivyo kuomba kupewa fedha kwa ajili ya kuweka uzio kuzuia watu hao.

“Haiwezekani kuweka uzio kwani watu wanaofanya vitendo hivyo wanajitafutia laana kwani hawawezi kupata utajiri kwa kufanya vitendo hivyo kwenye makaburi hayo ya umma ambayo yanatumika kuzika watu kwenye mji wa Kibaha na hiyo ni laana kwani wanaofanya hivyo wanasema kuwa kwa kuwa ajali hiyo iliua watu wengi hivyo na wao watapata utajiri mkubwa jambo ambalo ni dhana ambayo haipaswi kupewa nafasi kwani uchawi unarudisha nyuma maendeleo na mji unaoendekeza imani hizo hauwezi kupiga hatua,” alisema Mshama.

Aidha alisema ili wananachi wa weze kujiletea maendeleo wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na si kuwa na imani za kishirikina ili kupata maendeleo suala hilo halipaswi kupewa kipaumbele bali jitihada za kufanya kazi kwa bidii ndizo zitakazowafanya wawe na maisha mazuri.

Awali akisoma risala ya Kata ya Tumbi mtendaji wa kata hiyo Msemakweli Karia amesema kuwa changamoto nyingine zilizopo katika eneo hilo ni ubovu wa barabara.

Mwisho.