Thursday, April 28, 2016

REA KUNUFAISHA VIJIJI KWA MRADI WA MABILIONI


Na John Gagarini, Kisarawe

SHIRIKA la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) mkoa wa Pwani kupitia mradi wa umeme vijijini (REA) unatarajia kusambaza umeme kwa wananchi 11,000 wenye thamani ya shilingi bilioni 30 kwenye vijiji 109 vya mkoa huo .

Kwa mujibu wa Mhandisi mkuu wa Mradi huo wa REA mkoa wa Pwani Leo Mwakatobe alisema mradi huo wa awamu ya pili utakamilika mwishoni mwa mwezi wa sita mwaka huu.

Mwakatobe alisema kuwa lengo kubwa kwa sasa ni kutekeleza agizo lililotolewa na serikali la kuhakikisha miradi hiyo ya umemem vijijini inawafiki wananchi wengi na kwa wakati uliopangwa.
“Tumeshaanza katika kutekeleza miradi hiyo katika maeneo ya Chalinze, Kisarawe na tutaendelea katika sehemu mbali mbali za Mkoa wetu wa Pwani na tunatarajia kufikia vijiji vipatavyo 109 vilivyopo katika Mkoa wetu,” alisema Madulu.   
Alisema kuwa kuwa mbali ya kuendelea kukutekeleza miradi hiyo hata hivyo wanakumbana na changamoto nyingi katika utekelezaji wa  wakati wanapotaka kupitisha miundomibu katika makazi ya watu.

“Baadhi ya watu wamekuwa hawataki kuridhia umeme kupita kwenye maeneo yao au kutaka fidia kubwa hali ambayo inasababisha kuwa na changamoto za hapa na pale lakini hata hivyo tunajitahidi kuwaelewe umuhimu wa miradi hiyo na kupata nishati hiyo ya umeme,” alisema Mwakatobe.

Kwa upande wake Meneja wa TANESCO Mkoa wa Pwani  Martin Madulu alisema kuwa kwa sasa wanatekeleza  agizo lililotolewa na serikali kuhakikisha wanawafikia wateja wao wote hususani wale wa vijijini  kwa lengo kuweza kuwaunganishia umeme kwa bei nafuu.

Madulu alisema kuwa watahakikisha wanafanya jitihada ili kuwafikia wateja wao ili waweze kuwa na nishati ya umeme katika maeneo mbai mbali hususan kwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya vijijini.

Wakati huo huo wakazi zaidi wa 100 katika  kijiji cha  Nyeburu  Wilayani Kisarawe waliokuwa na tatizo  la upatikanaji wa nishati ya umeme na kuishi  katika giza  kwa kipindi cha muda mrefu kwa sasa wamenufaika baada ya  kuunganishiwa umeme kutokana na  kukamilika kwa mradi wa umeme vijijini (REA) awamu wa pili.

Baadhi ya wakazi hao walisema kwamba kukamilika kwa mradi huo kutaweza kuleta chachu kubwa ya kimaendeleo katika kijiji hicho kwani mwanzoni   walikuwa wanashindwa tutimiza malengo yao waliyojiwekea kutokana na kutokuwa na nishati hiyo ya umeme.

Mwisho.

Tuesday, April 26, 2016

BODI YA MIKOPO TCU YASHAURIWA KUKOPESHA WANAFUNZI VYUO VYA KATI

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI na Bodi ya Mikopo Nchini (TCU) imeshauriwa kuviingiza kwenye mpango wa mikopo wanafunzi wanaosoma Vyuo vya Kati kama ilivyo kwa wanafunzi wa Vyuo Vikuu.
Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani Abdul Sharifu wakati mkutano wa Shirikisho la Wanafunzi wa Vyuo vya Juu wa (CCM).
Sharifu alisema kuwa wanafunzi hao ni sawa na wale wa vyuo vikuu na wengine wanatoka kwenye mazingira magumu na wanahitaji mikopo ili waweze kupata elimu ya juu.
“Hali ya sasa ni ngumu na wazazi ni wale wale wanahitaji kupunguziwa mzigo wa kulipa ada ambazo ni kubwa hivyo tunaona kuwa kuna haja ya serikali kuviingiza na vyuo vya kati kwenye mpango wa kutoa mikopo kwa wanafunzi,” alisema Sharifu.
Alisema kuwa kwa kuwa nchi imeamua kuwekeza kwenye elimu kwa lengo la kuhakikisha kuwa watoto wanapata elimu bora hadi kufikia elimu ya juu ambayo ndiyo inaweza kumsaidia mtoto.
“Kwa sasa elimu ya juu ndiyo inayotakiwa tofauti na elimu ya kawaida ambayo si ya juu ambayo kwa sasa haina nafasi ya muhitimu kupata ajira hivyo kulazimisha watu wapate elimu ya juu,” alisema Sharifu.
Aidha alisema kuwa shirikisho hilo ni mboni ya chama na linafanya kazi kubwa ya kukijenga chama kwani hapo ni tanuru la kuandaa viongozi wa baadaye wa kukiongoza chama pamoja na nchi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kibaha Maulid Bundala  ambaye alimwakilisha mwenyekiti wa Mkoa Mwinshehe Mlao alikuwa mgeni rasmi kwenye mkutano huo alisema kuwa Shirikisho la Vyuo Vikuu la CCM linafanya kazi kubwa ya kukitetea chama.
Bundala alisema kuwa CCM imeleta ukombozi ndani ya nchi na ni chama kikongwe hivyo kwa wanavyuo waliojiunga na shirikisho hilo wako sehemu salama kwani mawazo yao yataleta manufaa kwa nchi.
Aidha alisema kuwa nchi kwa sasa ina hitaji kuongozwa na wasomi hivyo wasomi hawa wataleta mabadiliko na chama kiko tayari kubadilika na wao wananafasi ya kumshauri Rais na wao ndiyo watakaoliinua taifa.
Naye naibu katibu mkuu wa shirikisho hilo Siraji Madebe alisema kuwa shirikisho lao linakabilia na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na wancahama wake wale wa vyuo vya kati kutotambuliwa na Bodi ya Mikopo hivyo kutopata mikopo.
Madebe alisema kuwa licha ya changamoto mbalimbali lakini watahakikisha wanaendeleza umoja wao ili kufanikisha malengo ya kuanzishwa shirikisho hilo ambayo ni kuwaunganisha wasomi walio vyuo kuwa na umoja wao ili kukipigania chama.

Mwisho.

Friday, April 22, 2016

SUMATRA POLISI KUWABURUTA MAHAKAMANI MADEREVA WA DALADALA WANAOKATISHA RUTI

Na John Gagarini, Kibaha
MADEREVA wa mabasi ya abiria yanayotoa huduma wilayani Kibaha yanayotokea Mbezi na Ubungo Jijini Dar es Salaam watakaokatisha ruti watafikishwa mahakamani badala ya kupigwa faini.
Akizungumza na gazeti hili Ofisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Usafirishaji Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoani Pwani Nashon Iroga alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo baada ya madereva hao kudharau faini hizo na kulipa kwa urahisi.
Iroga alisema kuwa wamiliki wa mabasi hayo maarufu kama Daladala wamekuwa wakilipa faini na kuendelea kukatisha ruti hivyo kuwapa usumbufu abiria wanokwenda maeneo mbalimbali.
“Madereva hawa wamekuwa kama sugu licha ya kupigwa faini lakini wanalipa kwani wanaona kama ni afadhili kulipa faini na kukatisha ruti kuliko kuwafikisha abiria kule waendako,” alisema Iroga.
Alisema kuwa abiria wengi wanaokwenda maeneo ya Chalinze, Mkata, Msata na Mlandizi wamekuwa wakilalamika kuwa madereva hao hukatisha ruti na kugeuzia Kongowe kwa madai kuwa abirai wanaobaki ni wacheche hivyo wanapta hasara kuwapeleka maeneo hayo.
“Utakuta basi limetokea Ubungo au Mbezi na leseni yake inaonyesha linakwenda mfano Chalinze, Mkata, Msata  na Mlandizi akianza safari anakuwa na abiria wa kutosha lakini njiani abiria wanashuka hivyo wakifika Kongowe wanageuza wakidai kuwa abiria ni wachache hivyo hawapatia faida ndiyo wanakatisha ruti,” alisema Iroga.
Naye Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Pwani (RTO) Abdi Isango alisema kuwa hadi juzi madereva sita walipandishwa kizimbani kutokana na kukatisha ruti hizo.
Isango alisema kuwa wao waliomba leseni kufika hayo maeneo ambayo yametajwa na yameandikwa kabisa lakini hawawafikishi abiria kule walikosema na wamekuwa wakiwafaulisha kwenye mabasi mengine.
“Tumeona ili kukomesha tabia hiyo ya kukatisha ruti ni kuwapeleka mahakamani madereva wao wenyewe kwani faini wanaidharau na kulipa lakini kwa sasa ni kuwafikisha mahakamani tumeona njia hii itasaidia kwani faini ya shilingi 30,000 au ile ya 250,000 ya SUMATRA zimekuwa zikilipwa na wamiliki wao,” alisema Isango.
Alisema kuwa madereva 25 wanatafutwa baada ya kutenda kosa hilo na kukimbia huku wawili wakiyaacha magari na kukimbia lakini bado wanatafutwa na mara watakapokamatwa watafikishwa mahakani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mwisho. 

SOKO LA MLANDIZI WALILIA USAFI

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA kwenye soko la Mlandizi Wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba serikali kuwajengea mitaro kwenye soko hilo ili kuruhusu maji kupita wakati wa mvua kwani soko hilo liko kwenye hali mbaya.
Akizungumza na waandishi wa habari Sauda Said alisema kuwa mvua inaponyesha maji yanajaa na kuwa kero kwa wateja wanaofika kununua bidhaa.
Said alisema kuwa mbali ya kutokuwa na mitaro pia soko hilo lina uchafu mwingi kutokana na kutotolewa kwa kipindi kirefu na kusababisha uchafu huo kutoa harufu kali.
“Changamoto nyingine ni ukosefu wa vifaa vya kufanyia usafi kwani mbali ya kutoa kiasi cha shilingi 200 kila siku kama ushuru usafi haufanyiki ipasavyo hivyo kufanya mazingira ya soko kuwa machafu,” alisema Said.
Alisema kuwa soko hili kwa sasa linazalisha uchafu mwingi sana lakini tatizo ni halmashauri kushindwa kuondoa uchafu kwa wakati na kufanya mlundikano wa uchafu kuwa mkubwa hali ambayo ina hatarisha afya za watumiaji.
Naye mwenyekiti wa soko hilo Thobias Michael alisema kuwa soko hilo ni kubwa kuliko masoko yote mkoani Pwani na linahudumia wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya za Bagamoyo, Kibaha na Kisarawe lakini mazingira yake si rafiki kwa watumiaji kutokana na uchafu kukithiri.
Michael alisema kuwa waliahidiwa kuwa watajengewa soko la kisasa ili kuondokana na changamoto wa soko hilo kwa sasa kuwa dogo kutokana na kuwa na wafanyabiashara wengi.
“Kwa sasa idadi ya wafanyabiashara ni 450 ni kubwa sana na uzalishaji wa uchafu ni mkubwa sana lakini uzoaji taka unakwenda taratibu sana na vifaa vya kufanyia usafi hakuna kwani hata gari la kuzolea taka hakuna inawabidi Halmashauri kukodisha,” alisema Michael.
Kwa upande wake mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Kibaha Dk Mariamu Maliwa alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo ni ukosefu wa gari la Halmashauri kwa ajili ya kuzolea uchafu lakini wanakodisha gari kwa ajili ya kuzoa uchafu huo.

Mwisho.

KIBAHA WADHIBITI KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imefanikiwa kuudhibiti ugonjwa wa Kipindupindu eneo la Mlandizi ambao uliolipuka Machi mwaka huu na kusababisha vifo vya watu watatu.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisni kwake mjini Kibaha Dk Mariamu Maliwa alisema kuwa walifanikiwa kuudhibiti kwa kufungia biashara za vyakula ambazo hazikutimiza masharti ya afya.
Dk Maliwa alisema kuwa mgonjwa wa mwisho aliyekuwa amelazwa kwenye kituo cha afya Mlandizi aliruhusiwa Aprili 21na kufanya kutokuwa na mgonjwa Kipindupindu hata mmoja kutoka wagonjwa 115 waliogundulika kuwa na ugonjwa huo kuanzia mwezi Machi mwaka huu.
“Kwa zaidi ya kipindi cha wiki moja tulizuia biashara zote za vyakula pamoja na matunda kwani tuliona kuwa sehemu hizo zilikuwa chanzo cha ugonjwa huo na tulipozifungia wagonjwa walipungua lakini kabla ya kuzifungia kulikuwa kunapatikana wagonjwa hadi nane kwa siku moja hali amabayo ilikuwa ni mbaya sana,” alisema Dk Maliwa.
Alisema kuwa mbali ya kuzuia biashara zote za vyakula pia walikuwa wakitoa elimu juu ya kujikinga na ugonjwa kuhamasisha usafi kwenye maeneo ya biashara, majumbani na sehemu zinazozalisha uchafu kwa wingi, uzoaji taka na kuhamasisha matumizi ya vyoo na kwa wale wasio na vyoo wachimbe vyoo.
“Walikaidi kujenga vyoo tumewapeleka mahakamani kwani wanaonekana kukaidi maagizo hayo kwani kujisaidia holela nako kuna changngia kuenea kwa ugonjwa huu,” alisema Dk Maliwa.
Aidha alisema kuwa wagonjwa hao walitoka kwenye maeneo mbalimbali ya Kibaha na nje ya Kibaha ambapo Ruvu walikuja wagonjwa 63, Mlandizi 27, Visiga na Kongowe 13, Dutumi wanane, Vingunguti na Mbezi wawili, Mzenga mmoja na wale waliokufa mmoja alifia hospitali huku wawili wakifia majumbani.
Alisema kuwa wataruhusu wauzaji wa vyakula mara watakapoona kuna mabadiliko ya ufuataji wa kanuni za afya mara baada ya maofisa wa afya kupita na kujiridhisha kuwa vyanzo vyote vya ugonjwa huo vimedhibitiwa na kuzingatiwa kwa kanuni za usafi na kuwataka wananchi kuweka mazingira yao kwenye hali ya usafi.
Mwisho.

KEC SACCOS YAKOPESHA WANACHAMA WAKE MABILIONI YA FEDHA

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Ushirika wa Mikopo cha Shirika la Elimu Kibaha (KEC SACCOS LTD) kimeweza kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.3 kwa wanachama wake kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mwenyekiti wa Ushirika huo Kachingwe Kaselenge alisema kuwa mtaji wao kwa sasa umefikia zaidi ya Bilioni 2.
Kaselenge alisema kuwa kwa sasa akiba ndani ya chama imefikia bilioni 1.7 hisa zikiwa ni shilingi milioni 213.9 na mkopo ni bilioni 2.2 ambapo kwa kila mwezi wanatoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 190.
“Tunamshukuru Mungu kwa sasa chama kinaendelea vizuri kwani marejesho ni asilimia 98 hadi 99 ni wanachama wachache tu ambao wanarejesha kwa matatizo nah ii inatokana na kuwa na mikopo sehemu nyingine kwani sheria inasema mtumishi anapokopa lazima ibaki asilimia 1/3 ya mshahara wake,” alisema Kaselenge.
Alisema kuwa wanachama wao ni watumishi wa Shirika hilo lakini kutokana na kuwa na uwezo mkubwa wameongeza wanachama ambao ni wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha (KDC) na wale wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha (KTC) pamoja na wafanyakazi waofisi ya mkuu wa mkoa.
“Chama chetu ni moja ya vyama vikongwe hapa nchini kwani kwa mwaka huu kinatimiza miaka 50 tangu kunzishwa kwake na tunajivunia mafanikio makubwa tuliyoyapata tangu kuanzishwa kwake kwani wanachama wameweza kunufaika na mikopo inayotolewa kwani zaidi ya watu 5,040 wananufaika kwa siku na mikopo hii kwani wanachama wana miradi mbalimbali kama ya mabasi, shule, ufugaji bodaboda na shughuli nyingine za kimaendeleo,” alisema Kaselenge.
Aidha alisema kuwa mtaji walio nao ni wa ndani kwani hawakopi kwenye mabenki kama baadhi ya vyama vinavyofanya hivyo hawana deni lolote wale mkopo kwenye taasisi za kifedha ambapo hubidi kuweka riba kubwa ili kufidia mikopo kwani kutokana na kuwa na mtaji wa ndani riba yao ni asilimia 1.6.
“Kuna mikopo ya aina mbalimbali ikiwa ni pamoja na ile ya Dharura kama vile misiba na majanga mbalimbali, Maendeleo ikiwa ni pamoja na ujuenzi wa nyumba usafiri na ufugaji, Elimu kusoma na kusomesha na mwanachama anapofariki familia inalipwa 300,000 na kama ni mwenza wake analipwa 200,000 kwani asilimia moja ni bima ya mkopo na endapo anafariki deni linakufa na fedha zake watalipwa ndugu bila ya kukatwa chochote kwani bima itakuwa inalinda mkopo huo,” alisema Kaselenge.
Alibainisha kuwa wanakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwa na ushindani mkubwa toka kwenye taasisi za kifedha ambazo zinawashawishi wanachama wao kujiunga nao kwa kuwalipia madeni wanayodaiwa kwenye chama, sheria kutaka vyama hivyo kutolipa kodi lakini wanaaambiwa walipe kodi na mwanachama anauwezo wa kukopa mara tatu ya akiba yake aliyojiwekea kati ya shilingi milioni moja hadi milioni zaidi ya 20.
Ushirika huo ulianzishwa mwaka 1966 ukiwa na wanachama ukiwa na wanachama 66 lakini kwa sasa una wanachama 840 na kilianzishwa kwa ajili ya  kusaidiana na kusaidia jamii inayowazunguka kwa kujitolea misaada sehemu mbalimbali kama hospitali na maeneo yenye uhitaji.
Mwisho.

Monday, April 18, 2016

SEKRETARIETI PWANI KUCHUNGUZA FEDHA ZILIZORUDISHWA HAZINA NA WAKURUGENZI WA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amesema kuwa ataituma sekretarieti ya mkoa wa Pwani kufuatialia kwa wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya za mkoa huo kuchunguza juu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 249, 452,390 kuwa zimerudishwa Hazina ikiwa ni sehemu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 641,361,239 ambazo ni hasara zilizolipwa kwa watumishi hewa 25.
Mbali ya kuituma sekretarieti kufuatilia suala la fedha hizo pia amewataka wakuu wa wilaya kutumia vyombo vya dola kama vile Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufuatilia watu waliohusika kuchukua fedha hizo.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Kibaha Ndikilo alisema kuwa serikali haijaridhishwa na majibu ya wakurugenzi hao kuwa fedha hizo wamezirejesha Hazina huku kukiwa hakuna viambatanisho vyovyote ambavyo vinaonyesha kuwa fedha hizo zilipelekwa hazina.
“Serikali inataka kujua ni nani aliyehusika kuchukua fedha hizo kinyume cha taratibu za kazi kwani watumishi hao ni hewa lakini cha ajabu walikuwa wakilipwa mishahara kwa kila mwezi na kuitia serikali hasara kiasi hicho,” alisema Ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa kati ya hao watumishi hewa ni wale ambao wamefariki dunia, wasio kuwepo kazini kuacha kazi na wastaafu lakini walikuwa wanalipwa kama vile wako kazini jambo ambalo ni kinyume cha sheria na wanastahili kuchukuliwa hatua kali mara watakapo kutwa na tuhuma hizo.
“Zoezi hili litaendelea kufanyika ili kubaini ni njia gani walizokuwa wakizitumia hadi kufikia kulipwa fedha hizo ili hali hawako kazini na kuisababishia serikali hasara kubwa kiasi hicho hali ambayo imefanya zoezi hilo kufanywa kwa watumishi wa serikali ili kuwabaini,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema alisema kuwa kama kuna watu walikuwa wakifoji na kujipatia fedha hizo endapo watabainika watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha wizi huo wa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwa kuiibia serikali.
Alisisitiza kuwa suala la watumishi hewa lilikuwa ni kama kansa ambayo inaitafuna nchi lakini baada ya Rais Dk John Magufulia kubaini na kuagiza kutafutwa watumishi hewa ni dhahiri hatua zitakazochukuliwa zitakomesha watumishi hewa waliokuwa wanaiibia serikali.
Mwisho.

KILUA YAUNGA MKONO DHAMIRA YA DK MAGUFULI KUJENGA VIWANDA

Na John Gagarini, Kibaha
KATIKA kuunga mkono dhamira ya Rais Dk John Magufuli ya uchumi wa nchi kutegemea viwanda kampuni ya Kilua Steel inatarajia kuanza uzalishaji wa bidhaa za vyuma zikiwemo nondo pamoja na vyuma mbalimbali ifikapo mwezi Mei mwaka huu.
Uzalishaji wa vyuma kwenye kiwanda hicho utapunguza bei ya bidhaa za vyuma kwa asilimia 25 ya bidhaa hizo ambazo nyingi zinaagizwa toka nje ya nchi hivyo kuongeza mapato ya ndani.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kiwanda hicho kilichopo Kitongoji cha Disunyala Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani mkurugenzi wa kiwanda hicho Mohamed Kilua alisema kuwa kiko kwenye hatua za mwisho za kuunganisha umeme mkubwa wa viwandani kwani uliopo ni mdogo na hauwezi kuendesha mashine za kiwanda hicho.
Kilua alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitakuwa ni cha kipekee hapa nchini na barani Afrika kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.5 kwa mwaka huku kwa siku kikitarajiwa kuzalisha tani 2,000 kwa awamu ya kwanza na kufikia tani 7,000 itakapofikia awamu ya tatu na itatoa ajira kwa watu zaidi ya 2,000.
“Tunatarajia kuzalisha vyuma vyenye ubora wa kimataifa ili viweze kuwa na soko sehemu yoyote ile duniani kwani tuna wataalamu kutoka nchi ya China ambao ndiyo tunaoshirikiana nao hapa,” alisema Kilua.
Alisema kuwa tayari malighafi za kutengenezea vyuma wanazo ambazo zinatoka nchi kama vile Brazil na nchi zinazotengeneza vyuma duniani lakini mara kitakapoanza kazi kitakuwa na malighafi zake.
“Tunarajia malighafi zote mara tutakapoanza uzalishaji zitapatikana hapa hapa hivyo bei ya vyuma itashuka na nchi itapata maendeleo kupitia kodi mbalimbali kwenye kiwanda,” alisemaKilua.
Aidha alisema kuwa vyuma vitakavyozalishwa hapo mbali ya nondo ni pamoja na vyuma vinavyo husika na ujenzi wa madaraja makubwa, mabomba yatakayotumia gesi, maghorofa kufikia urefu wa ghorofa 50 na kuendelea na vyuma vya engo tofautitofauti ambavyo vitapatikana na kuwapunguzia gharama wananchi katika shughuli zao zinazohitaji vyuma.
Kwa upande wake mkurunzi mwenza kutoka nchni China Wang Zuojin alisema kuwa aliamua kushirikiana na Kilua ikiwa ni moja ya njia za kuenzi urafiki wa nchi hizo ambao ulianzishwa na Mwalimu Julius Nyerere zaidi ya miaka 50 iliyopita.
Zuojin alisema kuwa nchi ya China miaka mingi iliyopita ya nyuma ilikuwa maskini lakini walijipanga hasa kupitia viwanda na kuifanya nchi hiyo kuwa yenye uchumi mkubwa duniani kupitia viwanda.
“Rais Dk John Magufuli ni mtu anayependa maendeleo na tumeamua kumuunga mkono kwa sera zake za kuinua uchumi wa wananchi wake kwa kuendeleza sekta ya viwanda ili kuwa na uchumi wa kati kwa kufanya mapinduzi ya viwanda,” alisema Zuojin.
Alisema kuwa anachokisema Dk Magufuli kinawezekana kwani hata China ilikuwa chini kiuchumi lakini walipoamua kuwekeza kwenye viwanda wamefanikiwa na kuwa nchi zenye uchumi mkubwa duniani na kuwaondoa wananchi wake kwenye umaskini.
Mwisho.
   





Friday, April 15, 2016

WATUMISHI HEWA WAITIA HASARA SERIKALI KIASI CHA SHILINGI MILIONI 641


Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani umebaini uwepo wa watumishi hewa 25 wakiwemo walio kufa na wameipa serikali hasara kiasi cha shilingi milioni 641,361,239 kutokana na kupokea mishahara pasipo kufanya kazi ambalo ni kosa kisheria.

Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evaristi Ndikilo alisema kuwa hasara hiyo imebainika baada ya kufanya uhakiki kwa mara ya pili na kuona kuwa fedha za mishahara ziliendelea kutolewa kwa watumishi hewa licha ya kutokuwepo kazini.

Ndikilo alisema kuwa kati ya watumishi 19 ni wale waliokufa, waliostaafu na kuacha kazi lakini mishahara yao ilikuwa ikiendelea kutoka na kusababisha hasara hiyo baada ya kuwafanyia uhakiki watumishi 150 ili kuwatafuta watumishi hewa kutokana na agizo la Rais Dk John Magufuli.

“Kundi hili la kwanza limeipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 69.1 huku wale ambao hawapo kabisa kazini wameipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 12.4 na watumishi watoro na wale walio na mashauri ya kinidhamu wameipa hasara serikali kiasi cha shilingi milioni 448.2,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa kati ya watumishi 150 waliohakikiwa 31 walibainika kuwa ni watoro na hawakujitokeza siku ya uhakiki lakini walionekana kuwa ni watumishi halali kwa kuonyesha nyaraka muhimu huku 18 wakibainika kuwa ni watoro na wanamashauri ya kinidhamu lakini waliendelea kulipwa mishahara.

“Watumishi 76 ambao ni watoro na wanamashauri ya kinidhamu mishahara yao imesimamishwa ili wasiendee kuitia hasara serikali wakati mashauri yao yanafanyiwa kazi,” alisema Ndikilo

Aidha alisema kuwa wakurugenzi wa Halmashauri saba za wilaya walisema kuwa kiasi cha shilingi milioni 249,452,390  zilirudishwa Hazina na kuwataka wapeleke viambatanisho kama ushahidi vinavyoonyesha kuwa walipeleka hazina na si maneno matupu.

“Kama ni kweli kiasi hicho cha fedha kilipelekwa hazina fedha ziltakazokuwa zimepotea ni kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 391.8 ambazo wanapaswa kuonyesha vielelezo vya kuzipeleka hazina kwani maelezo hayo bado hayajaturidhisha wanatakiwa watupe uthibitisho ili tuliamini hilo,” alisema Ndikilo.     


Mwisho.

Saturday, April 9, 2016

HOSPITALI YA BAGAMOYO YADAIWA M 220 NA MSD

Na John Gagarini, Kibaha
HOSPITALI ya Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani inakabiliwa na upungufu mkubwa wa dawa baada ya kukosa dawa kuanzia Januari mwaka huu kutoka Bohari Kuu ya Madawa (MSD) kutokana na kudaiwa deni la shilingi milioni 220.
Hayo yamesemwa na mganga mkuu mfawidhi wa Hospitali hiyo Tumaini Byron wakati Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo kutembelea wagonjwa na kuwapa misaada mablimbali katiaka kusherehekea miaka 61 ya kuanzishwa Jumuiya hiyo.
Dk Byron amesema kuwa kutokana na deni hilo Hospitali hiyo kwa sasa imeonekana haikopesheki kutokana na deni hilo hivyo kunywimwa dawa hadi pale watakapolipa deni hilo la madawa.
Amesema wanakosa dawa kutokana na deni hilo kwani hata wakiomba hawapati hivyo kuwapa wakati mgumu wao pamoja na wagonjwa ambao hutakiwa kwenda kununua kwenye maduka ya madawa.
Aidha amesema kuwa wanashindwa kupewa au kukopeshwa vifaa tiba pamoja na vipimo mbalimbali ikiwa ni pamoja na vipimo vya wingi wa damu mkojo na malaria.
Amebainisha kuwa changamoto nyingine ni upungufu wa watumishi kwani kwa sasa wana watumishi 147 huku mahitaji yakiwa ni watumishi 250, vitanda vilivyopo ni 24 tu ambapo walau vingepatika japo 100 pamoja na uchakavu wa miundombinu ya umeme..
Kwa upande wake Mfamasia wa wilaya ya Bagamoyo Mohamed Makarai amesema kuwa mbali ya deni hilo la dawa pia MSD kutokuwa na dawa hivyo kuwa ni tatizo la nchi nzima kuanzia Oktoba na Novemba mwaka jana.
Makarai amesema kuwa serikali ilibadilisha mfumo wa kutoa tenda kwa wazabuni kwa ajili ya kuwapelekea dawa ambapo kwa sasa utaratibu umebadilika kwani hakutakuwa na kutoa tenda tena.
Amesema kuwa walikuwa wakichukua dawa kwa mali kauli na kutoa fedha baadaye hata hivyo walitoa fedha kiasi cha shilingi milioni 100 ambapo moja ya changamoto ya kukosa fedha ni pamoja na kuwa na misamaa ikiwemo ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano, wazee, wajawazito na wale wenye magonjwa sugu hivyo serikali inapaswa kufidia pengo la makundi hayo ambayo yanapewa dawa bure.
Mwisho.

Monday, April 4, 2016

UVCCM WATAKIWA KUTUMIA KILIMO KAMA FURSA NA SIO KAMA ADHABU

Na John  Gagarini, Kibaha
VIJANA wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi  CCM (UVCCM) wilayani Kibaha wametakiwa kukitumia kilimo kama moja ya chanzo cha kujikomboa kiuchumi kwani hiyo ni fursa na si adhabu.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa CCM (MNEC) Rugemalila Rutatina wakati akifungua mkutano wa Baraza la (UVCCM) Kibaha Mjini na kusema kuwa kilimo endapo kitatumia vizuri kinaweza kuboresha uchumi wao badala ya kumtegemea mtu kuwasaidia.
Rutatina alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakiwafanya vijana kama ngazi ya kupandia kwa kuwafanikishia mambo yao kisha kuwaacha bila ya kuwajengea mazingira endelevu.
“Uzuri ni kwamba Chama pamoja na umoja wenu una mashamba ambayo ni kama mtaji wa kuanzia kwa ajili ya kilimo cha kisasa ambacho kitakuwa na tija kwa kutumia mipango mbalimbaili ya kuendeleza kilimo ikiwa ni pamoja na Kilimo Kwanza,” alisema Rutatina.
Alisema kuwa ili vijana wajikomboe wanapaswa kuanzisha miradi ya kudumu kupitia rasilimali za chama ambazo endapo zingetumika ipasavyo zingewaondoa vijana ndani ya chama na nje kuwa tegemezi katika kuendesha umoja wao.
“Kilimo ni moja ya njia za kuwakomboa na kuacha kumtegemea mtu lakini endapo mtaanzisha miradi ya kilimo itawaondoa huko mliko na kuwafanya mjitegemee na kuendesha mambo yenu bila kuwa tegemezi,” alisema Rutatina.
Aidha alisema kuwa kwa sasa fursa ni nyingi kwa vijana ikiwa ni pamoja na mikopo kwa ajili kujikwamua kiuchumi na zana za kilimo kama matrekta wanaweza kuazima kwenye chama.
Kwa upande wake katibu wa (UVCCM) Kibaha Mjini David Malecela alisema kuwa wana maeneo mengi ambayo hata hivyo hayajaendelezwa hali ambayo imesababisha watu kuyavamia.
Malecela alisema kuwa kwa sasa wako kwenye mipango ya kuhakikisha wanayamiliki kisheria ili kukabiliana na watu wanaoyavamia maeneo yao ambayo yakiendelezwa yatakuwa ni moja ya vyanzo vikuu vya mapato ya umoja.
Mwisho.

WAPEWA SIKU 60 KUHAMA ENEO LILILOFUTIWA HATI YA UMILIKI

Na John Gagarini, Kibaha
BAADHI ya wakazi wa Kitongoji cha Vinziko Kijiji cha Kikongo wilayani Kibaha mkoani Pwani wameitaka Halmashauri ya wilaya kutowaondoa kwenye eneo ambalo wanaishi kwani hawana pa kwenda.
Serikali iliwapa siku 60 wawe wameondoka kwenye eneo hilo ambalo lilikuwa chini ya kampuni ya United Framing Cooperation (UFC) ambao walishindwa kuliendesha na kuwa shamba pori kabla ya serikali haijalifutia hati Mei 28 mwaka 2015.
Moja ya wakazi wa eneo hilo Athuman Fundi (90) alisema kuwa wao wako hapo muda mrefu tangu operesheni vijiji ambapo walihamishwa toka maeneo ya mbali na kupelekwa maeneo ambayo yalikuwa karibu na huduma za kijamii.
“Sisi tulifikiri ni vema wakatuacha kwenye maeneo yetu haya na si kutuondoa kwani hatuna pa kwenda na sisi hapa tumeshawekeza kwa kujenga makazi ya kudumu leo wakituambia tuondoke tutakwenda wapi vinginevyo watulipe ili tukatafute sehemu nyingine au watupatie maeneo mengine,” alisema Fundi.
Fundi alisema kuwa mbali ya kutakiwa kuondoka pia vyombo vya dola vimekuwa vikitumia nguvu kubwa kutaka wao waondoke ambapo wenzao wamekuwa wakikamatwa kutokana na mgogoro huo ambao umewanyima raha.
“Tunaomba tusaidiwe na Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi ili tupate haki yetu kwani wao kututaka tuondoke bila ya kutupa chochote au kutotupa maeneo mengine tunaona kama hatujatendewa haki kwani tuna nyumba zetu, mazao ambavyo vimo humo leo wanatuambia tuviondoe tutaishi wapi,” alisema Fundi.
Kwa upande wake Sabina Benedict alisema kuwa wamekuwa wakiteseka sana kutokana na mgogoro huo kwani wazee na vijana wamekuwa wakikamatwa na polisi na kuwekwa rumande hivyo kuishi kwa woga.
Benedict alisema kuwa tatizo kubwa linatokana na viongozi ambao wanataka kumuuzia mwekezaji ambaye anatumia kila njia kuhakikisha wao wanaondoka ili alipate eneo hilo kirahisi.
Naye mwenyekiti wa Kijiji cha Kikongo Sultan Ngandi alisema kuwa shamba hilo lenye ukubwa wa hekta 3,285 lilikuwa likimilikiwa na kampuni hiyo ya UFC ambayo ilikuwa ikilima mazao mbalimbali kama vile Pamba, Mbaazi, Alizeti na mazao mengine ilishindwa kuliendeleza na kuliacha pori ambalo lilikuwa likitumiwa na wahalifu kuzuru watu.
Ngandi alisema kuwa wananchi waliomba kulima ikiwa ni pamoja na Umoja wa wakulima wa Ondoa Njaa Kikongo (ONJAKI) lakini walitakiwa wasilime mazao ya kudumu wala kujenga nyumba za kudumu badala yake walime mazao ya muda mfupi.
“Hata hivyo baadhi ya watu walikiuka makubaliano na wengine walianza kujenga nyumba za kudumu, mazao ya muda mrefu na hata wengine walifikia hatua ya kuayauza kienyeji baadhi ya maeneo nao kuondoka na kuwaacha watu ambao ndiyo wanaolalamika,” aisema Ngandi.
Akizungumzia suala hilo mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa ni kweli wametoa siku 60 kwa watu walioko kwenye eneo hilo kwani wamevamia na hawakutakiwa kuwa kwenye neo hilo kwani liko chini ya serikali.
Kihemba alisema kuwa hilo ni moja ya mashamba 16 ambayo yalifutiwa hati na kwa sasa wanaendelea na mchakato wa kulitengea matumizi na waliwataka watu walioko kwenye eneo hilo wapeleke vielelezo vya kuonyesha walipataje maeneo hayo na kusema si kweli kwamba kuna mwekezaji wanataka kumpa eneo hilo.
Aidha alisema kuwa hadi sasa watu zaidi ya 100 wamepeleka vielelezo vyao nab ado wanawasubiri watu wengine ambao wako wengi ili wapeleke vielelezo vyao ili serikali iangalie namna ya kuwasaidia na kuwataka watu hao waondoke kwenye eneo hilo.
Mwisho.

Friday, April 1, 2016

SAKATA WAFANYAKAZI HEWA RC AWATAKA WAKURUGENZI KUBAINISHA WALIOKUWA WAKICHUKUA MISHAHARA PASIPO KUWA WAFANYAKAZI

Na John Gagarini, Kibaha
SAKATA la wafanyakazi hewa mkoani Pwani limeingia hatua mpya baada ya Wakurugenzi wa Halmashauri za mkoa huo kutakiwa kutoa taarifa zaidi juu ya wafanyakazi hewa 42 ambao hawapo kabisa kazini lakini wamekuwa wakipokea mishahara kila mwezi.
Jumla ya wafanyakazi 42 kwenye mkoa huo majina yao yapo lakini wao hawapo kazini lakini walikuwa wakipokea mishahara kila mwezi hali ambayo imeisababishia hasara kubwa serikali kutokana na kulipa hewa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kiwake mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa wafanyakazi hao hewa wamewekwa kwenye madaraja mbalimbali ikiwa ni pamoja na hao 42 ambao hawapo kabisa kazini lakini walikuwa wanalipwa.
“Kutokana na hali hii nimewapa wakurugenzi hadi siku ya Jumatano Aprili 6 wawe wameniletea taarifa juu ya watu waliokuwa wakipokea fedha hizo kwani haiwezekani ni nani aliyekuwa akipokea fedha hizo licha ya kutokuwepo kabisa kwa wafanyakazi hao,” alisema Ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa haiwezekani fedha zilipwe kwa wafanayakazi ambao hawapo kazini kwani ni jambo la kushangaza na lazima ajulikane ambaye alikuwa akipokea fedha hizo kwani kundi hili ni hewa kabisa.
“Kundi lingine ni la wafanyakazi 58 ambao wamesimamishwa kazi kwa tuhuma mbalimbali lakini wamekuwa wakipokea mishahara kama kawaida tunataka tujuea kwa undani ni tuhuma gani zinazowakabili na hatua zilizochukuliwa dhidi yao,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa kundi lingine ni la wafanyakazi ambao wako kazini lakini ni watoro hawaendi kazini lakini mishahara wanachukua kama kawaida licha ya kwamba hawawajibiki kazini kama ilivyo taratibu za utumishi wa umma.
“Tunataka kila mkurugenzi atoe taarifa sahihi bila ya kuficha kwani endapo atabainika ameficha taarifa hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake hivyo ni vema wakawea wazi taarifa za hao wafanyakazi hewa,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa juu ya hasara waliyoiingiza wafanyakazi hao hewa ambapo kwa mkoa wa Pwani ni 150 bado wanaendelea na uchunguzi ili kubaini ni kiasi gani ambacho wameliingizia Taifa hasara na mara watakapokamilisha watatoa taarifa hizo.

Mwisho.

SELEMAN TALL ATWAA MKANDA WA TPBO

Na John Gagarini, Kibaha
BONDIA Said Seleman maarufu kama Tall juzi usiku alitwaa ubingwa wa taifa wa ngumi uzito wa kati kupitia shirikisho la ngumi la TPBO baada ya kumshinda kwa pointi Ambokile Chusa.
Pambano hilo ambalo lilipigwa kwenye ukumbi wa Container wilayani Kibaha mkoani Pwani lilikuwa la vuta ni kuvute kutokana na umahiri wa mabondia hao ambao hata hivyo walikuwa wakicheza kwa kuogopana kwa hofu ya kupoteza ushindi.
Hata hivyo Tall alikuwa mjanja na kumzidi mbinu mpinzani wake ambaye muda mwingi alikuwa akijihami kwa kuficha uso ili kukwepa ngumi kali zilizokuwa zikirushwa na mpinzani wake.
Kwenye mapambano mengine Yasini Said alimpiga Julius Jackson, Emanuel Endrew alimpiga Ramadhan Keshi, Ramadhan Kamage alimtwanga Kassim Chuma, Salehe Muntari alimtwanga Aziz Pendeza, Hassan Mgosi alimtwanga Hemed Hemed, Said Chino alimtwanga Idd Mgwinyo kwa TKO, huku Alfred Masinda na Nurdin Mijibwa na Abdala Luwanje na Rajabu Mbena walitoka sare.
Akikabidhi mkanda huo kutoka TPBO mgeni rasmi katika pambano hilo Selina Wilson Diwani wa Viti Maalumu aliwapongeza waandaaji wa pambano hilo Butamanya Promotion kwa kuleta shindano hilo Kibaha.
Wilson alisema kuwa kuleta mchezo huo Kibaha ni kuibua vipaji vilivyopo mikoani na kuwapa uzoefu mabondia wa hapa kuweza kujifunza mbinu za ngumi.
“Mimi ni kijana na nimeona jinsi gani watu wanavyopenda mchezo huu hapa Kibaha na mkoa wa Pwani nitahakikisha naunga mkono mchezo huu na kupeleka halamashauri changamoto zinazowakabili ili ziweze kufanyiwa kazi kwa lengo la kuboresha mchezo huu,” alisema Wilson.
Kwa upande wake bondia wa zamani Habibu Kinyogoli alisema kuwa mabondia wa mkoa wa Pwani wameonyesha uwezo lakini walichokosa ni mbinu za mapigano hivyo atajitolea kuwafundisha mabondia wa mkoa wa Pwani.

Mwisho.