Monday, April 18, 2016

KILUA YAUNGA MKONO DHAMIRA YA DK MAGUFULI KUJENGA VIWANDA

Na John Gagarini, Kibaha
KATIKA kuunga mkono dhamira ya Rais Dk John Magufuli ya uchumi wa nchi kutegemea viwanda kampuni ya Kilua Steel inatarajia kuanza uzalishaji wa bidhaa za vyuma zikiwemo nondo pamoja na vyuma mbalimbali ifikapo mwezi Mei mwaka huu.
Uzalishaji wa vyuma kwenye kiwanda hicho utapunguza bei ya bidhaa za vyuma kwa asilimia 25 ya bidhaa hizo ambazo nyingi zinaagizwa toka nje ya nchi hivyo kuongeza mapato ya ndani.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kiwanda hicho kilichopo Kitongoji cha Disunyala Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani mkurugenzi wa kiwanda hicho Mohamed Kilua alisema kuwa kiko kwenye hatua za mwisho za kuunganisha umeme mkubwa wa viwandani kwani uliopo ni mdogo na hauwezi kuendesha mashine za kiwanda hicho.
Kilua alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitakuwa ni cha kipekee hapa nchini na barani Afrika kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.5 kwa mwaka huku kwa siku kikitarajiwa kuzalisha tani 2,000 kwa awamu ya kwanza na kufikia tani 7,000 itakapofikia awamu ya tatu na itatoa ajira kwa watu zaidi ya 2,000.
“Tunatarajia kuzalisha vyuma vyenye ubora wa kimataifa ili viweze kuwa na soko sehemu yoyote ile duniani kwani tuna wataalamu kutoka nchi ya China ambao ndiyo tunaoshirikiana nao hapa,” alisema Kilua.
Alisema kuwa tayari malighafi za kutengenezea vyuma wanazo ambazo zinatoka nchi kama vile Brazil na nchi zinazotengeneza vyuma duniani lakini mara kitakapoanza kazi kitakuwa na malighafi zake.
“Tunarajia malighafi zote mara tutakapoanza uzalishaji zitapatikana hapa hapa hivyo bei ya vyuma itashuka na nchi itapata maendeleo kupitia kodi mbalimbali kwenye kiwanda,” alisemaKilua.
Aidha alisema kuwa vyuma vitakavyozalishwa hapo mbali ya nondo ni pamoja na vyuma vinavyo husika na ujenzi wa madaraja makubwa, mabomba yatakayotumia gesi, maghorofa kufikia urefu wa ghorofa 50 na kuendelea na vyuma vya engo tofautitofauti ambavyo vitapatikana na kuwapunguzia gharama wananchi katika shughuli zao zinazohitaji vyuma.
Kwa upande wake mkurunzi mwenza kutoka nchni China Wang Zuojin alisema kuwa aliamua kushirikiana na Kilua ikiwa ni moja ya njia za kuenzi urafiki wa nchi hizo ambao ulianzishwa na Mwalimu Julius Nyerere zaidi ya miaka 50 iliyopita.
Zuojin alisema kuwa nchi ya China miaka mingi iliyopita ya nyuma ilikuwa maskini lakini walijipanga hasa kupitia viwanda na kuifanya nchi hiyo kuwa yenye uchumi mkubwa duniani kupitia viwanda.
“Rais Dk John Magufuli ni mtu anayependa maendeleo na tumeamua kumuunga mkono kwa sera zake za kuinua uchumi wa wananchi wake kwa kuendeleza sekta ya viwanda ili kuwa na uchumi wa kati kwa kufanya mapinduzi ya viwanda,” alisema Zuojin.
Alisema kuwa anachokisema Dk Magufuli kinawezekana kwani hata China ilikuwa chini kiuchumi lakini walipoamua kuwekeza kwenye viwanda wamefanikiwa na kuwa nchi zenye uchumi mkubwa duniani na kuwaondoa wananchi wake kwenye umaskini.
Mwisho.
   





No comments:

Post a Comment