Friday, April 1, 2016

SAKATA WAFANYAKAZI HEWA RC AWATAKA WAKURUGENZI KUBAINISHA WALIOKUWA WAKICHUKUA MISHAHARA PASIPO KUWA WAFANYAKAZI

Na John Gagarini, Kibaha
SAKATA la wafanyakazi hewa mkoani Pwani limeingia hatua mpya baada ya Wakurugenzi wa Halmashauri za mkoa huo kutakiwa kutoa taarifa zaidi juu ya wafanyakazi hewa 42 ambao hawapo kabisa kazini lakini wamekuwa wakipokea mishahara kila mwezi.
Jumla ya wafanyakazi 42 kwenye mkoa huo majina yao yapo lakini wao hawapo kazini lakini walikuwa wakipokea mishahara kila mwezi hali ambayo imeisababishia hasara kubwa serikali kutokana na kulipa hewa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kiwake mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa wafanyakazi hao hewa wamewekwa kwenye madaraja mbalimbali ikiwa ni pamoja na hao 42 ambao hawapo kabisa kazini lakini walikuwa wanalipwa.
“Kutokana na hali hii nimewapa wakurugenzi hadi siku ya Jumatano Aprili 6 wawe wameniletea taarifa juu ya watu waliokuwa wakipokea fedha hizo kwani haiwezekani ni nani aliyekuwa akipokea fedha hizo licha ya kutokuwepo kabisa kwa wafanyakazi hao,” alisema Ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa haiwezekani fedha zilipwe kwa wafanayakazi ambao hawapo kazini kwani ni jambo la kushangaza na lazima ajulikane ambaye alikuwa akipokea fedha hizo kwani kundi hili ni hewa kabisa.
“Kundi lingine ni la wafanyakazi 58 ambao wamesimamishwa kazi kwa tuhuma mbalimbali lakini wamekuwa wakipokea mishahara kama kawaida tunataka tujuea kwa undani ni tuhuma gani zinazowakabili na hatua zilizochukuliwa dhidi yao,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa kundi lingine ni la wafanyakazi ambao wako kazini lakini ni watoro hawaendi kazini lakini mishahara wanachukua kama kawaida licha ya kwamba hawawajibiki kazini kama ilivyo taratibu za utumishi wa umma.
“Tunataka kila mkurugenzi atoe taarifa sahihi bila ya kuficha kwani endapo atabainika ameficha taarifa hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake hivyo ni vema wakawea wazi taarifa za hao wafanyakazi hewa,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa juu ya hasara waliyoiingiza wafanyakazi hao hewa ambapo kwa mkoa wa Pwani ni 150 bado wanaendelea na uchunguzi ili kubaini ni kiasi gani ambacho wameliingizia Taifa hasara na mara watakapokamilisha watatoa taarifa hizo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment