Monday, April 18, 2016

SEKRETARIETI PWANI KUCHUNGUZA FEDHA ZILIZORUDISHWA HAZINA NA WAKURUGENZI WA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amesema kuwa ataituma sekretarieti ya mkoa wa Pwani kufuatialia kwa wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya za mkoa huo kuchunguza juu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 249, 452,390 kuwa zimerudishwa Hazina ikiwa ni sehemu ya fedha kiasi cha shilingi milioni 641,361,239 ambazo ni hasara zilizolipwa kwa watumishi hewa 25.
Mbali ya kuituma sekretarieti kufuatilia suala la fedha hizo pia amewataka wakuu wa wilaya kutumia vyombo vya dola kama vile Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufuatilia watu waliohusika kuchukua fedha hizo.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Kibaha Ndikilo alisema kuwa serikali haijaridhishwa na majibu ya wakurugenzi hao kuwa fedha hizo wamezirejesha Hazina huku kukiwa hakuna viambatanisho vyovyote ambavyo vinaonyesha kuwa fedha hizo zilipelekwa hazina.
“Serikali inataka kujua ni nani aliyehusika kuchukua fedha hizo kinyume cha taratibu za kazi kwani watumishi hao ni hewa lakini cha ajabu walikuwa wakilipwa mishahara kwa kila mwezi na kuitia serikali hasara kiasi hicho,” alisema Ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa kati ya hao watumishi hewa ni wale ambao wamefariki dunia, wasio kuwepo kazini kuacha kazi na wastaafu lakini walikuwa wanalipwa kama vile wako kazini jambo ambalo ni kinyume cha sheria na wanastahili kuchukuliwa hatua kali mara watakapo kutwa na tuhuma hizo.
“Zoezi hili litaendelea kufanyika ili kubaini ni njia gani walizokuwa wakizitumia hadi kufikia kulipwa fedha hizo ili hali hawako kazini na kuisababishia serikali hasara kubwa kiasi hicho hali ambayo imefanya zoezi hilo kufanywa kwa watumishi wa serikali ili kuwabaini,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema alisema kuwa kama kuna watu walikuwa wakifoji na kujipatia fedha hizo endapo watabainika watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha wizi huo wa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwa kuiibia serikali.
Alisisitiza kuwa suala la watumishi hewa lilikuwa ni kama kansa ambayo inaitafuna nchi lakini baada ya Rais Dk John Magufulia kubaini na kuagiza kutafutwa watumishi hewa ni dhahiri hatua zitakazochukuliwa zitakomesha watumishi hewa waliokuwa wanaiibia serikali.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment