Friday, April 22, 2016

SUMATRA POLISI KUWABURUTA MAHAKAMANI MADEREVA WA DALADALA WANAOKATISHA RUTI

Na John Gagarini, Kibaha
MADEREVA wa mabasi ya abiria yanayotoa huduma wilayani Kibaha yanayotokea Mbezi na Ubungo Jijini Dar es Salaam watakaokatisha ruti watafikishwa mahakamani badala ya kupigwa faini.
Akizungumza na gazeti hili Ofisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Usafirishaji Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoani Pwani Nashon Iroga alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo baada ya madereva hao kudharau faini hizo na kulipa kwa urahisi.
Iroga alisema kuwa wamiliki wa mabasi hayo maarufu kama Daladala wamekuwa wakilipa faini na kuendelea kukatisha ruti hivyo kuwapa usumbufu abiria wanokwenda maeneo mbalimbali.
“Madereva hawa wamekuwa kama sugu licha ya kupigwa faini lakini wanalipa kwani wanaona kama ni afadhili kulipa faini na kukatisha ruti kuliko kuwafikisha abiria kule waendako,” alisema Iroga.
Alisema kuwa abiria wengi wanaokwenda maeneo ya Chalinze, Mkata, Msata na Mlandizi wamekuwa wakilalamika kuwa madereva hao hukatisha ruti na kugeuzia Kongowe kwa madai kuwa abirai wanaobaki ni wacheche hivyo wanapta hasara kuwapeleka maeneo hayo.
“Utakuta basi limetokea Ubungo au Mbezi na leseni yake inaonyesha linakwenda mfano Chalinze, Mkata, Msata  na Mlandizi akianza safari anakuwa na abiria wa kutosha lakini njiani abiria wanashuka hivyo wakifika Kongowe wanageuza wakidai kuwa abiria ni wachache hivyo hawapatia faida ndiyo wanakatisha ruti,” alisema Iroga.
Naye Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Pwani (RTO) Abdi Isango alisema kuwa hadi juzi madereva sita walipandishwa kizimbani kutokana na kukatisha ruti hizo.
Isango alisema kuwa wao waliomba leseni kufika hayo maeneo ambayo yametajwa na yameandikwa kabisa lakini hawawafikishi abiria kule walikosema na wamekuwa wakiwafaulisha kwenye mabasi mengine.
“Tumeona ili kukomesha tabia hiyo ya kukatisha ruti ni kuwapeleka mahakamani madereva wao wenyewe kwani faini wanaidharau na kulipa lakini kwa sasa ni kuwafikisha mahakamani tumeona njia hii itasaidia kwani faini ya shilingi 30,000 au ile ya 250,000 ya SUMATRA zimekuwa zikilipwa na wamiliki wao,” alisema Isango.
Alisema kuwa madereva 25 wanatafutwa baada ya kutenda kosa hilo na kukimbia huku wawili wakiyaacha magari na kukimbia lakini bado wanatafutwa na mara watakapokamatwa watafikishwa mahakani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mwisho. 

No comments:

Post a Comment